Thursday, July 27, 2017

AOMBA WALIMU WA SEKONDARI HURIA WAPEWE MOTISHA

Na John Gagarini, Kibaha

SERIKALI imeombwa kuwalipa walimu wanaofundisha vituo vya shule huria ambazo ziko chini ya Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima ili kuwapa motisha walimu hao.

Hayo yalisemwa na meneja wa shule ya Pangani Remedial Open School iliyopo wilayani Kibaha Ally Mohamed na kusema kuwa kuwalipa walimu hao itakuwa moja ya motisha kuwafanya wafundishe kwa moyo.

Mohamed alisema kuwa shule hizo zimekuwa mkombozi kwa wanafunzi ambao wamekosa nafasi za kwenda shule za sekondari na watu wazima waliokosa nafasi hiyo.

“Shule hizi ambazo zamani zilikuwa ni kwa ajili ya watu wazima kwa sasa zimeboreshwa na zinatoa elimu ya sekondari kama kawaida na wanapofaulu mitihani ya kidato cha nne wanakwenda kidtao cha tano kama wale walio kwenye mfumo rasmi hivyo kuna haja ya walimu wake kulipwa kama walimu wenzao wa shule za serikali,” alisema Mohamed.

Alisema kuwa walimu hao kwa sasa wanalipwa na shule hizo lakini kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakijitolea kwani uwezo wa kuwalipa mishahara hawana ambapo Taasisi hiyo imekuwa ikisimamia mitihani ya Kujipima huku ile ya kidato cha pili na ile ya kidato cha nne ikisimamiwa na Baraza la Mitihani la Taifa (NACTE).

“Shule hizi kwa sasa zimekuwa mkombozi kwa wanafunzi hao ambao zamani walikuwa hawana pa kwenda hivyo tunaomba serikali kuliangalia suala la kuwalipa walimu hao ili kuwapa hamasa ya kufundisha ili kuongeza ufaulu kwa wanafunzi wa shule hizo,” alisema Mohamed.

Alisema kuwa mfumo huo uliboreshwa mwaka 2014 ambapo ulisajili vituo hivyo ambavyo vinachukua wanafunzi ambao walishindwa kuendelea na masomo kama vile ukosefu wa ada, mimba, mazingira magumu, yatima na watu wazima waweze kujiendeleza.

Aidha alisema kuwa kwa sasa zinachukua wanafunzi wenye umri kati ya miaka 12 hadi 24 ambao wanasoma kwa miaka minne huku wale wenye kuanzia miaka 25 husoma kwa miaka miwili,shule hiyo ilianza mwaka 1997 na ina wanafunzi 100.

Mwisho.


GARI LATUMBUKIA MTO WAMI WAWILI WAFA

                                   
                                         Na John Gagarini,Kibaha

MADEREVA wawili wamekufa baada ya gari walilopanda kugonga kingo za daraja la mto wa wami na kuangukia mtoni

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kamanda wa polisi mkoa wa Pwani Jonathan Shana amesema kuwa gari lililopata ajali ni mali ya kampuni ya Usangu Logistics.

Shana amesema kuwa ajali hiyo ilitokea majira ya saa saba usiku na kulihusisha gari lenye usajili namba T 857 ARP aina ya Scania likiendeshwa na Yahaya Karimu miaka kati ya (30)  na (35) akiwa na dereva mwenzake ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja likitokea Dar es Salaam kwenda Arusha.

Amesema kuwa chanzo cha ajali hiyo ni breki za gari hilo kukatika na kugonga kingo za daraja hilo kisha kuanguka mtoni 

Na John Gagarini, Kibaha

MTU mmoja aliyetambulika kwa jina la Mwesigwa Mberwa (23) amekutwa amekufa kwenye nyumba ya kulala wageni ya Msukuma iliyopo Mlandizi wilayani Kibaha.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana zimesema kuwa marehemu alikuwa amelala chumba namba 38.

Shana amesema kuwa tukio hilo lilitokea Julai 22 majira ya saa 12 jioni eneo la kitongoji cha Usalama wilaya ya Kipolisi Mlandizi ambapo marehemu alipanga kwenye nyumba hiyo tangu Julai 19.

Amebainisha kuwa muhudumu Kulekwa Kulwa ndiye aliyegundua kufa kwa marehemu baada ya kutia mashaka kutokana na kutomwona kutoka nje mteja wake tangu alipoingia na kwenda kutoa taarifa polisi.

Amesema kuwa polisi walipofika kwenye chumba hicho iliwabidi kuvunja mlango na kuukuta mwili wa marehemu ukiwa hauna jeraha lolote mwilini mwake na kupelekwa hospitali Teule ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi na ulifanyiwa uchunguzi na utakabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

ABIRIA waliokuwa wakisafiri na basi la kampuni ya Tashirifu waliokuwa wakisafiri kutokea Dar es Salaam kwenda mkoani Tanga wamenusurika kifo baada ya basi hilo kuwaka moto.

Kwa mujibu wa taarifa ya kamanda wa polisi mkoani Pwani kwa vyombo vya habari Jonathan Shana imesema kuwa basi hilo liliteketea lote na moto huo haukuleta madhara yoyote kwa binadamu na kusababisha hasara ikiwemo mizigo ya abiria.

Kamanda Shana amesema kuwa ajali hiyo ilitokea Julai 22 majira ya usiku eneo la Kwa Zoka kata ya Vigwaza wilaya ya Kipolisi Chalinze barabara kuu ya Dar es Salaam Morogoro.

Amesema kuwa basi hilo lenye namaba za usajili T 681 DFX aina ya Yutong lilikuwa likiendeshwa na dereva aitwaye Salum Issa (42) liliwaka moto hata hivyo chanzo cha moto huo hakikuweza kufahamika mara moja na polisi wanaendelea na uchunguzi kujua chanzo cha moto huo.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia watu sita kwa tuhuma za kuchoma moto nyumba za watu watatu na kusababisha hasara ikiwa ni pamoja na pikipiki mbili zenye thamani ya shilingi milioni 3.8

Kamanda wa polisi mkoani humo Jonathan Shana amesema kuwa mbali ya kuchoma nyumba hizo pia waliingia kwenye mazizi na kuchinja ngombe ambao idadi yao haijajulika kisha kuondoka na nyama na kubakiza utumbo.

Shana amesema kuwa tukio hilo lilitokea Kijiji cha Vikumburu kata ya Vikumburu Tarafa ya Chole wilaya ya Kisarawe ambapo hata hivyo haikuweza kufahamika chanzo cha uhabifu huo wa mali ambao thamani yake haijajulikana.

Amewataja watu waliochomewa nyumba zao kuwa ni Joseph Simboyi (55), Rebeka Yona (23) na Selina Simon (28).

Aidha amewataja watuhumiwa wa tukio hilo kuwa ni Abdala Shomary (53), Omary Athuman (42) Seifu Shomary (38), Uzalimata Selasela (36) Salum Shomary (40) na Jumanne Omary (49) wote wakazi wa Vikumburu.


Mwisho. 

AUWAWA NA WANANCHI HASIRA KWA TUHUMA WIZI WA BODABODA

                                   
                                      Na John Gagarini,Kibaha

MTU mmoja anayedhaniwa kuwa ni jambazi mmoja ameuwawa na wananchi wenye hasira kali kwa kupigwa kisha kuchomwa moto kwa tuhuma za kupora pikipiki.

Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana alisema kuwa kuwa tukio hilo lilitokea Julai 23 majira ya saa 1:45 usiku kitongoji cha Amani kata ya Kerege tarafa ya Yombo wilaya ya Bagamoyo.

Kamanda Shana alisema kuwa marehemu akiwa na wenzake watatu wakiwa na silaha inayodhaniwa kuwa ni bastola walimvamia mwendesha pikpiki aitwaye Mbaraka Joel (25) mkazi wa Amani walimpora pikipiki yake yenye namba za usajili T 852 BRA aina ya Sanlg.

“Watu hyao kabla ya kufanya uporaji walimsimamisha wakijifanya kuwa ni abiria lakini ghafla walimbadilikia kwa kufayatua risasi mbili hewani na kumtaka awape pikipiki ambayo aliiachia na kutoweka nayo kusikojulikana,” alisema Shana.

Alisema baada ya taarifa kulifikia jeshi la polisi wilaya ya Bagamoyo waliendesha msako mkali kwa kushirikiana na wananchi kupitia vikundi vyao vya ulinzi shirikishi kwenye maeneo mbalimbali likiwemo eneo la Mtambani.

“Wananchi hao waliweza kuwakurupusha watu hao wakiwa wanapanga mipango ya kwenda kufanya uhalifu sehemu nyingine na kutokana na idadi ya wananchi kuwa kubwa watu hao walikimbia na kutelekeza pikipiki mbili moja walioipora kwa Joel na nyingine yenye namba za usajili T MC 972 AJM aina ya Boxer,” alisema Shana.

Aidha alisema kuwa wananchi hao waliendelea kuwakimbiza na kufanikiwa kumkamata marehemu ambapo walimpiga kwa mawe na marungu kisha kumchoma moto na kupoteza maisha papo hapo.

“Wananchi hawapaswi kujichukulia sheria mikononi kwa kuwaua wahalifu wanapaswa kuwakabidhi polisi kwa ajili ya hatua za kisheria pia wataweza kubaini mtandao wa wizi kuliko kuwaua,” alisema Shana.

Mwisho.


MWANAMKE AUWAWA KINYAMA

                                      
                                         Na John Gagarini, Kibaha

MWANAMKE mmoja ambaye ni mfanyabiashara Mariamu Omary (31) mkazi wa Mtaa wa Muharakani wilayani Kibaha mkoani Pwani ameuwawa kwa kupigwa na kitu kizito kichwani.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na Blasius Chatanda kwa niaba ya kamanda wa polisi mkoani Pwani alisema kuwa marehemu aliuwawa na watu wasiofahamika.

Kamanda Chatanda alisema kuwa tukio hilo lilitokea eneo la Kwa Mathias majira ya saa 7 usiku umbali wa mita 40 toka kwenye nyumba aliyokuwa akiishi.

“Marehemu alikutwa asubuhi huku akiwa amevuja damu nyingi sehemu za usoni na kichwani na alikutwa na jeraha kubwa kichwani upande wa kushoto,” alisema Chatanda.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa wa Muharakani Hamis Mwarizo alisema kuwa marehemu alipigiwa simu usiku na mtu ambaye jina lake linaonekana kwenye simu ya marehemu.

Mwarizo alisema kuwa waliingia kwenye chumba cha marehemu na kuzikuta simu zake mbili na moja inaonyesha ilipigwa usiku huo na inaonekana baada ya kupigiwa ndipo alipotoka ndipo alipokutwa na umauti.

Naye mama mwenyenyumba Miriamu John alisema kuwa marehemu alikuwa ni mgeni kwenye nyumba yake akiwa na miezi akiwa na miezi miwili tu na siku ya tukio hawakuweza kusikia kitu chochote.

Mwisho.


MBUNGE ATOA MAGARI MAWILI YA KUBEBA WAGONJWA

Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa kulia akimkabidhi kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha Beda Mmbaga funguo za magari mawili ya kubebea wagonjwa na moja liliotolewa na Rais Dk John Magufuli kwa vituo vya afya vya Halmashauri hiyokulia ni mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mansour Kisebengo.
 
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiwasha gari lililotolewa na Rais Dk John Magufuli kwa ajili ya kituo cha Afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani wanaoshuhudia ni Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha na mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya Mansour Kisebengo.
Vitanda vitatu vya kuzalishia wanawake wajawazito vilivyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa kwa ajili ya vituo vya afya vya Jimbo hilo. 

POLISI PWANI WAKAMATA VIFAA VYA UVUVI HARAMU




                          Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia Makamba Sixbert (32) na Doto Mwinyi (45) wakazi wa Mlingotini wilayani Bagamoyo kwa tuhuma za kukutwa na vifaa vya uvuvi haramu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana alisema kuwa watu hao walikamatwa kwenye msako.

Shana alisema kuwa mtuhumiwa Sixbert  na Mwinyi walikamatwa Julai 25 majira ya saa 8 usiku maeneo ya Mlingotini kata ya Zinga baada ya msako maalumu wa makosa mbalimbali ukihusisha askari wa Jeshi la polisi wilaya ya Bagamoyo, Polisi Makao makuu, Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na maofisa uvuvi na mifugo wa wilaya hiyo.

“Mtuhumiwa huyo wa kwanza alikutwa na Scoopy Net moja, vioo vya kuogelea vitatu, mitarimbo mitatu, bunduki moja ya kuulia samaki, mikuki ya kuulia samaki mitatu na viatu vya kuogelea (Slipers) pea tatu huku mtuhumiwa wa pili akishikwa na Cylinder Gas walivyokuwa wakivitumia kwenye uvuvi haramu,” alisema Shana.

Kwenye tukio lingine madereva wawili wa pikpiki Juma Ally (37) na Mduga Agustino (25) kwa tuhuma za kupatikana na mitambo mitano ya kutengenezea pombe ya Moshi maarufu kama Gongo.

Kamanda Shana alisema kuwa tukio hilo limetokea Julai 25  majira ya saa tano asubuhi maeneo ya Lugoba kata ya Lugoba wilaya ya Kipolisi Chalinze wilayani Bagamoyo.

“Madereva hao wa pikipiki pia walikutwa na pombe ya Moshi lita 40 na lita 60 za Molasesi wakiwa wamezipakiza kwenye pikipiki yenye namba za usajili T 399 BHS aina ya Sanlg,” alisema Shana.

Aidha walifanikiwa kuwakamata Ahmada Hassan (45) mkazi wa Gogoni na wenzake watano kwa tuhuma za wizi wakiwa na Sabufa aina ya Kodec inayodhaniwa kuwa ni ya wizi.

Shana alisema watu hao walikamatwa maeneo ya Dunda kata ya Dunda Tarafa ya Mwambao wakituhumiwa kujihusisha na matukio ya uhalifu ikiwa ni pamoja na uporaji nyakati za usiku kwenye maeneo mbalimbali wilayani

“Misako wanayoifanya ni endelevu na askari shupavu wametawanywa kila kona kuhakikisha hali ya amani inakuwepo kwenye makazi ya wananchi na sehemu za biashara,” alisema Shana.

Aliwataka watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu kuacha mara moja kwa kutafuta shughuli nyingine za kufanya za kuwaingizia kipato halali kwani hawatasita kuwachukulia hatua kali za kisheria.

Mwisho 


WAZIRI WA AFYA ARIDHIA MLANDIZI HOSPITALI WILAYA





                                       Na John Gagarini, Kibaha

WAZIRI wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amekubali maombi ya Kituo cha Afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani kuwa Hospitali ya wilaya.

Alitoa tamko hilo kwenye uwanja wa Mtongani Mlandizi wilayani Kibahya wakati akipokea Magari mawili ya kubeba wagonjwa na vitanda vitatu vya kuzalishia mama wajawazito kutoka kwa Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa na gari moja kutoka kwa Rais Dk John Magufuli.

Alisema kuwa ombi lililotolewa na Mbunge huyo kwa viongozi wa ngazi za juu na kwake amelikubali hivyo mganga mkuu wa wilaya anapaswa kuandika barua na kuzipeleka sehemu husika kisha zifikishwe wizarani kwa ajili ya utekelezaji.

“Mbunge wenu amekuwa akipigania kituo hichi kwa muda mrefu kama alivyosema hivyo naona hakuna kipingamizi ili mradi tu taratibu zifuatwe ili kufikia hatua hiyo lengo kubwa ni kuboresha huduma kwa wananchi,” alisema Mwalimu.

Awali mbunge wa Jimbo hilo Hamoud Jumaa lisema kuwa maombi hayo alishayatoa kwa viongozi mbalimbali ikiwemo kwa Rais wa Awamu ya nne Dk Jakaya Kikwete na Rais Dk John Magufuli.
Jumaa alisema kuwa kituo hicho kwa sasa kinahudumia watu wengi tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo kwa sasa wanakaribia watu 100,000 hivyo kuna haja kabisa ya kuwa hospitali ya wilaya.

“Tuliambiwa tufanye maboresho mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujenga jengo la upasuaji, chumba cha kuhifadhia maiti pamoja na kuweka uzio vitu vyote hivyo tayari tumevifanya hivyo ombi letu hilo tunaomba ulifanyie kazi kwani tunaamini huduma zitaboreka,” alisema Ummy.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Kibaha Beda Mmbaga alisema kuwa watahakikisha wanaboresha mahitaji yote yanayotakiwa ili kutoa huduma za ubora kwa wananchi wanaokwenda kuhudumiwa hapo.


Mwisho.