Friday, August 4, 2017

KIJANA WA KIUME MVAA DERA BADO ASHIKILIWA NA POLISI


Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi limesema kuwa bado linaendelea kumshikilia kijana wa kiume mkazi wa Mbagala Jijini Dar es Salaam ambaye alivalia mavazi ya kike ikiwemo dera hijabu na kuficha sura yake kwa kuva nikabu.

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana alisema kuwa kijana huyo alikamatwa Agosti 2 maeneo ya Picha ya Ndege barabara ya kuelekea Magereza huku akiwa amevaa mavazi hayo.

Shana alisema kuwa kwa sasa jeshi hilo bado linamshikilia kijana huyo kwa ajili ya mahojiano ili kubaini mtandao anaoshirikiana nao kwenye matukio ya uhalifu.

“Kijana huyu tulimkamata baada ya kumwekea mtego uliowekwa na makachero wetu waliokuwa wamepata taarifa kutoka kwa wasiri waliokuwa wanamtilia mashaka na walifanikiwa kumkamata akiwa kwenye bodaboda akielekea maeneo ya Magereza,” alisema Shana.

Alisema kuwa hadi sasa bado hawajajua kijana huyo alikuwa na lengo gani la kuvaa nguo hizo za kike hali ambayo hadi sasa bado haijafahamika hasa alidhamiria nini.

“Hadi sasa tunaendelea kumhoji kujua ni kwanini avae mavazi ya kike na tunawashukuru wananchi na wasiri wetu kwa kuendelea kutupa ushirikiano wa kufanikisha kukamatwa kwa wahalifu,” alisema Shana.


Mwisho.

Thursday, August 3, 2017

WAZIRI NCHEMBA ALIA NA WANAOWASIDIA WAHAMIAJI HARAMU





                                    Na John Gagarini, Kibaha

SERIKALI imesema imefika wakati kuwakamata watu wanaowasaidia kuwalipia faini wanazopigwa wahamiaji haramu mara wanapohukumiwa mahakamani.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mwigulu Nchemba alipotembelea ofisi za Uhamiaji mkoa wa Pwani na kusema kuwa watu hao ndiyo wanaosababisha kuendelea kuingia kinyume cha sheria wahamiaji haramu.

Nchemba alisema kuwa nchi imekuwa ikiingia gharama kubwa kuwatunza wahamiaji haramu wanapoingia nchini na nchi kutumia muda mwingi kuhangaika na wahamiaji hao.

“Hii ni mipango kwani wameshafanya biashara hii kama halali na kuona kuwa hata wakiwalipia adhabu za fedha zinazotolewa na mahakama na kufanya wahamiaji hawa kuingia mara kwa mara hivyo wanaokuja kuwalipia nao kamateni, magari wanayosafirishia wahamiaji haramu taifisheni na boti wanazotumia kamateni,” alisema Nchemba.

Alisema inashangaza kuona Watanzania eti wanawalipia faini wanazopigwa kama adhabu baada ya kubainika kuingia nchini bila ya kibali jambo hilo halikubaliki.

“Hii ni biashara ambayo kuna baadhi ya wenzetu wanajihusisha nayo ndiyo maana tatizo hili haliishi na pia kuna baadhi ya watumishi wa serikali nao wanahusika na tutawachukulia hatua kali watakaobainika kushiriki kwenye mtandao huu wa kuwaingiza wahamiaji haramu,” alisema Nchemba.

Aidha alisema kuwa nchi haiwezi kutumia fedha ambazo zingetumika kwa ajili ya kununulia dawa za wagonjwa mahospitalini, kujenga barabara, kuboresha mazingira ya upatikanaji wa elimu na fedha hizo kuzipeleka kuwahudumia wahamiaji haramu jambo hilo hatutakubali liendelee.

Awali Ofisa Uhamiaji mkoa Plasid Mazengo alisema kuwa changamoto kubwa inayowakabili ni upungufu wa vitendea kazi ikiwa ni pamoja usafiri na boti kwa ajili ya kudhibiti wahamiaji haramu ambao wamekuwa wakitumia bandari ya Bagamoyo ambayo ina vipenyo vingi vya kuingilia nchini.

Mazengo alisema kuwa changamoto nyingine ni ukosefu wa wakalimani kwa ajili ya kutafsiri lugha za Kihabeshi na upungufu wa watumishi kwenye baadhi ya wilaya.

Mwisho.

PICHA YA NDEGE WAPATA ENEO UJENZI SHULE YA SEKONDARI

Na John Gagarini,Kibaha

KATA ya Picha ya Ndege imepata eneo lenye ukubwa wa hekari 11 kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari ya Kata ambapo kwa sasa wanafunzi wanaotoka kata hiyo wanasoma shule ya sekondari ya kata kwenye mtaa wa Mkuza.

Hayo yalisemwa na Diwani wa Kata hiyo Robert Machumbe wakati wa mkutano wa kata uliofanyika kwenye shule ya Msingi ya Lulanzi na kusema kuwa eneo hilo limepatikana kutokana na jitihada zake na wananchi.

Machumbe alisema kuwa licha wanafunzi wanaotoka kwenye kata yake wanasoma kwenye mazingira magumu kwani darasa moja linawanafunzi 450 hali ambayo inafanya usomaji kuwa mgumu.

“Watoto wetu wanapata shida kwanza kule ni mbali na pia madarasa yao yamejaa wanafunzi hivyo hupunguza ari ya usomaji na ufaulu kuwa mdogo,” alisema Machumbe.

Naye Thomas Raymond alisema kuwa ujenzi wa shule hiyo itakuwa mkombozi kwa wanafunzi wanaotoka kwenye kata hiyo ambayo ni mpya ikiwa haina shule yake ya sekondari.
Raymond alisema kuwa wao wako tayari kuchangia ujenzi wa shule hiyo mara wakati utakapofika ili kuhakikisha shule hiyo inajengwa haraka kwenye kata yao.

Mwisho.


HALMASHAURI YA MJI KIBAHA YAOMBWA KUTENGA FEDHA KWA WATU WENYE ULEMAVU

Na John Gagarini, Kibaha

WADAU wa watu wenye ulemavu kwenye Halmashauri ya Mji Kibaha wameiomba Halmashauri hiyo kutenga asilimia moja ya mapato ya ndani kwa ajili ya kukabili changamoto za ulemavu.

Hayo yalisemwa na Methew Chungu mwezeshaji wa  mafunzo yaliyoandliwa na Shirikisho la Watu wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) Kibaha Mjini kwa wadau wa huduma za afya kwa watu wenye ulemavu.

Chungu alisema kuwa mapato hayo yangesaidia kuwapatia huduma mbalimbali watu wenye ulemavu zikiwemo za kiafya, elimu, kiuchumi na huduma nyingine za kiutu.

Naye katibu wa SIVYAWATA Kibaha Mjini Happiness Matagi alisema kuwa kwa sasa changamoto za upataji huduma kwa watu wenye uelemavu zimepungua ambapo kumwona daktari kwa ni bure.

Matagi alisema kuwa kupitia kituo chao cha watu wenye ulemavu kilichopo Kwa Mfipa wanatoa huduma mbalimbali za kiafya hasa kwa wale walemavu wa viungo pamoja na shughuli za ujasiriamali.

“Pale watu wenye ulemavu wanafanya shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na kufuma, kushona nguo na mradi wa matofali ambao uko mbioni kuanza lengo kuwakwamua watu wenye ulemavu ili wasijione wanyonge na kuachana na tabia ya kuomba ambayo itawafanya washindwe kujitegemea,” alisema Matagi.

Kwa upande wake mwakilishi wa mganga mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Dk Mariamu Mgaya alisema kuwa watu wenye ulemavu wamekuwa wakisaidia ili kuhakikisha wanapata huduma za afya bila ya usumbufu kwa kuwapa kipaumbele.

Akijibu baadhi ya hoja ofisa mipango wa Halmashauri ya Mji Kibaha Amkauane Ngilangwa alisema kuwa katika bajeti iliyopitishwa watu wenye ulemavu wametengewa kiasi cha shilingi milioni 10.


Ngilangwa alisema kuwa pia wanapatiwa vitu mbalimbali ikiwa ni pamoja na mafuta ya kuwasaidia watu wenye ulemavu wa ngozi albino ili ngozi zao zisiharibike na fimbo kwa ajili ya wasioona. 

UCHAGUZI CHAMA CHA NETIBOLI PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA Cha Netiboli mkoa wa Pwani (CHANEPWA) kinatarajia kufanya uchaguzi wake Agosti 5 mwaka huu.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na ofisa michezo mkoa wa Pwani Grace Bureta na kusema kuwa uchaguzi huo utafanyika Tanita mjini Kibaha.

Bureta alisema kuwa mchakato wa uchaguzi huo unaendelea ambapo usaili unatarajiwa kufanyika wiki hii ili kuwapitisha wadau watakaogombea nafasi mbalimbali.

“Mchakato unaendelea na tunasubiri taarifa kutoka kwenye wilaya za mkoa wetu ili watuletee majina ya wagombea na baadaye tufanye usaili wiki hii ili kuwapata wale wenye sifa,” alisema Bureta.
Alisema kuwa fomu zilianza kutolewa tangu Aprili lakini baadye uchaguzi huo uliahirishwa kutokana na sababu mbalimbali ambapo sasa unafanyika kesho endapo taratibu zitakuwa ziko sawa.

“Fomu zote zinatakiwa zirejeshwe kwa maofisa michezo wa wilaya ambao nao wataziwasilisha mkoani kwa ajili ya taratibu za uchaguzi huo ambao utawaweka madarakani viongozi wapya kwa kipindi cha miaka minne,” alisema Bureta.

Aidha alisema kuwa uchaguzi huo unatarajiwa kusimamiwa na kamati ya michezo ya mkoa na kuwataka wagombea hao kutimiza taratibu ili wawanie nafasi hizo.


Mwisho. 

MWIGULU ATAKATAARIFA ZA WATANZANIA ZIUNGANISHWE MTANDAONI


                                     Na John Gagarini, Kibaha

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mwigulu Nchemba ametaka taarifa za Watanzania ziunganishwe kwenye mtandao tangu wanapozaliwa ili wasipate usumbufu wa kupata barua za utambulisho wanapotaka huduma mbalimbali.

Aliyasema hayo wakatia alipotembelea jengo jipya la kisasa la vitambulisho vya Taifa (NIDA) na kusema hakuna haja ya mtu kila anapoomba huduma fulani awe na barua ya utambulisho toka kwenye mtaa anaoishi.

Nchemba alisema kuwa kwa sasa mifumo inakwenda kisasa na mtu anapotaka huduma fulani wanakwenda kwenye mtandao na kupata taarifa zote za muhusika.

“Mfano mtu anataka paspoti, leseni, kusajili biashara, laini za simu na huduma nyingine hapaswi kuwa na mabarua kwa kila huduma anayoitaka bali wanaangalia tu kwenye mifumo hii na kuzipata taarifa za mtu,” alisema Nchemba.

Alisema kuwa uunganishaji wa taarifa za wananchi na kuwa na utambulisho wa aina moja utasaidia kupata taarifa na itaonyesha kama ni dereva kujua ni makosa gani aliyokwisha kuyafanya hivyo ni rahisi kumdhibiti.

 “Mifumo hii ya kimtandao itasaidia sana kuhuisha huduma nyingi ambazo mtu anapaswa kwenda kwenye ofisi mbalimbali bali anaweza kutumia ofisi moja kupata taarifa zozote zinazotakiwa,” alisema Nchemba.

Aidha alisema kuwa taarifa hizo zitasaidia hata kupunguza kuwabaini raia wageni ambao wanaingia nchini kinyemela ambao hawaeleweki wako kwa ajili ya madhumuni gani.

Naye kaimu mkurugenzi wa uzalishaji wa Vitambulisho Alfonce Malibiche alisema kuwa ujenzi huo umefikia hatua za mwisho na wanatarajia utakamilika mwishoni mwa mwezi huu au mwanzoni mwa mwezi ujao.

Malibiche alisema kuwa mara ujenzi huo utakapokamilika vitambulisho vya uraia vitakuwa vikizalishwa hapo ambapo kwa sasa ujenzi huo uko mwishoni.

Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka aliomba serikali ikitoa ajira izingatie wakazi wa wilaya hiyo na mkoa wa Pwani ili iwe manufaa kwa kujengwa ofisi hizo.

Koka alisema kuwa uzingatiaji wa kuajiri vijana na wataalamu kutoka kwenye eneo husika utaleta manufaa makubwa kwa mkoa huo ambao unainukia kwa kasi katika uwekezaji ukiwemo wa viwanda.

Mwisho.

KIJANA AIGIZA SAUTI YA KIKE AVAA DERA NA HIJABU BODABODA AINGIA MKENGE


Na John Gagarini, Kibaha

KIJANA mmoja anayekadiriwa kuwa na miaka (19) mkazi wa Mbagala Maji Matitu amejikuta yuko kwenye wakati mgumu baada ya kukutwa akiwa amevaa nguo za kike aina ya dera na kusababisha taharuki kwa wakazi wa Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa wa Picha ya Ndege Joseph Zambo alisema kuwa kijana huyo alikuwa akiwasiliana na mtu akijifanya kuwa yeye ni mwanamke.

Zambo alisema kuwa kijana huyo alifika kwenye mtaa wake Agosti 2 majira ya sa 4:30 asubuhi akimfuata mtu waliokuwa wakiwasiliana naye kwa njia ya simu ambaye inadaiwa kuwa ni dereva bodaboda.

“Watu hawa walikuwa wakiwasiliana kwa njia ya simu na kijana huyo alikuwa akiigiza sauti ya kike na dereva bodaboda alijua fika kuwa aliyekuwa anawasiliana naye ni mwanamke,” alisema Zambo.

Alisema kuwa dereva bodaboda huyo alimwona kijana huyo kupitia ukurasa wake wa facebook ambapo ulipambwa na picha za msichana hali ambayo ilimfanya avutiwe naye.

“Mawasiliano yalianza kama siku tatu zilizopita na walikubaliana na ndipo bodaboda huyo alimwambia njoo Picha ya Ndege Kibaha lakini kijana huyo alipitiliza hadi Kongowe na ilibidi arudi ashukie Picha ya Ndege na alimwelekeza akishuka apande bodaboda ili aende kwake eneo la Sofu,” alisema Zambo.

Aidha alisema kuwa aliposhuka waendesha pikipiki walikuwa wakimfuatilia na wlimwona amevaa dira na usoni kajifunga kitambaa ambacho kiliacha wazi macho tu kama vile ninja akapandishwa kwenye pikipiki na kuanza safari ya kwenda kwa mtu wake.

“Wakiwa njiani upepo ulipuliza na dereva wa bodaboda akashangaa kuona miguu ya kiume lakini amevaa viatu vya kike akashtuka na kugeuza pikipiki kule alikotoka na ndipo madereva bodaboda walipojaa na kuanza kumzonga hali iliyowabidi wamlete ofisini kwangu na ilikuwa tafrani kubwa huku wengine wakitaka kumpiga wakidai ni mwizi wa pikipiki,” alisema Zambo.

Alibainisha kuwa baada ya kumfikisha walimfunua na kukuta kuwa ni mwanaume na kuanza kumhoji ndipo aliposema kuwa alikuja Kibaha kuja kuchukua hela na haikujulikana alikuja kuzichukua hizo fedha kwa njia gani.

“Zogo lilizidi pale huku bodaboda wakitaka kumpiga ndipo ikabidi tuchukue gari na kumpeleka polisi kwa ajili ya usalama wake na kueleza ni kwa sababu gani alijifanya mwanamke na fedha hizo anazichukua kwa njia gani,” alisema Zambo.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa atalitolea taarifa tukio hilo baada ya kutoka kwenye msafara wa kiongozi.


Mwisho.