Monday, February 9, 2015

WAFUGAJI WASIOPELEKA WATOTO WA KIKE WALIOFAULU SEC KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA

Na John Gagarini, Bagamoyo
WAZAZI wa watoto wa wafugaji  kwenye Kijiji cha wafugaji cha Chamakweza kata ya Pera wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wametakiwa kuwapeleka shule watoto wao wakike waliofaulu kwenda kidato cha kwanza mwaka huu kwenye shule mbalimbali wilayani humo.
Hayo yalisemwa na mjumbe wa kamati ya wafugaji ya kata ya Pera, Yohana Kipojo, wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa shule ya awali ya Ekishomi inayomilikiwa na kanisa la Gosheni Inland lililopo kwenye kitongoji cha Chamakweza.
Kipojo alisema kuwa lengo la kuwahimiza wazazi hao kuwapeleka shule watoto wao wakike waliofaulu ni kuhakikisha wanapata elimu ya juu na kuachana na tabia ya kuwaoza huku wale wakiume wakipatiwa elimu.
“Tunatoa hadi Machi 30 endapo mfugaji yoyote kama hajampeleka shule mtoto wake wakike aliyefaulu hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake hivyo lazima wahakikishe wanawapeleka ili wapate elimu,” alisema Kipojo.
Aidha alisema kuwa elimu ni haki kwa watoto wote na si watoto wa jinsia moja ambapo baadhi ya wazazi hawawapeleki watoto wakike shule na kuwapelendelea wakiume jambo ambalo linalosababisha watoto wakike kukosa elimu.
Kwa upande wake mlezi wa shule hiyo Rehema Ishengoma alisema kuwa kuwaoza watoto wadogo ni kuwanyima haki yao ya msingi ya kupata elimu ambayo iko kikatiba.
Ishengoma amesema kuwa wanafunzi wakike wanaoozwa kwenye umri mdogo wanapata mateso makubwa hasa wakati wa kujifungua kwani miili yao bado haijawa na uwezo wa kujifungua na endapo mtoto wakike atapata elimu atajua haki zake na kuweza kuyatawala maisha yake.
Naye Mchungaji wa Kanisa hilo Jackson Bukelebe alisema kuwa lengo la kujenga shule hiyo ya awali ni kuwasogezea shule karibu watoto wawafugaji kwani shule zilizopo ziko mbali nao.
Mch Bukelebe alsema kuwa eneo hilo halina shule jambo ambalo linawafanya wanafunzi ambao ni wadogo kuwa na wakati mgumu kwenda shule ambapo kitongoji hicho hakuna shule.
Mwisho.  





No comments:

Post a Comment