Sunday, November 9, 2014

TALGWU KUTOT

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (TALGWU) kwenye Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani kimesema kuwa kitadai haki za wanachama wake kwa kukaa mezani na si kwa kufanya migomo au maandamano.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mwenyekiti wa chama hicho Tawi la Kibaha Mji, Adolf Masawa wakati wa kufunga mafunzo ya viongozi wapya wa matawi kwenye halmashauri hiyo
Masawa alisema kuwa baadhi ya vyama vya wafanyakazi vimekuwa vikidai haki zao kwa kufanya migomo na maandamano jambo ambalo linasababisha utoaji huduma kuwa mbaya.
“Sisi tutafuata taratibu na sheria katika kudai haki na hatutakuwa tayari kuwatetea wanachama ambao hawawajibiki kwani haki inakwenda sambamba na uwajibikaji,” alisema Masawa.
Aidha alisema kuwa wao hawana ushabiki na ndiyo sababu chama chao huwa hakifuati mkumbo katika kudai haki zao kama ilivyo kwa baadhi ya vyama hali ambayo inasababisha usumbufu kwa wateja wanaowahudumia.
Kwa upande wake katibu wa TALGWU wa mkoa wa Pwani Amina Darabu alisema kuwa chama chao kina lengo la kuwaunganisha wafanyakazi ili waweze kuwa na mahusiano mazuri na mwajiri wao ili kuboresha huduma kwa wateja.
“Tuna sisitiza umoja ujshirikiano na upendo baina ya wanachama pamoja na mwajiri na wateja wanaowahudumia kwani kwa pamoja huduma zitakuwa bora mahali pa kazi,” alisema Darabu.
Awali akifungua mafunzo hayo mwenyekiti wa mkoa Mohamed Mahingika alisema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia viongozi hao wapya kujua wajibu na majukumu yao kwa wanachama.
Mahingika aliwataka viongozi hao kuhamasisha watumishi wa serikali za mitaa kujiunga na chama hicho ili kuwa na nguvu ya pamoja katika kuboresha utendaji kazi wao.
Mafunzo hayo ya siku moja yaliwahusisha viongozi kutoka matawi ya Kituo cha  Afya Mkoani sasa Hospitali ya Wilaya ya Kibaha, Kituo cha Afya Mwendapole na kata Kibaha.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment