Sunday, April 21, 2013

KIAMA KWA MADEREVA WANYWA VIROBA KIMEFIKA


 Na John Gagarini, Kibaha
HATIMAYE baada ya kilio cha muda mrefu cha abiria juu ya madereva ambao wamekuwa wakiweka pombe za viroba kwenye chupa za maji na kujifanya wanakunywa maji, kimesikika baada ya jeshi la polisi mkoani Pwani kupata vipima ulevi 100.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Nasoro Sisiwaya alisema kuwa vifaa hivyo vitasaidia kukabiliana na madereva walevi ambao wamekuwa wakisababisha ajali kutokana na ulevi.
Sisiwaya alisema kuwa kutokana na kero ya ulevi kuwa kubwa kwa baadhi ya madereva wamekuja na njia hiyo ili kuwadhibiti madereva hao ambao wamekuwa wakinywa pombe huku safari ikiendelea.
“Vifaa hivi vitatusaidia katika kukabiliana na madereva hao ambao ni chanzo kikubwa cha ajali kwani hupoteza umakini wakati wa kuendesha na kusababisha ajali ambazo zingeweza kuepukika,” alisema Sisiwaya.
Aidha alisema kuwa kitengo cha usalama barabarani kinaendelea kukabiliana na changamoto za ajali kwa kuweka askari mbalimbali wakiwemo ambao wanakuwa wamevaa kiraia ili kudhibiti madereva ambao wanakiuka sheria za usalama barabarani.
“Tunamshukuru Mungu kuwa ajali zinaendelea kupungua kutokana na udhibiti kuwa mkubwa ambapo kwa sasa makosa madogo yameongezeka ambayo yanaashiria kupungua kwa ajali katika mkoa,” alisema Sisiwaya.
Aliongeza kuwa kwa sasa wanashirikiana na mamlaka ya kudhibiti usafiri wa majini na nchi kavu (SUMATRA) katika kuwakamata madereva wanaovunja sheria ambapo mafanikio yameanza kuonekana kwani makosa makubwa ya barabarani yamepungua kwa asilimia 26.
Aliwataka wananchi na abiria kutoa taarifa mbalimbali kuhusiana na madereva ambao hawazingatii taratibu za uendeshaji wawapo barabarani na wataendelea kufanya operesheni za mara kwa mara ili kuwabaini madereva wazembe.
Mwisho.
  

No comments:

Post a Comment