Tuesday, January 27, 2015

ZAKIA MEGHJI SHEREHE ZA CCM PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MLEZI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Pwani Zakia Meghji anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za (CCM) kutimiza miaka 38 zitakazofanyika Kata ya Visiga wilayani Kibaha.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana mjini Kibaha katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa sherehe hizo zitaadhimishwa kwa shughuli mbalimbali za kuimarisha chama ambazo tayari zilishaanza tangu Januari 26 kwenye kata ya Mkuza.
Mdimu alisema kuwa Meghji ambaye ni Mbunge na Mjumbe wa Halmashauri Kuu (MNEC) atahitimisha sherehe hizo Februari Mosi kwenye kata hiyo ambayo imepewa upendeleo kutokana na chama hicho kuchukua mitaa yote saba kwenye uchaguzi wa wenyeviti wa Mitaa uliofanyika hivi karibuni.
“Wakati wa sherehe hizi kutakuwa na shughuli mbalimbali kama vile kukagua uhai wa chama ngazi ya mashina, matawi, kata wilaya pamoja na uhakiki wa daftari la uanachama ili kuwa na takwimu sahihi za wanachama,” alisema Mdimu.
Aidha alisema kuwa kazi nyingine ni kufanya mikutano ya kuhamasisha wanachama kujitokeza kujiandikisha katika daftarai la wapiga kura msisitizo ukiwa ni kwa wananchi wote wenye sifa kujiandikisha upya hata wale wenye vitambulisho vya kupiga kura miaka iliyopita.
“Tunatarajia Halmashauri kuu za kata zitafanyika kwenye kata hizo za Kibaha Mjini ambazo ni 14 ambapo wajumbe wa mkoa watasambaa kwenye kata hizo kabla ya mkutano mkubwa wa hadhara wa kuhitimisha sherehe hizo ambapo Meghji ndiye atakayefunga akiwa ndiyo mgeni rasmi,” alisema Mdimu.
Aliwataka wanaccm kujitokeza kwa wingi siku hiyo ili kwenda kumsikiliza mlezi wa chama siku hiyo ili waweze kuimarisha chama katika maeneo yao pia kujiandaa na uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili kuhakikisha chama kinapata ushindi mkubwa wa kishindo huku kaulimbiu ya mwaka huu ikisema Umoja ni Ushindi (Katiba Yetu, Taifa Letu).
Mwisho.

  

WANASIASA WASIMWAGE DAMU WAKATI WA UCHAGUZI

Na John Gagarini, Kibaha
WANASIASIA nchini wametakiwa kuwa na hofu ya Mungu na kuacha kutumia lugha za kusema kuwa watamwaga damu wakati wa kipindi cha uchaguzi.
Hayo yalisemwa na Mchungaji wa kanisa la Gosheni Inland Church lililopo kitongoji cha Chamakweza wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Jackson Bukelebe, wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa shule ya awali kituo cha kuhudumia watoto wa wafugaji inayomilikiwa na kanisa hilo.
Mch Bukelebe alisema wao kama kanisa wanataka uchaguzi wa amani na utulivu na hawataki wanasiasa watakaotuvunjia hali ya amani iliyopo na kutuletea vurugu kwani hao hawafai na hawastahili kuwa viongozi na wanapaswa kutumia lugha za ustaarabu na siyo zile zitakazosababisha uvunjifu wa amani ambayo imedumu kwa kipindi kirefu tangu nchi imepata uhuru,
“Viongozi hawa wanapaswa kuwa na hofu ya Mungu na si kuwa na roho ya uharibifu na wakiwa na hofu ya Mungu watakuwa na upendo wa kuwapenda wengine na wataachana na mambo binafsi bali wataangalia mambo ya watu kwa ujumla,” alisema Mch Bukelebe.
Kwa upande wake mgeni rasmi kwenye harambee hiyo mwenyekiti wa CHADEMA Jimbo la Chalinze Mathayo Torongey alisema kuwa muda wa siasa umekishwa kinachotakiwa ni kuhakikisha shughuli za maendeleo zinafanyika ili kuwaondolea wananchi changamoto mbalimbali zinazowakabili.

“Kuhusu uchangiaji wa fedha kwa ajili ya elimu ni muhimu lakini kuna baadhi ya jamii ya wafugaji inaona kama elimu siyo jambo la muhimu hivyo kuwa wagumu kuchangia maendeleo ya elimu,” alisema Torongey.

Torongey ambaye alikuwa mgombe kwenye uchaguzi mdogo wa Jimbo la Chalinze aliwataka wanajamii ya kifugaji kutokuwa wagumu kuchangia elimu na kuacha tabia ya kuwaozesha watoto wao wakike badala yake wawapleke shule.

Awali akisoma risala kwa mgeni rasmi moja ya wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo Amina Simbilwa alisema kuwa wamekuwa wakipata changamoto ya kukosa elimu kutokana na baadhi ya wazazi wao kuhamahama kutafuta malisho.

Shule hiyo ilianzishwa mwaka 2014 kwa lengo la kuwapatia elimu ya awali watoto hao kwani iliyopo iko mbali na wao ambao Kijiji chao ni cha Wafugaji na ina jumla ya wanafunzi 72.


Mwisho.   

Monday, January 26, 2015

MAJAMBAZI WALIOUA ASKARI BADO KUKAMATWA MSAKO WAENDELEA

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la polisi mkoani Pwani,linaendelea na msako mkali wa kuwatafuta watu waliohusika kufanya mauaji ya askari wawili wa jeshi hilo pamoja na kuiba silaha mbalimbali kwenye kituo cha polisi Ikwiriri,wilayani Rufiji .

Pia limekanusha uvumi wa kuwa siku ya tukio hilo kuliwa na askari wengine ambao walikimbia kwa lengo la kujihami baada suala ambalo si la ukweli. 

Kamanda wa polisi mkoani humo kamishna msaidizi mwandamizi Ulrich Matei alisema kuwa hakuna hadi sasa hakuna mtu aliyekamtwa na msako  unafanywa usiku na mchana ili kuhakikisha wanawapata wahusika na kuwachukulia hatua za kisheria.

Aidha Matei aliitaka jamii kuacha tabia ya kuvumisha mambo yasiyo ya ukweli ama kuibua hoja zisizokuwa za ukweli baada ya matukio mbalimbali kutokea na badala yake anaetaka ukweli anatakiwa kuuliza kwa wahusika ili kupata taarifa za ukweli na si vinginevyo.

Wakati huo huo Mkuu wa wilaya ya rufiji Nurdin Babu amesema emesikitishwa na mauaji ya polisi wawili kwenye kituo cha ikwiriri wilayani humo juzi.
Akizungumza na gazeti hili Babu alisema kuwa tukio hilo ni la kusikitsha na halistahili kuungwa mkono na jamii iliyostaarabika.
"Inasikitisha sana na jambo hili ni ukatili na tunalilaani kwa nguvu zote na tutahakikisha tunawasaka watu waliohusika na tukio hili," alisema Babu.
Babu alisema kuwa wanaendelea kufuatilia na kufanya misako kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo ili kubaini waliohusika na tukio hilo la kikatili.
"Kuwaua watu wanaolinda usalama wa raia ni jambo la kusikitisha kwani linakatisha tamaa sana," alisema Babu.
Babu ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya alisema kuwa wananchi wanapaswa kutoa ushirikiano kuhakilisha watu hao wanatiwa mikononi mwa vyombo vya sheria na jeshi la polisi bado linaendelea na uchunguzi kubaini watu waliohusika na tukio hilo.
Mwisho.

HALMASHAURI YA MJI KUJENGA SOKO NA STENDI VYA KISASA

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Mji wa Kibaha inatarajia kuanza mradi mkubwa wa ujenzi wa Soko la kisasa pamoja na Stendi utakaogharimu kiasi zaidi ya shilingi bilioni 20 kuanzia Februari mwaka huu.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Adhu Mkomambo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi na kusema kuwa taratibu za mwisho zinakamilika kuanza ujenzi huo.
Mkomambo alisema kuwa ujenzi huo wa soko na setndi vitakuwa mkombozi kwa wananchi wa Kibaha na mkoa mzima wa Pwani kutokana na kukosa vitu hivyo kwa muda mrefu.
“Pale kuna soko na stendi lakini havina hadhi ya Mji hivyo kupitia benki ya uwekezaji (TIB) tutajenga vitu hivi kwa lengo la kuboresha mji na kuleta maendeleo kwa wananchi wa wilaya ya Kibaha,” alisema Mkomambo.
Aidha alisema kuwa vitu hivyo ni moja ya vyanzo vya mapato ya Halmashauri hivyo ujenzi wake utazingatia ubora na viwango ili kuwa na hadhi kwani soko lililopo halina ubora kulingana na mji wa Kibaha
“Mbali ya miradi hiyo ambayo itaanza kwa pamoja pia Halmashauri itaendelea na miradi yake ya ujenzi wa barabara na uboreshaji wa sekta mbalimbali za jamii ili huduma ziweze kuwa bora,” alisema Mkomambo.
Alibainisha kuwa wataendeleza ushirikiano kati ya Halmashauri yake wananchi pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuendelea kuuboresha mji huo unaoelekea kuwa Manispaa.
Mwisho.  




  

Friday, January 23, 2015

ASKARI ALIYEUAWA AAGWA

Na John Gagarini, Kibaha
KONSTEBO wa Polisi aliyeuwawa na majambazi waliovamia kituo cha Polisi cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani Judith Timoth (32) juzi aliagwa mjini Kibaha na mamia ya watu wakiwemo askari wenzake aliowahi kufanya nao kazi kabla ya kuhamia Rufiji.
Mwili huo uliagwa kwenye hospitali ya Polisi mkoa na kuongozwa na ofisa wa jeshi hilo Thabita Makaranga, kwa safari ya kuelekea mkoani Mbeya kwa ajili ya mazishi  na kuliibua simanzi kubwa kwa watu waliohudhuria tukio hilo na kuvuta hisia na vilio kutoka kwa waombolezaji.
Akiongoza kwenye ibaada ya kumwaga marehemu mwinjilisti wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Maili Moja alikokuwa akisali kabla ya kuhamia wilayani Rufiji, Josephine Urio alisema kuwa watu wanapaswa kujiandaa kwa kusali muda wote kwani hawajui siku wala wakati watatwaliwa.
“Wanadamu wanapaswa kuacha roho za mauaji kama hao waliofanya mauaji hayo kwani hawako salama kama wanavofikiri Mungu atawapa pigo kama walivyotoa roho za watu wasiokuwa na hatia na watu wenye uovu waache njia hizo,” alisema Urio.
Akisoma wasifu wa marehemu moja ya wafanyakazi wenzake Robert Munisi alisema kuwa jeshi hilo litapambana na watu wote waliohusika na tukio hilo na kuliomba kanisa lilisaidie polisi kukabiliana na wahalifu hao na watasimamia amri kumi za Mungu.
Munisi alisema marehemu alizaliwa mkoani Mbeya na kupata elimu ya Msingi na Sekondari na kupata mafunzo ya sheria mkoani Mbeya kisha kujiunga na Chuo cha Mafunzo ya Polisi huko Moshi kuanzia Oktoba 30 mwaka 2004 na kuhitimu Fabruari 25 mwaka 2005 pia alipata mafunzo mbalimbali yakiwemo ya Upelelezi.
Aidha amesema marehemu kabla ya umauti alikuwa akisoma masomo ya Sociology mwaka wa pili Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) ameacha mtoto mmoja wa kiume aitwaye Bryan.Marehemu alivamiwa juzi akiwa kazini na mwenzake majira ya saa 8 usiku na kushambuliwa na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi waliokuwa na silaha na kufariki dunia yeye na mwenzake Koplo Edger Milinga.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAZAZI wa shule ya Msingi Juhudi kata ya Visiga wilayani Kibaha wameulalamikia uongozi wa shule hiyo kwa kuwarudisha watoto wao wanaojiunga darasa la kwanza kwa kushindwa kulipa kiasi cha shilingi 15,000 kwa ajili ya kuwaandikisha.
Moja ya wazazi hao Mabeka Mabeka akizungumza kwenye kikao cha wazazi alisema kuwa wanashangazwa na taratibu za kuwatoza kiasi hicho licha ya kuwa serikali imekataza michango hiyo na kusababisha wazazi kuwa kwenye wakati mgumu kupata fedha hizo.
Mabeka alisema kuwa wanaushangaa uongozi wa shule hiyo kwa  kuwaandikisha wanafunzi wa darasa la kwanza kwa kututoza fedha hizo jambo ambalo ni kinyume cha sheria kwani serikali ilitamka kuondoa michango kwa wanafunzi wanaoanza ili kuondoa kero kwa wazazi.
“Michango hii ni kikwazo kwa wazazi kuwapeleka watoto shule huku serikali ikitaka watoto wote waliofikia umri wa kwenda shule waandikishwe ili waweze kupata elimu ya msingi,” alisema Mabeka.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Theobad Rwegalulila alikiri kuwepo kwa jambo hilo na kusema kuwa limekuwa changamoto kubwa kwa wazazi ambao wamekuwa wakilalamika kupinga malipo hayo ili watoto waweze kupata fursa ya kujiunga na darasa la kwanza.
Naye mwalimu mkuu wa shule hiyo Hawa Mgogolo alikiri kuwepo kwa michango hiyo na kusema kuwa walikubaliana na wazazi kwenye kikao cha wazazi mwaka 2012 lakini anashangaa wazazi hao kuanza kulalamika wakati wao wenyewe walikubali mchango huo.
Mgololo alisema kuwa ni kweli walikuwa wakiwatoza fedha hizo kwa ajili ya matumizi mbalimbali na fedha hizo zinatumika kununulia vitu mbalimbali kama vile chaki, madaftari ya maendeleo na vifaa mbalimbali kwa ajili ya wanafunzi hao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHULE ya Msingi ya Maili Moja iliyopo wilayani Kibaha inakabiliwa na ubovu wa madarasa ambayo yanaweza kuanguka wakati wowote hali ambayo inahatarisha usalama wa wanafunzi na walimu kwenye shule hiyo.
Kutokana na ubovu huo madarasa matano kati ya 11 ndiyo yanayotumika ambapo wanafunzi wanasoma zaidi ya wanafunzi 150 hadi 200 kwenye darasa moja.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kikoa cha dharura cha wazazi kuzungumzia ubovu wa madarasa hayo, mwalimu mkuu wa shule hiyo Reginald Fanuel alisema kuwa madarasa hayo yamebomoka vibaya.
“Madarasa hayo yako kwenye hali mbaya na wakati wowote yanaweza kuanguka na kusababisha maafa kwa wanafunzi na walimu endapo hazitachukuliwa hatua za haraka za kunusuru hali hiyo ambayo sasa imefikia hatu mbaya,” alisema Fanuel.
Fanuel alisema kuwa kutokana na hali hiyo wanaomba msaada wa kusaidiwa ujenzi ili kunusuru hali hiyo ambayo ni hatari kwa wanafunzi na walimu wanaotumia madarasa hayo pia mlundikano kwenye madarasa mazima ni mkubwa sana.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule Said Chitenje alisema kuwa tatizo hilo lilianza muda mrefu ambapo wamekuwa wakiakabiliana na hali hiyo kwa kuchangisha michango wazazi lakini michango imekuwa ikisusua.
“Kweli hali ni mbaya na kutokanana hali kuzidi kuwa mbaya tumekubaliana na wazazi kuwa kila mzazi ambaye ana mwanafunzi shuleni hapa atoe kiasi cha shilingi 5,000 kwa ajili ya kufanya ujenzi wa madarasa hayo,” alisema Chitenje.
Naye diwani wa kata ya Maili Moja Andrew Lugano alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ujenzi wa madarasa hayo yaliyoharibika ili kuwanusuru wanafunzi hao.
Lugano alisema kuwa wazazi hao waliomba wakutane na mkurugenzi wa halmashauri ya Mji ili wazungumzie suala hilo na namna ya kuwez akukabiliana na tatizo hilo na kuwaomba watu na wafadhilimbalimbali kujitokeza kusaidia ujenzi wa majengo hayo.

Mwisho.  

Wednesday, January 21, 2015

MAJAMBAZI YAUA ASKARI WAWILI

Na John Gagarini, Kibaha

ASKARI wawili wa Jeshi la Polisi Kituo cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani wamekufa baada ya watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kuwashambulia kwa silaha baada ya kuvamia kituo hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya simu toka eneo la tukio Ikwiri wilayani Rufiji Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alisema kuwa majambazi hao walitumia silha kuwaua askari hao.

Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 8 kwenye kituo hicho cha Polisi cha Ikwiriri. Aliwataja askari waliokufa kuwa ni usiku Askari waliokufa ni namba E 8732 CPL Edger Milinga na WP 5558 PC Judith Timoth.

Alisema kuwa licha ya kufanya mauaji hayo pia walifanikiwa kupora silaha aina mbalimbali zikiwemo SMG 2, SAR 3, Ant Riot 1, mali ya serikali na S/Gun Protector mali ya kampuni ya Sigara Tanzania.

Aidha alisema kuwa pia watu hao waliharibu kwa kulipiga risasi gari la polisi la kituo  hicho lenye namba za usajili PT 1965.


Mwisho.

Wednesday, January 14, 2015

MRADI WAMI CHALINZE KUNUFAISHA 271,000

Na John Gagarini, Chalinze

MRADI wa Maji wa Wami Chalinze awamu ya tatu  mara utakapokamilika unaratajia kuwafikia wananchi 271,000 wa Jimbo la Chalinze wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani.

 Aidha mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni 60 unatarajia kuanza mwezi Machi mwaka huu utapunguza tatizo la upatikanaji wa maji kwa wakazi wa Chalinze ambao wanahudumiwa na mradi huo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Meneja wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) Mhandisi Christer Mchomba alisema katika awamu hiyo itaongeza mitandao ya maji kwenye vitongoji 210 kutoka kwenye vijiji 47 ambavyo vilifikiwa kwenye utekelezaji wa awamu ya pili iliyoanza mwaka 2008.

 “Katika awamu ya tatu ya mradi huu yatajengwa pia matenki ya kuhifadhia maji kwenye vijiji 20 vya awamu ya kwanza kikiwamo kijiji cha Bwiringu, Msata, Lugoba, Msoga, Mandela na vingine ambavyo havikujengewa matenki,” alisema Mhandisi Mchomba.

Mhandisi Mchomba alisema kwa sasa awamu ya pili ,wizara inakamilisha ujenzi wa nyongeza ya chujio la maji ambalo litaongeza wingi wa maji yanayosafishwa na kuzalishwa.

Alisema kuwa watajenga tanki kubwa eneo la Mazizi lenye uwezo wa kuhifadhi maji yenye ujazo wa lita 200,000 pamoja na vituo vya maji kwenye vijiji na vitongoji vyote kwenye Jimbo hilo.

“Kwa sasa wanazalisha maji kwa asilimia 85 tu kutokana na mashine kushindwa kufanya kazi kikamilifu ambapo kwa siku ni mita za ujazo 2,000 badala ya 5,000 kwa siku,” alisema Mhandisi Mchomba.  

Kwa upande wake ofisa maabara wa mradi huo Riziki Kacheche alisema  kuwa maji ghafi yanapokuwa machafu zaidi tope huziba na kuzuia maji kuchukuliwa katika kiwango kinachotakiwa kwenda kusafishwa na hivyo kusabababisha uwezo wa kuzalisha maji na kuyasafisha kuwa mdogo.

Mwisho