Tuesday, August 30, 2016

MBUNGE AITAKA DAWASCO KUUNGANISHA MAJI BILA YA UPENDELEO WA FEDHA


Na John Gagarini, Kibaha

MAMLAKA ya Maji Safi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO) wilaya ya Kibaha mkoani Pwani imetakiwa kuwaunganishia maji wananchi wa Mlandizi bila ya kujali uwezo wa mtu ili kila mtu aweze kunufaika na mradi wa maji kwenye Kitongoji cha Janga.
Hayo yalisemwa na mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijni Hamoud Jumaa wakati alipofanya ziara kutembelea mradi wa maji wa ya mkopo kwenye kitongoji cha Janga kata ya Janga wilayanai Kibaha.

Mbunge huyo alitoa wito huo kufuatia mwenyekiti wa kitongoji hicho Josephine Maendaenda kudai kuwa baadhi ya wananchi wanalalamika kuwa watu wanaotoa fedha taslimu ndiyo wanaounganishiwa maji huku wale wanaokopa kutakiwa kusubiri.

“Kwanza nawapongeza wananchi kwa kuchimba mitaro ya kulaza mabomba hivyo thamani ya nguvu zao lazima zithaminiwe sawa na wale wanaotoa fedha taslimu kwani mitaro hiyo isingechimbwa na wananchi hao maji yasingeweza kufika kwenye maeneo ya watu,” alisema Jumaa.

Alisema kuwa thamani ya watu iko palepale lakini haiwezi kwani wanaotoa fedha na wale waliotumia nguvu zao kuchimba mitaro wamefanya kazi kubwa ambayo inapaswa kuungwa mkono na siyo ya kubezwa.

“Wananchi hawa wameonyesha uzalendo wa hali ya juu kwa kufanyakazi ya kujitolea na ndiyo tunataka utamaduni huu ufanyike kwenye kila jambo na si kusubiri serikali iwafanyie wananchi kila kitu kwani hata kwenye mikoa iliyoendelea kama Moshi na Arusha imefanikiwa kwa wananchi kujitolea kama huku,” alisema Jumaa.

Kwa upande wake meneja wa Dawasco wilaya ya Kibaha Erasto Emanuel alisema kuwa suala hilo watalifanyia kazi kwa kuwaunganishia wananchi bila ya kujali kama ni malipo ya moja kwa moja au mkopo.

Emanuel alisema kuwa hadi sasa wameweza kuwaunganishaia maji wananchi 40 huku wakitarajia kuwafikia wateja 300 katika hatua ya pili huku wakitarajia maji kuanza kutoka mwezi Oktoba na kuwafikia wateja 600.

Alisema kuwa mradi huo ulikumbwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vifaa jambo ambalo lililalamikiwa na wananchi lakini yote hiyo ilitokana na kila mwaka kuwa na zoezi la kufunga mwaka ambalo huambatana na uhakiki wa vifaa.

Naye mwenyekiti wa Kitongoji cha Janga Josephine Maendaenda alisema kuwa changamoto ya maji ni kubwa kwenye kitongoji hicho na wananchi wamekuwa wakilalamika kiu yao kubwa ikiwa ni kupata maji ambapo wamekuwa wakienda mwendo mrefu kufuata maji ambapo huuziwa dumu la lita 20 kwa shilingi 500.

Mwisho. 

KAMPUNI YA UUNGANISHAJI MAGARI YAZIMAMOTO MBIONI KUANZA USZALISHAJI

Na John Gagarini, Kibaha

KAMPUNI ya Equator Suma Jkt inatarajia kuanza kuunganisha magari ya zimamoto na matrekata mwishoni mwa mwaka huu ikiwa ni moja ya njia ya kukabiliana na majanga ya moto pamoja na kuinua kilimo cha Tanzania ambacho ni uti wa mgongo wa uchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari ambao walitembelea kiwanda hicho kilichopo Ruvu Mlandizi wilayani Kibaha mkurugenzi Robert Mangazeni alisema kuwa kwa sasa kiwanda hicho kiko kwenye hatua za mwishi ikiwa ni pamoja na uunganishaji wa mitambo na mashine.

Mangazeni alisema kuwa teknolojia ya uunganishaji wa magari ya zimamoto ambapo watatumia magari ya kawaida kwa kuyabadilisha na kuwa ya zimamoto wameitoa nchi ya Urusi kutoka kwenye makampuni ya St Auto na Ural huku ile ya matekta wakiitoa kwenye kampuni za Escort kutoka nchini India na Farmtrac kutoka nchini Poland.

“Tukizungumzia kuhusu uunganishaji wa magari ya zimamoto ni teknolojia ambayo imeboreshwa na kuwa ya kisasa zaidi ambapo tutakuwa na uwezo wa kuunganisha magari ya aina mbalimbali kutegemeana na mteja anavyotaka ambayo yatakuwa na ujazo wa aina tofauti tofauti kuanzia magari makubwa hadi madogo siyo lazima yawe makubwa kama tulivyozoea hivyo hata majanga haya ambayo yamezikumba shule sasa taasisi zitaweza kudhibiti moto,” alisema Mangazeni.

Alisema kuwa ujazo huo utaanzia lita za maji 300 hadi 10,000 kutegemea na ukubwa hivyo kulinagana na miuondombinu ya barabara za mitaani wataunganisha hata magari madogo ili yaweze kufika kwenye eneo lililopata maafa ya moto.

“Ikumbukwe Tanzania itakuwa nchi ya pili kuwa na teknolojia hii ya uunganishaji wa magari ya zimamoto baada ya Afrika Kusini ambapo kwa nchi za Maziwa Makuu itakuwa ni ya kwanza na itaweza kuokoa asilimia 30 ya gharama ya kununua gari jipya la zimamoto pia watakuwa na uwezo wa kuyatengeneza magari hayo badala ya kuagiza wataalamu toka nje ya nchi mara yanapoharibika,”alisema Mangazeni.

Aidha alisema kuwa kwa upande wa matrekta wataweza kuyaunganisha ambapo kwa miaka ijayo watakuwa na uwezo wa kutengeneza trekta ambalo litakuwa ni zao la Tanzania tofauti na ilivyo sasa kuagizwa toka nje ya nchi.

“Miaka ijayo tutatengenza trekta la kwetu ambapo kwa sasa vitakuwa vinakuja vifaa vyake na kuunganishiwa hapa na tatizo la matrekta kufa haraka litakwisha kwani mafundi wa matrekta watazalishwa hapa na yatadumu kwani wengi hawana utaalamu wautengenzaji bali wanatumia uzoefu tu,” alisema Mangazeni.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho umekuja wakati mwafaka kwa upande wa janga la moto na kilimo bora.

Mshama alisema kuwa kiwanda hicho ambacho kitafanya shghuli hizo kwa pamoja itakuwa mwarobaini wa changamoto hizo ambazo ni kubwa na pia ni kutekeleza sera ya Rais John Magufuli ya kutaka Tanzania kuwa nchi ya viwanda ili baada ya miaka ijayo nchi kuwa na uchumi wa kati.

Ujenzi wa kiwanda hicho ulianza ulianza 2011 ambacho hadi kukamilika kwake kitakuwa na thamani ya shilingi bilioni tatu kitaajiri wafanyakazi 100 na kamapuni hiyo imeingia ubia na Suma Jkt na inaundwa na wanajeshi wastaafu.
 

Mwisho. 

WAILILIA HALMASHAURI KUWAJENGEA SOKO BAADA YA SOKO KUTAKIWA KUVUNJWA

Na John Gagarini, Kibaha
USHIRIKA wa Wafanyabiashara wa Soko la mkoa la Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwapatia eneo lingine la kufanyia biashara baada ya eneo wanalofanyia shughuli zao ambalo liko chini ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa kuvunjwa baada ya miezi mitatu kuanzia mwezi Agosti.

Akizungumza mara baada ya mkutano mkuu wa wanachama uliofanyika mjini Kibaha mwenyekiti wa ushirika huo Ally Gonzi alisema kuwa hadi sasa hawajui hatma yao mara zoezi hilo litakapofanyika.

Gonzi tunaiomba Halmashauri kutujengea soko au kama hawataweza kujenga ndani ya muda huo wa miezi mitatu ni vema wakaiomba wakala hao kutuongezea muda wa kuwa hapa hadi pale tutakapokuwa tumejengewa soko jipya.

“Tunamwomba Rais John Magufuli kutuangalia kwani hapa tuko zaidi ya miaka 30 na hadi sasa Halmashauri bado haijatujengea soko ambalo waliahidi kutujengea kutokana na eneo hilo kutokuwa la halmashauri,” alisema Gonzi.

Alisema kuwa kwa kipindi kirefu Halmashauri hiyo imekuwa ikiahidi kuwajengea soko la kisasa kwenye kitovu cha mji lakini hadi wanapewa barua za kutakiwa kuondoka kwenye eneo hilo na Tanroads hadi sasa hawajajengewa soko.

“Tunachoona kwa sasa kwa kuwa soko bado halijajengwa ni vema wakatuongezea muda hata wa miaka miwili kwani Halmashauri ilisema itakuwa imejenga soko ndani ya miezi 18 hivyo kwa kipindi hicho ni bora tungebaki hapa kwanza lakini vinginevyo hatujui tutakwenda wapi,” alisema Gonzi.

Aidha alisema kuwa mbali ya wao kutokuwa na mahali pa kufanyia biashara pia Halmashauri itakosa mapato kwnai soko hilo ni moja ya vyanzo vikuu vya mapato pia wao walikuwa wakitegemea hapo kwa ajili ya kujipoatia kipato chao na familia zao.


Mwisho. 

UVUNJAJI SHERIA WASABABISHA MIGOGORO YA ARDHI

Na John Gagarini, Rufiji

IMEELEZWA kuwa kuwepo kwa migogoro ya ya wakulima na wafugaji  katika Halmashauri ya Rufiji mkoani Pwani kunatokana na  baadhi ya wafugaji kuvunja sheria na taratibu zilizowekwa na   kwenda kulisha mifugo yao katika maeneo yaliyotengwa maalumu kwa ajili ya shughuli mbali mbali za kilimo.

Hayo yalisemwa na Mbunge  wa Jimbo la Rufiji Mkoani humo Mohamed Mchengerwa alipokuwa akizungumza na viongozi wa Halmashauri Mpya ya Rufiji ambapo ameahidi kulivalia njuga suala la migogoro ya ardhi inayotokana na jamii ya wafugaji na wakulima ambao wamekuwa wakigombania maeneo ya mashamba na kusababisha kutokea kwa mapigano ambayo wakati mwingine yanapelekea uvunjifu wa amani.

Mchengerwa alisema kuwa hawezi kuwavumilia wale wote ambao wataonekana wanakwenda kinyume cha sheria za nchi, na kuhakikisha kila mfugaji na mkulima anatengewa maeneo yao rasmi kwa ajili ya kufanyia shughuli zake ili kuepukana na migogoro na  mapigano ambayo yamekuwa yakijitokeza kutokana na kugombania ardhi.

“Nitaweka mikakati kabambe ambayo itaweza kuwawasaidia wananchi wakiwemo wafugaji na wakulima kwa kushirikina na viongozi wa halmashauri katika kuwatenge maeneo yao maalumu ambayo yataweza kusaidia kuepukana na migogoro hiyo ya ardhi,” alisema Mchengerwa.

Alisema kuwa anatambua kuwepo kwa changamoto kubwa na  migogoro kati ya wakulima na wafugaji, lakini dhamira yake kubwa anataka kuona wanachi wake wa jimbo la rufiji wanakaa kwa amani bila ya kuwepo kwa mapigano yoyote na kuhakikisha kwamba sula la amani na utulivu linakuwepo.

“Natambua wananchi wengi wa Jimbo la Rufiji wanategemea sana shughuli za kilimo hivyo kwa sasa wameshaweka utaratibu wa kutenga maeneo ya wafugaji ili wasiweze kuingia katika mashamba ya wakulima na kupelekea vurugu za mara kwa mara kitu amabcho sio kizuri na kinarudisha nyuma maendeleo,” alisema Mchengerwa.

Naye Mwenyekiti mpya wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji Saidina Malenda mara baada ya kushinda katika uchaguzi huo  alisema  atahakikisha anasharikina bega kwa bega na viongozi wenzake kwa lengo la kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo kwa wananchi wa Rufiji.

Malenda alisema kuwa anawashukuru madiwani wenzake kwa kuweza kumchagua kuwaongoza na kubainisha kwamba atafanya kazi bidii zote na kwa kushirikina katika mambo mbali mbali ya kimaendeleo  bila ya kuwa na ubaguzi wa aina yoyote wa itikadi ya vyama  ili kuweza  kuwatumikia wananchi katika huduma mbali mbali wanazozihitaji.

Katika uchaguzi huo wa halmashauri mpya ya Wilaya ya Rufiji,uliofanyika utete nafasi ya Mwenyekiti ilikwenda kwa Saidani Malenda ambaye alipata kura 11 kati ya kura 19 zilizopigwa, ambapo nafasi ya Makamu mwenyekiti ilikwenda kwa Hawa Mtopa  ambaye aliyepata kura 10 katika ya kura 19 zilizopigwa.
     

MWISHO

PANGANI WALILIA ZAHANATI


Na John Gagarini, Kibaha

KATA ya Pangani wilayani Kibaha inatarajia kubadilisha ofisi za Mtaa wa Kidimu kuwa Zahanati ili kukabiliana na changamoto ya mtaa huo kutokuwa na zahanati hivyo kufanya huduma za matibabu kupatikana kwa ugumu.

Akizungumza na waandishi wa habari diwani wa kata hiyo Agustino Mdachi alisema kuwa gharama za kufuata matibabu kwa wakazi wa mtaa huo ni kubwa na kuwafanya wagonjwa kuwahatarini pale wanapokuwa wamepatwa au kuzidiwa na ugonjwa.

Mdachi alisema kuwa tegemeo kubwa ni hospitali ya wilaya ya Kibaha ya Mkoani ambayo iko umbali wa kilometa 18 na ile ya jirani ya Mpiji Magohe ambayo iko kata ya Mbezi wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam ambapo usafiri wa pikipiki ni shilingi 5,000.

“Mgonjwa anapotaka kwenda Mkoani humbidi kuwa na shilingi 50,000 hasa nyakati za usiku na mchana ni 40,000 au 30,000 gharama hizi kwa ajili ya kwenda kupata matibabu ni kubwa sana na kwa mwananchi wa kawaida kumudu ni ngumu sana,” alisema Mdachi.

Alisema kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo wameamua kuibadili ofisi hiyo na kuwa zahanati ya mtaa ambapo wananchi watapa huduma karibu.

“Kwa sasa tuko kwenye mchakato kwa kuwaomba Halmashauri ya Mji kuturuhusu na kuleta wataalamu wa afya ili waangalie namna ya kulifanya jengo hilo kuwa zahanati na tunaamini ombi letu litakubaliwa,” alisema Mdachi.

Aidha alisema kuwa kutokana na ukubwa wa jengo hilo la serikali ya mtaa kuwa vyumba vingi wanaamini kuwa litafaa kwa ajili ya kuanzia huduma za kiafya wakati wanafanya mipango ya kujenga sehemu nyingine.

“Kwa kuwa ya kata ina ofisi nyingi tunaweza kutoa chuma kimoja kwa ajili ya ofisi ya mtaa ili kufanikisha zoezi hilo ambalo litawafanya wananchi wa mtaa na kata hiyo kupata huduma za afya karibu,” alisema Mdachi.

Aliwataka wananchi kuunga mkono jitihada za serikali kwa kujitolea katika masuala mbalimbali ya maenedeleo ikiwa ni pamoja na kufanikisha zoezi hilo la ujenzi wa zahanati hiyo.


Mwisho.

MADARASA YAUNGUA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

MADARASA matatu na ofisi ya Mwalimu Mkuu shule ya Msingi Kongowe wilayani Kibaha mkoani Pwani zimeungua na moto ambao ulitokea juzi usiku na kusababisha hasara kubwa.

Akizungumza na Patapata mwenyekiti wa mtaa wa Kongowe Maimuna Jamhuri alisema kuwa moto huo ulitokea Agosti 28 majira ya saa nne usiku ambapo chanzo chake bado hakijafahamika mara moja.

Jamhuri alisema kuwa moto huo ulianzia kwenye ofisi hiyo ambayo ni ya mwalimu mkuu na kuenea kwenye madarasa pamoja na chumba cha kuhifadhia vitabu ambavyo navyo vimeteketea kwa moto huo ambao ulikuwa mkali.

“Moto huo ulizimwa na wananchi ambao walijitokeza kwa wingi ambapo gari la zimamoto lilifika kwa kuchelewa kutokana na kuwa kwenye harakati za kuzima moto sehemu nyingine”, alisema Jamhuri.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Kongowe Iddi Kanyalu alisema kuwa baada ya kutokea moto huo viongozi kadhaa walifika akiwemo mkurugenzi, Mwenyekiti na Injinia wa Halmashauri kwa ajili ya kuangalia athari za moto huo.

Kanyalu alisema kuwa kutokana na makisio ya harakaharaka zinahitajika zaidi ya milioni 50 kwa ajili ya kujenga upya madarasa hayo na ofisi kwani madarasa hayo yameharibika sana na hayafai kwa matumizi wala kufanyiwa ukarabati.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo leo kamati ya maenedeleo ya kata ina kaa kuangalia namna ya kukabiliana na tatizo hilo ambalo limewakumba wanafunzi 200 waliokuwa wanatumia madarasa hayo.

Naye mtendaji wa kata hiyo ya Kongowe Said Kayangu alisema kuwa mwalimu mkuu wa shule hiyo Beatus Lingumbuka alitapa athari kidogo kichwani na mikononi kwani alikuwa kwenye harakati za kujaribu kuokoa baadhi ya vitu wenye ofisi yake.

Kayangu alisema kuwa kutokana na jitihada za wananchi wameweza kuokoa madawati kwenye madarasa hayo ambayo yalikuwa hatarini kuungua lakini hata hivyo waliweza kuyatoa na hakuna dawati hata moja lililoungua

Mwisho.


WAAMUZI KIBAHA WAPATA VIONGOZI WAPYA

Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA cha Waamuzi wa Soka Tanzania (FRAT) mkoa wa Pwani kimemchagua  Jeremia Komba kuwa mwenyekiti wa chama hicho kwa kupata kura 15 huku mpinzani wake Kassim Safisha akipata kura tano.

Uchaguzi huo ambao ulifanyika mjini Kibaha na kusimamiwa na mwamuzi mkongwe Hussein Magoti na kuwashiriki waamuzi ambao ni wanachama wa chama hicho cha waamuzi.

Komba alikuwa akichuana na mwamuzi mwenzake Kassim Safisha nakumshinda kwa tofauti ya kura tano hivyo kumfanya Komba kuwa bosi wa waamuzi wilaya ya Kibaha.

Nafasi ya makamu mwenyekiti ilikwenda kwa Sayenda Lubisa ambaye hata hivyo hakuwa na mpinzani na kujipatia kura 17 huku tatu zikiharibika.

Upande wa katibu mkuu Endrew Kayuni alikuwa mshindi kwa kupata kura 15 huku Mohamed Juaji akipata kura tano, nafasi ya katibu msaidizi ilikwenda kwa Hamis Mpangwa ambaye alijinyakulia kura 11 akimshinda Mohamed Msengi aliyepata kura tisa.

Nafasi ya mweka hazina ilikwenda kwa Kassim Naroho aliyepata kura 16 akimshinda Nickson Haule aliyepata kura nne, kwa upande wa mwakilishi wa mkutano mkuu ilikuwa na mgombea mmoja Hamad Seif ambaye alipata kura 19..

Kwa upande wa kamati ya utendaji nafasi tatu walioshinda ni Kasule Ambogo kura 18, Leah Petro kura 16, Gabriel Kinyogoli kura 15 na Sultan Singa kura nane ambapo mwenyekiti mpya Komba aliwataka waamuzi kuwa na mshikamano.

Komba alisema kuwa jambo kubwa ili waweze kufikia malengo ni kuwa nidhamu na kuzingatia sheria kwa kuzitafsiri wawapo uwanjani ili kuondoa malalamiko dhidi yao kwani baadhi wamekuwa wakienda kinyume na sheria za mchezo huo.


Mwisho.