Wednesday, January 20, 2016

MAMA NA WATOTO WAKE WAWILI WAFA KWA RADI WATATU WAJERUHIWA

Na John Gagarini, Pwani
MVUA zinazoendelea kunyesha hapa nchini zimeendelea kuleta madhara baada ya Mama na watoto wake wawili kufa huku watu wengine watatu wakijeruhiwa baada ya kupigwa na radi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu ofisa mtendaji wa kata ya Mchukwi wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Ami Lipundundu alisema kuwa familia hiyo ilikuwa ikiota moto baada ya kuchota maji ya mvua.
Lipundundu alisema kuwa tukio hilo lilitokea Januari 18 mwaka huu majira ya saa 11 jioni kwenye Kijiji cha Mchukwi B walipokuwa wanaota moto baada ya mvua kunyesha.
Aliwataja marehemu hao kuwa ni Decilia Simba (42) watoto wake Debora Simba (4) na Amani Matimbwa 1 na nusu huku waliojeruhiwa wakiwa ni Maua Ngwande (13) anayesoma darasa la sita shule ya Msingi Mchukwi, Suzana Daudi (12) na mdogo wa marahemu aitwaye Mama Tariq.
“Marehemu alitoka kwenye kikundi cha kuweka na kukopa cha Jitegemee ambapo yeye ni mwanachama alipofika nyumbani mvua ikaanza kunyesha akawa anakinga maji ya mvua yeye na watoto wa ndugu yake,” alisema Lipundundu.
Alisema kuwa baada ya hapo waliwasha moto kwenye jiko lao ambalo liko jirani na mti wa Mfenesi na kuota kwani walikuwa wameloa ndipo radi ilipopiga ikakwepa mti ikawapiga wao.
“Marehemu na wanawe walifia njiani wakati wakipelekwa Hospitali ya Mchukwi kwa ajili ya matibabu ambapo majeruhi bado wamelaazwa hopsitalini hapo na hali zao zinaendelea vizuri,” alisema Lipundundu.
Aidha alisema kuwa wiki iliyopita mtu mmoja naye alifariki kwa kupigwa na radi na mwishoni mwa mwaka jana huko Ikwiriri mtu mmoja pia alifariki dunia. Polisi mkoa wa Pwani walithibitisha kutokea kwa tukio hilo la kusikitisha.
Mwisho.

Monday, January 18, 2016

NDC YAPEWA MIEZI MITATU

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imelipa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) miezi mitatu kuhakikisha linapata kiasi cha dola za Kimarekani Milioni 2.1 kwa ajili ya kiwanda cha Viuadudu vya Kuua Viluwiluwi vya Mmbu wanaoeneza Ugonjwa wa Malaria Tanzania Biotech Product Ltd kilichopo wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Aidha alishangazwa na shirika hilo kwa kuajiri wafanyakazi 143 Julai mwaka 2015 ambao wanalipwa mishahara pasipo kuzalisha kitu chochote kwani wanapokea mishahara ya bure jambo ambalo alisema kuwa halipendezi.
Agizo hilo limetolewa jana mjini Kibaha na katibu mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Dk Adelhelm Meru alipotembelea kiwanda hicho ambacho kilizinduliwa Julai 2015 na Rais mstaafu Dk Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu wa Ethiopia.
Dk Meru alitoa agizo hilo kutokana na kutoridhishwa na maombi ya NDC kuomba kiasi hicho serikalini kutoka kwa Godwill Wanga Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Shirika hilo kwa lengo la kufanya majaribio pamoja na kuanza uzalishaji.
“Serikali haiwezi kutoa kiasi hicho cha fedha ambazo zingetumika kwa ajili ya huduma za jamii hivyo fanyeni kila njia kwa kukopa kwa kufanya nini ombeni hata benki ya uwekezaji nchini TIB ili mhakikishe mnapata fedha hizo na majaribio yanaanza ili uzalishaji uanze tumechelewa kwa kipindi cha miaka minne,” alisema Dk Meru.
Alisema kuwa inatosha kwani serikali ililipa gharama zote za ujenzi wa kiwanda hicho dola milioni 22 na kilitakiwa kianze kazi tangu mwaka 2012 ikasogezwa hadi Julai 2015 lakini hadi sasa ni miezi sita imepita lakini uzalishaji bado.
“hatuwezi kuwa kioja tafuteni fedha hizo dola milioni 1 kwa ajili ya majaribio na dola milioni 1.2 kwa ajili ya mtaji kwani malengo ya serikali ilikuwa na lengo kiwanda kianze kazi kwa muda uliopangwa ili kiweze kukabiliana na ugonjwa wa Malaria na ziada ya dawa kuuzwa nje ya nchi hivyo kuweza kufikia malengo yaliyowekwa,” alisema Dk Meru.
“Nataka ifikapo Mei Mosi mwaka huu mimi nije na Waziri wangu ili tuone uzalishaji unaanza mara moja kwani moja ya sera za nchi hasa katika awamu hii ya tano ni kujenga uchumi kupitia viwanda na kuwa nchi yenye uchumi wa kati ili kuleta maendeleo ya wananchi pia iko kwenye dira ya mpango wa maendeleo wa miaka mitano,” alisema Dk Meru.
Awali akielezea juu ya maendeleo ya kiwanda hicho Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji wa NDC Wanga alisema kuwa baadhi ya vifaa kwenye mashine ziliathiriwa na umeme kutokana na na kukatika katika hali ambayo ilisababisha uzalishaji ushindwe kuanza.
Wanga alisema kuwa kutokana na ucheleweshaji huo wa kuanza kufanya kazi ilibidi wataalamu kutoka nchi ya Cuba inakotoka teknolojia hiyo Labio Farm kudai gharama zaidi za ujenzi hivyo kudai fidia.
“Kiwanda hichi kinahitaji msaada hata kwa mkopo kiasi cha dola milioni 2.1 ili kuweza kukamilisha hatua zilizobakia kwani wataalamu wetu wameishiwa mtaji baada ya muda kuongezeka na kutokana na matatizo ya kuharibika vifaa vya mashine za kiwanda hichi,” alisema Wanga.
Alisema kuwa teknolojia hiyo ni mpya na mara uzalishaji utakapoanza itasaidia kukabiliana na ugonjwa wa Malaria kwani dawa hiyo ina uwezo wa kuua mazalia ya mbu na baadaye kitakuwa na uwezo wa kuzalisha bidhaa nyingine ikiwa ni pamoja na mbolea na madawa mbalimbali.
Mwisho.

Thursday, January 14, 2016

PANGANI YAPIGA MARUFUKU MUZIKI WA VIGODORO

Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA vijana wawili kuchomwa moto na mmoja kujeruhiwa mwishoni mwanzoni mwa wiki hii kwenye mtaa wa Vikawe kata ya Pangani wilayani Kibaha mkoani Pwani kamati ya ulinzi na usalama ya kata imepiga marufuku muziki wa vigodoro ili kuepusha mauaji kama hayo.
Marufuku hiyo inakuja baada ya tukio la kufa vijana hao ambao ni Alex Kapungu (18), Godfrey Ernest huku Omary Mohamed akijeruhiwa kwenye tukio lililotokea januari 10 mwaka huu majira ya saa 2:50 usiku kwenye mtaa huo, baada ya vijana hao kutuhumiwa kuwa ni wezi baada ya kuibuka kwa vurugu zilizosababisha baadhi ya vijana waliokuwa kwenye mziko huo kufanya uporaji kwenye maduka.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana diwani wa kata ya Pangani Agustino Mdachi alisema kuwa kamati ya ulinzi na usalama ilifikia hatua hiyo baada ya kujiridhisha kuwa muziki huo umekuwa chanzo cha vurugu ambazo zimesababisha vifo pamoja na wizi kwenye maeneo unakopigwa muziki huo.   
Mdachi alisema kuwa hilo ni tukio la pili la mauaji ambayo yametokeo kwenye muzikio huo ambao unatumiwa sana na waendesha pikipiki ambapo imebainika kuwa waendesha bodaboda hao hasa wale wanaofanya biashara nyakati za usiku maarufu kama Mapopo wengi wao ni wezi na hujificha kwenye mgongo wa kazi hiyo.
“Uchunguzi umebaini kuwa wengi wa wa mapopo hao hujihusisha na vitendo vya wizi kwani wakati muziki unaendelea huanzisha vurugu na na kuwaibia watu ambapo wengi wao huwa na mapanga wanapokwenda kwenye muziki huo ambao unatamba kwa sasa,” alisema Mdachi.
Alisema kuwa kutokana na kubaini kuwa muziki huo umekuwa ukichangia vitendo vya uhalifu katika kata ya Pangani waliamua kwa pamoja kuzuia upigwaji wa muziki huo kwa kipindi kisichojulikana ili kuepukana na vitendo hivyo vya uhalifu pamoja na mauaji.
“Kwa ujumla Kigodoro mara nyingi hakiishi salama kwani mara nyingi vurugu zimekuwa zikitokea na vijana wanauana kutokana na muziki huu hivyo tumeamua kusitisha muziki huu ili kupunguza wimbi hili la uhalifu na mauaji,” alisema Mdachi.
Aidha alisema kuwa kwa sasa wameamua kufanya doria kwa muda wote kwa kushirikiana na vyombo vya dola ili kukabiliana na matukio hayo ya kihalifu ambayo mengi yanafanywa na waendesha pikipiki.
Mwisho.

ARDHI KUPIMWA KWA NJIA YA KILETRONIKI KWA MAJARIBIO MIKOA MITATU HATI KUPATIKANA KWA SIKU MOJA

Na John Gagarini, Kibaha

WIZARA ya Ardhi na Makazi iko kwenye mpango wa kupima maeneo yote hapa nchi kupitia mpango wa majaribio wa kutoa hati za kumiliki ardhi kwa njia ya Kieletroniki ndani ya siku moja ili kila mwananchi aweze kumiliki ardhi kisheria.
Hayo yalisemwa  hivi karibuni mjini Kibaha na Waziri wa Ardhi na Makazi Wiliam Lukuvi wakati alipofanya zaiara ya siku moja wilayani Kibaha kuangalia changamoto zinazoikabili idara ya ardhi kwenye mkoa huo.
Lukuvi alisema kuwa utoaji hati za kumiliki ardhi kwa haraka itasaidia kupunguza migogoro ambayo imejitokeza kutokana na kuchelewa kutolewa kwa hati hizo ambapo watu wamekuwa wakivamia maeneo yaliyowazi.
“Upatikanaji wa hati unasaidia kuepusha migogoro pia uvamizi kwani kutokana na uchelewaji wa kupatikana hati kunasababisha mtu kushindwa kumiliki kihalali eneo lake hivyo tunataka tuondokane na ucheleweshaji huo,” alisema Lukuvi.
Alisema kuwa majaribio hayo yataanza kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Morogoro kupitia mfumo wa Kieletroniki ambapo mfumo huo endapo utafanikiwa utasamabazwa nchi nzima na kuweza kufikia malengo ya kupima ardhi ya nchi nzima.
“Utashangaa mfumo huu wa sasa kuna baadhi ya watu wamekuwa kwenye mchakato wa kupatiwa hati kwa muda mrefu tangu mwaka 2013 lakini wamekuwa wakitumia ofa pekee jambo ambalo hatulitaki tena,” alisema Lukuvi.
Aidha alisema ametoa hadi mwisho wa mwezi huu Halmashauri kuhakikisha unawapatia hati watu wote walioomba hati kwani ofa hazitatambuliwa tena hivyo wanatakiwa kufanikisha zoezi hilo ili kuondoa kero kwa wananchi.
“Tunataka tuondokane na kero ya kucheleweshwa kupatikana kwa hati kwani mbali ya maeneo kuvamiwa na changamoto nyingine pia watu wanaweza kuzitumia hati zao katika kukopa kwenye mabenki au taasisi za kifedha kwa  ajili ya shughuli zao za maenedeleo,” alisema Lukuvi.
Mwisho.    


OFISA ARDHI AWEKWA KITI MOTO LUKUVIA AMTAKA AWALIPE WANANCHI

Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA baadhi ya wakazi wa Mtaa wa Mwanalugali wilayani Kibaha mkoani Pwani kulalamika mbele ya Waziri wa Ardhi na Makazi Wiliam Lukuvi juu ya kushindwa kulipwa fidia ya viwanja vyao vilivyochukuliwa na Halmashauri kwa zaidi ya miaka 18 iliyopita wakazi hao sasa watalipwa ifikapo Machi mwaka huu.
Ahadi hiyo ilitolewa na Halmashauri mbele ya Waziri Lukuvi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani hapa kujua kero mbalimbali zitokanazo na masuala ya ardhi na kusema kuwa ofisa ardhi wa Mji huo endapo atashindwa kutekeleza hilo basi atakuwa amejifukuzisha kazi mwenyewe.
Akitoa ahadi hiyo ofisa ardhi wa halmashauri ya Mji wa Kibaha Edward Mbala baada ya kubanwa na wananchi hao ambao walisema kuwa wamekuwa wakizungushwa kwa kipindi hicho huku wakiwa hawajui hatma yao.
Moja ya wakazi hao aliyejitambulisha kwa jina la Merry Yohana alisema kuwa maeneo yao yalichukuliwa na Halmashauri kipindi hicho na kuahidiwa kuwa wangelipwa fidia na wengine wangepewa viwanja katika maeneo hayo lakini hakuna utekelezaji wowote uliofanyika licha ya kuwa viwanja hivyo tayari walishaviuza kwa watu wengine.
“Tunapata shida sana kwani walichukua maeneo yote licha ya kuwa ni jambo zuri la maendeleo lakini kwa kipindi cha miaka 18 tumekuw atukifuatilia bila ya mafanikio kwani tunazungushwa tu na hakuna majibu ya uhakika kuwa  ni lini tutalipwa kwenye eneo la Kitalu E,” alisemaYohana.
Kufuatia malalamiko hayo Waziri Lukuvi alimwita ofisa ardhi ili atoe majibu ambapo alisema kuwa ni kweli watu hao wamekuwa wakidai kwa kipindi hicho lakini Hlamashauri iko kwenye utaratibu wa kuwalipa majibu ambayo hayakumridhisha waziri.
“Mkuu ni kweli kuna watu wanadai fidia na wengine wanadai viwanja na huu ulikuwa ni mradi lakini tuko kwenye utaratibu wa kuwalipa na tutawalipa wakati wowote mara taratibu zitakapokamilika kwani tunahangaika kuhakikisha madai yao yanapata majibu,” alisema Mbala.
Hata hivyo waziri alimwambia atoe ahadi kuwa ni lini watakuwa wamekamilisha zoezi hilo ambapo alisema kuwa baada ya miezi miwili kutoka sasa fedha hizo zitakuwa zimepatikana kiasi cha shilingi bilioni 1.4 pamoja na kuwapatia viwanja wengine.
Kwa upande wake Waziri Lukuvi alisema kuwa haipendezi wananchi kukaa muda mrefu bila ya kulipwa fidia ya maeneo yao ambayo yalichukuliwa na Halmashauri kwani kuchelewesha kulipa kunasababisha migogoro isiyo ya lazima.
“Wananchi ofisa ardhi ameahidi hapa mbele yangu na ninyi hivyo msiwe na wasiwasi Bw Ardhi kwa kuwa umeahidi mwenywe muda mtkaowalipa hawa wananchi endapo utashindwa utakuwa umejifukuzisha kazi mwenyewe,” alisema Lukuvi.
Lukuvi aliwataka wananchi hao kukubali muda huo wa miezi miwili kwani walishakaa muda wa miaka 18 hivyo atahakiki wanaodai fidia na wale wanaodai viwanja kwani muda umekuwa mrefu sana na watu wanataka wafanye maendeleo yao.
Mwisho.

Sunday, January 10, 2016

WAAZIMIA KUJENGA SHULE YA SEKONDARI KWA SASA WATOTO WAO WANASOMA UMBALI WA KILOMETA ZAIDI YA 8

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Mbwate kata ya Mkuza wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwapatia greda kwa ajili ya kuchimba visiki kwenye eneo ambalo wamelifyeka kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari.
Wametoa ombi hilo baada ya kuanza kusafisha eneo kwa ajili ya sekondari kutokana na watoto wanaokaa mtaa huo kusoma kwenye sekondari ya kata ya Nyumbu ambayo iko umbali wa kilometa zaidi ya 8 hali ambayo inawafaya wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa huo na jirani kukumbuna na changamoto nyingi hivyo kushindwa kumaliza shule.
Akizungumza na waandishi wa habari mkazi wa mtaa huo Alex Mathias alisema kuwa wamefikia hatua hiyo ya kujenga sekondari ili kuwapunguzia adha watoto wao kusoma mbali hivyo kushindwa kusoma kwa ufanisi hivyo wakipatiwa greda litasaidia kusafisha eneo hilo.
“Kule ni mbali sana kama mzazi huna fedha za kumlipia pikpiki kila siku kiasi cha shilingi 2,000 kwenda na kurudi basi mwanafunzi anakutana na mitihani mingi ambapo wengine wanakuwa hawafiki shule na kufikia hatua ya kuacha shule huku kwa upande wa wale wa kike wamekuwa kijiingiza kwenye vishawishi na kudanganywa na waendesha pikipiki na kujikuta wakiambulia kupata mimba,” alisema Mathias.
Kwa upande wa Salama Rajab alisema kuwa wanafunzi wamekuwa wakipata taabu ya kufika na kurudi kutoka shule kwani umbali wanaposoma kunawapunguzia ari ya kusoma.
Rajab alisema kuwa ujenzi wa shule hiyo itakuwa mkombozi kwa watoto wao hali ambayo itawafanya wafanye vizuri kwenye masomo yao kwani watakuwa na mazingira mazuri ya kusomea tofauti na ilivyo sasa.
Naye mwenyekiti wa mtaa huo Abdala Mtandio alisema kuwa kutokana na eneo hilo na maeneo jirani kukosa shule ya sekondari walifikia maamuzi ya kuanzisha wazo la kujenga shule ili kuwapunguzia watoto wao kero ya kusoma mbali.
Mtandio alisema kuwa wanalishukuru Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kambi ya Nyumbu kwa kuwapatia eneo lenye ukubwa wa hekari 10 kwa ajili ya ujenzi wa huduma za jamii ambapo ndo wamenza na maandalizi ya shule ya sekondari.
“Tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutusaidia kuweza kuanza ujenzi wa shule yetu ya sekondari kwani kwa sasa tunasafisha eneo letu ambapo kila Jumamosi tunalifyeka kwa ajili ya ujenzi huo,” alisema Mtandio.
Alisema kuwa wameazimia kuwa ifikapo 2017 wanafunzi waanze kusoma hapo ambapo watakuwa wamekamilisha angalau madarasa matatu kwa kuanzia ambapo kila kaya inajitolea kufyeka ambapo kuna kaya 554 zenye wakazi 2,863.

Mwisho.  

Friday, January 8, 2016

PWANI YAPATA ZAIDI YA MILIONI 500 KWA AJILI YA ELIMU BURE

Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani umepokea kiasi cha shilingi milioni 579.5 kwa ajili ya utekelezaji wa dhana ya elimu bure kwa wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa fedha hizo zimetolewa na Serikali kupitia Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Ndikilo alisema kuwa fedha hizo tayari zimetumwa kwenye akaunti za shule hizo ambapo kwa shule za Msingi zimepokea kiasi cha shilingi milioni 167,297,00 na sekondari wamepewa kiasi cha shilingi milioni 412,249,000.
“Fedha hizo ni kwa ajili ya maendeleo ya shule ikiwa ni pamoja na ada, chakula ,gharama za mitihani na gharama nyingine ambazo zimetolewa maelekezo kwa walimu wakuu,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa fedha hizo zitasimamiwa na mkoa ambapo mwalimu mkuu yoyote atakayetumia kinyume cha utaratibu kwa ubadhirifu atachukuliwa hatua kali za kisheria.
“Walimu wakuu, Wakurugenzi wa Halmashauri na wakuu wa Wilaya wanatakiwa kukiri kwa maandishi mara watakapoziona fedha hizo kwenye akaunti zao,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa kutokana na kutolewa fedha hizo walimu wakuu hawatakiwi kutoza mchango wa aina yoyotea kama vile ulinzi, maji, umeme na michango mingine kwani fedha hizo zitatumika kwenye masuala yote.
“Michango yoyote kwa wadau kama watakuwa wamekubaliana lazima wapate kibali cha Waziri wa TAMISEMI kupitia mkuu wa mkoa ili kuchangisha michango kwa wananchi ambapo mkoa wetu una jumla ya shule za msingi 553 na sekondari 108,” alisema Ndikilo.

Mwisho.