Wednesday, November 19, 2014

DC KUDHIBITI MADK WEZI WA DAWA

Na John Gagarini, Rufiji
MKUU wa Wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Nurdin Babu amesema atawachukulia hatua kali baadhi ya madaktari watakaobainika kuiba dawa na kuziuza kwenye maduka ya dawa.
Aliyasema hayo kwenye Kijiji cha Nyambili-Bungu wilayani humo wakati akielezea umuhimu wa wananchi kujiunga na mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
Babu alisema kuwa baadhi ya madaktari kwenye zahanati vijijini wamekuwa wakiiba dawa muhimu kisha kuziuza kwenye maduka hayo na kuacha maboksi matupu wakidai kuwa zimetumiwa na kuisha.
“Dawa hizi si sukari kusema watu wanalamba kila wakati lakini ni baadhi ya madaktari wasiokuwa waaminifu wamekuwa wakiziuza dawa hizo na kila wananchi wanapoandikiwa dawa wanaambiwa zimekwisha je zinakwishaje wakati wagonjwa hawajapewa tutawashughulikia nyie tupeni taarifa,” alisema Babu.
Alisema kutokana na hali hiyo anaacha namba yake ya simu ili apewe taarifa za madaktari wanaofanya mchezo huo ili akabiliane nao na kuwataka wananchi kutoa taarifa.
Kwa upande wake mganga mkuu wa wilaya ya Rufiji Dk Michael Michael alisema njia rahisi ya kupata matibabu ni kujiunga na mfuko huo ambapo familia ya watu sita inalipa 10,000 kwa mwaka lakini kwa wasiojiunga wanalipa 3,000 kila wanapomwona daktari.
“Uzuri wa sasa ni kwamba kutakuwa na kamati ya Kijiji ya afya ambayo itakuwa na uwezo wa kununua dawa wanazoona zimekwisha au zinazohitaji kutokana na tatizo la eneo husika,” alisema Dk Molel.
Aidha alisema kuwa wataingia mikataba na wamiliki wa maduka ili dawa zinapokwisha wawe wanawapa wagonjwa ili kuondoa kero na kusema kuwa mfumo huu utaondoa changamoto ya dawa.
Naye mratibu wa CHF wilaya hiyo Rashid Mihuka alisema kuwa kutaanzishwa madirisha ya dawa kwa ajili ya wanachama wa mfuko huo ili kuboresha huduma kwa wateja wa mfuko huo.
Mwisho.


No comments:

Post a Comment