Friday, February 24, 2017

MWIJAGE AWEKA JIWE LA MSINGI KIWANDA CHA VIGAE PWANI










Na John Gagarini,Chalinze

WIZARA ya Biashara Viwanda na Uwekezaji imesema kuwa imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kuzitaka taasisi zinazohusika na uwekezaji kutokuwa na ukiritimba.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Biashara Viwanda na Uwekezaji Charles Mwijage kwenye Kitongoji cha Pingo Chalinze wakati akiweka jiwe la Msingi kwenye kiwanda cha Vigae cha Twyford Ceramics Ltd.
Mwijage alisema kuwa uwekezaji kama huu unaendana na dhana ya Rais Dk John Magufuli wa kuifanya nchi kuwa ya Viwanda ambapo itaongeza pato la nchi na itazalisha ajira kwa wingi.
“Baadhi ya idara ambazo zinafanikisha uwekezaji ikiwa ni pamoja na brela, idara ya uhamiaji, idara ya kazi, mamlaka ya mapato TRA, wizara ya ardhi, shirika la viwango TBS, Baraza la Mazingira NEMC na nyinginezo zinapaswa kufanya kazi kwa wepesi ili kufanikisha uwekezaji,” alisema Mwijage.
Alisema kuwa kati ya idara hizo baadhi zimekuwa zikifanya vizuri lakini nyingine zimekuwa zikiwapa usumbufu mkubwa wawekezaji hali ambayo inawakatisha tamaa.
“Kwa upande wa wizara yangu hakuna tatizo lolote lakini kuna baadhi ya idara zimekuwa kero kubwa kwa wawekezaji kwa kuwa na ukiritimba usio na sababu naomba kama kuna idara zinakuwa kikwazo niambieni ili tuwachukulie hatua,” alisema Mwijage.
“Viwanda vikiwa vingi nchi itapata mapato makubwa kupitia kodi ambazo zitalipwa kutokana na uuzwaji wa bidhaa zitakazokuwa zinazalishwa viwandani,” alisema Mwijage.
Alisema kuwa nchi zilizofanikiwa kukuza uchumi wake kupitia viwanda zimeweza kutoa ajira nyingi hasa kwa vijana kupitia sekta rasmi na isiyo rasmi.
Kwa upande wake mkurugenzi mkuu wa kiwanda hicho Jack Feng alisema kuwa kiwanda hicho asilimia 95 ya malighafi itakuwa inatoka hapa nchini ambapo kigae kinatumia maligahafi zaidi ya 10.
Feng alisema kuwa mara kiwanda hicho kitakapokamilika Agosti mwaka huu kitaweza kupunguza asilimia 30 ya uagizaji wa vigae toka nje ya nchi.
“Tunatarajia kuajiri wafanyakazi 2,000 moja kwa moja na 4,000 kazi za muda na gharama ya mradi huu ni dola milioni 56 sawa na bilioni 120 ambapo tunatarajia kuuza hadi nje ya nchi kama vile Zambia, Uganda, Rwanda na Burundi,” alisema Feng.
Alisema kuwa wanaunga mkono nchi ya Tanzania kuwa na mpango wa kuwa nchi ya viwanda na wao wanapenda kuwa mfano kwa wawekezaji.
Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa kituo cha uwekezaji Cliford Tandari alisema kuwa uwekezaji wa kiwanda hicho ni wa mfano kwani utavutia makampuni mengi.
Tandari alisema kuwa hadi sasa kituo chake kimeweza kutoa wigo mkubwa katika kuandikisha miradi mbalimbali toka china na kufikia miradi 667 ambayo itazalisha ajira 83,141 kwa watanzania ambapo miradi 452 ni miradi inayohusiana na sekta ya uzalishaji viwandani.
Naye mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kwa sasa mkoa huo umeweza kuwa na viwanda 264 huku vikubwa vikiwa ni viwili.
Ndikilo alisema kuwa uwekezaji huo ni mkubwa na unatarajia kukuza ajira kwa vijana wa mkoa wa Pwani na Tanzania kwa ujumla.
Alisema kuwa mkoa wa Pwani bado una maeneo makubwa ya uwekezaji na tayari kuna eneo lenye bukubwa wa hekari 5,000 linahitaji mwekezaji na wameamua mkoa huo kuwa kituo cha uwekezaji.
Naye Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete aliwapongeza wawekezaji hao kutoka nchi ya China na kusema kuwa Chalinze nayo imejipanga kuwa sehemu ya uwekezaji ambapo kuna ujenzi wa viwanda mbalimbali.
Ridhiwani alisema kuwa changamoto kubwa inayokabiliwa wananchi na wawekezaji ni ukosefu wa maji ambapo wamekuwa wakijitahidi kuikabili lakini bado hawajafanikiwa kuidhibiti aliomba wawekezaji hao kutoa ajira bila ya kuwabagua wenyeji.
Mwisho.









Ramani ya kiwanda cha vigae cha Twyford kilichopo Pingo Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani 


Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji Charles Mwijage akiongea wakati wa uwekeji jiwe la msingi kiwanda cha vigae cha Twyford kilichopo Pingo Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.




Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wa pili kulia akiwa na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kulia wakifuatilia jambo wakati wa uwekaji jiwe la msingi kwenye kiwanda cha vigae cha Twyford kilichopo Pingo Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.




Katikati Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji Charles Mwijage akifunua kitambaa kuashiria uwekeji jiwe la msingi kwenye kiwanda cha vigae cha Twyford kilichopo Pingo Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani kushoto mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo kulia kwa waziri ni Jack Feng mkurugenzi wa kiwanda hicho na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Riziwani Kikwete.


  


Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo kushoto Magid Mwanga akifuatiwa na mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo, mkurugenzi wa kiwanda cha vigae cha Twyford Jack Feng na mbunge wa Jimbo la Chalinze Riziwani Kikwete wakiweka udongo kwenye jiwe la msingi.



No comments:

Post a Comment