Sunday, February 8, 2015

MKOA KUENDELEA KUSAIDIA MICHEZO

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amesema kuwa mkoa utaweka mazingira mazuri kwa wanamichezo ili waweze kufanya vema kwenye michuano mbalimbali ya ndani na ile ya Kitaifa ili kuendeleza vipaji.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati akipokea kombe la ushindi wa tatu kwa timu ya mpira wa Pete ya Ruvu JKT Mlandizi wilayani Kibaha ambayo ilishika nafasi hiyo kwenye mashindano ya Taifa yaliyofanyika mwaka jana.
Mhandisi Ndikilo alisema kuwa ofisi yake itahakikisha kuwa michezo ndani ya mkoa inasonga mbele kwa ili kuleta mafanikio kwenye sekta hiyo ambayo imekuwa ikiuletea sifa kubwa mkoa wa Pwani ambapo timu za soka za Ruvu Stars na Ruvu Shooting zinazoshiriki ligi kuu ya Tanzania Bara zinatokea kwenye mkoa huo.
“Fedha ni changamoto kubwa kwenye sekta ya michezo lakini tutajitahidi kwa hali na mali kw akushirikiana na wadau wa michezo kuhakikisha timu zilizondani ya mkoa wetu zinafanya vizuri kwenye mashindano mbalimbali ya kimkoa na kitaifa ili kuendeleza sifa nzuri ya michezo iliyopo kwa sasa,” alisema Mhandisi Ndikilo.
 Aidha alisema kuwa licha ya mkoa kuwa na changamoto kubw aya ukosefu wa fedha lakini mkoa umekuwa ukipiga hatua kubwa na kuufanya kuweza kutamba kwenye nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na timu ya mpira wa soka la wanawake kushika nafasi ya pili kwenye mashindano ya Taifa yaliyomaliziki hivi karibuni .
Kwa upande wake mwenyekiti wa baraza la michezo la mkoa ambaye ni katibu Tawala wa mkoa huo Mgeni Baruhani alisema kuwa kwa bahati mbaya hakuna fedha zinazotengwa kwa ajili ya michezo lakini ofisi ya mkoa imekuwa ikisaidia michezo kwa kuzichangia timu na vilabu vya mkoa ili vishiriki kwenye michuano mbalimbali hapa nchini.
Kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha mpira wa Pete mkoani Pwani Fatuma Mgeni alisema kuwa timu hiyo kwa sasa iko kwenye maandalizi ya mashindano ya Afrika Mashariki itakayofanyika Zanzibar kuanzia mwezi Machi mwaka huu na kuwaomba wadau kujitokeza kuisaidi ili iweze kufanya vizuri kwenye michuano hiyo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment