Monday, May 19, 2025

WAANDISHI WA HABARI WATAKIWA WARIPOTI HABARI ZA UCHAGUZI KWA UMAKINI

 VYOMBO vya Habari nchini vimetakiwa kutoa taarifa za vyama vyote vya siasa kwenye kampeni wakati wa uchaguzi wa mwaka huu ili wananchi waweze kujua sera za vyama na kuchagua viongozi bora.

Hayo yalisemwa Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Asasi ya Maendeleo ya Vijana (YPC) Israel Ilunde alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi.

Ilunde alisema kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kutoa elimu ambayo itasaidia kujua sera za vyama vyote bila ya kupendelea baadhi ya vyama.

"Vyombo vya habari vitoe taarifa za vyama vyote kwa usawa bila ya upendeleo hata kwa vyama vidogo navyo vipate nafasi ili vieleze sera zao na wananchi wachague wagombea ambao wataona wanawafaa,"alisema Ilunde.

Alisema kuwa wananchi wakisikia sera za vyama vyote watakuwa na maamuzi mazuri ya kuchagua viongozi ambao wataona wana sera nzuri na watakuwa wamechagua wakiwa na uhakika wa wanao wachagua wana sera nzuri.

"Pia vyama vya siasa nchini vinatakiwa vitoe kauli za kulinda amani iliyopo na kuachana na kauli za chuki na uchochezi ambazo zinaweza kusababisha uvunjifu wa amani.

Aidha alisema kuwa amani ni tunu ya Taifa ambayo inabidi ilindwe ambapo kauli zisizo nzuri husababisha amani kutoweka na wananchi kutoelewana.

"Nayo Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) ihakikishe inakutana na wadau wa siasa mara kwa mara ili kuweka mazingira mazuri ya uchaguzi ambapo itasaidia kuondoa malalamiko wakati wa uchaguzi,"alisema Ilunde.

Aliongeza kuwa wananchi kwa maeneo zoezi la uhakiki wapiga kura linafanyika wajitokeze kuangalia taarifa zao na ikifika muda wa kupiga kura wajitokeze kwa wingi kwa wale wenye sifa.

"Kwa makundi ya vijana wanawake na watu wenye ulemavu wanaotaka kuwania nafasi za uongozi wajitokeze kuwania nafasi hizo kupitia  vyama vyao na vyama vitoe nafasi,"alisema Ilunde.

SERIKALI IDHIBITI FEDHA HARAMU

SERIKALI imeshauriwa kutumia sheria zilizopo kudhibiti utoroshwaji wa fedha haramu kwenda nje ya nchi ambapo husababisha kushindwa kuanzisha miradi mipya ya maendeleo na inayoendelea kukwama.

Hayo yalisemwa Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Asasi isiyokuwa ya kiserikali ya Maendeleo ya Vijana (YPC) Israel Ilunde alipokuwa akizungumza na Mwandishi wa habari hizi.

Ilunde ambaye pia ni Mwentekiti wa Policy Forum alisema kuwa mbali ya miradi kushindwa kufanyika hata ajira kwa vijana hukosekana na hali hiyo huathiri bajeti ya nchi ambapo fedha nyingi hupotea.

"Watu wanaotorosha fedha haramu au utakatishaji wa fedha hufanya udanganyifu kwenye baadhi ya maeneo kwa wafanyabiashara hutumia hati za kibiashara kuweka gharama kubwa, kusafirisha bidhaa kutoka au kwenda nje ya nchi na kudanganya gharama za uendeshaji wa kampuni,"alisema Ilunde.

Alisema kuwa endapo sheria zitawabana watu hao itasaidia kulipa kodi halali kwani kupitia udanganyifu huo hawalipi kodi stahiki hivyo kuitia nchi hasara kubwa.

"Tungeomba sheria ziboreshwe ili kudhibiti watu hao kwa kuwa na mifumo ambayo itadhibiti utoroshwaji wa fedha haramu na watachukuliwa hatua kali za kisheria,"alisema Ilunde.

Aidha aliiomba serikali kuongeza bajeti kwa Wizara ya Habari Sanaa Utamaduni na Michezo ili waandishi waweze kupata mafunzo yatakayoweza kuwafichua watu hao wanaotumia fedha haramu na watu kulipa kodi kwa haki na wasifanye udanganyifu.

"Serikali mashirika yasiyokuwa ya kiserikali taasisi za elimu zitenfeneze vijana kuwa wazalendo watakaochukia udanganyifu ili fedha zinazotokana na kodi zilete maendeleo na itasaidia vijana kuwa na ajira,"alisema Ilunde.

Aliongeza kuwa athari zinazotokana na fedha haramu ni kuathiri sekta muhimu za kimaendeleo kama vile elimu, afya, kilimo na miundombinu na sekta nyingine.

"Vyanzo vinavyosababisha hali hiyo ya utoroshwaji wa fedha haramu ni pamoja na rushwa, hati za kibiashara, usafirishaji wa binadamu, usafirishaji wa madini na utakatishaji wa fedha,"alisema Ilunde. 

Friday, May 16, 2025

WATAKIWA KUWATIA MOYO VIONGOZI

WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilayani Kibaha Mkoani Pwani wametakiwa wasiwakatishe tamaa viongozi wanaotokana na CCM bali wawatie moyo.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Mwajuma Nyamka wakati wa Mkutano Maalum wa Kata ya Maili Moja wa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya miaka mitano.

Nyamka amesema kuwa kuna baadhi ya wanachana wa CCM wamekuwa wakibeza mambo yaliyofanywa na viongozi hali ambayo inawakatisha tamaa.

"Ilani inayotekelezwa ni ya CCM hivyo kuwabeza viongozi wake ni kuonyesha mnakataa yaliyofanyika kwani maendeleo ni suala la mchakato ambao ni wa muda mrefu,"amesema Nyamka.

Amesema kuwa chama kiliingia mkataba wa maendeleo na wananchi na kama kuna changamoto ni vema zikawasilishwa kwenye vikao maalumu kuliko kuwatolea maneno mabaya viongozi.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Maili Moja Ramadhan Lutambi amesema kuwa anawashukuru wajumbe kwa kupitisha ilani ya kata hiyo licha ya tawi la Msufini kuwa na changamoto za miundombinu na afya.

Lutambi amesema kuwa changamoto hizo watazifanyia kazi kwa kushirikiana na wananchi na wataalamu mbalimbali wa Halmashauri ili kukabili changamoto za tawi hilo lililopo kwenye Mtaa wa Muheza

Kwa upande wake katibu wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Method Mselewa amesema kuwa Kata hiyo imeandaa taarifa nzuri ambayo imeonyesha jinsi ilani ilivyotekelezwa.

Mselewa amesema kuwa chama kimefanya kazi kubwa na maendeleo hayawezi kupatikana kwa mara moja ni hatua ambapo kwa vile ambavyo havijakamilika vitafanyiwa kazi.

Naye Mke wa Mbunge huyo Selina Koka amesema kuwa wataendelea kushirikiana na wananchi katika suala la maendeleo ili kuhakikisha wananchi wanakuwa na ustawi.

Koka amesema kuwa kwa upande wa wanawake watahakikisha wanazifikia fursa mbalimbali ikiwemo za mikopo ya wanawake ili waweze kufanya shughuli za ujasiriamali ili wajikwamue kiuchumi.

Tuesday, May 13, 2025

WAFANYABIASHARA SOKO LA LOLIONDO WARIDHIA KUJENGWA UPYA

KUFUATIA mpango wa Halmashauri ya Mji Kibaha kulibomoa na kujenga upya soko la Loliondo liwe a kisasa uongozi wa soko hilo umeridhia lakini umetoa maombi kwa Halmashauri hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mwenyekiti wa soko hilo lililopo Kata ya Tangini Mohamed Mnembwe alisema kuwa wamekubali kubomolewa soko hilo ikiwa ni sehemu ya kuleta maendeleo.

Mnembwe alisema kuwa wametoa maombi yao kwa Halmashauri ya kuongezewa muda wa notisi kutoka miezi mitatu hadi sita, bei ya gharama za kodi kwa mita za mraba zibaki zile zile mara soko litakapokamilika.

"Kuwe na mkataba kati ya Halmashauri na soko juu ya wao kupewa kipaumbele cha kurudi kufanya biashara sokoni hapo bila ya masharti, ukubwa wa fremu ubaki uleule na waongezewe muda wa malipo nafuu hadi mwaka 2042 kwani fremu zitazobomolewa walijenga wao wenyewe kwa gharama zao,"alisema Mnembwe.

Alisema kuwa wanaomba makubaliano waliyoingia juu ya uboreshaji wa soko hilo yasibadilike kwani wao wanachotaka ni maendeleo na kuboresha mazingira ya biashara.

"Tunaunga mkono jitihada za serikali hivyo yale tuliyokubaliana na Halmashauri yawe ni yale yale na kutoa kipaumbele kwa wafanyabiashara waliopo na nafasi zikabaki wapewe wafanyabiashara wapya,"alisema Mnembwe.

Aidha alisema kuwa ujenzi huo utakuwa ni wa miezi 15 ambapo kwa kipindi hicho watahamishia biashara zao kwenye eneo jirani panapotumika kuuza mitumba na watajenga mabanda ya muda.

Soko hilo lina fremu 338 kati ya hizo zinazofanya kazi ni 155, mapaa sita na vibanda 155 ambapo kuna wafanyabiashara zaidi 800 wakiwa wanauza bidhaa za aina tofauti tofauti.

Sunday, May 11, 2025

ALIYE OKOLEWA NA MKUNGU WA NDIZI AJALI YA MV BUKOBA MIAKA 29 ILIYOPITA ASIMULIA MKASA MZIMA

ILIKUWA mwaka 1996 majira ya asubuhi nilisikia wimbo wa Taifa kupitia Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD) wakati huo kwa sasa ni TBC Taifa jambo ambalo si la kawaida kwani unapopigwa wimbo huo basi kuna tukio kubwa la kitaifa ambapo Rais wa Awamu ya Tatu Benjamini Mkapa alitangaza kutokea tukio la ajali ya Mv Bukoba iliyotokea Mkoani Mwanza.

Wakati taarifa hiyo inatangazwa nilikuwa nikielekea shule ambapo nilikuwa nasoma Sekondari ambapo imepita miaka 29 tangu kutokea ajali hiyo mbaya ambayo iliacha simanzi kwa Watanzania na hata baadhi ya raia wa nchi mbalimbali.

Meli hiyo ya Mv Bukoba wakati ikisafiri ilibeba watu wa aina mbalimbali kuanzia wafanyabiashara, wataalamu, watu wa dini, rangi tofauti tofauti na rika tofauti ambao walikuwa wakitokea Bukoba Mkoani Kagera kwenda Mkoani Mwanza kwa shughuli zao za kawaida.

Ni takribani miaka 10 imepita tangu nimfahamu moja ya watu walionusurika kwenye ajali hiyo nikijaribu kumshawishi ili anisimulie mkasa huo bila ya mafanikio kwani alishindwa kutokana na huzuni kubwa aliyokuwanayo kutokana na tukio hilo ambalo hataweza kulisahau maishani mwake.

Baada ya kumshawishi kwa muda mrefu hatimaye alikubali na kunisimulia juu ya mkasa huo ambapo alifahamika kutokana na ajali hiyo kwa kunusurika kwa kupitia Mkungu wa ndizi ambao ndiyo uliookoa maisha yake kwa kuushikilia kwa zaidi ya masaa mawili.

Huyo si mwingine bali ni Happy Leopard ambaye kwa wakati ule alikuwa ni mtoto mdogo mwenye umri wa miaka (17) wakati ajali hiyo inatokea akiwa na dada yake ambaye kwa bahati mbaya alifariki dunia katika ajali hiyo.

Akielezea juu ya kilichotokea wakati wa ajali hiyo alisema kuwa yeye na dada yake Emiliana walikuwa wakiishi Singida ambapo dada yake alikuwa ni mtumishi wa Shirika la Bima Tanzania (NIC) walikwenda Bukoba ambapo ndiyo nyumbani kwao kwa ajili ya mazishi ya mama yao mzazi.

Leopard alisema kuwa baada ya mazishi ilibidi waondoke kwenda Mwanza kwa ajili ya kupeleka msiba Moshi ambako ni nyumbani kwa mama yao alikozaliwa.

"Nilipanda kwenye meli majira ya saa 1 jioni ambapo saa 3 safari ndipo ilipoanza nilipanda lakini sikuwa na furaha tulikata tiketi ya meli ya Mv Victoria lakini meli hiyo ilikuwa kwenye matengenezo na tukapanda meli ya Mv Bukoba,"alisema Leopard.

Alisema kuwa yeye na dada yake walikata siti za VIP na abiria walikuwa wengi ambapo baadhi ya abiria walikosa nafasi na kupanda magari kwenda kupanda kituo cha mbele cha Kemondo na kupanda na wengine waliachwa ambapo ndi ilikuwa nusura yao.

"Mimi na dada tulikuwa ndani lakini nilishindwa kulala kila wakati alikuwa akija na kuniangalia akashangaa kwanini silali ambapo dada alilala lakini sikulala ikabidi nitoke nje ambapo pembeni kulikuwa na kwaya ilikuwa ikiimba pia alikuja kuniangalia na kunipa khanga ili nijifunike kwani kulikuwa na baridi,"alisema Leopard.

Alisema kuwa ilipofika majira ya saa 10 alfajiri walipokuwa wakikaribia kufika Mwanza walipofika eneo linaloitwa Kisiwa cha Juma yalitokea mawimbi makubwa na sehemu hiyo ni muingiliano wa maji na kuna mawimbi makali ambapo inasemekana huwa ajali za meli hutokea mara kwa mara ambapo manahodha wazoefu huwa hawapiti hapo na kukwepa eneo hilo.

"Baada ya muda meli ilianza kuyumba na vyombo jikoni vilianza kuanguka askari walikuwa wakisafirisha fedha walianza kuwaambia abiria kaeni upande huu mmeelemea sehemu moja nendeni huku wakati huo tulianza kuona taa za Bugando kwa mbali kidogo meli ilianza kuyumba sasa watu wakawa wanakimbia hawajui la kufanya,"alisema Leopard.

"Tulianguka kama vile mtu anamwaga kitu dada alibaki kule kwenye chumba, nikifanikiwa kushika boya lakini kuna mtu alininyanganya nikazama chini nilipoibuka nikakutana na Mkungu wa ndizi ambao niliungangania hivyo nikawa naelea licha ya mawimbi ya maji kutupiga na niliona watu wengine hao wakiwa na maboya huku wakiomba msaada,"alisema Leopard.

Alisema kuwa kwa mbali aliona baadhi ya watu wakiwa kwenye ubavu wa meli wakiwa wamejishikilia huku kwenye maji kukiwa na maiti nyingi zikiwa zinapelekwa na maji na vitu mbalimbali ikiwa ni pamoja na maburungutu ya fedha na vifaa mbalimbali.

"Tukiwa ndani ya maji nilikuwa nauomba Mungu atusaidie ili tuweze kupona na niliamini dada yangu ni moja ya watu waliokuwa kwenye ubavu wa meli naye atapona lakini kumbe haikuwa hivyo kumbe yeye alibaki kule chumbani na hakuweza kutoka na alikuja kupatikana baada ya kuvunjwa vile vyumba tena siku chache kabla zoezi la kutafuta maiti kusitishwa,"alisema Leopard.

"Ilikuja boti ya wavuvi wakauliza mna hela ili tuwaokoe kama hamna hela basi wakaanza kuchukua fedha na vitu mbalimbali vya abiria wakaweka kwenye boti yao wakaondoka lakini jambo la kushukuru wakatokea wavuvi wengine wakiwa na mtumbwi wakatuokoa na kisha kutupeleka kwenye meli nyingine ambayo ilitokea Uganda wakatuchukua baadhi ya watu walikufa baada ya kuchoka kushikilia maboya kwani walikaa majini muda mrefu sana,"alisema Leopard.

Alisema kuwa meli hiyo ilivuja mafuta ambayo yaliingia kwenye maji na kutupiga hivyo yalituumiza machoni, puani na masikioni na tulipokuwa kwenye ile boti tuliookolewa watu watano, maji yalikuwa yanaingia ikabidi awe anayachota na kuyamwaga nje huku wale wenzake wakiwa wamelala hoi yeye akiwa kidogo ana nguvu.

Alisema kuwa anamshukuru Mungu na siku hiyo alivaa rozari ambayo alipewa na babu yake ambaye alikuwa padri na anaamini Mungu ndiye aliyemwokoa katika ajali hiyo mbaya ya majini kutokea nchini.

"Tangu tunatoka Singida kwenda Bukoba moyo wangu haukutaka kabisa kusafiri nilimkatalia dada hiyo safari hadi majirani zetu walinishawishi kusafiri ambapo aliogopa kupanda meli na majirani waliniambia kuwa kwani umeshawahi kusikia ajali ya meli walinibembeleza ikabidi niende,"alisema Leopard.

"Cha ajabu ile sehemu niliyookolewa alitokea nyoka mkubwa mweusi watu wakanionyesha baada ya kuokolewa wakasema huyo ndiye alikuwa mzimu wake ambapo kama angemuona angemuokoa niliwaambia nikiwa majini niliogopa zaidi mtu na siyo kitu kingine kwani yule aliyeninganganya boya alinifanya nione adui ni binadamu na siyo mnyama au kitu kingine,"alisema Leopard.

Alisema kuwa miaka zaidi ya 10 bila ya kupanda meli baada ya tukio hilo licha ya siku alipopatikana dada yake ilibidi apande kwenda kuzika na walimbembeleza sana apande alikubali lakini aliogopa sana meli akikumbuka tukio hilo na fedha zote za pole alizopewa alizipeleka kanisani kama sadaka kwani hakuona thamani ya kitu chochote kwa wakati huo na ndoto zake zote zikitoweka.

"Dada alikuwa na mipango ya kwenda Uingereza ambapo aliniahidi tungeenda naye na aliahidi angenisomesha kwani mimi nilikuwa mtoto wa mwisho na dada yangu alikuwa akinipenda tulipendana sana nilitamani angepona ili tuje tusimulie kuwa sisi ni mashujaa lakini haikuwa hivyo tukio hilo limeniumiza sana sitaweza kulisahau maishani mwangu,"alisema Leopard.




Thursday, May 8, 2025

WANACHAMA WA CCM NYANG'WALE WATAKA KUHARAKISHWA UJENZI WA OFISI.

WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Nyang'hwale Mkoani Geita wametaka  ujenzi wa ofisi ya chama ufanyike kwani tayari baadhi ya wadau wamechangia fedha za ujenzi huo.

Wamesema moja ya wadau waliochangia fedha kwa ajili ya ujenzi huo ni Naibu Waziri Mkuu Dotto Biteko ambaye alichangia kiasi cha shilingi milioni 50.

Wamesema kuwa fedha hizo zilikabidhiwa kwa Mbunge wa Jimbo la Nyang'hwale Hussein Amar hivyo kutaka fedha hizo zifanye ujenzi huo ili kupata ofisi kwa kazi za chama.

"Tunataka ujenzi ufanyike kwani kama ni fedha zipo hakuna sababu ya kuchelewesha ujenzi huo wa ofisi ya chama ambapo endapo itajengwa itakuwa ya kisasa,"wamesema wanachama hao.

Waliongeza kuwa wanataka fedha hizo zijenge na kukamilisha ofisi ya chama na kwamba wao wanachotaka ni kuona CCM Wilaya ya Nyang'hwale inaendelea kama Wilaya nyingine zilivyoendelea.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Nyang'hwale Hussein Amar akizungumza kwa njia ya simu ameeleza kusitikishwa na malalamiko ya wananchama hao huku akisema jambo hilo halina usiri wowote.

Amar amesema kuwa yeye ndiye iliyemuomba  awasaidie na sio mara moja amekuwa akisaidia na bahati nzuri alipokuja yeye mwenyewe  alimkumbushia ombi hilo na akakubali kusaidia lakini hakutamka kiwango.

Aidha amesema kuwa fedha hizo zilivyoingia alimpa taarifa Mkuu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Chama, Mwenezi, kamati ya Siasa na kamati ya ujenzi na yeye ndiye aliyetafuta fundi na kuwashauri kuwa kuna fundi kwa hiyo ni vyema akatumika kwakuwa yupo vizuri.

Mbunge huyo ameongeza kuwa yeye binafsi amekuwa na mchango mkubwa sana katika ujenzi wa ofisi hiyo ya Chama maana alishawai kutoa mashine zake na magari yake (Tipa) kufanyakazi katika ujenzi huo.

"Fedha zipo mikono salama na Mei 3 niliongea na Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi kumweleza juu ya fedha kwani zinatakiwa kufanyakazi iliyokusudiwa kwa kuwa mimi sitaki kukaa nazo nipeni akaunti niwahamishie lakini alinijibu kuwa watakaa na kamati yake ya ujenzi na akasema wakati huu aendelee kukaa nazo na wakihitaji kununua vifaa watamjulisha ili atoe hizo fedha",amesema Amar.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Nyang'hwale Adam Mtore amesema kuwa kama kuna malalamiko ndani ya Chama kuuna utaratibu wake na mara nyingi huanzia ngazi ya chini ya tawi lakini kwakuwa suala hilo linagusa ngazi ya Wilaya ilitakiwa wapeleke malalamiko yao kwa Katibu wa Chama Wilaya.



Saturday, May 3, 2025

KECA YAUNGA MKONO SERIKALI UHIFADHI MAZINGIRA NA UFUGAJI NYUKI

SHIRIKA lisilo la kiserikali la Kibaha Environmental Conservation Action (KECA) limedhamiria kuunga mkono jitihada za serikali kwa uhifadhi wa mazingira na kukuza uchumi kupitia ufugaji wa nyuki.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mkurugenzi wa (KECA) ambalo linajihusisha na utoaji elimu ya ufugaji nyuki na utunzaji wa mazingira Ibrahim Mkwiru wakati wa uzinduzi wa jengo la ofisi yao.

Mkwiru alisema kuwa nia yao ni kuunga mkono juhudi za Serikali katika uhifadhi wa mazingira na kukuza uchumi wa wananchi kupitia ufugaji wa nyuki ili kuongeza kipato kwa wananchi.

"Tunaiomba Serikali kutupa kibali cha kupanda miti ya mianzi katika maeneo ya wazi karibu na chanzo cha Mto Ruvu ili kusaidia kuhifadhi mazingira na kuchochea maendeleo ya kijamii kupitia njia ya uhifadhi wa mazingira,"alisema Mkwiru.

Kwa upande wake Ofisa Tarafa ya Kibaha Catherine Njau alisema kuwa Serikali inaendelea na dhamira yake ya dhati ya kuunga mkono juhudi za wawekezaji katika sekta ya ufugaji nyuki ili kuhakikisha wafugaji wadogo waliopo vijijini wananufaika kiuchumi na kielimu. 

Njau alosema kuwa kwa muda mrefu wafugaji wa nyuki wanaoishi pembezoni mwa miji wamekuwa wakikosa elimu sahihi ya ufugaji wa kisasa na pia kukosa masoko ya uhakika kwa bidhaa zao.

Alilipongeza shirika la KECA kuwa kama daraja muhimu kwa wafugaji wa nyuki kupata elimu ya kitaalamu na fursa za kibiashara kwa wafugaji ili waweze kupata masoko makubwa.

"Nawasisitiza umuhimu wa kufanya tathmini ya kitaalamu kabla ya kupanda mianzi kwenye maeneo ya vyanzo vya maji,huku akisema baadhi ya miti ina uwezo wa kutumia maji mengi na hivyo inaweza kuhatarisha uhai wa vyanzo vya maji kama mito,"alisema Njau.

Naye Mjumbe wa Bodi ya KECA Edwin Shunda aliwahimiza wananchi na wadau wa mazingira kujitokeza kwa wingi kujifunza mbinu za ujasiriamali na ufugaji wa nyuki wa kisasa.

Thursday, May 1, 2025

MKUU WA MKOA WA PWANI ABUBAKARI KUNENGE ATOA WIKI MOJA KWA WAAJIRI WANAOKIUKA HAKI ZA WAFANYAKAZI

MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametaka utatuzi wa changamoto za wafanyakazi kufanyiwa kazi atoa wiki moja kwa taasisi zinazokiuka taratibu kufuata sheria za kazi.

Kunenge ameyasema hayo jana Mjini Kibaha wakati wa maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Duniani Mkoa wa Pwani yaliyofanyika kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha.

Amesema kuwa waajiri wanapaswa kutekeleza matakwa ya kisheria ya juu ya haki za wafanyakazi ili waweze kufanya kazi vizuri bila ya malalamiko.

"Katika risala yenu kuna baadhi ya waajiri wanakiuka taratibu ikiwa ni pamoja na kutotoa mikataba ya kazi na stahiki nyingine jambo ambalo ni kinyume cha sheria,"amesema Kunenge.

Awali mratibu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Mkoa wa Pwani Susan Shesha amesema kuwa wanaishukuru serikali kuvutia wawekezaji ambapo imewezesha vijana wengi kupata ajira.

Shesha amesema kuwa changamoto iliyopo ni baadhi ya waajiri kutotoa mikataba ya ajira, fedha za matibabu, kutothibitishwa kazini, mapunjo ya mishahara, kuzuia uwepo wa vyama vya wafanyakazi sehemu za kazi, likizo na fedha za matibabu, vitisho.