Friday, February 28, 2025

CCM KATA YA MKUZA YAKAGUA MIRADI YA MAENDELEO YENYE THAMANI YA SHILINGI BILIONI 9.4

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Kata ya  ya Mkuza Wilayani Kibaha kimefanya ukaguzi wa miradi ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 9.4 na kurudhishwa na kiwango cha utekelezaji wa miradi hiyo.

Akizungumza baada ya kukamilisha ziara ya Halmashauri ya Kuu ya Kata kutembelea miradi hiyo Mwenyekiti wa CCM Kata ya Mkuza Matata Ngolo amesema kuwa huo ni utekelezaji wa ilani ya CCM.

Ngolo amesema kuwa kabla ya kikao waliona ni vema wakatembelea miradi hiyo ya maendeleo ili kujionea uhalisia wa utekelezaji wa ilani ya CCM kwa kipindi cha miaka mitano.

Kwa upande wake diwani wa Kata ya Mkuza Fokas Bundala amesema  kuwa moja ya mafanikio makubwa ni ujenzi wa shule za sekondari mbili ambapo kiutaratibu kila kata inapaswa kujenga sekondari moja.

Bundala amesema kuwa changamoto kubwa iliyopo ni madawati na viti na meza lakini kwenye bajeti inayokuja fedha zimetengwa hivyo itapunguza changamoto hiyo.

Amesema kuwa katika kipindi hicho serikali kupitia mapato yake ya asilimia 10 ilitoa kiasi cha shilingi milioni 660 kwa ajili ya mikopo ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kwa vikundi.

MWENGE WA UHURU KITAIFA KUWASHWA PWANI APRILI 2,2025

WANANCHI wa Mkoa wa Pwani wametakiwa kutumia fursa za kiuchumi kwa kuwashwa mwenge wa uhuru mkoani humo Aprili 2 mwaka huu.

Hayo yamesemwa jana Mjini Kibaha na Mkuu wa Mkoa huo Abubakar Kunenge alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Amesema kuwa kuwashwa mwenge wa uhuru Mkoani Pwani ni fursa kiuchumi kwa wananchi pia ni chachu ya maendeleo kwani wananchi watafanya biashara za chakula, malazi, usafiri, vinywaji na utalii.

"Wananchi tumieni fursa hiyo ya uzinduzi wa mbio hizo za mwenge wa uhuru kwa kufanyabiashara ambapo kutakuwa na wageni wengi na hata wenyeji ambao watahitaji huduma mbalimbali,"amesema Kunenge.

Amesema kuwa sherehe hizo za uzinduzi zitapambwa na matukio mengi yakiwemo ya halaiki na burudani nyingine za wasanii.

"Baada ya uzinduzi huo mwenge wa uhuru utakimbizwa katika Halmashauri tisa za mkoa huo ambapo utakagua, kutembelea na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo,"amesema Kunenge.

Aidha amewahamasisha na kuwaomba wananchi wote wa Mkoa wa Pwani na maeneo jirani kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uzinduzi huo.

"Maandalizi yanaendelea vizuri ambapo muda bado unatosha na mwaka huu tumejipanga vyema kuhakikisha tunafanya vizuri,"amesema Kunenge.

mwisho. 


Monday, February 24, 2025

SHULE ZA AWALI NA MSINGI BINAFSI 101 ZANUFAIKA NA MRADI WA OPPORTUNITY INTERNATIONAL-MOSHA

Ofisa Elimu Taaluma wa Mkoa wa Dar es Salaam, Eva Mosha, ametoa rai kwa wamiliki na walimu wa shule binafsi za awali na msingi kuimarisha ufanisi wa ufundishaji na kuboresha ubora wa elimu, ili kuinua taaluma katika shule zao.

Amesisitiza ,shule hizo zinapaswa kuongeza ubunifu na kujiendeleza kwa kupata mafunzo mbalimbali ya namna ya kuendesha shule zao, ili kuepuka changamoto za kushindwa kuendeleza shule au kukosa wanafunzi.

Mosha alitoa rai hiyo katika hafla ya kupongeza walimu na wamiliki wa shule binafsi za awali na msingi, ambazo zinatoa ada nafuu, waliopatiwa mafunzo ndani ya miaka mitatu kupitia mradi wa Opportunity International ,kwenye ukumbi wa Victoria uliopo Kimara Temboni, Dar es Salaam. 

Mratibu wa Mradi wa Opportunity International Tanzania (HES Tanzania), Oliver Kapaya, alieleza kuwa mradi huo ulianza mwaka 2018 na umefanikiwa kuhusisha shule 101 katika kipindi cha miaka mitatu.

Alieleza, shule 74 zilipata mafunzo na kufuzu kwa kipindi cha miaka minne na shule 15 zimefanikiwa kupata tuzo za kutambua ufanisi wao huku, shule nane zimetunukiwa tuzo kwa utendaji bora.

Violet Oketch, mratibu wa Mradi wa Opportunity International Afrika (HES Africa), alieleza mradi huu unatekelezwa katika nchi nane za Afrika, ikiwa ni pamoja na Tanzania, Rwanda, Zambia, Ghana, DRC Congo, Uganda, Kenya, na Nigeria.

Violet Oketch alishukuru serikali ya awamu ya sita kwa ushirikiano wake na wawekezaji na wafadhili mbalimbali katika sekta ya elimu. 

Brayson Ephata Maleko, Ofisa Elimu Vifaa na Takwimu Temeke, alisema mradi huo umehusisha shule za awali na msingi, namna ya kuendesha shule kwa ufanisi, kupanga mipango, na kusimamia rasilimali fedha.

PWANI YAZINDUA KAMPENI YA MSAADA WA KISHERIA WA MAMA SAMIA

MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amewataka watumishi ambao ni wanasheria kwenye Mkoa huo kuwahudumia wananchi kwenye kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia.

Kunenge ameyasema hayo Mjini Kibaha wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo ya siku tisa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia Mkoani Pwani.

Amesema kuwa kampeni hiyo ni nzuri na itawasaidia wananchi wanyonge ambao hawana uwezo wa kulipia gharama za kisheria na kumshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kubuni kampeni hiyo.

Kwa upande wa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Jumanne Sagini amesema kuwa kampeni hiyo ni kuwezesha wanyonge wanapata haki zao kwa wakati.

Naye Naibu Waziri wa maendeleo ya jamii jinsia wanawake na makundi maalum Mwanaid Khamis amesema kuwa kumekuwa na changamoto ya ukatili wa kijinsia, matunzo ya watoto, ardhi na ubakaji.

Mwakilishi wa bodi ya ushauri wa msaada wa kisheria Nuru Awadh amesema kuwa siku tisa ni chache kwani changamoto ya masuala ya kisheria ni kubwa sana hivyo ili kuwafikia wananchi wengi hivyo huduma ziendelee kutolewa.

Mkurugenzi wa mashirika yanayotoa msaada wa kisheria (TANLAP) Christina Ruhinda amesema kuwa kila kata ina wasaidizi wa kisheria nchi nzima ambao wanasaidia kutoa elimu na msaada wa kisheria.


Saturday, February 15, 2025

WAANDISHI WA HABARI WAJENGEWA UWEZO JUU YA MALEZI MAKUZI MAENDELEO YA WATOTO

WAANDISHI wa Habari nchini wametakiwa kuleta mabadiliko chanya kwenye masuala ya malezi na makuzi ya watoto ili kuja kupata viongozi bora wa baadaye.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Osifa Programu kutoka Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) Victor Maleko ambaye alikuwa mwezeshaji wa mafunzo kuhusu uandishi wa habari zinazohusu Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (MMMAM).

Maleko alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwa ukuaji wa watoto ambao wanatakiwa kupata huduma muhimu katika ukuaji wao ili wawe na makuzi mazuri.

WAANDISHI WATAKIWA KUANDIKA HABARI SAHIHI ZA UCHAGUZI

NAIBU Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Hamis Mwinjuma amevitaka vyombo vya habari kuandika habari sahihi kipindi cha uchaguzi ili kudumisha amani.

Ameyasema hayo Mjini Dodoma alipokuwa akifunga Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Nchini.

Mwinjuma amesema kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kutoa taarifa sahihi ambazo zitawafanya wananchi kuchagua viongozi bora ambao watailetea nchi maendeleo.

"Kazi yenu kubwa ni kutoa taarifa sahihi kwa wananchi ambao wanaviamini vyombo vya habari kupata taarifa za ukweli na siyo za kupotosha ili kupata viongozi bora,"amesema Mwinjuma.

Kwa upande wake Mhandisi Endrew Kisaka ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) amesema kuwa vyombo vya habari vinapaswa kuandika habari za vyama vya siasa wakati wa uchaguzi bila ya upendeleo.

Kisaka amesema kuwa waandishi wazingatie kuandika sera na siyo majibizano au udini, ukabila na kutoingilia faragha za watu na kotoegemea upande wowote bali watoe nafasi kwa watu wote.

Naye katibu wa Mtandao wa Bloggers Tanzania (TBN) Khadija Kalili ameishukuru  TCRA na kuiomba kupunguza gharama za usajili ambapo kwa sasa ni shilingi 500,000 ambayo ni kubwa hivyo wengi kushindwa kulipia.

Kalili alisema kuwa TBN ilisajiliwa mwaka 2015 na ilianza na wanachama 100 hadi kufikia 300 ambapo baadhi walijitoa kutokana na kushindwa kusajili.

Mkutano huo wa mwaka ambao uliansaliwa na TCRA ulihusisha washiriki 528 ambao wanajihusisha na masuala ya utangazaji na watoaji maudhui mtandaoni nchini, waandishi wakongwe wa Redio Tanzania.

WAZIRI KABUDI ATAKA WATANGAZAJI KUACHA MBWEMBWE WATUMIE KISWAHILI SANIFU

WAZIRI wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Profesa Kabudi amewataka watangazaji kuacha mbwembwe na kubananga Kiswahili na kutumia Kiswahili Sanifu ili Tanzania iendelee kuwa nchi inayotumia Kiswahili fasaha.

Profesa Kabudi ameyasema hayo Mjini Dodoma wakati akifungua mkutano wa mwaka wa vyombo vya utangazaji nchini.

Amesema kuwa Tanzania ni nchi kinara wa lugha ya Kiswahili lakini endapo hakutakuwa na juhudi za makusudi za kukisimamia Kiswahili hatutakuwa vinara tena wa lugha hiyo.

"Watangazaji wanapaswa kutumia Kiswahili fasaha na sanifu kwani tuna utajiri wa misamiati hivyo tukitumie vizuri ili kuandaa vipindi vyenye tija kwa wasikilizaji,"amesema Kabudi.

Naye Mkurugenzi wa Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Dk Jabiri Bakari amesema kuwa wamekuwa wakifanya utafiti juu ya maudhui ya mtandaoni ili kutoa taarifa sahihi na za umahiri.

Bakari amesema kuwa kuna utafiti umefanywa ambapo utakamilika mwezi huu lengo kuu likiwa ni kuboresha utoaji wa maudhui mitandaoni.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui Saida Muki amesema kuwa watangazaji wa maudhui mitandaoni wanapaswa kuweka maslahi ya nchi mbele  na kujiepusha na maudhui yanayokiuka maadili.

 

Tuesday, February 11, 2025

WAANDIKISHAJI WASAIDIZI DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA HALMASHAURI YA MJI KIBAHA WAASWA





WAANDIKISHAJI wasaidizi wa zoezi la uboreshaji daftari la kudumu la wapiga kura Halmashauri ya Mji Kibaha wametakiwa kuwa waadilifu na waaminifu wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili kwa waandikishaji wasaidizi kwenye Halmashauri hiyo.

Shemwelekwa amesema kuwa waandikishaji hao wasaidizi wamepewa jukumu kubwa na wameaminiwa kwani zoezi hilo ni la Kitaifa hivyo wahakikishe wanalifanya kwa weledi ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza.

Amesema mafunzo hayo yawe chachu ya utendaji kazi wao kwenye zoezi la uboreshaji taarifa za wapiga kura na kuandikisha wapiga kura wapya litakuwa la siku saba kuanzia Februari 13 hadi 19.

Amewataka watumie lugha nzuri wakati wakiwahudumia wananchi ili iwe sehemu ya kuwavutia watu wengi wajitokeze kuboresha taarifa zao na kuandikisha wapiga kura wapya.

Jumla ya waandikishaji 262 wamepatiwa mafunzo hayo na kuna vituo 131 vitatumika kwenye zoezi hilo ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwaka huu.


Sunday, February 9, 2025

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA TAMISEMI YARIDHISHWA MIRADI YA ELIMU NA AFYA HALMASHAURI YA MJI KIBAHA





KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imekagua miradi ya ikiwemo ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Kibaha iliyogharimu kiasi cha shilingi bilioni 4.1.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji Kibaha Catherine Saguti kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashari wakati akitoa taarifa juu ya ujenzi wa hospitali hiyo.

Dk Saguti amesema kuwa mapokezi ya fedha za mradi wa Ujenzi wa Hospitali na ununuzi wa vifaa tiba kutoka Serikali Kuu yalitolewa kwa awamu nne 
jumla ya shilingi bilioni 3.3 kwa ajli ya ujenzi na shilingi milioni 400  kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. 

"Fedha hizo zimepokelewa kwa awamu kuanzia mwaka wa fedha 2019/2020, 2020/2021, 2021/2022 na 2024/25 na jumla ya majengo ambayo yamejengwa hadi sasa ni 14 na majengo 11 yamekamilika na yanatumika huku majengo matatu yanaendelea na utekelezaji katika hatua ya
ukamilishaji,"amesema Saguti.

Amesema kuwa Halmashauri imechangia jumla ya shilingi milioni 446.7 kwa ajili ya ukamilishaji wa
miundombinu na majengo ambayo hayakukamilika kwa fedha za Serikali Kuu.

Pia kamati hiyo imetembelea ujenzi wa kituo cha afya cha Kata ya Pangani kilichogharimu kiasi cha shilingi milioni 914 huku Halmashauri ya Mji Kibaha ikichangia kiasi cha shilingi milioni 189 kutokana na mapato ya ndani.

Wabunge hao wa Kamati ya Tamisemi walitembelea mradi wa shule mpya ya sekondari ya Kata ya Tangini iliyogharimu kiasi cha shilingi milioni 528.9.

Ujenzi huo umetokana na mradi wa Uboreshaji wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP) ina uwezo wa kuchukua wanafunzi 398 wa kidato cha kwanza na cha pili wanawake 191 na wanaume 207.

Katika hatua nyingine kamati hiyo ya kudumu ya Bunge ya Tamisemi pia ilitembelea ujenzi wa Shule ya Msingi Mtakuja Kata ya Pangani ambayo ina mfumo wa Kiingereza ambayo imegharimu kiasi cha shilingi milioni 309.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Zainab Katimba amesema kuwa serikali ya awamu ya sita imewekeza fedha nyingi kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya afya na elimu.

Katimba amesema kuwa Serikali imewekeza kwenye miradi mingi ili kuwaletea wananchi huduma karibu na maendeleo ili kupunguza changamoto.

Amesema kuwa maagizo na maelekezo yaliyotolewa na kamati ili kuboresha miradi hiyo wataifanyia kazi ili iwe na ubora na kuwa na manufaa kwa wananchi.  

Akitoa majumuisho ya ziara ya Kamati Mwenyekiti wa kamati hiyo Justin Kamoga amesema wameridhishwa na ujenzi wa miradi hiyo kwani imejengwa kwa viwango vizuri.

Kamoga amesema licha ya miradi hiyo kujengwa vizuri lakini kuna baadhi ya changamoto ndogo ndogo ikiwa ni pamoja na kukamilisha baadhi ya maeneo yaliyobakia.

Friday, February 7, 2025

KITUO CHA AFYA VIGWAZA MBIONI KUKAMILIKA

KITUO cha afya cha Kata ya Vigwaza Halmashauri ya Chalinze Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani kiko kwenye hatua za mwisho kukamilika ambapo kitatoa huduma mbalimbali zikiwemo za upasuaji hivyo kuwaondolea kero za akinamama za kujifungua.

Aidha serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 525 kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya kwenye Kata hiyo hivyo kuondoa changamoto hasa za mama wajawazito wakati wa kujifungua.
 
Diwani wa Kata ya Vigwaza Mussa Gama akizungumza Vigwaza wakati wa maadhimisho ya miaka 48 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amesema kwa sasa wananchi hususani wanawake waliokuwa wanashindwa kujifungulia kwenye Zahanati ya Vigwaza ambapo hawatapelekwa tena Mlandizi na Chalinze kupata huduma hizo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Lulu Rajabu kata ya Vigwaza amesema wanawake walikuwa wakikumbana na adha ya kutembea kilometa tisa na zaidi kipindi wanaposhindwa kujifungulia kwenye Zahanati.

Katika maadhimisho hayo wanachama wa CCM kutoka maeneo mbalimbali ya kata hiyo walioshiriki kupanda miti kwenye kituo hicho sambamba na kufanya harambee ya ujenzi wa ofisi ya chama ambapo zaidi ya milioni tatu zilichangwa