Friday, April 19, 2013

POLISI PWANI YAKUSANYA MAMILIONI


Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani limefanikiwa kukusanya kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 825 kutokana na makosa madogo madogo ya barabarani kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Hayo yalisemwa jana na kamanda wa polisi mkoani humo Ulrich Matei alipoongea na waandishi wa habari mjini Kibaha kuzungumzia mafanikio na changamoto zinazolikabili jeshi hilo.
Matei alisema kuwa katika kipindi hicho jumla ya makosa yliyokamatwa katika kipindi cha Januari mwaka  2011 hadi Machi 2013 ni 31,663 ambapo yaliyolipiwa yalikuwa ni 31,235.
“Katika kipindi hicho ajali zilikuwa 942 za vifo zilikuwa 190 waliokufa walikuwa 224, ajali za majeruhi zilikuwa 510 na waliojeruhiwa walikuwa 1,109 ambapo inaonyesha kupungua kwa asilimia 25 ukilinganisha na mikoa mingine,” alisema Matei.
Kwa upande wake kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Nasoro Sisiwaya alisema kuwa wanaendelea na mikakati mbalimbali ya kuzuia ajali ikiwa ni pamoja na kukamata magari mabovu.
Sisiwaya alisema kuwa wameunda vikosi maalumu viwili kwa ajili ya kukagua magari ambapo kimoja kinafanya ukaguzi kwenye barabara iendayo mikoa ya Kusini na kingine barabara ya Morogoro.
Aidha alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto kubwa kuyaondoa magari yanayoharibika barabarani kwani hawana gari la kuyaondolea na matokeo yake hutumia magari mengine kuyaondoa kwa kutumia mnyororo mgumu.
Mwisho.     

No comments:

Post a Comment