Sunday, April 28, 2013

ATOA MIPIRA KWA VIJANA


Na John Gagarini, Kibaha
MJUMBE wa Baraza Kuu Taifa kupitia Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) mkoani Pwani Mariamu Chaurembo ametoa mipira mitatu ya mpira wa miguu kwa chipukizi wa Kibaha Mjini na Kibaha Vijijini ili washindanie.
Alitoa mipira hiyo juzi mjini Kibaha wakati wa ziara ya mwenyekiti wa chipukizi Taifa Gabriel Amos Makala, alipotembelea mkoa wa Pwani kujua shughuli zinazofanywa na umoja huo.
Chaurembo alisema kuwa lengo la kutoa mipira hiyo ni chipukizi hao waweze kukuza, kuendeleza na kuibua vipaji kwa kufanya mashindano ambapo mshindi wa kwanza hadi watatu ndiyo watakaojinyakulia mipira hiyo.
“Nimetoa mipira hii ili iweze kuwaniwa na vijana kwenye wilaya ya Kibaha kwani mbali ya vipaji pia ni moja ya njia ya kuwajengea uwezo wa kujua wajibu wao katika kukitumikia chama,” alisema Chaurembo.
Alisema njia mojawapo ya kuwapata vijana ni kupitia michezo hivyo aliona kuna haja ya kuwaunganisha vijana kupitia michezo mbalimbali ambapo kwa sasa ameanza na soka.
“Mimi napenda sana michezo hivyo nimeona njia ya kuwaweka vijana pamoja ni michezo hivyo wazazi nao wanapaswa kuwaendeleza vijana wao kupitia michezo,” alisema Chaurembo.
Wakati huo huo katibu wa hamasa wa chipukizi Taifa Omary Moris ameahidi kutoa mipira 10 na jezi seti moja kwa chipukizi kwenye mkoa huo ili kuhamasisha michezo.
Moris alisema kuwa vifaa hivyo atavitoa baada ya wiki mbili kuanzia sasa ili vijana waweze kufanya michezo na kukuza vipaji vyao vya mpira wa soka.
Mwisho.    
  

HABARI PWANI


Na John Gagarini, Kibaha
VIKUNDI vya Ujasiriamali wilyani Kibaha mkoani Pwani vinakabiliwa na chanagamoto ya kutokuwa na akaunti jambo ambalo linasababisha fedha wanazopewa na wafadhili kutotumika kwa malengo waliyoziombea.
Hayo yalibainika wakati wa ziara ya ofisi ya mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka kukabidhi fedha na vifaa alivyoahidi kupitia fedha za mfuko wa Jimbo na binafsi kwenye kata mbalimbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mara baada ya ziara hizo msaidizi wa mbunge huyo Method Mselewa alisema kuwa vikundi vingi bado havijaweza kufungua akaunti kwa ajili ya kutunza fedha zao hivyo fedha hizo huishia kugawana.
“Jambo la kwanza kabla ya kuwapa fedha tunawashauri kufungua akaunti ili fedha hizo zipitie huko kuliko kuwakabidhi fedha taslimu na endapo tunawapa mkononi basi huwa tunawashirikisha wanachama wote pamoja na uongozi wa serikali ya mtaa pamoja na chama ili kila mtu ashuhudie,” alisema Mselewa.
Alisema changamoto hii ni kubwa na endapo wanahitaji vifaa Fulani hawawapi fedha bali wanawapatia vifaa ili kuepusha fedha kutumia vibaya ikiwa ni pamoja na kugawana jambo ambalo liatawarudisha nyuma kimaendeleo.
 “Lengo la kutoa fedha na vifaa kwenye sekta mbalimbali ni kuchochea maendeleo ya wananchi kwa kuunga mkono miradi ambayo wao wameiibua na ni changamoto kwao,” alisema Mselewa.
Alivitaka vikundi vya ujasiriamali kuhakikisha kuwa vinakuwa na akaunti ili fedha zao ziweze kuwa salama kwa ustawi wa kiuchumi na maendeleo ndani ya jamii.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Tumbi Charles Kapama alimshukuru mbunge huyo kwa kutekeleza ahadi zake kwa lengo la kuhamasisha maendeleo kwa wakazi wa Jimbo hilo. Katika awamu ya pili ya utekelezaji wa ahadi za mbunge jumla ya kiasi cha shilingi zaidi ya milioni 10 zimetumika.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WANAWAKE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Kibaha wametakiwa kujitokeza kuwania nafasi za uongozi kwenye ngazi ya vitongoji, vijiji na mitaa mwaka 2014 na si kusubiri viti vya kuteuliwa ili kufikia lengo la 50 kwa 50.
Hayo yalisemwa na mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Kibaha Mjini  Mwanaid Kiongoli alipokuwa akiongea na wajumbe wa baraza la utekelezaji la kata ya Kibaha.
Kiongoli alisema kuwa endapo kuna wanawake wanauwezo ni vema wakaungwa mkono na si kuwawekea ngumu ili waweze kuwania nafasi hizo za uongozi.
“Tusibweteke kwenye nafasi za kuteuliwa lazima nasi tujiamini kwa kuingia kwenye kinyanganyiro kwa wale wenye uwezo wa kuongoza kwani tumeshawezeshwa sasa na sisi tujitegemee kwa kuingia kwenye kinyanganyiro kuanzia 2014 hadi 2015 kwenye uchaguzi mkuu,” alisema Kiongoli.
Aidha alisema kuwa wanawake wasiwakatishe tama wale wanaotaka kuwania nafasi za uongozi kwa kuwaunga mkono na wawe na upende na mshikamano kwani wao ndiyo wapiga kura wakubwa hivyo ni rahisi kuwachagua kuwa viongozi.
 “Huku tukijiingiza kwenye harakati za kuwnaia uongozi pia tukumbuke kuwa na miradi ya maendeleo hasa ile ya ujasiriamali ili kuweza kuziinua familia zetu na kuacha kubweteka na kutochangamkia fursa za kiuchumi,” alisema Kiongoli.
Aliwataka wanawake kuwa na umoja na kuacha kutengana na manunguniko ambayo hayataweza kuwasaidia kujikwamua na hali ngumu ya kimaisha kwani endapo watakuwa na miradi wataweza kuwasomesha watoto wao na kuwapunguzia mzigo akinababa.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
CHIPUKIZI kupitia Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wametakiwa kuchagua viongozi bora na si kuchagua mtoto wa mkubwa fulani.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mwenyekiti wa Chipukizi Taifa Gabriel Amos Makala alipofanya ziara ya siku moja mkoani Pwani na kusema kuwa endapo watachagua watoto wa wakubwa wale wazazi wao ambao ni watu wachini hawataweza kupata fursa hiyo.
Makala alisema kuwa kwa kuwa mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi wa chipukizi kila mtu bila ya kujali kuw ani mtoto wa nani ana haki ya kuwa kiongozi.
“Chagueni kiongozi ambaye atafaa kuongoza na si kuangalia huyu ni mtoto wa Fulani kuwa ndiye anafaa kuongoza hapan hiyo si sahihi kila mtu ana mwenye sifa anauwezo wa kuongoza hata Yule wa mkulima anaweza kuja kuwa kiongozi,” alisema Makala.
Alisema kuwa kinachohitajika ni mshikamano baina ya viongozi na wanachama na kuachana na makundi ambayo si mazuri ndani ya chama kwani yanakigawa chama na kusabnabisha wapinzani kupata nguvu hasa kipindi ch auchaguzi.
Kwa upande wake Omary Moris ambaye ni katibu wa hamasa chipukizi Tiafa na mjumbe wa kiamati kuu ya (CCM NEC) alisema kuwa kazi yake kubwa ni kuifufua chuipukizi ambayo kwa kipindi Fulani iliyumba.
“Chipukizi wakithaminiwa watalisaidia Taifa na wasiwe wanatumikia kipindi cha uchaguzi pekee kwani endapo wataandaliwa kwenye miradi wanaweza kuwa tegemeo kubwa kwa chama na Taifa kwa ujumla,” alisema Moris.
Aliwataka vijana kuwa na mshikamano kwani wao ndiyo tegemeo la nchi na waache kuwa na makundi ambayo hayatasaidia zaidi ya kuleta mifarakano.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WATANZANIA wametakiwa kuacha kulalamika juu ya baadhi ya mambo kutokwenda vizuri badala yake watoe ufumbuzi ya nini kifanyike kuhusiana na masuala mbalimbali ya kimaendeleo.
Hayo yalisemwa na Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa (CCM NEC) kutokea Kibaha Mjini Rugemalila Rutatina, wakati wa hafla ya kuchangia ujenzi wa kituo cha afya cha kanisa la Living Weter Centre kinachojengwa Kilimahewa kata ya maili Moja wilayani Kibaha.
Rutatina alisema kuwa watu wamekuwa mahiri kulalamika kuwa jambo Fulani haliendi vizuri lakini hawatoi njia ya kufanyika ili jambo husika kwenda sawa.
“Tunalishukuru kanisa kwa kutoa jibu la changamoto ya huduma ya afya haya ndiyo watu wanapaswa kutoa majibu ya nini kifanyike na si kulaumu tu na hawa sasa baada ya kuona kuna tatizo la huduma hii wametoa suluhisho,” alisema Rutatina.
Aidha alisema kuwa ni kweli serikali inakabiliwa na chanagamoto nyingi lakini sekta binafsi nayo inatakiwa kushirikiana na wananchi ili kutoa majibu ya kero mbalimbali.
“Tunalipongeza kanisa kwa kuona chanagamoto hiyo katika kata ya Maili Moja ambayo haina kituo cha afya jambo ambalo linawafanya wananchi wa kata hiyo kupata huduma mbali na maeneo yao na nitatoa kiasi cha shilingi milioni 2 kuunga mkoni jitihada hizi,” alisema Rutatina.
Kwa upande wake mchungaji wa kanisa hilo Paschal Mnemwa alisema kuwa alifikia uamuzi wa kujenga kituo cha afya baada ya kuona mama mjamzito akitaabika kwa kubebwa kwenye pikipiki kupelkwa hospitali umbali wa kilomita zaidi ya saba.
“Kitu kingine kilichonifanya nifikirie kujenga kituo cha afya kwa kushirikiana na waumini na wadau wengine ni kifo cha mtoto ambaye alikuwa akifika kanisani hapo kufariki baada ya kuzidiwa na homa na kabla ya kupata matibabu kutokana na umbali alifariki dunia,” alisema Mch Mnemwa.
Mch. Mnemwa alisema kuwa wanahitaji kiasi cha shilingi milioni 335 katika awamu ya kwanza ya ujenzi itakayochukua mwaka mmoja na hadi kitakapokamilika kitatumia zaidi ya shilingi bilioni 1.5 hadi sasa wametumia kisi cha shilingi milioni 40 ikiwa ni sadaka za waumini wa kanisa hilo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka amelipongeza kanisa la Living Water Centre wilayani Kibaha kwa kuanzisha ujenzi wa kituo cha afya ili kukabiliana na chanagamoto ya ukosefu wa huduma za kiafya kwenye kata ya Maili Moja.
Aliyasema hayo mjini Kibaha alipokuwa mgeni rasmi alipomwakilisha Naibu Waziri wa Fedha Janeth Mbene wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa kituo hicho utakaogharimu kiasi cha shilingi milioni 335.
Koka alisema kuwa ni watu wachache ambao wamekuwa na maono kisha kuyafanyia kazi kwa lengo la kuisaidia jamii na kufikiri kuwa kila kitu kitafanywa na serikali.
“Hii ndiyo kazi ya Mungu kuisaidia jamii na serikali kwani kama tujuavyo mipango ya serikali ni mingi hivyo hata utekelezaji wake unachukua muda mrefu hivyo hawa wameonyesha njia ya kuwajibika hivyo lazima tuwaunge mkono kwa kazi nzuri,” alisema Koka.
Alisema kuwa kwa sasa kituo cha afya cha Mkoani kimeelemewa na wagonjwa na hospitali ya Tumbi baada ya kufanywa kuwa ya Rufaa imekuwa haichukui wagonjwa wa moja kwa moja hivyo ujenzi huu utasaidia kukabiliana na changamoto ya matibabu kwa wananchi wa Maili Moja na wilaya ya Kibaha.
“Hili ni jambo letu sote kwani mara kitakapokamilika kitapunguza msongamano kwani kwa sasa kituo cha Mkoani na Tumbi bado zinakabiliwa na changamoto kwani maandalizi ya kuwa kama inavyotakiwa yalikuwa bado hivyo changamoto ni nyingi,” alisema Koka.
Akielezea juu ya ujenzi huo Mchungaji wa kanisa hilo Paschal Mnemwa alisema kuwa maono ya kujenga kituo hicho kwa ushirikiano na wamuni yalikuja baada ya kuona wakazi wa kata ya maili Moja wakienda umbali mrefu kupata huduma za afya.
Alisema kuwa tayari wameshapata eneo na ujenzi umeshaanza ambapo tayari hadi sasa wameshatumia zaidi ya milioni 40 na wanahitaji kiasi cha shilingi milioni 335 kwa ajili ya awamu ya kwanza na hadi kukamilika zitatumika bilioni 1.5.
Koka aliahidi kuchangia kisi cha shilingi milioni 1.5, Profesa samweli Wangwe aliahidi kuchangia kiasi cha shilingi milioni 2, mjumbe wa halmashauri kuu ya CCM Nec Rugemalila Rutatina aliahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni 2 ambapo fedha taslimu ilikuwa milioni 70 na ahadi milioni 20.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
MKAZI wa Mwendapole Charles Beatus 31 Maarufu Ngoye amehukumiwa kwenda jela miaka 10 kwa kupatikana na hatia ya wizi wa Mtandaoni na kuaminiwa kiasi cha Milioni 7,610,000 za Gwelimo Wlfred mkazi wa Kongowe wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Alihukumiwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha HeriethMwailolo, baada ya mtuhumiwa kupatikana na makosa hayo mawili.
Kesi hiyo ambayo ilikuwa chini ya Wakili wa Serikali Salim Msemo ilimkuta na hatia, ambpo kosa la kwanza mahakama ililezwa kuwa mnamo 3.5.2011 ni alihamisha fedha kiasi cha m 3,180,000 Kwenye akaunti ya mlalamikaji Gwelino Wilfred mkazi wa Kongowe.
Ilielezwa kuwa mtuhumiwa alihamisha fedha hizo kutoka kwenye akaunti namba 2121606490 ya NMB kwa njia ya mtandao wa simu ya mkononi 0767122144 (Nmb Mobile) kwenda kwenye Akaunti yake namba 2031614880.
Kosa la iili ni wizi wa kuaminiwa kiasi cha shilingi milioni 4,430,000 hivyo kukutwa na hatia na baada mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa Mahakamani hapo mahakama iliamuru alipe kiasi hicho lakini alishindwa na kulipa shilingi milioni 2,800,000 tu hivyo kushindwa kujinusuru na kuhukumiwa kwenda jela miaka 10.
Mwisho.
   


  

Sunday, April 21, 2013

RIZIWANI KUKABIDHI KOMBE


Na John Gagarini, Kibaha
RIZIWANI Kikwete kesho anatarajiwa kuwakabidhi kombe la ubingwa mabingwa wa mkoa wa Pwani wa daraja la tatu timu ya Kiluvya United.
Kwa mujibu wa ofisa habari wa chama cha soka mkaoni Pwani (COREFA) Victor Masangu alisema kuwa Riziwani ndiye atakayekuwa  mgeni rasmi kwenye sherehe za kuikabidhi kombe timu hiyo kwenye uwanja wa Ruvu Jkt Mlandizi wilayani Kibaha.
Alisema kuwa maandalizi ya sherehe hizo za kuwakabidhi ubingwa United zimekamilika na kinachosubiriwa ni muda ili kuikabidhi ubingwa timu hiyo.
“Ili kunogesha sherehe hizo mabingwa hao wa mkoa wanatarajiwa kucheza siku hiyo na timu ya vijana chini ya miaka 20 ya Ruvu Shooting kwa lengo la kusindikiza sherehe hizo,” alisema Masangu.
Aidha alisema kuwa timu hiyo iliweza kunyakua ubingwa wa mkoa kwa kuifunga timu ya Baga Friends magoli 3-0 mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha.
“Tunawapongeza viongozi, wachezaji, wanachama na wadau wa timu hiyo ya Kiluvya United kwa ushindi walioupata na tunawataka wajipange vizuri kwa ajili ya kuwakilisha mkoa kwenye ligi ya Kanda ambako watakutana na mabingwa wa mikoa mingine,” alisema Masangu.
Aliwataka wadau na mashabiki wa soka mkoa Pwani kujitokeza kuipongeza timu yao kwa kufanikiwa kuwa mabingwa ili kuwapa hamasa ya kujiandaa vema na mashindano ngazi ya Taifa.
Mwisho.

WATOTO WACHANAGA KUPATIWA CHANJO

Na John Gagarini, Kibaha

JUMLA ya watoto 2,628 kati ya watoto 38,356 wenye umri chini ya mwaka mmoja wanatarajiwa kupatiwa chanjo mbalimbali mkoani Pwani.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Simon Malulu mratibu wa maandalizi ya uzinduzi wa chanjo kitaifa yatakayofanyika Aprili 22 hadi 28 shule ya Msingi Mlandizi wilayani Kibaha ambapo mgeni rasmi atakuwa mke wa Raisi Mama Salama Kikwete.

Malulu alisema kuwa hiyo ni awamu ya tatu ya chanjo ambapo watoto hao hawakuipata ilipoanza Januarimwakahuu    

“Jumla ya vituo kimkoa ni 258 na vinavyotoa chanjo ni 206 ambayo ni sawa na asilimia 80," alisema Malulu.

Alitaja chanzo zitakazotolewa kuwa ni homa ya matumbo, homa ya uwati wa mgongo na magonjwa mengine.

“Mkoa umeweza kupiga hatua katika kiwango cha utoaji chanjo zote na kuwa juu ya lengo la taifa la asilimia 90,” alisema Malulu.

Malulu ambaye pia ni ofisa afya wa mkoa alisema kuwa uzinduzi wa Chanjo hiyo inalenga watoto ambao hawakukamilisha ama hawajawahi kupatiwa chanjo mbalimbali.

Akizungumzia kukamilika kwa maandalizi ya shughuli hiyo mkuu wa wilaya
ya Kibaha  Halima Kihemba alisema anategemea wananchi kukusanyika
kwa wingi ili kupata uelewa wa chanjo mbalimbali zinazoweza kukinga
magonjwa kwa watoto.

mwisho.

KIAMA KWA MADEREVA WANYWA VIROBA KIMEFIKA


 Na John Gagarini, Kibaha
HATIMAYE baada ya kilio cha muda mrefu cha abiria juu ya madereva ambao wamekuwa wakiweka pombe za viroba kwenye chupa za maji na kujifanya wanakunywa maji, kimesikika baada ya jeshi la polisi mkoani Pwani kupata vipima ulevi 100.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Nasoro Sisiwaya alisema kuwa vifaa hivyo vitasaidia kukabiliana na madereva walevi ambao wamekuwa wakisababisha ajali kutokana na ulevi.
Sisiwaya alisema kuwa kutokana na kero ya ulevi kuwa kubwa kwa baadhi ya madereva wamekuja na njia hiyo ili kuwadhibiti madereva hao ambao wamekuwa wakinywa pombe huku safari ikiendelea.
“Vifaa hivi vitatusaidia katika kukabiliana na madereva hao ambao ni chanzo kikubwa cha ajali kwani hupoteza umakini wakati wa kuendesha na kusababisha ajali ambazo zingeweza kuepukika,” alisema Sisiwaya.
Aidha alisema kuwa kitengo cha usalama barabarani kinaendelea kukabiliana na changamoto za ajali kwa kuweka askari mbalimbali wakiwemo ambao wanakuwa wamevaa kiraia ili kudhibiti madereva ambao wanakiuka sheria za usalama barabarani.
“Tunamshukuru Mungu kuwa ajali zinaendelea kupungua kutokana na udhibiti kuwa mkubwa ambapo kwa sasa makosa madogo yameongezeka ambayo yanaashiria kupungua kwa ajali katika mkoa,” alisema Sisiwaya.
Aliongeza kuwa kwa sasa wanashirikiana na mamlaka ya kudhibiti usafiri wa majini na nchi kavu (SUMATRA) katika kuwakamata madereva wanaovunja sheria ambapo mafanikio yameanza kuonekana kwani makosa makubwa ya barabarani yamepungua kwa asilimia 26.
Aliwataka wananchi na abiria kutoa taarifa mbalimbali kuhusiana na madereva ambao hawazingatii taratibu za uendeshaji wawapo barabarani na wataendelea kufanya operesheni za mara kwa mara ili kuwabaini madereva wazembe.
Mwisho.
  

Friday, April 19, 2013

MICHEZO PWANI


Na  John Gagarini, Kibaha
BONDIA wa Maili Moja Kibaha mkoani Pwani Nzumba Nkukwe leo Jumamosi anatarajia kupanda ulingoni kupambana na bondia Yusuph Yusuph wa Chalinze wilayani Bagamoyo.
Kwa mujibu wa katibu wa katibu wa chama cha ngumi mkoa wa Pwani Halfan Mrisho “Swagala” alisema kuwa pambano hilo litachezwa kwenye ukumbi wa Ndelema uliopo Chalinze.
Swagala alisema kuwa pambano hilo litakuwa ni la kirafiki kwa kuwapima uwezo wao mabondia hao pamoja na kuhamasisha watu kucheza mchezo huo mkoa Pwani.
“Lengo kuu ni kumwandaa Nkukwe ambaye anatakiwa kucheza mapambano 12 ili aweze kushiriki kwenye mashindano ya ubingwa hapa nchini,” alisema Swagala.
Aidha alisema kuwa pambano hilo lililodhaminiwa na Big Right litakuwa la raundi 12 na linatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kwa mabondia hao wa mkoa huu.
“Nawaomba mashabiki waje kwa wingi ili kuwahamasisha mabondia wa nyumbani na kutakuw ana usafiri kutokea Maili Moja hadi Chalinze hivyo itakuwa ni nafasi kwa wadau wa ngumi kujionea vipaji vya vijana wao,” alisema Swagala.
Alitoa shukrani kwa mdhamini wa mapambano Omary Kimbau kwa jitihada zake za kuhamasisha mchezo huo kwa vijana wa mkoa wa Pwani kwani amekuwa akiwaandalia mapambano mbalimbali mabondia.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MCHEZO wa nusu fainali kati ya Fire na Lisborn ulishindwa kutoa mshindi baada ya mwamuzi wa pambano hilo Hamad Mbegu kutimua mbio kuhofia usalama wake baada ya kumaliza mpira zikiwa zimesalia dakika chache zikiwa hazijatiamia dakika 90 na kuamuru yapigwe matuta timu hizo zikiwa sare ya 1-1.
Mchezo huo wa nusu fainali ya pili kuwania kombe la Kibaha Super Cup ulipigwa kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani Kibaha ulizikutanisha timu hizo ili kupata mshindi ambaye angeungana na Mwanalugali kucheza hatua ya fainali.
Chanzo cha mwamuzi huyo kukimbia ni pale alipoashiria mpira kwisha huku zikiwa bado dakika 5 kutimia dakikia 90 alimaliza pambano na kuashiria matuta lakini washabaiki wa timu ya Lisborn walimfuata na kumzonga huku wakimtishia kumpiga.
Kutokana na mzozo huo mwamuzi aliwaita wachezaji wa Lsborn kwa ajili ya kupiga matuta lakini walionekana kusuasua hali iliyofanya muda mwingi upotee karibu dakika 10 hivi huku washabiki wakiwa wamezingira eneo la goli zilipotakiwa kupigwa penati hali iliyomtia hufo mwamuzi huyo na kukimbia.
Mbali ya hali hiyo pambano hilo lilikuwa na mvutano mkubwa huku timu hizo zikionyesha kandanda safi na walikuwa Lisborn walioandaika bao la kuongoza kupitia kwa Kulwa Mwanda dakika ya 72 na Fundikira Fundikira wa Fire alisawazisha kwenye dakika ya 80 ya mchezo, mchezo huu utarudiwa leo Jumamosi kwenye uwanja huo huo.
Mwisho.

POLISI PWANI YAKUSANYA MAMILIONI


Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani limefanikiwa kukusanya kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 825 kutokana na makosa madogo madogo ya barabarani kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Hayo yalisemwa jana na kamanda wa polisi mkoani humo Ulrich Matei alipoongea na waandishi wa habari mjini Kibaha kuzungumzia mafanikio na changamoto zinazolikabili jeshi hilo.
Matei alisema kuwa katika kipindi hicho jumla ya makosa yliyokamatwa katika kipindi cha Januari mwaka  2011 hadi Machi 2013 ni 31,663 ambapo yaliyolipiwa yalikuwa ni 31,235.
“Katika kipindi hicho ajali zilikuwa 942 za vifo zilikuwa 190 waliokufa walikuwa 224, ajali za majeruhi zilikuwa 510 na waliojeruhiwa walikuwa 1,109 ambapo inaonyesha kupungua kwa asilimia 25 ukilinganisha na mikoa mingine,” alisema Matei.
Kwa upande wake kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Nasoro Sisiwaya alisema kuwa wanaendelea na mikakati mbalimbali ya kuzuia ajali ikiwa ni pamoja na kukamata magari mabovu.
Sisiwaya alisema kuwa wameunda vikosi maalumu viwili kwa ajili ya kukagua magari ambapo kimoja kinafanya ukaguzi kwenye barabara iendayo mikoa ya Kusini na kingine barabara ya Morogoro.
Aidha alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto kubwa kuyaondoa magari yanayoharibika barabarani kwani hawana gari la kuyaondolea na matokeo yake hutumia magari mengine kuyaondoa kwa kutumia mnyororo mgumu.
Mwisho.