Friday, April 22, 2016

SUMATRA POLISI KUWABURUTA MAHAKAMANI MADEREVA WA DALADALA WANAOKATISHA RUTI

Na John Gagarini, Kibaha
MADEREVA wa mabasi ya abiria yanayotoa huduma wilayani Kibaha yanayotokea Mbezi na Ubungo Jijini Dar es Salaam watakaokatisha ruti watafikishwa mahakamani badala ya kupigwa faini.
Akizungumza na gazeti hili Ofisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Usafirishaji Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoani Pwani Nashon Iroga alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo baada ya madereva hao kudharau faini hizo na kulipa kwa urahisi.
Iroga alisema kuwa wamiliki wa mabasi hayo maarufu kama Daladala wamekuwa wakilipa faini na kuendelea kukatisha ruti hivyo kuwapa usumbufu abiria wanokwenda maeneo mbalimbali.
“Madereva hawa wamekuwa kama sugu licha ya kupigwa faini lakini wanalipa kwani wanaona kama ni afadhili kulipa faini na kukatisha ruti kuliko kuwafikisha abiria kule waendako,” alisema Iroga.
Alisema kuwa abiria wengi wanaokwenda maeneo ya Chalinze, Mkata, Msata na Mlandizi wamekuwa wakilalamika kuwa madereva hao hukatisha ruti na kugeuzia Kongowe kwa madai kuwa abirai wanaobaki ni wacheche hivyo wanapta hasara kuwapeleka maeneo hayo.
“Utakuta basi limetokea Ubungo au Mbezi na leseni yake inaonyesha linakwenda mfano Chalinze, Mkata, Msata  na Mlandizi akianza safari anakuwa na abiria wa kutosha lakini njiani abiria wanashuka hivyo wakifika Kongowe wanageuza wakidai kuwa abiria ni wachache hivyo hawapatia faida ndiyo wanakatisha ruti,” alisema Iroga.
Naye Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Pwani (RTO) Abdi Isango alisema kuwa hadi juzi madereva sita walipandishwa kizimbani kutokana na kukatisha ruti hizo.
Isango alisema kuwa wao waliomba leseni kufika hayo maeneo ambayo yametajwa na yameandikwa kabisa lakini hawawafikishi abiria kule walikosema na wamekuwa wakiwafaulisha kwenye mabasi mengine.
“Tumeona ili kukomesha tabia hiyo ya kukatisha ruti ni kuwapeleka mahakamani madereva wao wenyewe kwani faini wanaidharau na kulipa lakini kwa sasa ni kuwafikisha mahakamani tumeona njia hii itasaidia kwani faini ya shilingi 30,000 au ile ya 250,000 ya SUMATRA zimekuwa zikilipwa na wamiliki wao,” alisema Isango.
Alisema kuwa madereva 25 wanatafutwa baada ya kutenda kosa hilo na kukimbia huku wawili wakiyaacha magari na kukimbia lakini bado wanatafutwa na mara watakapokamatwa watafikishwa mahakani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Mwisho. 

SOKO LA MLANDIZI WALILIA USAFI

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA kwenye soko la Mlandizi Wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba serikali kuwajengea mitaro kwenye soko hilo ili kuruhusu maji kupita wakati wa mvua kwani soko hilo liko kwenye hali mbaya.
Akizungumza na waandishi wa habari Sauda Said alisema kuwa mvua inaponyesha maji yanajaa na kuwa kero kwa wateja wanaofika kununua bidhaa.
Said alisema kuwa mbali ya kutokuwa na mitaro pia soko hilo lina uchafu mwingi kutokana na kutotolewa kwa kipindi kirefu na kusababisha uchafu huo kutoa harufu kali.
“Changamoto nyingine ni ukosefu wa vifaa vya kufanyia usafi kwani mbali ya kutoa kiasi cha shilingi 200 kila siku kama ushuru usafi haufanyiki ipasavyo hivyo kufanya mazingira ya soko kuwa machafu,” alisema Said.
Alisema kuwa soko hili kwa sasa linazalisha uchafu mwingi sana lakini tatizo ni halmashauri kushindwa kuondoa uchafu kwa wakati na kufanya mlundikano wa uchafu kuwa mkubwa hali ambayo ina hatarisha afya za watumiaji.
Naye mwenyekiti wa soko hilo Thobias Michael alisema kuwa soko hilo ni kubwa kuliko masoko yote mkoani Pwani na linahudumia wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya za Bagamoyo, Kibaha na Kisarawe lakini mazingira yake si rafiki kwa watumiaji kutokana na uchafu kukithiri.
Michael alisema kuwa waliahidiwa kuwa watajengewa soko la kisasa ili kuondokana na changamoto wa soko hilo kwa sasa kuwa dogo kutokana na kuwa na wafanyabiashara wengi.
“Kwa sasa idadi ya wafanyabiashara ni 450 ni kubwa sana na uzalishaji wa uchafu ni mkubwa sana lakini uzoaji taka unakwenda taratibu sana na vifaa vya kufanyia usafi hakuna kwani hata gari la kuzolea taka hakuna inawabidi Halmashauri kukodisha,” alisema Michael.
Kwa upande wake mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Kibaha Dk Mariamu Maliwa alisema kuwa changamoto kubwa iliyopo ni ukosefu wa gari la Halmashauri kwa ajili ya kuzolea uchafu lakini wanakodisha gari kwa ajili ya kuzoa uchafu huo.

Mwisho.

KIBAHA WADHIBITI KIPINDUPINDU

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani imefanikiwa kuudhibiti ugonjwa wa Kipindupindu eneo la Mlandizi ambao uliolipuka Machi mwaka huu na kusababisha vifo vya watu watatu.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisni kwake mjini Kibaha Dk Mariamu Maliwa alisema kuwa walifanikiwa kuudhibiti kwa kufungia biashara za vyakula ambazo hazikutimiza masharti ya afya.
Dk Maliwa alisema kuwa mgonjwa wa mwisho aliyekuwa amelazwa kwenye kituo cha afya Mlandizi aliruhusiwa Aprili 21na kufanya kutokuwa na mgonjwa Kipindupindu hata mmoja kutoka wagonjwa 115 waliogundulika kuwa na ugonjwa huo kuanzia mwezi Machi mwaka huu.
“Kwa zaidi ya kipindi cha wiki moja tulizuia biashara zote za vyakula pamoja na matunda kwani tuliona kuwa sehemu hizo zilikuwa chanzo cha ugonjwa huo na tulipozifungia wagonjwa walipungua lakini kabla ya kuzifungia kulikuwa kunapatikana wagonjwa hadi nane kwa siku moja hali amabayo ilikuwa ni mbaya sana,” alisema Dk Maliwa.
Alisema kuwa mbali ya kuzuia biashara zote za vyakula pia walikuwa wakitoa elimu juu ya kujikinga na ugonjwa kuhamasisha usafi kwenye maeneo ya biashara, majumbani na sehemu zinazozalisha uchafu kwa wingi, uzoaji taka na kuhamasisha matumizi ya vyoo na kwa wale wasio na vyoo wachimbe vyoo.
“Walikaidi kujenga vyoo tumewapeleka mahakamani kwani wanaonekana kukaidi maagizo hayo kwani kujisaidia holela nako kuna changngia kuenea kwa ugonjwa huu,” alisema Dk Maliwa.
Aidha alisema kuwa wagonjwa hao walitoka kwenye maeneo mbalimbali ya Kibaha na nje ya Kibaha ambapo Ruvu walikuja wagonjwa 63, Mlandizi 27, Visiga na Kongowe 13, Dutumi wanane, Vingunguti na Mbezi wawili, Mzenga mmoja na wale waliokufa mmoja alifia hospitali huku wawili wakifia majumbani.
Alisema kuwa wataruhusu wauzaji wa vyakula mara watakapoona kuna mabadiliko ya ufuataji wa kanuni za afya mara baada ya maofisa wa afya kupita na kujiridhisha kuwa vyanzo vyote vya ugonjwa huo vimedhibitiwa na kuzingatiwa kwa kanuni za usafi na kuwataka wananchi kuweka mazingira yao kwenye hali ya usafi.
Mwisho.

KEC SACCOS YAKOPESHA WANACHAMA WAKE MABILIONI YA FEDHA

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Ushirika wa Mikopo cha Shirika la Elimu Kibaha (KEC SACCOS LTD) kimeweza kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.3 kwa wanachama wake kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mwenyekiti wa Ushirika huo Kachingwe Kaselenge alisema kuwa mtaji wao kwa sasa umefikia zaidi ya Bilioni 2.
Kaselenge alisema kuwa kwa sasa akiba ndani ya chama imefikia bilioni 1.7 hisa zikiwa ni shilingi milioni 213.9 na mkopo ni bilioni 2.2 ambapo kwa kila mwezi wanatoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 190.
“Tunamshukuru Mungu kwa sasa chama kinaendelea vizuri kwani marejesho ni asilimia 98 hadi 99 ni wanachama wachache tu ambao wanarejesha kwa matatizo nah ii inatokana na kuwa na mikopo sehemu nyingine kwani sheria inasema mtumishi anapokopa lazima ibaki asilimia 1/3 ya mshahara wake,” alisema Kaselenge.
Alisema kuwa wanachama wao ni watumishi wa Shirika hilo lakini kutokana na kuwa na uwezo mkubwa wameongeza wanachama ambao ni wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha (KDC) na wale wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha (KTC) pamoja na wafanyakazi waofisi ya mkuu wa mkoa.
“Chama chetu ni moja ya vyama vikongwe hapa nchini kwani kwa mwaka huu kinatimiza miaka 50 tangu kunzishwa kwake na tunajivunia mafanikio makubwa tuliyoyapata tangu kuanzishwa kwake kwani wanachama wameweza kunufaika na mikopo inayotolewa kwani zaidi ya watu 5,040 wananufaika kwa siku na mikopo hii kwani wanachama wana miradi mbalimbali kama ya mabasi, shule, ufugaji bodaboda na shughuli nyingine za kimaendeleo,” alisema Kaselenge.
Aidha alisema kuwa mtaji walio nao ni wa ndani kwani hawakopi kwenye mabenki kama baadhi ya vyama vinavyofanya hivyo hawana deni lolote wale mkopo kwenye taasisi za kifedha ambapo hubidi kuweka riba kubwa ili kufidia mikopo kwani kutokana na kuwa na mtaji wa ndani riba yao ni asilimia 1.6.
“Kuna mikopo ya aina mbalimbali ikiwa ni pamoja na ile ya Dharura kama vile misiba na majanga mbalimbali, Maendeleo ikiwa ni pamoja na ujuenzi wa nyumba usafiri na ufugaji, Elimu kusoma na kusomesha na mwanachama anapofariki familia inalipwa 300,000 na kama ni mwenza wake analipwa 200,000 kwani asilimia moja ni bima ya mkopo na endapo anafariki deni linakufa na fedha zake watalipwa ndugu bila ya kukatwa chochote kwani bima itakuwa inalinda mkopo huo,” alisema Kaselenge.
Alibainisha kuwa wanakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwa na ushindani mkubwa toka kwenye taasisi za kifedha ambazo zinawashawishi wanachama wao kujiunga nao kwa kuwalipia madeni wanayodaiwa kwenye chama, sheria kutaka vyama hivyo kutolipa kodi lakini wanaaambiwa walipe kodi na mwanachama anauwezo wa kukopa mara tatu ya akiba yake aliyojiwekea kati ya shilingi milioni moja hadi milioni zaidi ya 20.
Ushirika huo ulianzishwa mwaka 1966 ukiwa na wanachama ukiwa na wanachama 66 lakini kwa sasa una wanachama 840 na kilianzishwa kwa ajili ya  kusaidiana na kusaidia jamii inayowazunguka kwa kujitolea misaada sehemu mbalimbali kama hospitali na maeneo yenye uhitaji.
Mwisho.

Monday, April 18, 2016

SEKRETARIETI PWANI KUCHUNGUZA FEDHA ZILIZORUDISHWA HAZINA NA WAKURUGENZI WA HALMASHAURI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amesema kuwa ataituma sekretarieti ya mkoa wa Pwani kufuatialia kwa wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya za mkoa huo kuchunguza juu ya fedha kiasi cha shilingi milioni 249, 452,390 kuwa zimerudishwa Hazina ikiwa ni sehemu ya fedha kiasi cha shilingi milioni 641,361,239 ambazo ni hasara zilizolipwa kwa watumishi hewa 25.
Mbali ya kuituma sekretarieti kufuatilia suala la fedha hizo pia amewataka wakuu wa wilaya kutumia vyombo vya dola kama vile Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufuatilia watu waliohusika kuchukua fedha hizo.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Kibaha Ndikilo alisema kuwa serikali haijaridhishwa na majibu ya wakurugenzi hao kuwa fedha hizo wamezirejesha Hazina huku kukiwa hakuna viambatanisho vyovyote ambavyo vinaonyesha kuwa fedha hizo zilipelekwa hazina.
“Serikali inataka kujua ni nani aliyehusika kuchukua fedha hizo kinyume cha taratibu za kazi kwani watumishi hao ni hewa lakini cha ajabu walikuwa wakilipwa mishahara kwa kila mwezi na kuitia serikali hasara kiasi hicho,” alisema Ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa kati ya hao watumishi hewa ni wale ambao wamefariki dunia, wasio kuwepo kazini kuacha kazi na wastaafu lakini walikuwa wanalipwa kama vile wako kazini jambo ambalo ni kinyume cha sheria na wanastahili kuchukuliwa hatua kali mara watakapo kutwa na tuhuma hizo.
“Zoezi hili litaendelea kufanyika ili kubaini ni njia gani walizokuwa wakizitumia hadi kufikia kulipwa fedha hizo ili hali hawako kazini na kuisababishia serikali hasara kubwa kiasi hicho hali ambayo imefanya zoezi hilo kufanywa kwa watumishi wa serikali ili kuwabaini,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema alisema kuwa kama kuna watu walikuwa wakifoji na kujipatia fedha hizo endapo watabainika watachukuliwa hatua kali za kisheria ili kukomesha wizi huo wa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwa kuiibia serikali.
Alisisitiza kuwa suala la watumishi hewa lilikuwa ni kama kansa ambayo inaitafuna nchi lakini baada ya Rais Dk John Magufulia kubaini na kuagiza kutafutwa watumishi hewa ni dhahiri hatua zitakazochukuliwa zitakomesha watumishi hewa waliokuwa wanaiibia serikali.
Mwisho.

KILUA YAUNGA MKONO DHAMIRA YA DK MAGUFULI KUJENGA VIWANDA

Na John Gagarini, Kibaha
KATIKA kuunga mkono dhamira ya Rais Dk John Magufuli ya uchumi wa nchi kutegemea viwanda kampuni ya Kilua Steel inatarajia kuanza uzalishaji wa bidhaa za vyuma zikiwemo nondo pamoja na vyuma mbalimbali ifikapo mwezi Mei mwaka huu.
Uzalishaji wa vyuma kwenye kiwanda hicho utapunguza bei ya bidhaa za vyuma kwa asilimia 25 ya bidhaa hizo ambazo nyingi zinaagizwa toka nje ya nchi hivyo kuongeza mapato ya ndani.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kiwanda hicho kilichopo Kitongoji cha Disunyala Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani mkurugenzi wa kiwanda hicho Mohamed Kilua alisema kuwa kiko kwenye hatua za mwisho za kuunganisha umeme mkubwa wa viwandani kwani uliopo ni mdogo na hauwezi kuendesha mashine za kiwanda hicho.
Kilua alisema kuwa kiwanda hicho ambacho kitakuwa ni cha kipekee hapa nchini na barani Afrika kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani milioni 1.5 kwa mwaka huku kwa siku kikitarajiwa kuzalisha tani 2,000 kwa awamu ya kwanza na kufikia tani 7,000 itakapofikia awamu ya tatu na itatoa ajira kwa watu zaidi ya 2,000.
“Tunatarajia kuzalisha vyuma vyenye ubora wa kimataifa ili viweze kuwa na soko sehemu yoyote ile duniani kwani tuna wataalamu kutoka nchi ya China ambao ndiyo tunaoshirikiana nao hapa,” alisema Kilua.
Alisema kuwa tayari malighafi za kutengenezea vyuma wanazo ambazo zinatoka nchi kama vile Brazil na nchi zinazotengeneza vyuma duniani lakini mara kitakapoanza kazi kitakuwa na malighafi zake.
“Tunarajia malighafi zote mara tutakapoanza uzalishaji zitapatikana hapa hapa hivyo bei ya vyuma itashuka na nchi itapata maendeleo kupitia kodi mbalimbali kwenye kiwanda,” alisemaKilua.
Aidha alisema kuwa vyuma vitakavyozalishwa hapo mbali ya nondo ni pamoja na vyuma vinavyo husika na ujenzi wa madaraja makubwa, mabomba yatakayotumia gesi, maghorofa kufikia urefu wa ghorofa 50 na kuendelea na vyuma vya engo tofautitofauti ambavyo vitapatikana na kuwapunguzia gharama wananchi katika shughuli zao zinazohitaji vyuma.
Kwa upande wake mkurunzi mwenza kutoka nchni China Wang Zuojin alisema kuwa aliamua kushirikiana na Kilua ikiwa ni moja ya njia za kuenzi urafiki wa nchi hizo ambao ulianzishwa na Mwalimu Julius Nyerere zaidi ya miaka 50 iliyopita.
Zuojin alisema kuwa nchi ya China miaka mingi iliyopita ya nyuma ilikuwa maskini lakini walijipanga hasa kupitia viwanda na kuifanya nchi hiyo kuwa yenye uchumi mkubwa duniani kupitia viwanda.
“Rais Dk John Magufuli ni mtu anayependa maendeleo na tumeamua kumuunga mkono kwa sera zake za kuinua uchumi wa wananchi wake kwa kuendeleza sekta ya viwanda ili kuwa na uchumi wa kati kwa kufanya mapinduzi ya viwanda,” alisema Zuojin.
Alisema kuwa anachokisema Dk Magufuli kinawezekana kwani hata China ilikuwa chini kiuchumi lakini walipoamua kuwekeza kwenye viwanda wamefanikiwa na kuwa nchi zenye uchumi mkubwa duniani na kuwaondoa wananchi wake kwenye umaskini.
Mwisho.
   





Friday, April 15, 2016

WATUMISHI HEWA WAITIA HASARA SERIKALI KIASI CHA SHILINGI MILIONI 641


Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani umebaini uwepo wa watumishi hewa 25 wakiwemo walio kufa na wameipa serikali hasara kiasi cha shilingi milioni 641,361,239 kutokana na kupokea mishahara pasipo kufanya kazi ambalo ni kosa kisheria.

Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evaristi Ndikilo alisema kuwa hasara hiyo imebainika baada ya kufanya uhakiki kwa mara ya pili na kuona kuwa fedha za mishahara ziliendelea kutolewa kwa watumishi hewa licha ya kutokuwepo kazini.

Ndikilo alisema kuwa kati ya watumishi 19 ni wale waliokufa, waliostaafu na kuacha kazi lakini mishahara yao ilikuwa ikiendelea kutoka na kusababisha hasara hiyo baada ya kuwafanyia uhakiki watumishi 150 ili kuwatafuta watumishi hewa kutokana na agizo la Rais Dk John Magufuli.

“Kundi hili la kwanza limeipa hasara serikali kiasi cha shilingi milioni 69.1 huku wale ambao hawapo kabisa kazini wameipa hasara serikali kiasi cha shilingi milioni 12.4 na watumishi watoro na wale walio na mashauri ya kinidhamu wameipa hasara serikali kiasi cha shilingi milioni 448.2,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa kati ya watumishi 150 waliohakikiwa 31 walibainika kuwa ni watoro na hawakujitokeza siku ya uhakiki lakini walionekana kuwa ni watumishi halali kwa kuonyesha nyaraka muhimu huku 18 wakibainika kuwa ni watoro na wanamashauri ya kinidhamu lakini waliendelea kulipwa mishahara.

“Watumishi 76 ambao ni watoro na wanamashauri ya kinidhamu mishahara yao imesimamishwa ili wasiendee kuitia hasara serikali wakati mashauri yao yanafanyiwa kazi,” alisema Ndikilo

Aidha alisema kuwa wakurugenzi wa Halmashauri saba za wilaya walisema kuwa kiasi cha shilingi milioni 249,452,390  zilirudishwa Hazina na kuwataka wapeleke viambatanisho kama ushahidi vinavyoonyesha kuwa walipeleka hazina na si maneno matupu.

“Kama ni kweli kiasi hicho cha fedha kilipelekwa hazina fedha ziltakazokuwa zimepotea ni kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 391.8 ambazo wanapaswa kuonyesha vielelezo vya kuzipeleka hazina kwani maelezo hayo bado hayajaturidhisha wanatakiwa watupe uthibitisho ili tuliamini hilo,” alisema Ndikilo.     


Mwisho.