Thursday, July 6, 2023

WIZARA YA MALIASILI NA UTALII YAZIDI KUJIZATITI KUTOA ELIMU YA UHIFADHI KWA JAMII

Wizara ya Maliasili na Utalii inaendelea na jitihada za kuelimisha jamii ikiwa ni pamoja na kutembelea Ofisi za Vyama katika kila Mkoa na kuelezea juu ya umuhimu wa uhifadhi na utunzaji wa rasilimali za Taifa pamoja na fursa zitokanazo na Sekta ya Maliasili na Utalii kwa lengo la kukuza uchumi kwa wananchi. 

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) ameyasema hayo leo katika mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa uliofanyika leo  jijini Mwanza.

"Moja ya maelekezo tuliyoyapata kutoka kwa Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Mohamed Mchengerwa ni wahifadhi kushuka kwenda kila mkoa kuzungumza na chama kuelezea fursa zilizopo katika maeneo yote ya hifadhi tunayoyasimamia na changamoto tunazozipata" Mhe. Masanja amesema.

Amefafanua kuwa lengo la uelimishaji huo ni kuelezea shughuli zinazofanywa na Taasisi za Uhifadhi, kufafanua kuhusu namna ya kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika maeneo ya  pamoja na namna ya kutumia fursa mbalimbali za uwekezaji katika Utalii.

Amesema endapo elimu ya uhifadhi na fursa za utalii ikielezewa kwa ufasaha vijana wataweza kujiajiri wenyewe na hivyo  kuchangia  uchumi wao binafsi na wa Taifa kwa ujumla. 

Amezitaja mojawapo ya  fursa zilizopo kuwa ni pamoja na upandaji miti na uanzishwaji wa mashamba ya miti ambapo Wakala ya Huduma za Misitu Tanzania ( TFS)  imekuwa ikigawa miche hiyo  ya miti kwa watu binafsi.

Amesema kupitia shughuli za upandaji miti wananchi wanaweza kujiongezea kipato na pia kuchangia kwenye uchumi wa Taifa.

WAZIRI KAIRUKI AKABIDHI MAGARI 43 KWA TARURA NA MAKATIBU TAWALA MIUNDOMBINU.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI), Mhe. Angellah Kairuki amekabidhi magari 43 kwa Watendaji wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) katika ngazi ya Makao Makuu, Mikoa na Makatibu Tawala Wasaidizi wanaoshughulika na Miuondombinu katika ngazi za Mikoa.

Makabidhiano hayo yamefanyika Julai 05, 2023 Makao Makuu ya TARURA - Mtumba Dodoma kwa watendaji hao kwa ajili ya kuwawezesha kuboresha utendaji kazi wao.

Waziri Kairuki amesema magari 30 kati ya 43 ni kwa ajili ya matumizi ya Ofisi za Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) makao makuu na mikoa na magari 13 ni kwa ajili ya ofisi za wakuu wa mikoa kwa ajili ya usimamizi wa kazi za miundombinu.

Amesema lengo kuu kukabidhi magari haya kwa TARURA na mikoa ni kuwawezesha kuboresha utendaji kazi, hususan katika utekelezaji wa majukumu ya usimamizi wa ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barabara." 

“Serikali ya Awamu ya Sita katika kuendelea kuhakikisha kuwa inatoa huduma bora kwa wananchi, imeendelea kuwezesha taasisi za umma, hususan Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini, kwa kuwapatia fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari ili kuimarisha utendaji kazi na usimamizi wa miradi”

Aidha, Waziri Kairuki amesema hadi sasa wakala imefanya manunuzi ya magari 270, ambapo magari hayo yamekuwa yakiwasili kwa vipindi tofauti, na kukabidhiwa kwa wahusika na hivyo kufanya magari yaliyokabidhiwa kuwa 241, tangu wakala ulipoanza ununuzi wa magari Julai 2017 hadi Juni 2023.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuwezesha wananchi kuwa kitovu cha maendeleo na kuimarisha ubia baina ya wananchi na Serikali.

“magari haya yatasaidia kurahisisha huduma ya usafiri kwa watendaji wa TARURA na makatibu tawala wasaidizi sehemu ya miundombinu katika kusimamia, kuratibu na kufuatilia shughuli ujenzi  katika mikoa” amesema Waziri Kairuki

Kadhalika, Waziri Kairuki amesema magari hayo yatagawiwa kwenye Ofisi za TARURA na Ofisi za Sekretatieti za Mikoa zenye changamoto na uhitaji zaidi wa magari kwa sasa, na zenye maeneo makubwa ya kusimamia. 

Amesema Sekretarieti za mikoa zitakazopata magari awamu hii ni Mtwara, Ruvuma, Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi, Kigoma, Kagera, Mara, Lindi, Dodoma, Tabora na Tanga. 

Ameagiza magari yatumike kwa kuzingatia miongozo na taratibu za Serikali, ili yalete tija katika kuboresha huduma kwa wananchi ikiwemo kuongeza ushiriki wa wananchi katika shughuli za kijamii na kiuchumi, kutokana na kuwa na miundombinu bora, na sio kutumika katika matumizi binafsi kinyume na taratibu.

𝗪𝗔𝗭𝗜𝗥𝗜 𝗕𝗔𝗦𝗛𝗘 𝗔𝗭𝗜𝗡𝗗𝗨𝗔 𝗠𝗙𝗨𝗠𝗢 𝗪𝗔 𝗨𝗦𝗜𝗠𝗔𝗠𝗜𝗭𝗜 𝗪𝗔 𝗩𝗬𝗔𝗠𝗔 𝗩𝗬𝗔 𝗨𝗦𝗛𝗜𝗥𝗜𝗞𝗔 (𝗠𝗨𝗩𝗨)

Waziri wa Kilimo Mhe.Hussein Bashe, amezindua Mfumo wa kielektroniki wa Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (MUVU) unaowezesha na kurahisisha uhamasishaji, usimamizi na uendeshaji wa Vyama vya Ushirika kidijitali.

Uzinduzi huo ulifanyika hivi karibuni wakati wa kilele cha maadhisho ya siku ya ushirika duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Nanenane Ipuli Mjini Tabora, na kushuhudiwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wananchi pamoja na waandishi wa habari.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe.Bashe alisema mfumo wa MUVU utasaidia kutatua changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili sekta ya Ushirika kwa muda mrefu ikiwemo changamoto ya soko la mazao ya wakulima.

“Kupitia mfumo huu, wakulima hawatadhulumiwa tena mazao yao kwakuwa mkulima atapata taarifa ya kila hatua kupitia simu yake ya kiganjani na kumuwezesha kujua masoko ya mazao yake”, alisema Mhe.Bashe. 

Vilevile, Mhe.Bashe aliipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) kwa kushirikiana kikamilifu na Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC) katika kujenga na kusanifu mfumo huo kuanzia hatua ya awali mpaka kukamilika pamoja na usimamizi wa mfumo huo.

Aidha, alisisitiza mfumo huo kutumika katika mazao yote ikiwemo  zao la pamba na tumbaku na kuitaka e-GA kuhakikisha mfumo huo unawasiliana na  mfumo wa kusajili wakulima wa nchi nzima, sambamba na kuwa na mfumo mmoja ambao utamsajili mkulima na kuonesha miamala yake ya kila siku.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu e-GA, Mkurugenzi wa Huduma za TEHAMA e-GA, Bw. Ricco Boma alisema katika mwaka wa fedha 2023/24 e-GA imejipanga kujenga Mfumo mkuu wa sekta ya kilimo wenye dirisha moja tu kwa Mkulima, msambazaji wa pembejeo na mfanyabishara wa Kilimo yaani ‘Agriculture Single Window’, mifumo mingine itakuwa ni mifumo saidizi yaani ‘backend supporting systems’ itakayokuwa inazungumza na mfumo mkuu wa Kilimo.

‘’Mfumo huu utakuwa umebeba mnyororo mzima wa thamani wa kilimo, hivyo basi ninaomba kutoa wito kwa wadau wa sekta ya kilimo kuunga mkono juhudi hizi  na kutoa ushirikiano ili Mamlaka ya Serikali Mtandao iweze kutekeleza agizo la Mhe Rais na Sheria ya Serikali Mtandao inayoitaka Mamlaka kutengeneza mifumo michache inayowasiliana’’ Alisema Bw.Ricco

Naye Mrajisi wa Vyama vya Ushirika Tanzania Dkt. Benson Ndiege, alisema zoezi la utengenezaji wa mfumo limekamilika na tayari vyama vya ushirika vinaendelea na usajili, na kuanzia sasa vyama vyote vya Ushirika vitahitajika kutoa taarifa zake kupitia mfumo wa MUVU.

WAZIRI MKUU AWATAKA MADAS KUZINGATIA MIIKO NA MAADILI YA UONGOZI WA UMMA.

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Makatibu Tawala wa Wilaya zote Tanzania Bara watekeleze majukumu yao kwa kuzingatia utawala bora, miiko na maadili ya viongozi wa umma.

“Kila mmoja akazingatie utumishi wa umma unaongozwa kwa misingi ya sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali ya Serikali. Misingi hiyo, ndio chachu ya ujenzi wa taswira nzuri ya Serikali ya Awamu ya Sita.”

Ametoa maagizo hayo leo (Jumanne, Julai 04, 2023) wakati akifungua semina elekezi kwa Makatibu Tawala wa Wilaya katika ukumbi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Dodoma.

Pia, Waziri Mkuu amewasisitiza viongozi hao wahakikishe wanadhibiti matumizi mabaya ya fedha za umma katika maeneo yao na wanapobaini kuwepo kwa ubadhirifu wasisite kuchukua hatua.

Waziri Mkuu amesema ili viongozi hao waweze kutekeleza  majukumu yao ipasavyo wanatakiwa waweke mikakati namba ambavyo wilaya zao ya  zitakavyoweza wilaya kubeba na kusimamia vizuri ajenda za kitaifa.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene amesema lengo ya mafunzo hayo ni kuwaongezea weledi viongozi hao ili kuimarisha utawala bora.

Naye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Angela Kairuki amewataka viongozi hao watimize majukumu yao ipasavyo na wahakikishe wanasimamia utekelezaji wa maagizo ya viongozi katika maeneo yao ya kazi.

Awali, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete alitoa wito kwa  viongozi hao wahakikishe mafunzo wanayopatiwa wanakwenda kuyafanyia kazi katika maeneo yao.

Mafunzo hayo ya siku tatu yameandaliwa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kushirikiana na Taasisi ya Ungozi yamehusisha Makatibu Tawala wa Wilaya 135 za Tanzania Bara.

Tuesday, July 4, 2023

WAKAZI WA DODOMA WATAKIWA KUJITOKEZA KWA WINGI MAONYESHO YA MIAKA 60 YA JKT


Wakazi wa Mkoa wa Dodoma na Mikoa ya jirani wametakiwa  kujitokeza kwa wingi katika maonyesho ya Jeshi la kujenga Taifa (JKT) yanayoendelea katika viwanja vya Jengo la SUMA JKT Medeli Mashariki ikiwa ni wiki ya maadhimisho ya miaka 60 tangu kuanzishwa  kwake.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule leo  Julai 4, 2023 wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Jengo la Mkapa Jijini Dodoma. 

Mhe. Senyamule amesema kuwa Maonyesho hayo  yameanza  Julai 1 hadi 9 ndio itakuwa ni kilele chake na yanatarajiwa  kufanyika katika viwanja vya Jamhuri Mkoani Dodoma.

"Niko hapa kutoa rai kwa wakazi wa Dodoma na watanzania wa mikoa ya jirani kutenga muda wao kutembelea maonesho hayo kwa lengo la kujifunza mambo mbalimbali yaliyofanywa na Jeshi letu”, amesisitiza Mhe. Senyamule

Vile vile amesema katika maonyesho hayo kuna teknolojia mbalimbali kuhusu masuala ya kilimo, uvuvi, useremala na kadha wa kadha.

Aidha, Mhe. Senyamule ametoa wito kwa vijana kujitokeza kwa wingi kushiriki maonyesho hayo ili kupata fursa mbalimbali zilizopo katika maonyesho hayo. 

"Ni fursa kubwa sana kwa jamii  hususan vijana kutembelea eneo hilo la maonesho kwa lengo la kujifunza namna ya kujiajiri kwa kutumia fursa zilizopo hapa nchini" amebainisha Mhe. Senyamule 

Hata hivyo,   ameendelea kutoa wito kwa wananchi wote kwa ujumla wa Mkoa huo kujitokeza kwa wingi siku ya kilele ya maadhimisho hayo katika  Viwanja vya Jamhuri na kusisitiza kuwa viwanja vitakuwa wazi kuanzia saa 12 asubuhi.

Monday, July 3, 2023

WAZIRI MKUU MAJALIWA ATAKA UFAFANUZI KWA MAKATIBU WAKUU UNUNUZI WA MARUMARU TOKA NJE


Na. Wellu Mtaki Dodoma.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Kassim Majaliwa amewaagiza makatibu wakuu kukaa ili kuweze kujua sababu za tiles za ndani hazitumiki mpaka wakandarasi wanaosimamia ujenzi wa majengo ya wizara wanaziagiza kutoka nje ya nchi.

Waziri mkuu ametoa agizo hilo leo Julai 3,2023 Jijini Dodoma wakati akikagua mradi wa ujenzi wa majengo ya ofisi za wizara na taasisi katika mji wa serikali Mtumba.

Amesema vipo viwanda vingi vya utengenezaji wa vifaa hivyo nchni maeneo ya Mkulanga, Chalinze na Mbagara hivyo ni lazima wajitahidi kutumia bidhaa za ndani ili kuongeza mzunguko wa fedha, dola wanayo ipeleka nje iweze kubakia.

“Tulitarajia viwanda vya ndani ndivyo vinapata haya malipo, watu wa TBS wamekataa bidhaa zetu? Wakatudhibitishia hizo za Uturuki na Ujerumani kwanza tunapoteza muda mwingi kusubulia bidhaa kutoka nje ya nchi tulitegemea viwanda vya ndani ndo viwe vianapata haya malipo, ”amesema Majaliwa.

Majaliwa amesema kama wanaona bidhaa zinazo zalishwa hazina ubora wawaambie waongeze ubora kuliko kuwaacha wanazalisha lakini hazitumiki na haziuziki ndani ya nchi, maana ya uwekezaji ambao Rais anautaka na unaonekana pamoja na kuwatia matumani wakiwekeza faida itapatikana.

Akitoa tadhmini kuhusu ujenzi wa maradi Waziri Mkuu amesema kazi zinaendelea vizuri, hivyo hawana budi kufuta mbinu sahihi ya kukamilisha ujenzi wa majengo na moja kati ya mbinu rahisi ni kufanya kazi usiku na mchana, pamoja na kuongeza wafanyakazi na kupeana zamu za usimamizi.

“Wakandarasi ndiyo wenye majukumu ya kusimamia kazi kufanyika usiku na mchana, simamieni ujenzi wa majengo ili muhakakikishe unakamilika kwa kiwango bora zaidi kinachohtajika ili magorofa yasije kuporomoka,”amesema.

Naye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Jenista Mhagama amesema mbali na mradi wa ujenzi wa majengo ya wizara pia mradi mwingine unaotekelezwa katika eneo hilo ni ujenzi wa uwanja wa Mashujaa ambao utakuwa na mnara utakaoongoza kwa urefu barani Afrika. Mnara huo utakuwa na urefu wa mita 110.

Awali, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi alisema watahakikisha wanasimamia kikamilifu ujenzi wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati na kwa viwango vinavyostahili. “Ifikapo Septemba 30, 2023 mradi huo utakuwa umekamilika.”

WAZIRI DKT. GWAJIMA ASEMA JUMUIYA ZA WANAWAKE ZINA NAFASI KUTOKOMEZA UKATILI.




WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amefungua Warsha ya Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) ambapo ametoa wito kwa taasisi hiyo kushirikiana na Serikali katika kuwainua wanawake kiuchumi na  kutokomeza ukatili wa kijinsia katika jamii.

Dkt. Gwajima ameyasema hayo, Julai 03, 2023 wakati akifungua warsha ya Umoja wa Wanawake Wakatoliki Duniani (WUCWO) ukumbi wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) Dar es Salaam ambapo wajumbe kutoka nchi mbalimbali za Afrika wameshiriki ufunguzi huo.

"Warsha hii imelenga kukuza usawa wa kijinsia na kutokomeza ukatili na unyanyasaji kwa wanawake na inawapa nafasi kubwa ya kujifunza na kushirikishana mbinu za kukabiliana na changamoto hizo kwa kuwa na sauti ya pamoja.

"Jambo hili ni jema kwani siku zote umoja unaleta matunda chanya na ya haraka zaidi." amesema Dkt. Gwajima.

Dkt. Dorothy Gwajima ameongeza kuwa,  amefarijika kwakuwa WAWATA pia ina lengo la kumfanya mwanamke ajitambue kuwa yeye ni muhimu ndani ya Jamii na maendeleo ya kiroho na kimwili.

Kwa upande wake Rais wa  Umoja wa Wanawake Wakatoliki Afrika, World Union of Catholic Women Organization (WUCWO) na Mwenyekiti wa WAWATA, Eveline Ntenga amesema, kwenye vipaumbele nane vya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa bajeti ya mwaka 2023/24 vipo vipaumbele viwili vinavyoendana na Mradi wa World Women Observatory (WWO) ambavyo ni kuratibu hatua za kukuza usawa wa kijinsia, uwezeshaji wanawake kiuchumi na kiungozi, kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake, Watoto na wazee na kuratibu utoaji wa huduma za msingi kwa watu wenye mahitaji maalum.

Aidha Eveline ameiomba Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii kuweka mkazo juu ya suala la kuwataka wazazi waone umuhimu wa watoto wa kike kupata elimu kwanza badala ya kufikiria kuwaozesha mapema.

Aidha Rais huyo ameiomba Wizara iwasaidie kuendelea kuweka utaratibu sahihi na wa haraka kuanzia ngazi ya Msingi  ili kufikisha taarifa za unyanyasaji na ukatili zinazofanywa na jamii kwa makundi yote katika vyombo husika.

“Tunaomba zichukuliwe hatua kali na kwa haraka kwa wale wote wanaohusika na vitendo vya ukatili kwa makundi yote “ amesema Bi. Aveline. 

Kwa upande wake Katibu Mkuu Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Pd. Dkt. Charles Kitima, amesema katika kufikia maendeleo halisi kama ilivyolengwa kwenye ajenda ya maendeleo ya Dunia (Suistainable Development Goals)  ya mwaka 2030, Kanisa linawaona  wamama kama watendaji wakuu, na wakishikwa mkono na kanisa na Serikali wanaweza wakaifanya Dunia kuwa imara. 

Dkt. Kitima amesema,  jina la Wizara  Wizara ya Maendeleo ya Jamii linasawidi  mambo mengi yanayohusu utu wa mwanadamu ambapo ndipo Mungu Muumba anatukuka, Utukufu wa Mungu uko katika Utu wa mwanadamu, kwani wizara inashughulikia mambo ya Watoto, makundi yaliyotengwa, na akina mama hii ni heshima kubwa kwamba Waziri wa Wizara hii ni mama.