Thursday, August 20, 2015

MAILI MOJA WAENDELEA NA UJENZI WA SHULE ILIYOBOMOKA

> Na John Gagarini, Kibaha
UJENZI wa madarasa manne kwenye shule ya msingi Maili Moja umeanza ambapo kwa sasa wanafunzi 200 wanasoma kwenye darasa moja kutokana na baadhi ya madarasa kushindwa kutumika kutokana na kuwa mabovu hivyo kuhatarisha usalama wa wanafunzi.
Shule hiyo ambayo ndiyo shule ya kwanza kujengwa kwenye mji wa Kibaha kwenye miaka ya 70 madarasa yake yamebomoka na baadhi yameanguka kutokana na kutumika kwa muda mrefu sasa kwani yamefikisha umri wa miaka 40 sasa.
Akizungumza na waandishi wa habari shuleni hapo mwalimu mkuu wa shule hiyo Reginald Fanuel alisema kuwa ujenzi huo ambao ambao utaanza na madarasa mawili tayari ujenzi umefikia hatua ya msingi na unatarajiwa kukamilika baada ya miezi mitatu kuanzia sasa.
Fanuel alisema kuwa fedha zilizotumika kujenga msingi huo wa madarasa manne ni michango ya wazazi na wadau mbalimbali huku wakisubiria kutoa fedha ambazo ziko benki kiasi cha shilingi milioni 36 zilizotolewa na Halmashauri ya Mji wa Kibaha ambazo ndiyo zitakamilisha ujenzi wa madarasa hayo mawili
“Kwa kweli hali ni mbaya kwa sasa kwani darasa moja linachukua wanafunzi 200 tofauti na wastani wa wanafunzi 45 kwa darasa moja lakini kutokana na ubovu madarasa imebidi mengine yasitumike kutokana na kubomoka na yanaweza kuanguka hivyo usalama wa wanafunzi na walimu kuwa mdogo,” alisema Fanuel.
Alisema kuwa shule hiyo ina jumla ya madarasa 14 lakini mazima ni manne tu ndiyo yenye unafuu kidogo licha ya kuwa si mazima huku mawili ndiyo mazima na yako imara na yanafaa kwa matumizi ya kufundishia.
“Ujenzi ulisimama kidogo kutokana na kukosekana vitabu vya hundi kutoka benki hivyo kushindwa kuwalipa wazabuni na wakandarasi na tulitumia muda mrefu zaidi ya mwezi mmoja kupata vitabu hivyo kwani akaunti ya shule ilikufa hivyo tukaanza kuifufua upya hali iliyotumia muda mrefu kufunguliwa lakini kwa sasa zoezi hilo limekamilika na wataanza kulipwa ili ujenzi uendelee,” alisema Fanuel.
Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Lusanda Wiliam alisema kuwa michango iliyochangwa ni mizuri kwani walitoa mifuko 250 ya saruji ambayo iilifyatuliwa tofali zaidi ya 585 na mifuko 50 ilitumika kwa ajili ya msingi uliojengwa.
Wiliam alisema kuwa wazazi ambao watoto wao wanasoma shuleni hapo walitakiwa kulipia shilingi 5,000 kila mmoja kwa ajili ya ujenzi huo na walifanikiwa kupata kiasi cha shilingi 500,000 na kuwaomba wadau wengine wajitokeze kuchangia ujenzi huo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment