Tuesday, August 27, 2024

HALMASHAURI KIBAHA YATAKA MBWA WACHANJWE


HALMASHAURI ya Wilaya ya Kibaha imeagiza kuuwawa mbwa wote wanaozurura ambao wamekuwa wakingata watu na kuwaletea madhara.

Aidha imetaka kufanyika sensa ya wanyama hao ili idadi yake iweze kutambulika kwa wale wanaowafuga kwa utaratibu unaotambulika rasmi na kisheria.

Akitoa azimio hilo kwenye kikao cha Baraza la Madiwani kwa kipindi cha robo ya Aprili hadi Juni Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Erasto Makala alisema kuwa mbwa hao wamekuwa kero kwa watu.

Makala alisema kuwa mbwa hao wanaozurura hawana chanjo na wamekuwa wakingata watu hivyo kuhatarisha afya zao.

"Madhara ya mtu kungatwa na mbwa ni makubwa hivyo lazima kuwamaliza mbwa wanaozurura ambao hawana mwenyewe kwani hawana chanjo ya kuwakinga na magonjwa,"alisema Makala.

Alisema kuwa sensa ni muhimu kwa wanayama hao na Halmashauri ikiona kuna changamoto kuna haja ya kumpa mzabuni kwa ajili ya kuchanja mbwa ili kuwafikia mbwa wengi.

Akiibua hoja kuhusiana na mbwa wengi kutochanjwa Diwani wa Viti Maalum ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri Halima Jongo alisema mbwa hawajachanjwa ni wengi ukilinganisha na mbwa waliopo.

Jongo alitoa mfano wa Kata ya Ruvu kuna mbwa 361 lakini waliochanjwa ni 35 na Mtambani kuna mbwa 53 lakini hawajachanjwa ambapo Kata za Kwala na Magindu hakuna taarifa ya kuchanjwa mbwa.

Naye Diwani wa Kata ya Kilangalanga Mwajuma Denge alisema kuwa mbwa wasio na wamiliki ambao huzurura ndiyo wanaoleta madhara.

Mwajuma alisema kuwa ikifanyika sensa itakuwa vizuri kwani itakuwa rahisi kujua idadi na kutoa chanjo kwa mbwa na kwa wale wanaozurura wauliwe ili kuepusha madhara kwa wananchi.

Sunday, August 25, 2024

WAHITIMU WAASWA KUEPUKA VISHAWISHI

WANAFUNZI wanaohitimu masomo ya kidato cha nne na darasa la saba nchini watakiwa kuepukana na tamaa na vishawishi ili visikatishe ndoto zao za kuendelea na masomo.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa Chuo cha Diplomasia Jacob Nduye wakati wa mahafali ya Darasa la saba na Kidato cha nne Shule za Filbert Bayi.

Nduye alisema kuwa ili wanafunzi hao waweze kufikia ndoto zao wanapaswa kujiepusha na tamaa na vishawishi ambavyo vimekuwa kikwazo kufikia kule walikopanga kufika.

"Epukeni tamaa na vishawishi na vitu ambavyo havina maadili kwani ili ufikie malengo yako unapaswa kukaa mbali navyo ili ufikie ndoto zako ambazo umejiwekea,"alisema Nduye.

Alisema kuwa wazazi wanawasomesha wanatumia gharama kubwa wanajinyima ili wasome lakini baadhi wamekuwa wakikatisha masomo kutokana na kujiingiza kwenye vishawishi.

"Nyie ni tegemeo la Taifa kwa siku za baadaye lakini ili muwe tegemeo lazima msome na kuachana na matendo yasiyofaa ndani ya jamii hivyo lazima mjilinde,"alisema Nduye.

Aidha alisema kuwa wazazi nao wanapaswa kuwalea watoto wao kwenye maadili mema na washirikiane na walimu katika kuwalea watoto ili wawe na maadili mema kwani ni viongozi wa baadaye.

Naye Mwenyekiti wa bodi Taasisi ya Filbert Bayi alisema kuwa mbali ya shule hizo kufanya vizuri lakini inakabiliwa na changamoto ya ubovu wa barabara.

Bayi alisema barabara inayotoka Picha ya Ndege kwenda Jamaica na kutoka Jamaica kwenda Picha ya Ndege barabara hiyo ambayo inapita kwenye shule hizo ni mbaya na haijachongwa muda mrefu hivyo jamii inayozunguka shule inapata changamoto kubwa kwenda kupata huduma ya afya kwenye zahanati ya Bayi.

Akisoma risala ya wahitimu wa kidato cha nne Mariam Msabaha alisema kuwa mbali ya masomo ya kawaida pia walisoma masomo ya ujasiriamali ambayo yatawasaidia mara wamalizapo shule.

Msabaha alisema kuwa masomo hayo ni pamoja na ususi, mapishi, upambaji na utunzaji wa mazingira na masuala ya michezo ambapo shule imekuwa ikifanya vizuri kitaifa na kimataifa.



Thursday, August 22, 2024

HALIMA JONGO ACHAGULIWA MAKAMU MWENYEKITI BARAZA LA MADIWANI HALMASHAURI YA WILAYA YA KIBAHA.

BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha limemchaguaHalima Jongo kuwa makamu mwenyekiti baada ya aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo Shomari Mwinshehe kumaliza muda wake.

Sambamba na uchaguzi huo wa makamu mwenyekiti ambaye alipata kura zote 17 pia kamati mbalimbali nazo zilichaguwa wenye viti wake.

Jongo ameshukuru madiwani wenzake kwa kumchagua kwa kura nyingi na kusema atashirikiana nao pamoja na watumishi wa Halmashauri ili kuleta maendeleo kwa wananchi.

Amesema kuwa ataendeleza yale ambayo aliyoyafanya mtangulizi wake ili Halmashauri iweze kupata mafanikio ambayo itakuwa ni sehemu ya wananchi kujiletea maendeleo.

"Katika ukusanyaji mapato tumefanya vizuri kwenye awamu hii iliyopita kwa kushirikiana na wenzangu, wataalamu na wananchi kuhakikisha tunakuwa na makusanyo makubwa,"amesema Jongo.

Amesema kuwa jambo kubwa ni kupambana kuleta maendeleo kwa wananchi ambao wanawategemea kuwaonyesha njia.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Regina Bieda amesema kuwa anampongeza Makamu mwentekiti aliyepita na anamkaribisha Makamu mpya katika kuendeleza jitihada za maendeleo.

Bieda amesema watashirikiana wote kwa pamoja ili kuwapambania wananchi lengo waweze kupata maendeleo.



Wednesday, August 21, 2024

DC KIBAHA ATAKA MADIWANI KUKAGUA NA SI KUTEMBELEA MIRADI YA MAENDELEO











MKUU wa Wilaya ya Kibaha Nickson John amewataka Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya Kibaha kukagua miradi ya maendeleo na siyo kuitembelea.

John ameyasema hayo wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani cha robo ya nne Aprili hadi Juni kilichofanyika Mlandizi.

Amesema kuwa kukagua miradi ni tofauti na kutembelea ambapo unapokagua unaupata taarifa za kina tofauti na unapoitembelea.

"Tusitembelee miradi bali tuikague kwani pale tutapata fursa ya kujua mambo mengi tofauti na ukitembelea hupati taarifa za kina juu ya miradi ya maendeleo kwa wananchi,"amesema John.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Erasto Makala amesema kuwa wataongeza nguvu katika ukusanyaji mapato ili waweze kufikia malengo.

Makala amesema mafanikio kwenye ukusanyaji mapato ni mkubwa na kadri makusanyo yanavyoongezeka na miradi nayo inaongezeka hivyo kusogeza maendeleo kwa wananchi.

Wakati huo huo Baraza hilo limemchagua Diwani Halima Jongo kuwa makamu mwenyekiti baada ya aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo Shomari Mwinshehe kumaliza muda wake.

Sambamba na uchaguzi huo wa makamu mwenyekiti ambaye alipata kura zote 17 pia kamati mbalimbali nazo zilichaguwa wenye viti wake.

Jongo alishukuru madiwani wenzake kwa kumchagua kwa kura nyingi na kusema atashirikiana nao pamoja na watumishi wa Halmashauri ili kuleta maendeleo kwa wananchi.


Sunday, August 18, 2024

TAKUKURU PWANI KUTOA ELIMU KUELEKEA UCHAGUZI


KATIKA kukabiliana na vitendo vya rushwa kwenye mchakato wa uchaguzí Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani imejipanga kuzuia na kupambana na vitendo hivyo kwa kutoa elimu kwa makundi mbalimbali.

Hayo yalisemwa na Naibu Kamanda wa Takukuru mkoani humo Ally Haji wakati akizungumza na
waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha wanatarajia kuyafikia makundi yote yanayohusika na masuala ya uchaguzi.

Haji alisema kuwa baadhi ya makundi ni pamoja nan a vyama vya siasa, wasimamizi wa uchaguzi,
waandishi wa habari wananachi na jamii kwa ujumla.

"Kwa kipindi hichi cha mchakato wa uchaguzi tumeshaanza kufanya ufuatiliaji wa vitendo vya rushwa kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa, vitongoji na vijiji utakaofanyika mwaka huu na uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani,"alisema Haji.

Alisema kuwa wanatoa elimu ya madhara ya rushwa ambapo ni kosa kisheria endapo ikitumika
itasababisha kupatikana víongozi ambao siyo wazuri na hawataweza kuongoza wananchi kwa
weledi ambapo kauli mbiu inasema Kuzuia Rushwani Jukumu lako na langu Tutimize wajibu wetu. 

"Malengo ya kutoa elimu kwa makundi hayo ni kujiandaa kufanya uchaguzi usiokuwa na vitendo vya rushwa ili kupata viongozi bora wasiotokana na vitendo vya rushwa kwani ni adui wa haki na watu wote wana wajibu wa kupambana na vitendo hivyo,"alisema Haji.

Aidha alisema kuwa wataendelea kufanya udhibiti wa mapato ya serikali na usimamizi wa rasilimali za umma ikiwa ni pamoja na ufuatiliaji wa fedha zinazotolewa na serikali kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

"Tunatoa wito kwa wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada za kufichua vitendo vya rushwa na wala rushwa kwa kutoa taarifa sahihi zitakazowezesha kuwachukulia hatua wahusika hasa katika kipindi hichi tunapoelekea uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu,"alisema Haji.

Aliwataka watumishi wa umma na wa sekta binafsi watakeleze majukumu yao kwa kuzingatia sheria,
kanuni na taratibu za kazí zao ili kuzuia vitendo vya rushwa na kuleta tija katika kuhudumia wananchi ili
kuwaonyesha njia kwa ajili ya kujiletea maendeleo.

mwisho.

Friday, August 16, 2024

MUHARAKANI/MKUZA WAITAKA TARURA KUBORESHA BARABARA YA MTAA HUO

KUFUATIA changamoto ya ubovu wa barabara ya Jamaika kupitia shule ya Filbert Bayi wakazi wa Mtaa wa Muharakani Kata ya Picha ya Ndege Wilayani Kibaha wameitaka Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) kuifanyia matengenezo barabara hiyo ili kuwaondolea adha.

Wakizungumza na waandishi wa habari Mtaani hapo Mohamed Lukemo, Mathias John na Felix Swai walisema kuwa kutokana na ubovu huo umesababisha kalavati lililopo kwenye barabara hiyo kuwa hatarini kuvunjika ambapo kipindi cha mvua magari yalikuwa yakishindwa kupita.

Walisema kuwa barabara hiyo ilichongwa miaka sita iliyopita hali ambayo imeiacha barabara hiyo kwenye hali mbaya na kufanya wakazi hao kupata changamoto hasa kipindi cha mvua kutokana na kuwa na mashimo mengi.

"Tunawaomba Tarura waikumbuke barabara yetu kwani imeharibika vibaya sana na kwa wagonjwa ni changamoto kubwa sana hata magari yanayobeba wanafunzi yapita kwa taabu pale kwenye kalavati,"walisema wakazi hao

Aidha walisema magari yanapata ubovu na kwa wale wanaotumia pikipiki hupandishiwa nauli hasa kipindi cha mvua au wakati mwingine wanakataa kabisa kubeba abiria wanaopita barabara hiyo.

Ally Mohamed alisema kuwa wanashirikiana na wananchi ambapo wanajitolea kuikarabati barabara hiyo kwa baadhi ya maeneo korofi ili ipitike.

Mohamed alisema kuwa taarifa juu ya ubovu wa barabara hiyo wamezipeleka sehemu husika lakini utekelezaji ndo imekuwa changamoto ambapo waliambiwa wasubiri bajeti ya mwaka huu.

Naye meneja wa Tarura Wilaya ya Kibaha Mhandisi Samwel Ndoveni alikiri kuwa barabara hiyo ina changamoto lakini iko kwenye mpango wa kuchongwa.

Ndoveni alisema kuwa tayari wameshapeleka wataalamu kufanya tathmini na wiki ijayo watachonga barabara pamoja na kukarabati sehemu ya kalavati hivyo wananchi wasiwe na wasiwasi.


Wednesday, August 14, 2024

SERIKALI YATAKIWA KUWA NA VITUO VYA KULEA VIPAJI VYA WACHEZAJI WA UMISSETA NA UMITASHUMTA ILI KUINUA MICHEZO NCHINI

SERIKALI imetakiwa kuwa na vituo vya kuwaandaa wachezaji wenye vipaji wanaoshinda kwenye michezo ya UMISSETA na UMITASHUMTA ili viweze kushindana kwenye mashindano ya kimataifa.

Aidha imetakiwa kuwezesha shule au vituo vya watu binafsi ambavyo vinakuza vipaji vya wanafunzi ili kuja kupata wanamichezo wenye uwezo na kuliletea sifa Taifa.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) Filbert Bayi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya ushiriki wa Tanzania kwenye mashindano ya Kimataifa hususani ya Olimpiki.

Bayi alisema kuwa ili kuwa na timu bora ambazo zitashindana kwenye mashindano za kimataifa lazima kuwe na vituo ambavyo vitawaandaa vijana mahiri ambapo wataandaliwa.

"Siri ya kufanya vizuri ni kuwa na vituo maalum au shule ambazo zitawachukua vijana hao ambao wanafanya vizuri kwenye mashindano hayo na kuwaandaa kwa muda mrefu ili waweze kufanya vizuri kwenye mashindano mbalimbali ikiwa ni pamoja na Olimpiki,"alisema Bayi.

Alisema kuwa kuwe na uwekezaji kwenye kambi maalum siyo kwa ajili ya kushiriki mashindano makubwa bali kuwaandaa wale wenye vipaji ambapo kwa sasa hao wanaofanya vizuri haijulikani wanaenda wapi.

"Tuliambiwa kutakuwa na vituo au shule 56 lakini jatujui imeishia wapi kwani kwa sasa michezo inakwenda kisayansi ambapo wenzetu wamewekeza kwa vijana wao wenye vipaji ambap ndiyo wanaleta mafanikio,"alisema Nyambui.

Alibainisha kuwa fedha zinazorudishwa kwa wananchi kupitia uwekezaji zipelekwe kwenye masuala ya michezo ambapo asilimia tano ya michezo ya kubahatisha inapelekwa Baraza la Michezo BMT lakini ni ndogo inapaswa kuongezwa ili ilete matokeo.

"Kuna shule au vituo kama vile Allince, Kipingu, Makongo, Bagamoyo na Filbert Bayi ni sehemu ambazo zinafanya jitihada kuandaa vijana ni vema vikawezeshwa na serikali ili viweze kuandaa vizuri vijana kwani wanawagharamia vijana hao kwani wazazi wao hawana uwezo wa kuwasomesha,"alisema Bayi.

 Akizungumzia timu iliyoshiriki mashindano ya Olimpiki yaliyomalizika huko Ufaransa alisema wachezaji waliokwenda walikuwa na viwango vizuri lakini ilitokea tu bahati mbaya lakini waliandaliwa vizuri na kushinda au kushindwa ni matokeo tu.