Tuesday, April 16, 2013

12,500 KUNUFAIKA MIRADI YA MAJI KIBAHA


Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya watu 12,500 kwenye vijiji vinne kwenye Halmashauri ya wilaya ya  Kibaha mkoani Pwani watanufaika  na mradi wa kitaifa wa maji wa Wami – Chalinze awamu ya pili wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni tatu.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha kuelezea mafanikio ya wilaya kwa kipindi cha miaka saba iliyopita mkuu wa wilaya Halima Kihemba alisema kuwa mradi huo utakamilika wakati wowote mwaka huu.
Kihemba alisema kuwa kwa sasa mradi huo umefikia asilimia 35 ya utekelezaji wake na kuvitaja vijiji hivyo kuwa ni Magindu, Lukenge, Gwata na Gumba.
“Mbali ya vijiji vilivyotajwa hapo juu pia tunatarajia jumla ya vijiji 45 vitanufaika na mradi mwingine ambao utasaidia kukabiliana na changamoto ya maji ambayo ni kubwa kwenye wilaya,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa kwa upande wa miradi hiyo yenye thamani ya zaidi ya shilingi zaidi ya bilioni mbili itategemeana na upatikanaji wa fedha kutoka wadau mbalimbali.
Ameitaja miradi hiyo kuwa ni mradi wa bomba Vikuruti, Boko Mnemela, Dutuni, bwawa la maji Mperamumbi uchimbaji wa kisima kirefu chenye uwezo wa kutoa lita 36,000 za maji kwa saa.
“Miradi hiyo itakuwa katika vijiji vya Lupunga, Mwabwito, Kisabi, Madimla, Disunyala na Makazi Mapya,” alisema Kihemba.
Ameongeza kuwa kwa upande wa Kibaha Mjini mitaa 15 ambayo ni Sofu, Muheza, Vikawe, Bondeni, Vikawe Shuleni, Kidenge, Galagaza, Sagale, Mikongeni, Mwanalugali, Saeni, Jonugha, Zogawale na Viziwaziwa miradi hii itakuwa na thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja.
Alibainisha kuwa changamoto kubwa ni pamoja na kutegemea vyanzo vya maji vya ya juu ya ardhi, mabwawa, mito ambayo hukauka wakati wa ukame na kusababisha shida ya maji hivyo kuweka mikakati ya kuhamasisha jamii kutunza vyanzo vya maji, kuandaa andiko la miradi ya maji ili kupata wafadhili na kutumia visima virefu kwa kuwa ni vyanzo vya uhakika zaidi kulinganisha na mabwawa.
Mwisho.



No comments:

Post a Comment