Thursday, August 20, 2015

WAWEZESHAJI KAYA MASKINI KIBAHA WAASWA

Na John Gagarini, Kibaha
WAWEZESHAJI wa mradi wa kutoa ajira za muda kwa kaya maskini kwenye Halmashauri ya wilaya ya Kibaha mkoani Pwani kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Nchini (TASAF) wametakiwa kutowapangia miradi kwa utashi wao bali wao wabaki kama washauri tu.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha Tatu Suleiman wakati akifungua mafunzo kwa wawezeshaji wa mradi huo awamu ya tatu na kusema kuwa wananchi ndiyo wenye kufahamu wanahitaji mradi gani.
Seleman alisema kuwa waratibu hao kazi yao ni kutoa ushauri kwa wananchi wanapobainisha mradi wanaoutaka kwani wanaopata changamoto ni wao na si kuelekezwa na wawezeshaji hao ila wao wanatakiwa kushauri namna ya kutekeleza miradi hiyo.
“Nyie ni wataalamu mnapaswa kuwapa ushauri wananchi ili wafanikishe miradi hiyo lakini siyo kuwapangia kuwa wafanye mradi gani kwani wao ndiyo wanaojua mahitaji yao lengo likiwa ni wao kutatua changamoto zinazowakabili,” alisema Suleiman.
Alisema kuwa utekelezaji wa miradi ya kunusuru kaya maskini umefikia hatua nzuri ambapo kaya maskini za vijijini zimeweza kuongeza kipato na kuzifanya zisiwe kwenye hali ngumu wakati wa kaipindi cha Hari ambacho kinakuwa baada ya muda wa mavuno kupita.
“Tumeona akaya nyingi sasa zimeweza kupita mwaka mzima zikiwa bado na hali nzuri ya chakula kwani kwa kipindi cha nyuma zilikuwa zinaishiwa chakula kutokana na kuuza chakula ili kupata kipato cha kujikimu,” alisema Suleiman.
Awali mwakilishi wa mkurugenzi mkuu wa TASAF Mercy Mandawa alisema kuwa mradi huo wa awamu ya tatu emelenga kaya maskini zenye hali duni kwa lengo la kuongeza kipato kwenye mamlaka za serikali 161 nchini.
Mandawa ambaye ni Mtaalamu wa Mafunzo na Ushirikishaji wa Jamii TASAF makao makuu alisema kuwa hadi sasa miradi hiyo imeweza kuzifikia kaya milioni moja kote nchini tangu kuanzishwa mpango wa kuzisaidia kaya maskini mwaka 2012 ambayo ilizinduliwa na Rais Dk Jakaya Kikwete.
“Lengo la mradi huu ni kuhakikisha kaya maskini zinakuwa na kipato cha kuweza kujikimu kwa kuwapa ajira za muda ambapo mafanikio yameonekana kwani zimeweza kuwa na kipato na kuondokana na umaskini,” alisema Mandawa.
Aidha alisema kuwa Halmashauri zinatakiwa kuhakikisha zinapeleka fedha kwa wakati ili kuondoa malalamiko kwa walengwa ambapo kulikuwa na tatizo la ucheleweshaji wa utoaji wa fedha za ruzuku kwa kaya maskini.
Mradi huo kwa wilaya ya Kibaha utazifikia kaya 5,690 kwenye miradi ya kuhifadhi maji ya mvua, hifadhi ya misitu, miradi midogo midogo ya umwagiliaji, kilimo misitu cha kuchanganya mazao na miti, usafi wa mazingira maeneo ya mjini  (uzoaji wa taka ngumu), mafunzo hayo yamewahusisha wawezeshaji 24.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment