Thursday, August 20, 2015

WATUMISHI WA DINI WAASWA KUELEKEA UCHAGUZI

Na John Gagarini, Morogoro
WATUMISHI wa Dini nchini wametakiwa kumtanguliza Mungu katika utumishi wao ili kuendelea kudumisha amani ya nchi iliyopo hasa katika kipindi hichi cha kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Ushauri huo umetolewa huko Lugoba wilayani Bagamoyo mkoani Pwani na Mtawa Sista Perpetua Mlamwaza (72) wakati wa maandalizi ya Jubilei ya miaka 50 ya Utawa kwenye kanisa la Katoliki na kusem akuwa siri kubwa ya mafanikio yake ya utendaji yanatokana na kumtanguliza mbele Mungu.
Mlamwaza alisema kuwa watumishi wa Mungu wana nafasi kubwa ya kuifanya nchi iendelee kudumu ni kwa wao kumtanguliza Mungu na kuliombea Taifa letu ili liwe amani ambayo imedumu tangu nchi kupata Uhuru.
“Kipindi hichi tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu hivyo lazima tupige magoti kumwomba Mungu azidi kutudumishia amani yetu iliyopo kwani yeye ndiye mwenye uwezo wa kutunusuru na hali yoyote ambayo inaashiria uvunjifu wa amani,” alisema Mlamwaza.
Mlamwaza ambaye aliwalea kiroho hadi kufanikiwa kupata upadri Mhashamu Askofu Antony Banzi wa Jimbo la Tanga na padri Peter Kunambi alisema kuwa watumishi ni kiungo muhimu kati ya wanadamu na Mungu.
“Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuweza kumtumikia Mungu kwa kipindi chote cha miaka 50 ya utumishi wangu lakini amani hii iliyopo inapaswa kulindwa na kuendelezwa ili tuendelee kupata mafanikio ya kimaendeleo,” alisema Mlamwaza.
Aidha alisema kuwa Watanzania wote wanapaswa kufanya maombi ya kila wakati ikiwa ni pamoja kufunga ili kumwomba Mungu aendelee kutudumishia amani iliyopo hasa ikizingatiwa Tanzania ni Kisiwa cha amani.
Aliwataka wazazi kuhakikisha wanawapeleka shule watoto wao hususani wale wa kike ili waweze kuwarithisha elimu ambayo itakuwa ni mkombozi katika maisha yao na si mali kama baadhi ya watu wanavyofikiri.
Mwisho.
  

   

No comments:

Post a Comment