Thursday, February 26, 2015

MA DC WATAKIWA KUKAMILISHA MAABARA ZIKAMILIKE MACHI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amewataka wakuu wa wilaya mkoani humo kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wa maabara za sayansi kwenye kata ifikapo Machi mwaka huu.
Ndikilo alitoa agizo hilo jana mjini Kibaha wakati wa kuwakaribisha  wakuu hao wa wilaya ambao waliteuliwa na Rais hivi karibuni na kusema kuwa wanapaswa kufanya jitihada madhubuti ili kufikia malengo hayo.
Alisema kuwa mkoa huo unatakiwa kujenga maabara 327 lakini zilizokamilika ni maabara 144 hivyo kuna upungufu wa maabara 183 ili kukamilisha idadi hiyo inayotakiwa.
“Hizi maabara 183 ziko kwenye hatua mbalimbali ili kukamilika kwake kwa hiyo kila mkuu wa wilaya ahakikishe kuwa ujenzi wa maabara unakamilika ifikapo Machi ambapo anapaswa kuwa amekamilisha,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa ikifika kipindi hicho kila mkuu wa wilaya ahakikishe anamkabidhi maabara hizo kufuatia agizo la Rais la ujenzi huo ukamilike ifikapo Juni mwaka huu.
“Agizo la Rais hali jail kuwa muda muda mfupi katika uongozi wenu kinachotakiwa ni maabara hizo kukamilika kwa wakati uliopangwa hivyo hakutakuwa na kisingizio chochote cha kushindwa kukamilisha ujenzi,” alisema Ndikilo.
Katika hatua nyingine mkuu huyo wa mkoa wa Pwani alisema kuwa wakuu hao wanapaswa kuondoa urasimu katika kuwapatia maeneo wawekezaji kwani fursa za uwekezaji ni nyingi sana.
Alisema wakuu hao watenge maeneo kwa ajili ya uwekezaji baada ya Jiji la Dar es Salaam kujaa hivyo fursa iliyopo ni kwa mkoa wa Pwani hivyo wanapaswa kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji.

Mwisho.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akiongea na wakuu wapya wa Wilaya hawapo pichani alipokuwa akiwatambulisha na kuwakaribisha mkoani humo baada ya kuteuliwa na Rais hivi karibuni, hafla ilifanyika leo mjini Kibaha.

 Wakuu wapya wa wilaya kuanzia kushoto kwenda kulia ni Subira Mgalu wilaya ya Kisarawe, Majid Mwanga wilaya ya Bagamoyo, Dk Hassan Mohamed wilaya ya Mafia na Abdala Kihato wilaya ya Mkuranga hafla ilifanyika leo mjini Kibaha.

 Baadhi ya wakuu wapya wa wilaya kuanzia kushoto Dk Hassan Mohamed wilaya ya Mafia, Abdala Kihato wilaya ya Mkuranga, Majid Mwanga wilaya ya Bagamoyo na Nurdin Babu wilaya ya Rufiji ambaye hakubadilishwa hafla ilifanyika leo mjini Kibaha. 


 Wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Pwani wakimsikiliza mkuu wa mkoa huo hayupo pichani Mahandisi Evarist Ndikilo, wakati wa kuwakaribisha na kuwatambulisha wakuu wa wilaya wapya waliohamishiwa mkoa huo kutoka mikoa mbalimbali hafla ilifanyika leo mjini Kibaha.

 Moja ya kiongozi wa dini ambaye alihudhuria sherehe za kukaribishwa na kutambulishwa kwa wakuu wa wilaya wapya leo mjini Kibaha.

 Baadhi ya watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Pwani wakimsikiliza mkuu wa mkoa huo Evarist Ndikilo hayupo pichani wakati wa kukaribishwa na kutambulishwa kwa wakuu wapya wa wilaya waliohamishiwa mkoani hapo wakitokea mikoa mbalimbali hafla ilifanyika leo mjini Kibaha. 

WAHARIRI NA HALI YA HEWA

Na John Gagarini, Kibaha
WAHARIRI hapa nchini wametakiwa kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa kuhakikisha vyombo vya habari vinatoa taarifa za hali ya hewa kwa wakati kwa usahihi na kwa lugha rahisi kupunguza majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa kwa ajili ya kulinda maisha ya wananchi wa Tanzania na mali zao.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na mkurugenzi wa Mamlaka ya hali ya hewa Tanzania Dk Agnes Kijazi wakati akifungua mafunzo ya siku moja kwa wahariri wa vyombo vya habari na wadau wa sekta mbalimbali kuhusu utabiri wa mvua za msimu wa Machi na Mei 2015.
Dk Kijazi alisema kuwa Mamlaka ya Hali ya Hewa kwa muda mrefu sasa imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kuhakikisha kuwa inaboresha huduma zake kwa kuongeza wigo wa kuwafikishia wananchi taarifa na tahadhari za hali ya hewa kwa wakati na hivyo kutumika pamoja na mambo mengine kuweka mikakati ya kupunguza athari za majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa ili kulinda maisha ya watu na mali zao.
“Tunaomba wahariri kwa kushirikiana na mamlaka kuweza kutoa taarifa sahihi juu ya hali ya hewa kwa wananchi ili waweze kuweza kujua jinsi gani ya kukabiliana na majanga yakiwemo ya mvua au madhara mengine yanayotokana na hali ya hewa,” alisema Dk Kijazi.
Dk Kijazi alisema kuwa kwa sasa Mamlaka iko katika maandalizi ya kutoa utabiri wa msimu wa mvua za masika (Machi-Mei) utabiri ambao wanatatarajia kuutoa tarehe tatu mwezi wa tatu mwaka huu.
”Ushauri wa kisekta ni muhimu sana katika kuhakikisha kuwa utabiri utakaotolewa utasaidia kupanga mipango mbalimbali ya sekta husika na kupunguza athari ambazo zinaweza kujitokeza kutokana na hali ya hewa inayotarajiwa,” alisema Dk Kijazi.
Aliongeza kuwa ili kuhakikisha hilo linafanikiwa hutegemea kwa kiasi kikubwa huduma na taarifa sahihi za hali ya hewa zinazotolewa kwa wakati muafaka.
Mkurugenzi huyo wa mamlaka ya hali ya hewa nchini alisema taarifa za hali ya hewa hutumika katika shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi katika kufanikisha shughuli za sekta mbalimbali kama vile Usafiri wa anga na kwenye maji, Nishati, Afya, Utalii, Misitu, Mazingira, Mifugo, Uvuvi, Usimamizi wa mipango miji, Umwagiliaji, Utalii, Kilimo na usalama wa chakula, Mipango ya shughuli za kijamii na kiuchumi, pamoja na huduma nyinginezo nyingi.


Mwisho.

Monday, February 23, 2015

SIMBA ISITAFUTE MCHAWI TATIZO NI

Na John Gagarini, Kibaha
TIMU ya soka ya Simba imetakiwa isimtafute mchawi kutokana na matokeo mabaya inayoyapata uwanjani kwani hali hiyo inatoka na usajili ambao haukuwa mzuri kwa kutosajili wachezaji wenye uzoefu.
Wachezaji wengi waliosajiliwa ni wale ambao wanahitaji uzoefu wa muda mrefu kabla ya kutegemewa na timu ya Simba ambayo ni timu kubwa hapa nchini.
Akizungumza na gazeti hili msemaji wa Tawi la Simba wilayani Kibaha mkoani Pwani lililopo Kwa Mfipa maarufu kama “Simba Tishio” Fahim Lardhi alisema kuwa wachezaji waliyopo wengi ni chipukizi ambao walipaswa kuwa na wachezaji wenye uzoefu.
“Timu ni nzuri lakini wachezaji wengi ni chipukizi na hawana uzoefu wa michezo mikubwa kama hii ya ligi kuu ambayo ni ngumu na inahitaji uzoefu mkubwa ambapo wachezaji hawa wanashindwa kumudu dakika 90 za mchezo,” alisema Lardhi.
Lardhi alisema kuwa hakuna haja ya kumtafuta mchawi na kutuhumiana kuwa kuna kundi fulani linahujumu timu hiyo si kweli kwani hali halisi inaonekana kuwa wachezaji wa Simba wengi hawawezi kumudu mikimikiki ya ligi.
“Hakuna cha Simba Ukawa wala nini bali timu yetu inashindwa kuhimili vishindo ni dhahiri kuwa kamati ya Usajili msimu huu imesajili timu ya Vijana wadogo wengi ambao walitakiwa kusaidiana na wachezaji wenye uzoefu,” alisema Lardhi.
Aidha alisema kwa upande wa kocha hawezi kulaumiwa kwani uwezo wake ni mzuri na timu aliikuta hata hivyo amejitahidi kuhakikisha timu inacheza vizuri tatizo ni kukosa wachezaji wazoefu.
Alibainisha kuwa huu ni msimu wan ne timu ya Simba haiku vizuri wanaifanya kama timu ya majaribio ligi kuu ni ngumu na inahitaji wachezaji wenye uzoefu mkubwa hivyo viongozi wasitoe lawama zozote.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha

TIMU ya soka ya Kiluvya United ya Mkoani Pwani imefanikiwa kupanda daraja la kwanza baada ya kutoka sare ya goli 1- 1 na timu ya Mshikamano ya Jijini Dar es Salaam kwenye mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa Ruvu JKT Mlandizi wilayani Kibaha.

Kiluvya United imefanikiwa kupanda licha ya kuwa bado ina michezo miwili mkononi kwenye mashindano ya ligi daraja la Pili  Taifa ilianza mbio zake za kuwania kupanda daraja tangu mwaka jana.

Katika mchezo wa huo ulioifanya timu hiyo kupanda hadi daraja la Kwanza kutoka la pili ulishuhudiwa na mashabiki wengi toka timu hizo mbili ulikuwa na ushindani mkubwa na kufanya kuwa na mvuto uliowafanya mashabiki kupata burudani ya nguvu.


Mashabiki wa United walifurahia matokeo hayo ambayo yameipandisha timu hiyo ya mkoa wa Pwani ambayo imepania msimu ujao kupanda ligi kuu ya Voda Com ili kuungana na timu za Ruvu Shooting na Ruvu Stars.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mchezo kwisha kocha mkuu wa United Yahaya Issa alisema kuwa kwa kwa sasa kikosi chake kina jumla ya pointi 20 na kwamba kimebakiza michezo miwili, Mshikamo ikiwa na pointi 13 ikifuatiwa na Abajalo ikiwa na pointi 12 zote za Jijini Dar es Salaam.

‘Ndugu waandishi kwanza kabisa napenda kumshukuru mungu kwa timu yangu kupanda daraja la kwanza na hii yote nikutokana na juhudi za wachezaji na uongozi mzima wa United pamoja na mwamko wa mashabiki wa Pwani ndiyo waliofanikisha kupanda daraja,” alisema Issa.

Issa alisema kuwa kwa sasa wao ndiyo vinara kwa pointi 20 na bado wana michezo miwili dhidi ya Abajalo na Cosmo hivyo hakuna timu yoyote ambayo itaweza kufikia pointi zao hata kama wakishinda michezo yote.

Naye Mkrugenzi wa timu hiyo ya United Edward Mgogo “Eddo Master” alisema kwamba ndoto yao kubwa ni kuhakikisha timu hiyo inafika mbali ili kuweza kushiriki katika ligi kuu ya Tanzaania Bara.

Aidha alitoa wito kwa wadau mbali mbali na mashabiki wa Mkoa wa Pwani kuiunga mkono timu yao ili kuweza kutimiza azama yao ya kuweza kufika mabli na hatimaye katika siku zijazo iweze kushiriki hata michuano mbali mbali ya Kimataifa.

Kikosi hicho ambacho kwa sasa kimeacha gumzo ya hali ya juu kutokana na wachezaji wake kuonyesha kandanda la aina yake siku ya jumamosi kinatarajia kushuka dimbani kumenyana na timu ya Abajalo katika nyasi za uwanja wa Karume Jijiji Dar es Salaam ikiwa kama kumalizia michezo yake miwili ya mzunguko wa mwisho.

  Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

SHIRIKA la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Pwani limepata hasara ya zaidi ya shilingi milioni 12 ikiwa ni pamoja na wateja wake kujiwekea nguzo kinyemela na kujiunganishia nyaya za umeme zenye urefu wa mita 2000.

Shirika hilo liliweza kubaini kuwa kuna baadhi ya wateja wake ambao wameamua kujiunganishia umeme kwa kujiwekea nguzo pamoja na nyaya za umeme zenye urefu huo kinyume cha utaratibu.

Hayo yalisemwa na ofisa Usalama wa TANESCO Mkoa wa Pwani Henry Byarugaba na kusema kuwa tukio hilo la kuhujumu miundombinu hiyo  limetokea katika eneo la  Matumbi Wilayani Bagamoyo.

“Shirika iliweza kubaini kuna baadhi ya wateja wake ambao wameamua kujiwekea nguzo kinyemela pamoja na nyaya za umeme zenye urefu wa mita 2000 bila ya TANESCO ambao ndiyo waunganishaji wa umeme kufahamu jambo ambalo ni kinyume cha sheria,” alisema Byarugaba.

Byarugaba alisema kuwa Shirika limepata hasara kuwaba kutokana na kuwakuta wateja wawili kujiunganishia nguzo saba bila ya TANESCO kufahamu kwani mbali ya hujuma hiyo pia ni hatari sana maana miundombinu hiyo inahujumiwa na watu wachache hivyo hawataweza kuvumilia hali hiyo.

“Baada ya kukuta nguzo hizo zimewekwa hatua ambazo tulizichukua ni kuziondoa nguzo zote saba kwani hazikuwa zimezingatia taratibu katika uwekaji wa miundombinu hiyo hivyo hazikuwa halali kuwepo katika eneo hilo,” alisema Byarugaba.

Aidha alisema kuwa kubainika kuwepo kwa nguzo hizo ni kutokana na juhudi za makusudi ambazo zinafanywa na wafanyakazi wa Shirika hasa nyakati za usiku na mchana ili kuweza kuangalia miundombinu yake na kuwabaini wateja ambao wamekuwa wakivunja sheria kwa kujiunganishia  nguzo wenyewe.

“Hivi kweli jamani mtu anafanya maamuzi ya kuamua kuhujumu miundombinu yetu bila ya woga wowote ule hii ni hatari sana na ndio maana sisi jukumu letu ni kuhakikisha miundombinu yetu inakuwa katika hali ya usalama, na siyo wateja wetu kujichukulia maamuzi wao wenyewe bila ya kuwaona wahusika kutoka,”alisema Byarugaba.

Ofisa usalama huyo wa TANESCO alisema kuwa kutokana na kuwepo kwa hali hiyo wameshapeleka taarifa polisi ili kuweza kuwasaka watuhumiwa wote ambao wamehusika katika tukio hilo la kujiunganishia nguzo na nyaya kiholela ili waweze kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Alibainisha kuwa kwa sasa bado wanendelea kufanya uchunguzi wa  kina ili waweze kuwafahamu ni watu gani ambao wamehusika katika zoezi hilo la kuwawekea wateja hao nguzo na nyaya bila ya uongozi  wa Shirika kufahamu lolote juu ya tukio hilo.
Mwisho.


Sunday, February 22, 2015

RIDHIWANI ATOA MSAADA WA CHAKULA KWA WAHANGA WA MVUA

 Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete, Idd Swala kushoto akimkabidhi moja ya wahanga wa mvua ambazo ziliharibu nyumba za wakazi wa Chalinze hivi karibuni.  

 Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Idd Swala kushoto akimkabidhi vyakula moja ya wananchi ambao walipata janga la mvua ambayo iliharibu nyumba za wakazi wa Chalinze.

Na John Gagarini, Chalinze
MBUNGE wa Jimbo la Chalinze mkoani Pwani amewasaidia chakula watu 131 ambao nyumba zao ziliharibika kutokana na mvua kubwa iliyonyesha hivi karibu.
Mvua hizo zilinyesha Februari 16 kwenye Kijiji cha Msoga na Februari 19 mwaka huu na kusababisha watu 11 kujeruhiwa huku nyumba zaidi ya 100 zikibomoka hali iliyosababisha wengine kuhifadhiwa na majirani zao.
Akitoa vyakula hivyo kwa niaba ya Mbunge huyo wa Jimbo la Chalinze, katibu wake Iddi Swala alisema kuwa vitu hivyo ni kuwawezesha wananchi hao angalau waweze kujipatia mlo huku mipango mingine ya kuwasaidia ikiendelea.
“Mbunge ameamua kujitolea vyakula hivyo ambavyo ni mchele kilogramu tano, maharage kilogramu tano,  unga wa sembe kilogramu tano na sukari kilogramu mmoja ili kuwasidia katika kipindi hichi kigumu hivyo ameona awasaidie,” alisema Swala.
Swala alisema kuwa anawaomba watu wengine nao waweze kuwasaidia wahanga hao kwa hali na mali ili waweze kupata huduma zingine za kiutu.
Naye mmoja ya waathirika hao Ramadhan Madewa ambaye mbali ya nyumba yake kubomoka pia alijeruhiwa usoni alisema kuwa anashukuru msaada huo kwani utawasaidia wakati wakiendelea kuangalia namna gani watakavyojipanga kurjesha makazi yao katika hali ya kawaida.
Kwa upande wake diwani wa Bwiringu Nasa Karama alimshukuru Mbunge huyo kwa kujitolea kuwapatia chakula waathirika wa mvua hizo ambazo kwenye kata yake jumla ya nyumba 84 ziliharibiwa na mvua hizo.
Naye mtendaji wa kata ya Msoga Hassan Mtamani alisema kuwa msaada huo utawasaidia waathirika wa janga hilo kwa kipindi hichi ambacho wanaendelea kufanya tathmini ya uharibifu uliotokea.
Mwisho.



    

JAMII ISIMAMIE UKIUKWAJI HAKI ZA WATOTO

Na John Gagarini, Kibaha
JAMII mkoani Pwani imetakiwa kusimamia malezi ya watoto wadogo na kuacha kuwafanyia vitendo vya ukatili ambavyo vimekuwa vikiwaletea athari kubwa katika makuzi yao.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mratibu wa mtandoa wa Malezi Makuzi na Maendeleo ya Watoto wadogo Tanzania (TECDEN) mkoa wa Pwani Feliciana Mmasi wakati wa mafunzo ya Sera ya Haki ya Mtoto Tanzania kwa walimu na walezi wa vituo vya watoto wadogo wilayani Kibaha.
Mmasi alisema kuwa baadhi ya watoto mkoani Pwani wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya ukatili na ndugu wa karibu hata baadhi ya wazazi hasa wale wa kike.
“Kumekuwa na vitendo vingi vya ukatili ambavyo watoto wadogo wamekuwa wakifanyiwa huku baadhia ya jamii ikiviangalia na kuvifumbia macho hivyo kuendeleza unyanyasaji kwa watoto wadogo,” alisema Mmasi.
Aidha alisema kuwa baadhi ya vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa watoto wadogo ni pamoja na ubakaji, vipigo, kuuwawa, kunyimwa chakula na vitendo ambavyo ni kinyume cha haki za binadamu.
“Utafiti uliofanyanyika mwaka 2010 kuhusu hali ya ukatili nchini umeonyesha kuwa watoto 6 kati ya 10 wamefanyiwa vitendo vya ukatili katika mikono ya ndugu na jamaa wa karibu huku mtoto mmoja kati ya wawili wamefanyiwa vitendo vya ukatili na walimu,” alisema Mmasi.
Kwa upande wake ofisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Joannes Bigirwamungu alisema kuwa wamekuwa wakiunda timu kwenye ngazi mbalimbali kwa ajili ya kupokea taarifa za vitendo vya ukatili na kuripoti kwenye vyombo vya sheria.
Bigirwamungu aliitaka jamii kutoa taarifa za baadhi ya watu wanaofanya vitendo vya ukatili kwa watoto ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa kwa wahusika wa matukio hayo ambayo yanawanyima haki watoto.
Mwisho.

Monday, February 9, 2015

WAFUGAJI WASIOPELEKA WATOTO WA KIKE WALIOFAULU SEC KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA

Na John Gagarini, Bagamoyo
WAZAZI wa watoto wa wafugaji  kwenye Kijiji cha wafugaji cha Chamakweza kata ya Pera wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wametakiwa kuwapeleka shule watoto wao wakike waliofaulu kwenda kidato cha kwanza mwaka huu kwenye shule mbalimbali wilayani humo.
Hayo yalisemwa na mjumbe wa kamati ya wafugaji ya kata ya Pera, Yohana Kipojo, wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa shule ya awali ya Ekishomi inayomilikiwa na kanisa la Gosheni Inland lililopo kwenye kitongoji cha Chamakweza.
Kipojo alisema kuwa lengo la kuwahimiza wazazi hao kuwapeleka shule watoto wao wakike waliofaulu ni kuhakikisha wanapata elimu ya juu na kuachana na tabia ya kuwaoza huku wale wakiume wakipatiwa elimu.
“Tunatoa hadi Machi 30 endapo mfugaji yoyote kama hajampeleka shule mtoto wake wakike aliyefaulu hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake hivyo lazima wahakikishe wanawapeleka ili wapate elimu,” alisema Kipojo.
Aidha alisema kuwa elimu ni haki kwa watoto wote na si watoto wa jinsia moja ambapo baadhi ya wazazi hawawapeleki watoto wakike shule na kuwapelendelea wakiume jambo ambalo linalosababisha watoto wakike kukosa elimu.
Kwa upande wake mlezi wa shule hiyo Rehema Ishengoma alisema kuwa kuwaoza watoto wadogo ni kuwanyima haki yao ya msingi ya kupata elimu ambayo iko kikatiba.
Ishengoma amesema kuwa wanafunzi wakike wanaoozwa kwenye umri mdogo wanapata mateso makubwa hasa wakati wa kujifungua kwani miili yao bado haijawa na uwezo wa kujifungua na endapo mtoto wakike atapata elimu atajua haki zake na kuweza kuyatawala maisha yake.
Naye Mchungaji wa Kanisa hilo Jackson Bukelebe alisema kuwa lengo la kujenga shule hiyo ya awali ni kuwasogezea shule karibu watoto wawafugaji kwani shule zilizopo ziko mbali nao.
Mch Bukelebe alsema kuwa eneo hilo halina shule jambo ambalo linawafanya wanafunzi ambao ni wadogo kuwa na wakati mgumu kwenda shule ambapo kitongoji hicho hakuna shule.
Mwisho.  





Sunday, February 8, 2015

MKOA KUENDELEA KUSAIDIA MICHEZO

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amesema kuwa mkoa utaweka mazingira mazuri kwa wanamichezo ili waweze kufanya vema kwenye michuano mbalimbali ya ndani na ile ya Kitaifa ili kuendeleza vipaji.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati akipokea kombe la ushindi wa tatu kwa timu ya mpira wa Pete ya Ruvu JKT Mlandizi wilayani Kibaha ambayo ilishika nafasi hiyo kwenye mashindano ya Taifa yaliyofanyika mwaka jana.
Mhandisi Ndikilo alisema kuwa ofisi yake itahakikisha kuwa michezo ndani ya mkoa inasonga mbele kwa ili kuleta mafanikio kwenye sekta hiyo ambayo imekuwa ikiuletea sifa kubwa mkoa wa Pwani ambapo timu za soka za Ruvu Stars na Ruvu Shooting zinazoshiriki ligi kuu ya Tanzania Bara zinatokea kwenye mkoa huo.
“Fedha ni changamoto kubwa kwenye sekta ya michezo lakini tutajitahidi kwa hali na mali kw akushirikiana na wadau wa michezo kuhakikisha timu zilizondani ya mkoa wetu zinafanya vizuri kwenye mashindano mbalimbali ya kimkoa na kitaifa ili kuendeleza sifa nzuri ya michezo iliyopo kwa sasa,” alisema Mhandisi Ndikilo.
 Aidha alisema kuwa licha ya mkoa kuwa na changamoto kubw aya ukosefu wa fedha lakini mkoa umekuwa ukipiga hatua kubwa na kuufanya kuweza kutamba kwenye nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na timu ya mpira wa soka la wanawake kushika nafasi ya pili kwenye mashindano ya Taifa yaliyomaliziki hivi karibuni .
Kwa upande wake mwenyekiti wa baraza la michezo la mkoa ambaye ni katibu Tawala wa mkoa huo Mgeni Baruhani alisema kuwa kwa bahati mbaya hakuna fedha zinazotengwa kwa ajili ya michezo lakini ofisi ya mkoa imekuwa ikisaidia michezo kwa kuzichangia timu na vilabu vya mkoa ili vishiriki kwenye michuano mbalimbali hapa nchini.
Kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha mpira wa Pete mkoani Pwani Fatuma Mgeni alisema kuwa timu hiyo kwa sasa iko kwenye maandalizi ya mashindano ya Afrika Mashariki itakayofanyika Zanzibar kuanzia mwezi Machi mwaka huu na kuwaomba wadau kujitokeza kuisaidi ili iweze kufanya vizuri kwenye michuano hiyo.

Mwisho.

WEKENI MFUKO WA KUSAIDIA WENYE UHITAJI

Na John Gagarini, Kibaha
VYAMA vya Kuweka na Kukopa (SACCOS) wilayani Kibaha mkoani Pwani vimetakiwa kuweka mifuko kwa ajili ya kuwasaidia watu wenye shida mbalimbali wakiwemo watu wenye mahitaji maalumu na watoto waishio kwenye mazingira hatarishi.
Hayo yamesemwa mjini Kibaha na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (MNEC) Kibaha Mjini Rugemalila Rutatina wakati wa kuwakabidhi  vifaa vya shule wanafunzi wa shule za msingi na  sekondari waishio kwenye mazingira hatarishi kwenye mtaa wa Kwa Mfipa wilayani humo vilivyotolewa na chama cha kuweka na kukopa cha Upendo cha mtaa huo.
Rutatina alisema kuwa ili jamii iweze kunufaika na vyma hivyo ni vema vikawa na mifuko hiyo ili kuwezesha makundi hayo ambayo hayana msaada wowote kutokana na hali zao.
“Ni vema vyama hivyo vikatenga fedha kidogo kwa ajili ya kuisaidia jamii kwani SACCOS zimeonekana kuwa ni msaada mkubwa kwa wanachama ambao wengi wao ni wajasiriamali kwa kujikwamua na hali ngumu ya kiuchumi,” alisema Rutatina.
Alisema kuwa kuwasaidia watu wenye shida ni ibaada ambayo inafanywa na mtu anayetoa hivyo Mungu humbariki na kumuongezea kwa kuwa amewajali wale wasio na uwezo kama vile wazee, wajane, yatima na  wenye ulemavu.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Kibaha Said Nangurukuta alisema kuwa chama hicho kimeonyesha mfano kwa kutenga fedha kwa ajili ya kuwasaidia watoto waishio kwenye mazingira hatarishi hivyo kuwasaidia walezi wa watoto hao.
Naye Ofisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Faustina Kayombo alisema kuwa watoto wenye mahitaji maalumu wamekuwa wakiongezeka kila mara kutokana na utengano wa wazazi au mazingira magumu ya kwenye familia na kuwapatia vifaa hivyo chama hicho kimeisaidia serikali kubeba mzigo wa kuwasaidia wanafunzi wanaoishi kwenye mazingira hatarishi na kuwataka watu wenye uwezo kuwasaidia watoto kama hao.
Awali akisoma risala mbele ya mgeni rasmi Mwajuma Teya alisema kuwa mbali ya chama chao kukopesha kimetenga fedha kwa ajili ya kuwasaidia watoto wanoishi kwenye mazingira magumu ambapo kimekuwa kikitoa vifaa mbalimbali pamoja na kuwalipia ada baadhi yawanafunzi.
Teya alisema kuwa mbali ya mafanikio hayo pia wanakabiliwa na changamoto ya udogo wa mtaji wao hali inayosababisha mzunguko wa kukopeshana kutokwenda kwa wakati, jumla ya wanafunzi 25 walipewa misaada hiyo na kinajumla ya wanachama 30 ambao ni wajasiriamali wanaojihusisha na ufumaji, ushonaji, ulimaji wa bustani, utengenezaji wa sabuni na kukopeshana na kilianzishwa mwaka 2012.
Mwisho.