Friday, December 30, 2022

DOREFA YAFANYA MKUTANO MKUU WA MWAKA



DOREFA YAFANYA MKUTANO MKUU WA MWAKA 2022

Na Elizaberth Paulo, Dodoma.

VIONGOZI wa michezo na wanamichezo nchini wameaswa kupambania tasnia ya michezo ili iwe na thamani na kupewa kipaumbele kama tasnia zingine ili ichangiae katika ukuaji wa uchumi wa nchini kama nchi zilizowekeza kwenye michezo Duniani. 

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa michezo Nchini Ally Mayai Tembele wakati akizungumza na wadau wa soka kwenye mkutano mkuu wa mwaka wa Chama Cha Mpira wa Miguu Dodoma(DOREFA).

Mkutano huo ulikuwa na lengo la kuweka wazi mambo yaliyofanywa na kamati tendaji tangu kuingia madarakani pamoja na changamoto zilizowakumba katika utendaji wao.

Mayai amesema kuwa ili tasnia hii ya michezo iendelee kukua ni wajibu wa kila mwanamichezo kuwajibika kwa nafasi yake katika kutoa elimu kwa jamii kuhusiana na Umuhimu wa michezo ikiwa ni sehemu ya kuimarisha afya zetu hata uchumi wetu hii itasaidia kukua kwa tasnia hii bila kusahau kuwa na nidhamu kwa kila mmoja kumuheshimu mwenzake bila kujali cheo.

“Nawapongeza chama cha soka cha Mkoa wa dodoma kwa kuweza kufanya kazi bila kuwa na tofauti katika utendaji na hii itasaidia soka la Dodoma kuweza kukua kwa kasi kwani maendeleo bora huletwa na viongozi bora,"amesema Mayai

Ameongeza kwa kupongeza mkoa wa Dodoma kwa kuwa na programu ya vijana chini ya miaka 17 kwani itawasaidia vijana kukua kisoka na kuweza kuvumbua vipaji wakiwa bado na umri mdogo.

"Milango ya serikali ipo wazi kwa yeyote mwenye nia njema na tasnia hii na tunawakaribisha wadau wote kuweza kujitokeza kusapoti vipaji vya watoto wetu kwani kila mtu anaelewa mpira ni ajira kwa ajili ya kukuza uchumi na kuondokana na umasikini na kila mtu ameshuhudia namna ambavyo familia nyingi zimejikwamua kiuchumi kupitia michezo,"amesema Mayai.

Aidha ametoa rai kwa wadau wa mpira wa miguu kupambania haki za watoto katika kupata maeneo ya wazi ya watoto hao kufanyia mazoezi ya michezo yao ikiwa ni haki ya msingi ya mtoto na serikali imetoa maeneo ya wazi katika kila mtaa kwaajili ya michezo na shughuli zingine za kijamii.

“Ndugu zangu wanamichezo tuingie mitaaani kwenda kusaka vipaji, tukaelimishe jamii kuhusiana na haki za watoto wetu katika suala zima la michezo alafu kuna maeneo ya wazi ambayo hayatumiki kwa kazi zilizopangwa sasa hili nawaachia fuatilieni maeneo ya wazi kwaajili ya hiyo michezo alafu huko mitaani ndiko kwenye chimbuko la mpira wa miguu na hata historia ya watu wengi maarufu waliofanikiwa kwenye soka historia yao inaonyesha wametokea mitaani,"amesema Mayai

Kwa upande wake mwenyekiti wa Chama Cha Mpira wa Miguu Dodoma (DOREFA) Mohamed Aden amesema kuwa anawashukuru wadau wa soka jijini hapa kwa kuendelea kutoa maoni na ushauri ili kuhakikisha wanaboresha sekta ya michezo haswa mpira wa miguu jijini Dodoma.

Naye mwakilishi wa wanamichezo Jijini Dodoma amesema sekta ya michezo iko vizuri ila wanaiomba serikali chini ya Waziri wa Michezo Mohamed Mchengerwa kuwatatulia changamoto inayojitokeza ya mara kwa mara ya uwanja wa Jamhuri kufungiwa mara kadhaa kutokana na matumizi mengine ambayo ni tofauti na michezo hivyo kufanya wapenzi wa soka Jijini hapa kukosa burudani ya mpira wa miguu na kutumia viwanja vingine vilivyopo nje ya Dodoma.


Friday, December 23, 2022

RAIS DK SAMIA ATOA VYAKULA VITUO VYA WATOTO

RAIS DK SAMIA ATOA ZAWADI VYAKULA KWA NYUMBA MALEZI YA WATOTO MKOA WA PWANI

Na John Gagarini Kibaha

RAIS wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan ametoa zawadi vyakula vya sikukuu ya Christmas na mwaka mpya makundi maalumu ili nao washerehekee kama walivyo watoto wanaoishi na wazazi.

Akimwakilisha Rais kukabidhi katika kituo cha kulelea watoto wanaoishi kwenye Mazingira magumu cha Makao ya Malezi Madina kilichopo Mtaa wa Vikawe kata ya Pangani Wilaya ya Kibaha Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge alisema kituo hicho kinawakilisha vituo 37 vilivyopo mkoa mzima.

Kunenge alisema kuwa Rais kwa kutambua makundi maalum ametoa zawadi hizo ili watoto hao washeherekee kama watakavyosheherekea wengine ambao wanaishi kwa furaha na familia zao.

"Nimekuja hapa kumwakilisha Rais wetu  amewaletea zawadi pamoja na salamu za sikukuu ya Christmas na mwisho wa mwaka ambapo amewaletea mbuzi wawili, mchele kilo 60, maharage kilo 40, mafuta lita 20, juisi na viungo mbalimbali,"alisema Kunenge.

Alisema kuwa wadau wa maendeleo na wenye uwezo kujenga tabia ya kujitolea kwa vituo vya watoto wenye mahitaji ambapo vitu vilivyotolewa ni pamoja na vitoweo ,mchele , maharage,mafuta ya kupikia ,vinywaji na viungo vingine mbalimbali vya kupikia.

Kwa upande wao watoto wa Makao ya Madina Zainab Athuman na Jumanne Manzi walimshukuru Mungu kwa kumwezesha Rais kupata na kuweza kuwapa zawadi hizo.

Naye Mlezi wa watoto Makao Malezi ya Madina Fatma Abdilai alisema kuwa wananchi waendelee kumuombea Rais Samia kwa mengi anayofanya nchini na kutekeleza ilani kwa kutambua makundi maalum.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kibaha Mjini Mwajuma Nyamka alimshukuru Mwenyekiti wa CCM Taifa Dk Samia kwa kuitendea haki ilani ya Chama na kujali watoto .

Mkoa huo una jumla ya makao ya malezi 37 yenye jumla ya watoto 1,301 na kituo hicho cha Madina kina watoto 30.


Mwisho

Saturday, December 10, 2022

WAJASIRIAMALI WATAKIWA KUWA WANYENYEKEVU

 


UNYENYEKEVU KWA WAJASIRIAMALI NI MSINGI WA BIASHARA-MAVUNDE

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

NAIBU Waziri  wa Kilimo ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini amewaasa wajasirimali wadogo wadogo kujifunza unyenyekevu pindi wanapokuwa katika shughuli zao. 

Mavunde ameyasema hayo katika ziara aliyoifanya pamoja na wajasirimali (Mama Lishe ) Mkoani Dodoma walipotembelea katika mashamba ya Waziri Mkuu Mstaafu Peter Pinda na kuishukuru  familia hiyo kwa ukarimu wao. 

Ziara hiyo ya kusherehekea maadhimisho ya Miaka 61 ya Uhuru wa Tanganyika na ambapo Naibu Waziri Mavunde aliitumia siku hiyo kwa kusaidia kuwaongezea mama lishe ujuzi katika ujasiriamali wao.

"Lipo jambo la kujifunza kwa sisi viongozi na kwenu nyie mliofika hapa tujifunze unyenyekevu jamani ukiagalia Waziri Mkuu Mstaafu Pinda kwa nafasi alizozishika lakini leo amekubali nimekuja na mama lishe na akakubali kututembeza shamba lote kwahiyo hapa ndipo tunajifunza Unyenyekevu,"alisema Mavunde.

Alisema kuwa ukiwa kiongozi ukiona watu hawaji kwako hata kuomba maji  ujue unashida kwani kiongozi maana yake ni kupokea watu hivyo Pinda na familia yake wana mioyo ya kipekee na ukarimu mkubwa sana. 

Aidha Mavunde ametumia ziara Hiyo kutangaza January kufanyika kongamano kubwa la siku ya MWANAMKE DODOMA JIJI ili kutathimi makubaliano ya mwaka mzima yalipofikia.

" Mimi nimejiitolea  kulilea  hili kundi ili nione mafanikio yao kila mmoja kwa nafasi yake nataka nione wanapiga hatua kutoka hatua moja kwenda hatua nyingine Serikali ya  CCM chini ya uongozi wa Rais Dk Samia imefanya kazi kubwa ya kuendeleza Dodoma inakuwa makao makuu  fursa zipo nyingi nataka nione akina mama  wa Dodoma wakichangamkia hizi fursa,"alisema Mavunde.

 "Siyafanyi haya ili mnichague kuwa mbunge wenu, Sifanyi siasa nafanya haya kwasababu niliomba dhamana ya kuwa kiongozi nina wajibu wa kuwasaidia watu wangu,"alisema Mavunde. 

Naye Waziri mkuu Mstaafu Mizengo Peter Pinda amewasihi kushirikiana kuifanya Dodoma kuwa ya Kijani kwani kila mtu mmoja akipanda mti itakua na mwonekano mzuri hiyo hudhihirishwa baada ya mvua kunyesha Dodoma inakuwa na muonekano mzuri.

Pinda alisema kuwa washirikiane katika kupanda miti ili kuifanya Dodoma ipendeze kwani mji ukiwa na kijani kingi ni mji unaovutia sana na kitu kingine yeye huwa anapenda kusema mjasiri wa mali na siyo mjasiriamali kwani ukishakua mjasiri wa mali utakuwa mbali kimaendeleo.

Alimwomba Mavunde amshirikishe kwenye hilo kongamano litakalofanyika Januari ili aweze kuhamasisha washiriki hao kupanda miti.
 
Nao baadhi ya wajasirimali waliozungumza kwa nyakati tofauti wametoa shukrani zao kwa Mavunde kwani hakuna mbunge aliyeifanya tukio kama hilo kwa kuwakutanisha na kuwapeleka katika mashamba ya Pinda kwani wamejifunza vitu vingi na kuahidi kwenda kufanyia kazi.

Mwisho. 

Monday, December 5, 2022

MIPANGO YAANDAA WATAALAMU


WAHITIMU WAANDALIWA KUAJIRIWA NA KUJIAJIRI.

Na Wellu Mtaki, Dodoma

CHUO cha Mipango na Maendeleo Vijijini kimejikita katika utoaji wa Elimu na vitendo katika kuhakikisha wanatoa wahitimu ambao watakaokwenda kujiajiri wenyewe na kuajiriwa.

Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Bi Jenifa Omolo akiwa mgeni rasmi aliyemwakilisha Waziri wa Fedha na Mipango Dkt Mwigulu Lameck Nchemba katika mahafali ya 36 ya chuo hiki cha Mipango ya Maendeleo Vijijini yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Bi Omolo amesema kuwa kutokana na Mafunzo yanayotokana katika chuo hiko Wahitimu Watatumia ujuzi huo waliopata katika Kujiajiri wenyewe na kwenda Kuisaidia jamii.

Aliwataka wahitimu na wale wanafunzi watakaoendelea na mafunzo kwa ngazi ya juu kuwa na chachu ya kuendelea kujifunza ili kuongeza maarifa,ujuzi na ubunifu unaohitajika katika kuboresha utendaji wao wa kazi.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Mipango Vijijini Prof. Hozen Mayaya ameeleza mafanikio waliyoyapata kwa mwaka 2021/2022 katika miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa Mabweni na Kumbi za mihadhara kwa kutumia fedha za vyanzo vya ndani ya chuo na Ruzuku kutoka Serikalini na kueleza matarajio yao ya 2022/2023 ya kujenga Maktaba kubwa na ya kisasa pamoja na bweni la wanafunzi katika eneo la Kisesa Jijini Mwanza.

Akisoma hotuba kwa niaba ya wanafunzi wenzake muhitimu Gift Kyando ameishukuru Serikali na Wizara ya Fedha na Mipango ambayo ni Wizara Mama ya chuo chao na kuomba Chuo kuendelea kuwasaidia ili waweze kusonga mbele zaidi hasa wanapohitaji kupata Barua za uthibitisho kutoka Chuoni .

Mahafali ya 36 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini ya mwaka 2022 yana jumlaya wanafunzi 6,225 waliohitimu wakiwemo wanaume 2,722 na wanawake 3,502 katika fani mbalimbali za Maendeleo vijijini.

Mwisho.

Wednesday, November 30, 2022

WAWEKA MIKAKATI KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA

WADAU WAENDELEA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA WILAYA YA KIBAHA



 IMEELEZWA kuwa uanzishwaji wa madawati kwenye shule na makundi mbalimbali ya jamii kutasaidia kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa matukio yanayohusiana na vitendo hivyo.


Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mwanasheria wa Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) Tanzania Zakia Msangi wakati wa kupita msafara unaotoa elimu ya kupambana ukatili wa Kijinsia ikiwa ni sehemu ya siku 16 za kupinga vitendo hivyo.

Alisema kuwa moja ya makundi yanayoathirika na vitendo hivyo ni watoto ambapo madawati hayo yataundwa kwa kushirikiana na walimu wa malezi kwenye shule.

"Madawati haya yatakuwa yakitoa elimu juu ya kupambana na ukatili wa Kijinsia na kuripoti vitendo hivyo kwenye vyombo husika ikiwemo dawati la jinsia na vyombo vingine vya sheria,"alisema Msangi.

Msangi alisema kwa shule kutakuwa na wanafunzi wawili vinara ambao watakuwa na ujasiri wa kujieleza na wenye usiri pia kutakuwa na sanduku la siri la kutolea maoni.

"Makundi mengine ndani ya jamii kama vile waendesha pikipiki nao wataunda madawati kwa ajili ya kupambana na matukio hayo ambapo itasaidia kukabili kwani ni kundi linalokumbana na mambo mengi,"alisema Msangi.

Aidha alisema kuwa Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) Tanzania ni waratibu wa kampeni hiyo ambapo wameungana na Mtandao wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia (MKUKI) ambao ndani yake kuna mashirika zaidi ya 100 kupambana na suala hilo.

Kwa upande wake ofisa Mawasiliano wa Shirika linalosaidia mashirika yanayotoa msaada wa sheria (LSF) Wilson Mtapa alisema kuwa wamewezesha msafara huo ili kupinga vitendo hivyo kwa kutoa elimu ya kupinga vitendo hivyo kwa kushirikiana na serikali na wadau wa maendeleo.

Mtapa alisema kuwa elimu hiyo inatolewa kwenye maeneo yenye mikusanyiko ya watu ikiwa ni pamoja na mashuleni madokoni na kwa vikundi vya waendesha bodaboda kwenye Wilaya msafara huo utakapopita kauli mbiu ikiwa ni Kila uhai unathamani tokomeza mauaji na ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Alisema kuwa mashirika hayo mbali ya kupambana na vitendo hivyo pia yanatetea haki za binadamu ambapo wanatoa elimu ya namna ya kukabiliana na vitendo hivyo ndani ya jamii na msafara huo ulioanzia Dar es Salaam Pwani utapita mikoa ya Morogoro, Singida, Shinyanga, Arusha na Musoma.

Naye mwakilishi wa Shirika la Maendeleo kwa Vijana YPC ambalo liko chini ya MKUKI ambao ndiyo walikuwa wenyeji wa msafara huo Fred Mtei alisema kuwa ujumbe uliotolewa wa kukabiliana na vitendo vya ukatili umewafikia watu wengi.

Mtei alisema kuwa wao kama wana harakati wataendelea kutoa elimu na kuielimisha jamii namna ya kukabiliana na vitendo hivyo.

Mkurugenzi wa Kituo Cha Msaada wa Kisheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga alisema kuwa wamekuwa wakipokea wateja ambao wengi wao ni wa vitendo vya ukatili wa Kijinsia.

Mlenga alisema kuwa wamekuwa wakishirikiana na vyombo vya sheria ikiwemo Polisi na mahakama kupambana na vitendo hivyo kwenye Wilaya na Mkoa mzima wa Pwani na wanatoa elimu kwenye maeneo mbalimbali na makundi ya kijamii.

 Kwa upande wake Mratibu wa Chama Cha Majaji na Mahakimu Tanzania kwa Mkoa wa Pwani Honorina Kambadu alisema kuwa wanazingatia haki na usawa mbele ya sheria na kukabili matukio ya ukatili wa Kijinsia.

Kambadu alisema kuwa baadhi ya matukio ni kama vile vipigo, unynyasaji na mauaji na kunyimwa haki zingine kwa wanawake na watoto ambao ndiyo waathirika wakuu wa vitendo hivyo.

Mwisho.

Tuesday, November 29, 2022

WAZIRI MKUU MAJALIWA ASEMA VIJANA WANAAJIRIKA


Na John Gagarini, Mkuranga

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa nchi inauwezo wa kuzingatia Utumishi kwenye sekta binafsi ili wawekezaji watumie vijana wa hapa nchini na kuachana na mawazo ya kuleta wafanyakazi kutoka nje ya nchi kwani Watanzania wanaajirika na ni waaminifu.

Majaliwa aliyasema hayo Kisemvule Wilayani Mkuranga Mkoani Pwani alipokuwa anazindua kiwanda na mabati cha Lodhia Group of Company na kusema kuwa vijana wa Kitanzania wanauwezo wa kufanya kazi na hakuna sababu ya wafanyakazi kutoka nje ya Tanzania.

Alisema kuwa vijana wa Kitanzania wanaajirika na wanafanya kazi kwa bidii na kwa sasa hata vitendo vya kutopenda kufanya kazi hilo halipo tena wanawajibika ipasavyo. 

"Waajiriwa zaidi ya 3,000 kitendo cha kutoa ajira umesaidia sana tutakuunga mkono uendelee kutoa vijana ambao wako mtaani itasaidia kufanya nchi kuwa na amani nchi imepanua wigo na fursa za uwepo wa viwanda,"alisema Majaliwa.

Aidha alisema uwepo wa kiwanda hicho umesaidia kutoa ajira na hiyo ni fursa kwa wengine inasaidia kuzalisha na kupanua wigo ili kusaidia watu wengine zaidi hapa ni ajira zaidi ya 2,500 hilo ni jambo kubwa.

"Serikali ya awamu ya sita imeweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji kuja kuwekeza kwa wale wa ndani na nje maelekezo tuliyopewa kuanzia kuomba kuwekeza na kuanza uwekezaji ni kuhakikisha hawapati shida wala kikwazo chochote ili kila upande unufaike mwekezaji na mwananchi,"alisema Majaliwa. 

Aliongeza kuwa kampuni hiyo ni moja ya kampuni inayolipa kodi kubwa nchini ambapo inalipa zaidi ya bilioni 40 kwa mwezi ni kama lulu watatatua changamoto zinazoikabili kwani nachangia pato la serikali na kusaidia huduma za jamii na inamuunga mkono Rais kwa kupunguza changamoto ya ajira.

"Hapa Tanzania ni sehemu salama ya uwekezaji tunatambua na tunaheshimu uwekezaji huu kwani huyu ni wa kuenziwa na Halmashauri ili wapate fedha zaidi na hatimaye nchi inufaike hakika leo nimefurahi sana kutembelea kiwanda hichi ambapo Arusha nlitembelea walikuwa na kiwanda kidogo sana uwekezaji mkubwa na malengo kuweka mradi mkubwa zaidi naifurahi kutembelea,"alisema Majaliwa.

Alibainisha kuwa kiwanda hicho kinachozalishwa chuma mbalimbali zikiwemo nondo ni kikubwa kuliko viwanda vyote alivyotembelea na kuweka jiwe la msingi la kiwanda ukubwa wake ni hekari nane na nusu kitatengeneza bati.

"Uwepo wa viwanda vya nondo, plastiki, mabomba ya maji na bati itasaidia bidhaa kwani zitapatikana hapa nchini badala ya kuagiza nje na pia zina ubora bado eneo dogo kufikia kiwanda cha Afrika Mashariki itafikia hatua hiyo na kuwa kiwanda kikubwa hapa Afrika Mashariki,"alisema Majaliwa.

Aliongeza kuwa uwepo wa viwanda vijana Teknolojia na hilo limepewa kipaumbele ili wajifunze kupitia mitambo hiyo ya kisasa ni faida ya uwepo wa viwanda nchi itakuunga mkono na milango itakuwa wazi na azma ya kutembelea ni kuangalia uwekezaji unaofanywa ukiwemo kwenye mabomba ya maji na serikali inaona kuwa anafunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan alisema na kuwahakikshia kuwa uwekezaji hautakwama hata kidogo.

Kwa upande wake Mwenyekiti na mwanzilishi wa kampuni hiyo Haroun Lodhia alisema kuwa kiwanda chao kinalipa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 22 kwa ajili ya umeme na gesi ambapo baadaye watakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 40,000 za chuma kwa mwezi.

Lodhia alisema kuwa kwa siku za baadaye watazalisha umeme wao wenyewe ambapo wataanza kuzalisha megawati tano na baadaye kva 25 na wanaishukuru serikali kwa kuwawekea mazingira mazuri kuendesha shughuli zao.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdala Ulega alisema kuwa kutokana na uwekezaji mkubwa uliopo kwenye Wilaya ya Mkuranga na wingi wa magari yanayokwenda mikoa ya Kusini wangeomba barabara ya Kusini ipanuliwe na kuwa ya barabara nne.

Ulega alisema kuwa barabara hiyo kuanzia Mbagala Rangitatu kwenda Mwandege Vikindu na kuendelea ingepanuliwa ili bidhaa ziweze kwenda kwa urahisi na pia hapo Mkuranga viwanda vingi tumia umeme mkubwa na hakuna gari la Zimamoto ikitokea moto itakuwa ni shida sana hivyo wapatiwe huduma ya gari hilo.

Mwisho.


Friday, November 25, 2022

CHANJO COVID-19


VIJANA WAJITOKEZE KUCHANJA COVID-19

VIJANA nchini wametakiwa kujitokeza kupata chanjo ya ugonjwa COVID 19 na waachane na dhana potofu kuwa hawawezi kuambukizwa ugonjwa huo.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mtaalam wa chanjo kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Caroline Akim alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na chanjo ya COVID 19. 

Akim alisema kuwa moja ya kundi kwenye jamii ambalo halijitokezi kuchanja wakidhani kuwa hawawezi kupatwa na ugonjwa huo hivyo kuwa hatarini kuambukizwa ugonjwa huo.

"Vijana wanadhana kuwa hawawezi kupata ugonjwa huo kwani baadhi hawana dalili ya maambukizi licha ya kuwa wao ndiyo wenye pilika pilika nyingi,"alisema Akim.

Alisema kuwa vijana ni kundi ambalo linahimizwa kupata chanjo kutokana na kuwa na mizunguko mingi kwenye jamii na kuwa rahisi zaidi kueneza ugonjwa huo pale wanapoupata.

"Wajawazito pia wanahimizwa kupata chanjo ya COVID-19 kwani wakipata ugonjwa huu wako kwenye hatari ya mimba kutoka au mtoto kuzaliwa kabla ya wakati na hata wanaonyonyesha wanakumbushwa kuwa chanjo ni salama kwao haina madhara kwa mtoto" alisema.

Aidha alisema kuwa waandishi wanatakiwa  sasa kuwakumbusha wananchi umuhimu wa kuchanja lakini pia faida zake ili kuepuka kuingia kwenye athari wanapopata ugonjwa huo.

Naye Mratibu wa chanjo mkoa wa Pwani Abas Hincha alisema kuwa wanatarajia kuanza kampeni ya chanjo ya COVID-19 inaanza Novemba 25 na watawafikia wananchi ambao bado hawajapata chanjo.

Hincha alisema kuwa Mkoa huo unatarajia hadi kufikia Desemba 30 kuwafikia wananchi 757,465 na kwamba hadi kufikia Novemba 22 walengwa 468,187 tayari wamepata chanjo sawa na asilimia 63.