Sunday, October 8, 2017

UJENZI WA BANDARI KAVU KWALA KIBAHA KUPUNGUMZA MSONGAMANO



Na John Gagarini, Kibaha

IMEELEZWA kuwa ukamilikaji wa Bandari Kavu ya Kwala wilayani Kibaha mkoani Pwani itasaidia kupunguza msongamao wa malori Jijini Dar es Salaam kwani makontena yote yanayoingia nchini hayatashushwa kwenye Bandari ya Dar es Salaam badala yake yatashushwa kwenye bandari mpya ya Kwala.

Kutokana na ujenzi huo wa Bandari Kavu ya Kwala mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha kupanga mipango mji kwenye Kijiji hicho cha Kwala kwani sasa inaenda kuwa Mji.

Ndikilo aliyasema hayo alipotembelea mradi huo ambao ulianza mwezi Machi mwaka huu ukiwa na thamani ya shilingi bilioni 7.2 ukijengwa na kampuni ya kizalendo ya Suma JKT chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA).

“Halmashauri mnapaswa kuhakikisha mnaweka mipango miji kwenye eneo hilo ili kusiwe na ujenzi holela pia kuwe na huduma zote kuanzia mahoteli sehemu ya magari kusubiria siyo zije kujengwa na watu binafsi, polisi, mabenki na huduma nyingine muhimu,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa Hlmashauri isisubiri hadi mradi uishe ndiyo ianze kuweka mipangomiji kwani wanatakiwa kwenda sambamba na ujenzi wa mradi ili kuwe na mpangilio mzuri.

“Hichi kitakuwa kitovu cha biashara na kutakuwa na shughuli nyingi hivyo lazima kuwe na mpangilio mzuri wa ujenzi kwani hata barabara ya kuja huku ni mbaya lazima mamlaka zinazohusika zianze kuboresha mazingira na mara kazi zitakapoanza mwakani serikali ijipatie mapato,” alisema Ndikilo.

Naye Meneja mradi Mhandisi Raymond Kweka alisema kuwa wanatarajia kukamilisha Novemba 30 mwaka huu kwa awamu ya kwanza ujenzi huo ambao unaendelea vizuri ukiwa umefikia asilimia 85 kwenye eneo la mradi lenye ukubwa wa hekta zaidi ya 150.

Kweka alisema kuwa baadhi ya changamoto kubwa ni mvua baada ya barabara ya Vigwaza Kwala kukatika na maji kujaa kwenye eneo la mradi, maji yanatoka mbali ambapo mwanzo walitegemea bwawa jirani na mradi ambao limeendelea kukauka na kukosa maji.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmshauri ya wilaya ya Kibaha Beda Mbaga alisema kuwa wanatarajia kuanza kupitia maeneo yanayozunguka mradi huo ili kuweka mipangomiji kuanzia wiki hii kwa 


Mwisho.

WAANDISHI WA HABARI NCHINI WAASWA










Na John Gagarini, Kibaha

WAANDISHI wa Habari mkoani Pwani na hapa nchini wametakiwa kutotumia vibaya kalamu zao ili kulinda amani ya nchi kwani maneno yao endapo yatatumika vibaya ni hatari zaidi ya bunduki.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama wakati akifungua kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Pwani mafunzo juu ya Haki za Binaadamu Utawala Bora na Amani nchini kwa Viongozi na watumishi wa serikali za mitaa mkoa wa Pwani yaliyoandaliwa na Alpha And Omega Reconciliation And Peace Building (AREPEB).

Mshama alisema kuwa waandishi wana nafasi kubwa ya kudumisha amani iliyopo kwa kutumia vyema kalamu zao katika kuleta mshikamano na kuepusha utengano.

“Nyie ndiyo mnanafasi kubwa ya kuifanya nchi iendelee kuwa na amani au mnaweza kuifanya nchi ikaingia kwenye machafuko hivyo mnatakiwa kutumia vizuri kalamu zenu kwa kutotumia vibaya kalamu zenu,” alisema Mshama.

Alisema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia viongozi hao kuwahamasisha wananchi kulinda amani ya nchi na kutokubali kuingia kwenye migogoro ambayo itasababisha amani kuvunjika.

“Tanzania bado tuna amani kubwa na ya kutosha hatuna sababu ya kuleta vurugu kwani nchi inatawaliwa kwa utawala wa sheria lakini kuna baadhi ya watu wanataka kutuingiza kwenye matatizo,” alisema Mshama.

Naye mkurugenzi wa  (AREPEB) Francis Luziga alisema kuwa lengo lao kubwa ni kujenga amani hapa nchini kwa kubadilishana uzoefu na viongozi na watendaji wa serikali za mitaa na wasimamizi wa watekelezaji wa sheria katika masuala ya haki za binadamu na utawala bora.

Luziga alisema kuwa pia mafunzo hayo yameambatana na uzinduzi wa mfumo wa kieletroniki wa kupokea maoni na malalamiko dhidi ya masuala mazima ya haki za binadamu.


Mwisho. 

MKUU WA WILAYA KIBAHA ATOA MAAGIZO MAZITO KWA WATENDAJI




Na John Gagarini, Kibaha

MKUU wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama amesema kuwa serikali inawafanyia tathmini watendaji wa mitaa vijiji na vitongoji na wale ambao watashindwa kufikia vigezo wataondolewa ili kupisha wale wenye weledi wafanyekazi ili kuwaletea maendeleo wananchi.

Ameyasema hayo mjini Kibaha wakati wa mkutano na viongozi hapo pamoja na wenyeviti kwenye Halmashauri za Mji na wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha na kusema baadhi ya watendaji wamekuwa hawawajibiki ipasavyo.

Nao baadhi ya wenyeviti walielezea changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili kwenye maeneo yao.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Marco Njau alikiri kuwepo kwa baadhi ya changamoto.

Naye kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Beda Mbaga amesema kuwa watakabili changamoto zilizo kwenye eneo lao ili kuleta maenedeleo kwa wananchi.

Naye Ernest Shalua ambaye ni mwakilishi wa Kamanda wa Polisi wilaya ya Kibaha amesema kuwa ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa watuhumiwa lazima viongozi na wananchi watoe tushahidi kwenye matukio mbalimbali.

mwisho.  



Saturday, October 7, 2017

CCM WILAYA YA BAGAMOYO YAPATA MWENYEKITI MPYA










Na John Gagarini, Bagamoyo

ABDUL Zahoro Sharifu amechaguliwa kuwa mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani baada ya kumshinda aliyekuwa mwenyekiti Alimasi Masukuzi.

Uchaguzi huo ambao ulifanyika Msata wilayani humo Sharifu alimshinda mpinzani wake kwa kupata kura 711 dhidi ya kura 383 za Masukuzi huku Tariq Kafuku akipata kura 185 na nafasi ya Katibu Mwenezi ilikwenda kwa John Francis maarufu kama Bolizozo aliyepata kura 112 akimshinda Hassan Sharifu aliyepata kura 4.

Kutokana na ushindi huo Sharifu amesema kuwa chama ndiyo kilichoshinda na siyo yeye na kuwataka wagombe na wanachama kuwa kitu kimoja ili kukijenga chama kwa ajili ya kuendelea kushika dola.

“Kuanzia sasa hakuna makundi makundi yamekwisha baada ya uchaguzi na kila mtu anahaki ya kuwa na mgombea anayempenda lakini kwa kuwa mshindi kashapatikana hakuna sababu ya kuwa na makundi,” alisema Sharifu.
Alisema kuwa baada ya uchaguzi kwisha malengo yake ni kujenga chama kwa kuanzisha vitega uchumi na kuachana na tabia ya kutegemea kuomba fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli za chama.

“Furaha yangu ni kuona chama kinajitegemea chenyewe kwa kujiendesha kwani kina miradi mingi na endapo itasimamiwa vizuri itakiletea manufaa chama,” alisema Sharifu.

Kwa upande wake Bolizozo alisema kuwa kwa kutumia nafasi yake atahakikisha anashirikiana na viongozi na wanachama kuleta maenedeleo ya chama ili kiweze kwenye chaguzi kuanzia ya serikali za mitaa 2019 na uchaguzi mkuu 2020.

Mwisho.


CCM KIBAHA MJINI WACHAGUA VIONGOZI WAKE








Na John Gagarini, Kibaha

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kibaha Mjini Mkoani Pwani Maulid Bundala amefanikiwa kutetea kiti chake baada ya kushinda kwenye uchaguzi wa chama hicho.

Bundala alifanikiwa kutetea nafasi yake hiyo kwa kipindi cha awamu tatu sasa baada ya kushinda kwenye uchaguzi ambao ulifanyika kwenye shule ya sekondari ya Filbert Bayi mjini Kibaha na kuwashinda wenzake wawili.

Wajumbe wa mkutano huo mkuu wa CCM Kibaha Mjini walimpa ushindi wa kishindo Bundala kwa kumpigia kura 288 kati ya kura 489 za wajumbe wote huku kukiwa hakuna kura iliyoharibika.

Aliyemfuatia mshindi alikuwa ni Batholomew Nyalusi ambaye alipata jumla ya kura 164 akifutaiwa na Joseph Masenga ambaye alipata kura 37.

Kwa upande wa uwakilishi wa mkutano mkuu wa mkoa washindi wawili walikuwa ni Rugemalila Rutatina kura 392 na Happines Mgalula kura 201 kwa upande wa uwakilishi Halmashauri Kuu wilaya wajumbe wawili ni Kabunda Bekari kura 238 na Philemon Mabuga  kura 209.

Nafasi nne za uwakilishi toka Umoja wa Vijana (UVCCM) nafasi nne ni Makwiro selaman kura 289, magreth Mbawala kura 283, Herman Kagaruki kura 269 na Jagala Salum kura 233.

Kwa upande wa uwakilishi Jumuiya ya Wanawake (UWT) nafasi nne washindi walikuwa ni Zamda Komba kura 276, Dk Alice Karungi kura 255, Joyce Mushi 230 na Joyce Shauri kura 185.

Washindi wa nafasi tatu za uwakilishi mkutano mkuu wa Taifa ni Abdulaziz Jaad kura 355, Catherine Katere kura 336, Dk Alice Kaijage 332 ambapo katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema uchaguzi huo ulikwenda vizuri na hakukuwa na malalamiko yoyote kutoka kwa wagombea.


Mwisho.

WAFANYABIASHARA MKOA WA PWANI WAFANYA UTALII WA NDANI MIKUMI















Na John Gagarini, Morogoro

WAFANYABIASHARA nchini wametakiwa kuungana na Serikali katika kutangaza vivutio vya Utalii ili kuongeza idadi ya watu wanaotembelea vivutio hivyo na kuongeza pato la Taifa kupitia utalii.

Hayo yalisemwa Mikumi na Abdala Ndauka mwenyekiti wa Jumuiya ya wafanyabiashara Tanzania (JWT) mkoa wa Pwani wakati waliotembelea Mbuga ya wanyama ya Mikumi iliyopo mkoani Morogoro.

Ndauka alisema kuwa wafanyabiashara wananafasi kubwa ya kutangaza vivutio vya Utalii vilivyopo nchini ambavyo havipatikani sehemu yoyote duniani kupitia bidhaa zao wanazozalisha.

“Sisi jumuiya ya wafanyabishara mkoa wa Pwani tumeamua kufungua ukurasa kwa wafanyabiashara kutembelea vivutio vya utalii ambavyo vinavutia watalii wengi nchini na duniani,” alisema Ndauka.

Alisema kuwa ili vivutio vya utalii vitambulike wafanyabishara wana nafasi kubwa ya kuvitangaza na kuongeza watalii wa ndani na nje ya nchi.

“Kwa kuja kwetu huku kuangalia vivutioo hivi tumeweza kujifunza na kuona mengi ambayo tulikuwa tukiyasikia na kuona kupitia vyombo vya habari lakini tumeona wenyewe kwa macho yetu wanyama kama vile Simba,Tembo Swala, Twiga, Nyati, Pundamilia,Viboko na Mamba,” alisema Ndauka.

Aidha alisema kuwa watalii wa ndani wanapaswa kutapembelea vivutio mbalimbali vilivyopo nchini kwani gharama za kuingia kwa sasa zimepungua japo zinapaswa kupungua zaidi ili watu wengi waweze kutembelea.

Kwa upande wake Salugroli Masaga alisema kuwa kwa kutembelea Mbuga hiyo ya Mikumi ameweza kujifunza mambo mengi ikiwiwa ni pamoja na fursa zilizopo kwa wafanyabiashara.

Masaga alisema moja ya fursa ambazo aliziona ni wafanyabiashara kufanyabiashara mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuanzisha migahawa, uuzaji bidhaa za kitalii kama mikufu hereni na mavazi yanayotengenezwa hapa nchini.

“Mbali ya kuona wanyama tumepata fursa ya kujua tabia zao na maisha yao ambayo ni kivutio kikubwa kwani baadhi ya wanyama wanaonekana kama wana tabia tofauti ambazo ni faida kwa wengine,”  alisema Masaga.


Aliwataka wafanyabiashara, vikundi na watu mmojammoja kutembelea pia kutangaza biashara zao kwa kutangaza vivutio hivyo vya kitalii adimu duniani.

Mbuga hiyo ilianzishwa mwaka 1964 ikiwa na ukubwa wa kilometa za mraba 1,070 na iliongezwa ukubwa na kufikia kilometa za mraba 3,200 mwaka 1975 ikiwa ni ya tano kwa ukubwa kwa Mbuga za Taifa.

Mbuga inayoongoza ni Ruaha yenye ukubwa wa Kilometa za mraba 20,226, Serengeti yenya ukubwa wa Kilometa za mraba 14,763 na Mkomazi yenye ukubwa wa Kilometa za mraba 3,245 ikiwa na wanyama wakubwa aina nne kati ya tano ambao ni Simba,Tembo, Nyati na Chui

Mwisho.  

MAMIA YA WANANCHI WALILIA AJIRA WAMOMBA RC AWASAIDIE






Na John Gagarini, Kibaha

MAMIA ya wananchi wa wilaya ya Kibaha na mkoa wa Pwani wamelilia mkuu wa mkoa huo Mhandisi Evarist Ndikilo awasidie kupata ajira wazuia msafara wake kwa mabango kwenye kituo cha ujenzi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro kilichopo kwenye Kijiji cha Soga inayojengwa na kampuni ya Yapi Merkezi ya nchini Uturuki.

Wananchi hao walifikia hatua hiyo wakati mkuu wa mkoa wa Pwani akiwa na kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa ilipotembelea kujionea ujenzi huo ambao tayari umeanza na kusema kuwa watu wa mkoa huo wamekuwa wakibaguliwa na kuajiriwa watu kutoka Jijini Dar es Salaam zaidi wananchi hao.

Kwa upande wa Rukia Ally amesema kuwa wametumia gharama kubwa kujenga mabanda wanayofanyia biashara hiyo ya chakula na wamekopa mikopo kwenye taasisia za kifedha hali ambayo inawapa wasiwasi huenda wakauziwa mali zao.

Ally amesema kuwa wanahofu kuuziwa mali zao kwani watashindwa kurudisha fedha walizokopa kwa ajili ya kujenga mabanda na kunuanua bidhaa kwa ajili ya biashara hiyo hivyo kumwomba mkuu wa mkoa kuwasaidia ili kampuni hiyo iruhusu waendelee kupata huduma ya chakula nje na si ndani kwa mzabuni.

Kwa upande wake meneja mradi kutoka kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) Mhandisi Maizo Mgedzi amesema kuwa wao wanaajiri kutokana na sifa za waombaji ambao wengi ni madereva na waendeshaji wa mitambo.
Kutokana na malalamiko hayo mkuu huyo wa mkoa wa Pwani ametoa siku saba kwa vyombo vya dola kufutailia suala la rushwa kama lipo na kutaka wahusika waliotajwa na wananchi hao kusimama kupisha uchunguzi.

Aidha ametaka kupelekewa majina ya watu waliajiriwa kama wanatoka mkoa wa Pwani au la kwani serikali imekuwa ikitaka wanufaika wa kwanza wawe wanaoishi kwenye eneo la mradi.

Pia ametaka utaratibu wa chakula nao uangaliwe ili akina baba na mama lishe walioko nje ya eneo hilo la mradi huo waruhusiwe kuendelea kufanyabishara badala ya kuwazuia wafanyakazi wasitoke nje baada ya kupewa mazabuni kwa ajili ya kuwapa chakula.

Naye mwakilishi wa mkandarasi wa kampuni hiyo Merz Oz alisema kuwa waliamua kuacha utaratibu wa wafanyakazi wao kula chakula nje kwa madai kuwa wanatumia muda mwingi na kufanya shughuli kushindwa kufanyika kwa wakati.

Oz alisema kuwa sababu nyingine ni kuhakikisha wafanyakazi wanapata chakula chenye ubora hasa ikizingatiwa kampuni yao ni ya kimataifa hivyo haiwezi kuwaacha wafanyakazi wao wanakula bila ya utaratibu na huwapatia bure chakula hicho jambo ambalo lilipingwa na wananchi.

Mwisho.