Friday, March 25, 2016

RC AUNDA TUME KUCHUNGUZA KIWANDA JUU YA HAKI ZA WAFANYAKAZI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo ameunda Tume kutoka idara ya kazi ya mkoa huo kutembelea kiwanda cha Hong Yu Steel cha kuzalisha nondo kilichopo wilayani Kibaha kwa kushindwa kuzingatia masharti ya uendeshaji wa kiwanda na maslahi ya wafanyakazi.
Aliunda tume hiyo ya watu watatu itakayofanya kazi kwa wiki moja kufuatilia malalamiko hayo ya wafanyakazi kwa lengo la kuleta uwajibikaji kwa pande zote mbili katia ya wafanyakazi na wamiliki hao baada ya malalamiko kuzidi na kufanya ziara kujionea hali halisi.
Ndikilo alifikia hatua hiyo baada ya kupata malalamiko toka kwa wafanyakazi kuwa wamiliki wa kiwanda hicho hawajali usalama kazini kwa wafanyakazi wao kwa kushindwa kuweka vifaa vya kuwalinda kutokana na mazingira wanayofanyia kazi ambayo ni hatarishi kwa maisha yao.
“Tumesikia wafanyakazi na tumeona wafanyakazi wakifanya kazi huku wakiwa hawana vifaa vya kufanyia kazi kama vile baadhi yao hawajavaa kofia ngumu, gloves na mabuti kwa ajili ya kujikinga na hatari zinazoweza kujitokeza wakati wa kufanya kazi,” alisema Ndikilo.
Alisema wafanyakazi wamelalamikia mambo mengi ikiwa ni pamoja na mshahara mdogo, kutokuwa na mikataba ya kazi, kutolipwa masaa ya ziada, kukatwa mishahara mara wanaposhindwa kwenda kazini kutokana na kuumwa au kuumia kazini, huduma ya kwanza kuchelewa pamoja na kutokuwa na mapumziko hata nyakati za sikukuu na mwisho wa wiki.
“Tumeona kuna matatizo mengi hivyo itaundwa tume kwa ajili ya kukaa na uongozi kwa ajili ya kurekebisha kasoro zilizopo kwa kuzingatia sheria za kazi kwani kila mtu anamtegemea mwenzake kati ya mwajiri na mfanyakazi hivyo hakuna sababu ya upande mmoja kumnyanysa mwenzake,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa tume hiyo itatembelea vitengo vyote kwa kuonana na viongozi wa vitengo husika na baadaye kukaa na uongozi ili kuangalia namna ya kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya wafanyakazi.
Kwa upande wake kaimu ofisa kazi wa mkoa Swalehe Njoma alisema kuwa haki nyingi za wafanyakazi zimevunjwa hivyo kuna haja ya kurekebisha na kuweka mazingira bora ya kazi ili haki iweze kupatikana kwani malalamiko ni mengi.
Njoma alisema kuwa moja ya haki za mfanyakazi ni kuwa na muda wa mapumziko na hata kama atafanya kazi kwa masaa ya ziada lazima alipwe na mfanyakazi anapoumwa au kuumia kazini hapaswi kukatwa fedha kutokana na kushindwa kwenda kazini kutokana na kujiuguza.
Naye ofisa mwajiri wa kiwanda hicho Asantemungu Filbert alikiri kuwepo na matatizo ambapo alisema kuwa yeye ni mgeni na hana muda mrefu ila kwa mtangulizi wake hakuweza kuweka mazingira mazuri ya wafanyakazi.
Filbert alisema kuwa tayari ameandaa utaratibu wa kushughulikia kero za wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi ili kukabiliana na changamoto zilizopo na kufanya utendaji kazi kuwa mzuri.
Mwisho.   

SUMATRA NA POLISI WAKAMATA MABASI

Na John Gagarini, Kibaha
MAMLAKA ya Usafirishaji Majini na nchi kavu SUMATRA kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi nchini wamefanya operesheni ya kushtukiza ya kukagua mabasi yaendayo mikoani na kubaini makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na baadhi ya madereva kutumia vilevi na kuwzidishia nauli abiria.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha wakati wa zoezi hilo Mkurugenzi wa SUMATRA, Johnsen Kahatano alisema kuwa operesheni hiyo imefanywa ili kuwadhibiti wamiliki pamoja na madereva ambao wanakiuka sheria za usalama barabarani.
Kahatano alisema kuwa operesheni hiyo imefanikiwa kwani wameweza kukamata makosa kadhaa ambayo mengine ni ya barabarani na mengine ni ya kuwazidishia nauli abiria jambo ambalo ni kosa kisheria ambapo mabasi yaliyofanya makosa wamiliki wake watafikishwa mahakamani.
“Tumefanikiwa kumkamata dereva mmoja alikutwa akiwa ametumia kilevi na tulimkamata na kulizuia basi hilo hadi walipoleta dereva mwingine kwa ajili ya safari  jambo ambalo ni la hatari kwa usalama wa abiria,” alisema Kahatano.
Alisema kuwa mabasi sita yalikamatwa yakiwa yamezidisha nauli ambpao abiria waliokuwa wakienda Moshi walkatiwa nauli ya kwenda Arusha ambayo ni shilingi 33,000 huku nauli halali kwa watu wanaoshukia Moshi ni shilingi 28,500.
“Mabasi yaliyowazidishia abiria walirudishiwa nauli zao kama taratibu zinavyoonyesha na hili ni kosa kisheria na abiria wanapaswa kulipa nauli halali ambazo zimepitishwa kisheria na wanapaswa kwenda kulalamika endapo watabaini wamezidishiwa,” alisema Kahatano.
Naye Kaimu Kamishna wa Usalama Barabarani Fortunatus Musilimu alisema kuwa abiria nao ni wadau muhimu katika vita ya kupambana na madereva au wamiliki wanaokiuka taratibu za usalama barabarani na kupunguza ajali hivyo wanapaswa kutoa taarifa kwao ili hatua ziweze kuchukuliwa.
Musilimu alisema kuwa watu wanataka kuishi na maendeleo si kukatishwa uhai kutokana na ajali ambazo zinaweza kuzuilika na kutoa taarifa polisi kwa kutumia njia ya simu ambazo ziko kwenye mabasi yote lengo likiwa ni kupunguza ajali.
Mwisho.     


Thursday, March 24, 2016

WAWILI WASHIKILIWA KWA UTAPELI WAWILI WAKIMBIA

Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kutaka kumtapeli mtu mmoja kiasi cha shilingi milioni tatu kwa kumuuzia madini aina ya Almasi ambayo ni bandia.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kamanda wa polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa watu hao ambao walikuwa wanne wengine wawili walifanikiwa kukimbia walikamatwa baada ya kutaka kukimbia kutokana na mlalamikaji kupiga kelele ya kuomba msaada.
Mushongi alisema kuwa tukio hilo limetokea juzi eneo la CCM Mkoani wilayani Kibaha majira ya saa 3:30 asubuhi baada ya mlalamikaji kutoka kuchukua fedha kwenye benki ya NMB Tawi la Kibaha.
“Mlalamikaji mara baada ya kuchukua fedha alikutana na watuhumiwa hao ambapo waliongea naye na kumwambia kuwa wanauza madini aina ya Almasi ambapo walikubalina na akawakabidhi fedha hizo,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa watuhumiwa hao wakiwa kwenye gari aina ya Primio lenye namba za usajili T 668 DFY walianza kuondoka lakini mlalamikaji akagundua kuwa madini yale si halisi na kuanza kupiga kelele za wezi kuomba msaada ndipo waendesha pikipiki walipoanza kuwafukuza na baadaye polisi nao wakatokea na kuwakamata.
“Watuhumiwa hao baada ya kuona wamezingirwa walikimbia hata hivyo wawili walikamatwa na wengine wawili walifanikiwa kutokomea kusiko julikana nab ado tunaendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine ili kuwafikisha mahakamani kujibu tuhuma hizo,” alisema Mushongi.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mwantumu Juma maarufau kama Hawa, Fidelis Buberwa au Finas Barongo ambao wanashikiliwa kutokana na tukio hilo ambapo gari hilo linashikiliwa.
Kufuatia tukio hilo kamanda aliwataka wananchi kutokubali kuuziwa madini mikononi badala yake waende sehemu husika ambazo ziko rasmi kwa ajili ya uuzaji wa madini ili kuepukana na watu kama hao.
Mwisho

MMOJA AFA 10 WALAZWA KIPINDUPINDU

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja amefariki dunia wilayani Kibaha mkoani Pwani kutokana na ugonjwa wa Kipindupindu huku wengine 10  wakiwa wanaugua ugonjwa huo kwenye hospitali mbalimbali wilayani humo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Ofisa afya wa mkoa wa Pwani Simon Malulu alisema kuwa ugonjwa huo uligundulika Aprili 17 mwaka huu katika Shule ya Sekondari ya Ruvu wilayani Kibaha.
Malulu alisema kuwa ugonjwa huo uliwakumba wanafunzi 21 wa shule hiyo ambapo awali waliona kuwa ni mchafuko wa matumbo kwani wanafunzi hao walikuwa wakiharisha.
“Baada ya kuona hali imezidi kuwa mbaya kwa wanafunzi walimu waliwapeleka wanafunzi kwenye Zahanati ya Kijiji cha hicho cha Ruvu Station na kuchukua sampuli ya kinyesi kwa wanafunzi tisa ambapo mmoja aligundulika kuwa na ugonjwa huo,” alisema Malulu.
Alisema kuwa baada ya kubaini hilo ilibidi mkuu wa wilaya aifunge shule hiyo ili kuwaepusha wanafunzi zaidi kuambukizwa ugonjwa huo ambapo wanafunzi waliokumbwa na ugonjwa huo wengi walikuwa ni wanafunzi wakike ambao wako bweni.
“Hadi sasa kwenye Zahanati ya Ruvu kuna wagonjwa wanne, Zahanati ya Dutumi watatu na Mlandizi wako watatu ambao wanendelea kupatiwa matibabu ya ugonjwa huo,” alisema Malulu.
Aidha alisema kuwa chanzo cha kuenea ugonjwa huo ni kinyesi ambacho kinatokana na watu wengi kujisaidia kwenye Mto Ruvu ambapo maji yake wanafunzi na wananchi wa Kijiji cha Ruvu Station.
“Tumechukua hatua za kufungua kambi kwenye maeneo yote yenye ugonjwa ikiwa ni pamoja na Ruvu Station, Dutumi na Mlandizi pia kuwaptia dawa ya kusafishia maji ili kutibu maji hayo ambayo wananchi wamekuwa wakiyatumia bila ya kuyachemsha,” alisema Malulu.
Aliongeza kuwa wananchi wanatakiwa kutumia vyoo pia wanatoa elimu ya jisni ya kujikinga na ugonjwa huo na kufanya ukaguzi  wa taasisi za umma, shule, nyumba za watumishi kuzuia upikwaji wa vyakula na uuzaji wa vinywaji na kuweka mazingira katika hali ya usafi.
Ugonjwa huo mwaka jana Agosti ulitokea mkoani Pwani na kuisha Desemba ambapo 293 waliambukizwa huku 98 walibainika kuwa na ugonjwa huo huku watu watatu walipoteza maisha.
Mwisho.

Saturday, March 19, 2016

SHULE YAKABILIWA NA UHABA WA WALIMU INA WALIMU WAWILI TU

Na John Gagarini, Bagamoyo
MAZINGIRA magumu yanayokikabili Kijiji cha Kitame Kata ya makurunge wilayani bagamoyo mkoani Pwani yamesababisha walimu walimu wawili wanaofundisha shule hiyo kufundisha kwa siku 90 kwa mwaka mzima.   
Kutokana na shule hiyo kuwa kwenye mazingira magumu walimu wengi wamekuwa hawako tayari kufundisha shule hiyo yenye wanafunzi 51 wa kuanzia darasa la kwanza hadi la saba ambayo ni idadi ndogo kutokana na mazingira hayo.
Akizungumza mbele ya Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa, moja ya wakazi wa Kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina la Adam Rashid alisema kuwa moja ya changamoto zinazowakabili ni pamoja na kutokuwa na usafiri wa uhakika kutokana na ubovu wa miundombinu.
“Usafiri wa kutokana Kijijini hapa hadi makao makuu ya wilaya ni kilometa 54 kwa njia ya barabara na usafiri wake ni pikipiki na gharama yake ni kiasi cha shilingi 50,000 huku ule wa kutumia njia ya bahari mitumbwi gharama yake ni kiasi cha shilingi 60,000 kwenda na kurudi,”  alisema Rashid.
Alisema gharama hizo ni kubwa sana ajambo ambalo linawafanya walimu washindwe kwenda kufundisha kutokana na mazingira hayo ambapo walimu hao wawili wamekuwa wakipokezana kufundisha madarasa hayo.
“Wanafunzi wanafundishwa siku chache kutokana na walimu hao wakati mwingine kutofika kabisa shuleni hali ambayo inawakatisha tamaa wanafunzi na kusababisha kuwa na idadi ndogo ya wanafunzi wanaosoma shuleni hapo,” alisema Rashid.
Aidha aliiomba serikali kusaidia kupatikana kwa walimu ili kukabiliana na hali ya wanafunzi hao kukosa masomo na kusababisha elimu kuwa duni hali ambayo itatoa matokeo mabaya kwa wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Makurunge Kabile Paulo alisema kuwa walimu wengi wanashindwa kwenda kufundisha shuleni hapo kutokana na mazingira magumu kwani hakuna huduma muhimu za jamii hivyo kushindwa kukaa huko.
Paulo alisema kuwa baadhi ya huduma ambazo hazipo ni pamoja na huduma ya afya kwani hakuna zahanati na huduma nyingine muhimu ambazo huwabidi kuzifuata Bagamoyo au maeneo mengine jambo ambalo limekuwa likiwagharimu.
Naye mbunge wa Jimbo hilo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa alisema kuwa kweli hiyo ni changamoto ambayo inawakabili wakazi na walimu hao lakini kwa kushirikiana na diwani wa kata hiyo watahakikisha wanaitatua.
Dk Kawambwa alisema kuwa Halmashauri itafanya mgao wa walimu na ataiomba itoe kipaumbele kwa shule hiyo kwa kuwapatia walimu ili waweze kwenda huko na kuongeza nguvu ya ufundishaji kwenye shule hiyo ambayo iko pembezoni na kuwataka vijana waliosoma vyuo vya ualimu na ni wenyeji wa kata hiyo kujitolea kwenda kufundisha kama njia mbadala ya upungufu huo wa walimu.
Mwisho.  
  

VIJANA KUENDESHA MRADI WA SAMAKI MTAA WA KIBONDENI

Na John Gagarini, Kibaha
MTAA wa Kibondeni Kata ya Mkuza wilayani Kibaha utawapatia mafunzo ya ufugaji wa samaki vijana 40 wa mtaa huo ili waendeshe mradi wa ufugaji wa samaki kwenye bwawa la mtaa ambalo limerudishwa baada ya kuuzwa kimakosa kwa mtu binafsi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Hamis Mwarizo alisema kuwa vijana hao watapewa mafunzo hayo kutoka ofisi ya kata ili vijana waweze kujua namna ya kufuga samaki.
Mwarizo alisema kuwa mafunzo hayo yatatolewa kwa vijana ambao watakuwa wameunda vikundi ambavyo vitaendesha mradi huo ambao utatoa ajira kwa vijana hao na watakuwa wakipeana zamu ya kusimamia.
“Lengo la mradi huo ni kuongeza ajira kwa vijana ambapo asilimia 70 ya mapato yatakwenda kwenye kikundi na asilimia 30 yatakwenda kwenye mtaa kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo ya jamii ya mtaa wetu,” alisema Mwarizo.
Alisema kuwa kwa sasa tayari vijana 16 wameshapatikana kwa ajili ya kuanzisha kikundi cha mwanzo na wengine wanaendelea kujiandikisha na baadaye kikundi hicho kitasajiliwa ili kitambulike kisheria baada ya mradi huo kupitishwa ana wananchi kwenye mkutano mkuu wa mtaa.
“Kundi la kwanza litaendesha kwa kipindi cha miaka 10 na baadaye litapewa kundi lingine kwa ajili ya kuendeleza mradi huo ambao mbali ya kuwapatia vijana ajira pia utaipatia jamii ya eneo hilo na maeneo jirani lishe kwa ajili ya kuboresha afya,” alisema Mwarizo.
Katika hatua nyingine alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na taratibu za kulipima eneo la bwawa hilo ili kujua mipaka yake halisi ambapo maji yake baada ya kupimwa yalibainika kuwa hayafai kwa kunywa kwani yana viluilui ambavyo vinaweza kusababisha maradhi ya ugonjwa wa tumbo hivyo yatatumika kwa ajili ya kulimia bustani pamoja na kufulia.
Mwisho.


WAFANYABIASHARA WA NAFAKA WAIOMBA HALMASHAURI KUWAONDOLEA USHURU

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA wa jumla na rejareja wa mazao ya nafaka kwenye soko la maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji huo kuondoa ushuru wa shilingi 1,000 kwa gunia la kilogramu 100 la nafaka linaloingia sokoni hapo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha katibu wa umoja wa wauzaji wa mazao ya nafaka sokoni hapo Ramadhan Maulid alisema kuwa sheria hiyo ya utozaji wa ushuru wa shilingi 1,000 kwa gunia la la nafaka lenye uzito wa kilogramu 100 ina kinzana na sheria mama ambayo inataka ushuru ukatwe mara moja tu.
Maulid alisema kuwa wao wanaponunua nafaka hizo huko mikoani wanatozwa ushuru wa shilingi kati ya 2,000 hadi 5,000 kutegemeana na Halmashauri hivyo wanashangaa kutozwa tena mara wanapofikisha mzigo sokoni hapo.
“Kututoza ushuru tena ni sawa na kuwatoza ushuru mara mbili kwani hata sheria ndogo hiyo iliyowekwa na Halmashauri haikuwashirikisha wao kama watekelezaji wa sheria hiyo ambayo ilipitishwa mwaka 2007 na kutakiwa kuanza kutumika mwaka 2008 lakini haikuwahi kutumika licha ya kwamba kwa miaka ya nyuma ilikuwa ikitumika,” alisema Maulid.
Alisema kuwa waliletewa taarifa ya kutakiwa kulipa ushuru huo hivi karibuni lakini walijaribu kuonana na viongoizi wa halmashauri bila ya mafanikio ili kuzungumzia suala hilo ambalo kwao ni moja ya ushuru ambao ni kero.
“Mbali ya kutakiwa kulipia kiasi hicho pia gharama nyingine ni pamoja na kulipia Kizimba kiasi cha shilingi 9,000, Ardhi 3,000 na mlinzi 6,000 ambazo hulipa kila mwezi hivyo malipo hayo ni sawa na kuwaongezea mzigo wa ushuru,” alisema Maulid.
Aidha alisema kuwa kwa sasa wanawasiliana na wanasheria ili kutoa tafsiri ya sheria hizo mbili kati ya sheria mama na sheria ndogo ya Halmashauri ambapo inaonekana kama zinakinzana na kuleta mkanganyiko kwao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa soko hilo Ally Gonzi alisema kuwa tangu walipoletewa sheria hiyo ndogo ambayo ilipitishwa kwenye baraza la madiwani walijaribu kufanya vikao mbalimbali na Halmashauri ili kuangalia namna ya kupunguza ushuru huo lakini ilishindikana ambapo Halmashauri iliwaambia kuwa kama wanataka uondolewe basi wafuate taratibu.
Naye mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Gladdys Dyamvunye alisema kuwa wafanyabiashara hao wanapaswa kulipa ushuru huo kwani uko kisheria na tayari vyombo vya sheria vimetoa siku 14 kwa wafanyabiashara hao kulipa na endapo hawatalipa watashitakiwa.
Mwisho.