Tuesday, November 25, 2014

WAFANYABIASHARA WATAKIWA KUKATIA BIMA BIASHARA ZAO KUKABILIANA NA MAJANGA

Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA maduka kadhaa kungua moto eneo la Maili Moja wilayani Kibaha  wafanyabiashara mkoani Pwani wameshauriwa kukatia bima biashara zao ili kukabiliana na hasara zinazoweza kujitokeza kutokana na majanga kama hayo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mara baada ya kuwakabidhi msaada wa fedha kiasi cha shilingi 810,000 wahanga wa moto huo mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) mkoa wa Pwani, Abdala Ndauka alisema kuwa moto huo umewapa hasara kubwa wafanyabiashara hao.
Ndauka alisema kuwa imefika wakati sasa kwa wafanyabiashara kukata bima za biashara zao ili mara wapatapo majanga kama ya moto au wizi bima itawafidia na wataweza kuendelea vizuri na biashara bila ya kuyumba.
“Ule moto umesababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara wenzetu kwani hawakuweza kuokoa bidhaa zote ziliteketea kwa moto hivyo umuhimu wa bima umeonekana kwani wangekuwa nayo wangelipwa,” alisema Ndauka.
Akizungumzia juu ya msaada huo alisema kuwa baada ya wenzao kupata tatizo hilo walichanga fedha hizo kama pole kwa wenzao watatu ambao walipata tatizo hilo la kuunguliwa maduka yao ya biashara mbalimbali.
Aidha alisema fedha hizo zimechangwa na sehemu ya wafanyabiashara wanachama wa JWT ambao ni zaidi ya 300 kati ya 800 wanaounda umoja huo.
“Kutokana na tukio  hili tumeazimia kuanzisha mfuko wa maafa ili tuweze kusaidiana mara yanapotokea matatizo kama haya na fedha zitakazopatikana ziweze kuwasaidia waathirika,” alisema Ndauka.
Naye Ally Gonzi moja ya waathirika wa moto huo aliwashukuru wanajumuiya hiyo kwa msaada walioutoa na kusema kuwa serikali inapaswa kuhakikisha mkoa huo unakuwa na huduma ya zimamoto kwani moto ulipotokea hawakuweza kupata huduma hiyo licha ya kuwa wanalipia huduma hiyo.
Gonzi alisema kuwa endapo mkoa huo ungekuwa na gari la zimamoto basi mali zilizoteketea zingeweza kuokolewa hasa ikizingatiwa  ofisi za kikosi hicho ziko jirani kabisa na tukio lilipotokea ambapo waathirika wengine ni Urisha Mwembamba na Adam Mwasha.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment