Sunday, November 9, 2014

MOTO WATEKETEZA MADUKA 6 MMOJA AJERUHIWA MWINGINE AZIRAI

Na John Gagarini, Kibaha
MFANYABIASHARA  mmoja wa duka la bidhaa mbalimbali Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani Urisha Mwembamba amenusurika kifo baada ya kujeruhiwa na moto ambao uliteketeza duka lake na mengine matano.
Moto huo ambao unadaiwa ulitokana na shoti ya umeme ulianzia kwenye jokufu la kuhifadhia vinywaji baridi ambavyo alikuwa akiuza pamoja na bidhaa nyingine viliteketea kabisa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mmoja wa wahanga wa tukio hilo Ally Gonzi alisema kuwa tukio hilo lilitokea juzi Novemba 10 majira ya saa 2 usiku
Gonzi alisema kuwa moto huo ulianza majira ya saa 2 usiku na ulianzia kwenye duka hilo na kusambaa kwenye maduka mengine baada ya kushindwa kuudhibiti. 
“Moto ulianzia kwenye duka la Mwembamba kwenye jokofu na wakati moto unaanza alikuwepo kwani aliingia kwa mlango wa dharura lakini alishindwa kutoka akiwa hajui nini cha kufanya huku moto ukiendelea ndipo wasamaria wema wakaingia na kumtoa ambapo alijeruhiwa na moto miguuni,” alisema Gonzi
Alisema kuwa moto ulipokuwa ukiendelea watu walifika na kuanza kujaribu kuzima lakini ulikuwa mkali sana kwani kuna pipa kubwa la maji kama lita 15,000 wakawasha mashine lakini moto huo haukuzimika.
“Dada wa Mwembamba aitwaye Nasra alipopata taarifa akaja kutoka Mbezi naye akazimia kutokana na tukio hilo ambapo wote walikimbizwa hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Tumbi kwa ajili ya matibabu hata hivyo gari la zimamoto lilifika saa moja na nusu baada ya moto kutokea hata hivyo walifika moto huo ukiwa tayari umedhibitiwa na wananchi,” alisema Gonzi.
Aidha alisema waliwasiliana na kikosi cha zimamoto lakini waliambiwa hakuna gari na askari wakuzuia ghasia FFU walifika na kuzuia wizi lakini hata hivyo watu waliiba vitu walipokuwa wakijidai kuokoa.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alisema kuwa jumla ya maduka sita yaliathirika na moto huo na mtu mmoja alijeruhiwa.
“Polisi ilibidi watumie mabomu ya machozi ili kuwatawanya watu ambapo baadhi yao walikuwa ni vibaka waliokuwa wakijaribu kuiba mali kwenye maduka mengine ya jirani,” alisema Kamanda Matei.
Kamanda Matei alisema kuwa chanzo cha moto huo bado hakijajulikana wala thamani ya mali zilizoteketea bado hakujafahamika na uchunguzi unaendelea aliwataka wananchi kutotumia fursa kuiba yanapotokea majanga kama hayo badala yake watoe msaada.

Mwisho. 

No comments:

Post a Comment