Wednesday, September 6, 2017

BABA WA KAMBO AMJERUHI MTOTO KWA KUIBA MAYAI MAWILI





Mtuhumiwa Abdala Machupa akiwa kituo cha Polisi Kongowe
Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi Mkoani Pwani linamshikilia Abdala Machupa (49) fundi ujenzi mkazi wa Kongowe kwa tuhuma za kumjeruhi kwa kumkata na kisu kichwani mwanae wa kufikia (jina limehifadhiwa) mwenye umri wa miaka (5) mwanafunzi wa shule ya awali ya Kongowe Kati kwa madai ya kuiba mayai mawili.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na kamanda wa Polisi mkoani humo Jonathan Shana alisema kuwa mtuhumiwa huyo alipata taarifa hizo mitaani za mwanae kuiba mayai hayo.
Kamanda Shana alisema kuwa  mtoto huyo alitutuhumiwa kuiba mayai kwa Bibi Baby Septemba 4 majira ya saa 2 usiku na kumfiki mama yake mzazi aliyefahamika kwa jina moja la Hadija ambaye alimkanya mwanae kwa kumchapa viboko.
“Mnamo Septemba 5 mtuhumiwa huyo alipata taarifa mtaani kuwa mtoto wake kaiba mayai alirudi nyumbani na kuanza kumchapa kwa fimbo na kama haitoshi alichukua panga lakini mwanae mwingine Hamis Abdala miaka (8) akamzuia ndipo alipochukua kisu na kumkata kichwani mara mbili,” alisema Shana.
Alisema kuwa wananchi baada ya kupata taarifa walifika na kuingilia kati ili kumwokoa mtoto huyo na wao ndipo walipomshambulia na kumjeruhi kichwani na kisogoni kisha walimfikisha polisi.
“Mtuhumiwa alipatiwa matibabu na kwa sasa bado yuko mahabusu na amekemea tabia ya vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto ambapo upelelezi umekamilika na mtuhumiwa alitarajiwa kufikishwa mahakamani jana,” alisema Shana.
Awali akizungumzia juu ya tukio hilo mwenyekiti wa mtaa wa Bamba Amri Mavalla alisema kuwa wakati mtuhumiwa huyo akimwadhibu mama mzazi wa mtoto huyo ambaye ni mjamzito alipoteza fahamu kwa hofu kwa mwanae.
Mavalla alisema kuwa aliletewa taarifa majira ya saa 6 ofisini kwake na ndipo alipokwenda kupata taarifa juu ya tukio hilo ambapo mama mzazi wa mtoto huyo alishindwa kuchukua yoyote wakati baba yake akimwadhibu kutokana na hali yake.
Alisema kuwa baada ya tukio hilo wasamaria wema walimpa huduma ya kwanza mama huyo wakati huo wakimkimbiza mtoto huyo kituo cha afya cha Kongowe kwa ajili ya matibabu ambapo anaendelea vizuri.
“Mtoto huyo alichukua mayai hayo akiwa anacheza na wenzake lakini yeye peke yake ndiye aliyeadhibiwa na wenzake hawakuchukuliwa hatua yoyote na ameshonwa nyuzi 12 utosini na nyuzi  nane karibu na sikio,” alisema Mavalla.
Aidha alisema kuwa mtuhumiwa huyo alibadilisha nguo akiwa na lengo la kutaka kukimbia na alipoulizwa kampiga mwanae na nini alisema kamchapa tu na fimbo.

Mwisho.

Monday, August 14, 2017

WATATU WAFA PWANI


Na John Gagarini, Kibaha

WATU watatu wamefariki dunia na wengine 11 wamejeruhiwa kutokana na ajali mbili tofauti zilizotokea mkoani Pwani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana imesema kuwa matukio hayo yalitokea wilaya za Kisarawe na Bagamoyo.

Kamanda Shana amesema kuwa tukio la kwanza lilitokea Agosti 10 majira ya saa 11:15 jioni eneo la Mwambisi wilaya ya Kisarawe basi dogo aina ya Eicher lenye namba za usajili T192 DDD likitokea Masanga kwenda Buguruni Jijini Dar es Salaam liliacha njia na kupinduka na kusababisha kifo cha mtu mmoja huku 11 wakijeruhiwa.

Amesema kuwa chanzo cha ajali hiyo ni breki kushindwa kufanya kazi na kusababisha gari hilo kupoteza mwelekeo na kupinduka na kusababisha kifo cha mwanamke mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka (60) ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja.

Amebainisha kuwa majeruhi wawili Fatma Hamis (35) aliyeumia kifuani na John Clement aliyevunjika mguu wa kulia wanapatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Aidha amesema kuwa baada ya gari hilo kupinduka liligonga mzinga wa nyuki ambao waliingia kwenye basi na kujeruhi watu tisa ambao wamelazwa kwenye hospitali ya Kisarawe na dereva wa gari hilo alikimbia baada ya tukio hilo ambapo jeshi hilo linamtafuta.

Katika tukio la pili dereva wa pikipiki na abiria wake wamefariki dunia baada ya kugongwa na gari.

Shana amesema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 13 majira ya saa 11:40 jioni ambapo pikipiki hiyo aina ya Boxer yenye namba za usajili MC 315 BLM iliyokuwa ikiendeshwa na Ally Seif (19) mkazi wa Kerege iligongana na gari aina ya Mitsubishi Fuso likitokea Dar es Salaam kwenda Bagamoyo likiendeshwa na dereva ambaye hakufahamika.

Amebainisha kuwa chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa bodaboda kulipita gari lililokuwa mbele yake kwa kasi bila ya kuchukua tahadhari na kugongana uso kwa uso na kusababisha vifo hivyo vya dereva na abiria wake Mohamed Rajabu (18) mkazi wa Kerege    

Amewataka wamiliki wa magari kufanya matengenezo ya magari yao pindi yanapokuwa na hitilafu na madereva wasikubali kuendesha magari mabovu pia wafanye ukaguzi wa kina katika magari yao kabla ya kuanza safari kwani ubovu wa magari huchangia ajali kwa kiasi kikubwa.


Mwisho.

Sunday, August 13, 2017

PAKISTANI KUENDELEA KUSAIDIA MIRADI YA MAENDELEO NCHINI





















































Na John Gagarini, Chalinze

NCHI ya Pakistani imesema kuwa itaendelea kusaidia miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano wa nchi hiyo na Tanzania.

Hayo yalisemwa na Balozi wa Pakistani hapa nchini Amir Khan wakati wa sherehe za kupokea majengo ya madarasa ya Shule ya Msingi Pakistani Mtete yaliyokarabatiwa na marafiki wa Pakistani.

Khan alisema kuwa nchi yake imekuwa na miradi mbalimbali ya kimaendeleo hapa Tanzania na hiyo inatokana na urafiki uliopo baina ya nchi hizo.

“Tumekuwa na miradi mingi hapa Tanzania na tutaendelea kushirikiana kama walivyofanya wenzetu na kujitolea kukarabati shule hii,” alisema Khan.

Alisema kuwa miradi kama huo uliofanyika kwenye shule hiyo ni fedha ambazo walitoa marafiki wa Pakistani kwa ajili ya kuhakikisha sekta ya elimu inaboreka.

“Suala la elimu ni muhimu kwa watoto ambao baadaye tunatarajia watakuwa wataalamu wazuri hivyo lazima kuwawekea mazingira mazuri ya kusomea,” alisema Khan.

Aidha aliwataka wananchi kuwa walinzi wa miundombinu ya shule hiyo ili ukarabati uliofanyika uwe na maana hata mazingira yanaendelea kuwa mazuri.

“Kuhusu uzio kwenye shule hiyo alisema kuwa atapeleka ombi hilo kwa marafiki wa Pakistani ili walifanyie kazi kama ilivyoombwa na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete,” alisema Khan.

Naye Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete aliwapongeza Marafiki hao wa Pakistani kwa kuisaidia shule hiyo na kusema kuwa watahakikisha wanenzi ukarabati huo kwa kuitunza miundombinu ya shule.

Ridhiwani alisema kuwa jambo watakalolifanya ni kuhakikisha eneo hilo linapimwa na kuwekewa mipaka ili kukabiliana na wavamizi.

“Tutahakikisha linapimwa na kuwekewa mipaka yake kwani baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo yakiwemo yale ya taasisi,” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa pia watahakikisha miundombinu mingine inatengenezwa ili kuifanya shule hiyo kuwa na mazingira mazuri ya utoaji elimu.


Mwisho.

MBUNGE APONGEZA KAMATI MALIASILI UTALII







Na John Gagarini, Chalinze

MBUNGE wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete ameipongeza serikali kwa kuipeleka kamati ya Maliasili na Utalii kufuatilia changamoto zinazokabili Vijiji vinavyopakana na Hifadhi.

Aliyasema hayo kwenye kikao cha mwaka cha Madiwani wa Halmashauri ya Chalinze na kusema kuwa kumekuwa na changamoto nyingi kwenye vijiji hivyo.

Ridhiwani alisema kuwa baadhi ya changamoto ni mipaka baina ya vijiji hivyo na mbuga hiyo hali ambayo imejenga mahusiano mabaya baina ya vijiji na mbuga hiyo.

“Kamati hyo kuja itakuwa ni moja ya njia za kupata ufumbuzi wa changamoto nyingi zilizopo kwa pande zote na itasidia kupunguza tatizo lililopo, ” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa sehemu ya Hifadhi ya Wami Mbiki ambayo ni njia ya kupita wanyama nayo imeingiliwa hivyo kuna haja ya hatua kuchukuliwa ili kunusuru maeneo hayo.

Naye mwenyekiti wa Halmashauri Said Zikatimu alisema kuwa kamati hiyo itasaidia sana kuleta suluhu kwani migogoro kwenye vijiji vilivyojirani na hifadhi ni kero kubwa.

Zikatimu alisema kuwa wanaafiki kamati hiyo kuja na kusikiliza ili kutatua changamoto kwenye vijiji husika ili navyo vipate haki zao.


Mwisho.

Monday, August 7, 2017

SIMBA WATOA MISAADA WAFANYA USAFI ZAHANATI YA MWENDAPOLE KIBAHA













Na John Gagarini, Kibaha

TAWI la Simba wilayani Kibaha limepongezwa na zahanati ya Mwendapole wilayani Kibaha kwa kujitolea zawadi kwa wagonjwa pamoja na kufanya usafi.

Hayo yalisemwa na muuguzi mganga mfawidhi wa zahanati hyo Gloria Leonidas wakati wa kuushukuru uongozi wa tawi hilo baada ya kumaliza kufanya usafi na kutoa zawadi za sabuni kwa wagonjwa.

Dk leonidas alisema kuwa vilabu vyote vinapaswa kuunga mkono kitu kilichofanywa na tawi hilo la Simba kwa kufanya shughuli za usafi na kujitolea kile walichonacho.

“Timu zinapaswa kuangalia mbali zaidi kwa kujishughulisha na kuisaidia jamii kama walivyofanya Wanasimba hawa kwani wameonyesha uzalendo wa hali ya juu,” alisema Dk Leonidas.

Alisema kuwa kusaidia sehemu kama hizo za jamii kunaleta motisha kwa watumishi wanaofanya kazi sehemu hizo za kutolea huduma inawafanya kuona kuwa wanawajali.

“Mkitusaidia kama hivi tunapata faraja hata wagonjwa nao wanajisikia vizuri kufarijiwa kama walivyofanya Wanasimba Kibaha tunaomba na klabu za hapa nazo ziige mfano huu,” alisema Dk Leonidas.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa tawi la Simba Kibaha Said Tisa alisema kuwa wamekuwa na utaratibu wa kujitolea kwa jamii na sehemu za kutolea huduma.

Tisa alisema kuwa wanaungana na Simba makao makuu wakati wa kuelekea tamasha la Simba Day ambalo huazimishwa kila mwaka ambapo mwaka huu linafanyika leo uwanja wa taifa.

Alisema kuwa wataendelea na utamaduni huo ili kuisaidia jamii iweze kuona faida ya timu na siyo kushiriki uwanjani pekee bali hata kuwajibika kwa jamii.


Mwisho.  
                                         



NETIBOLI PWANI WACHAGUANA


Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA cha Netiboli mkoa wa Pwani kimefanya uchaguzi wa kuwachagua viongozi wake ambao wataongoza kwa kipindi cha miaka minne ambapo Fatuma Mgeni amechaguliwa kuwa mwenyekiti wa chama hicho.

Uchaguzi huo ambao ulifanyika mjini Kibaha na kusimamiwa na kamati ya michezo ya mkoa ikiongozwa na ofisa michezo wa mkoa huo Grace Bureta ulimrudisha madarakani mwenyekiti huyo.

Wengine waliochaguliwa ni makamu mwenyekiti Faraji Makale, katibu ni Steven Mzee, katibu msaidizi ni Rehema Kiharaza, mweka hazina Octavian Chuma.
Kwa upande wa wawakilishi mkutano mkuu taifa ni Ndimbumi Ifuge, Lonjin Mzava, Omega Shuma, Witnes Kitereja na Grace Paschal.

Akiwaasa viongozi waliochaguliwa ofisa michezo huyo aliwataka viongozi hao kuwa kitu kimoja na kushirikiana ili kuinua mchezo huo kwenye mkoa kwa manufaa ya wachezaji wa mchezo huo.

Bureta alisema kuwa uongozi imara ndiyo utakaofanikisha kukabili changamoto mbalimbali zilizopo za kuuboresha mchezo huo ambao ulikuwa maarufu kwenye mkoa wa Pwani kwa miaka ya nyuma.

“Muwe na maamuzi ya pamoja na si ya mtu mmoja na kusitokee akafanya kama ni mali yake hali ambayo itasababisha mchezo huo ushindwe kupiga hatua,” alisema Bureta.

Kwa upande wake mwenyekiti wa chama hicho Fatuma Mgeni alisema kuwa moja ya vitu atakavyovifanyia kazi ni kufanya mafunzo kwa walimu wa mchezo huo ili wajue sheria mpya za mchezo huo ambazo zilifanyiwa marekebisho mwaka 2016 nchini Afrika Kusini.

Mgeni alisema kuwa mafunzo hayo yatakuwa kwa walimu wa mashule, vyuo na kwa wadau mbalimbali wanaoupenda mchezo huo na wanaotaka kuwa walimu wa kufundisha netiboli.


Mwisho.

Sunday, August 6, 2017

WATOTO WAFA MTO RUVU MMOJA WA MIEZI MINNE













Na John Gagarini, Chalinze

WATU watatu wakiwemo mtoto wa miezi minne na wa mwaka mmoja wamekufa huku watu wawili wakinusurika kifo baada ya mtumbwi waliokuwa wakisafiria kuzama kwenye mto Ruvu.

Akizungumza na waandishi wa habari kamanda wa polisi mkoani Pwani Jonathan Shana alisema kuwa licha ya watu hao kubainika kufa dereva wa mtumbwi huo hajulikani alipo.

Shana alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 5 majira ya saa 4:00 asubuhi wakati watu hao walipokuwa wakijaribu kuvuka mto kutoka Vigwaza kwenda Mlandizi kwenye mto Ruvu wilaya ya kipolisi Chalinze.

“Ajali hiyo imepoteza maisha ya watoto wawili ambao ni Nusrat Haji miezi minne na Feisal Hamza mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu pamoja na Sikuzani Musa (41) ambaye mwili wake bado haujapatikana,” alisema Shana.

Alisema kuwa walionusurika ni Zuwena Ramadhan (29) na Tero Mziray (20) ambapo dereva wa mtumbwi huo hajulikani alipo na inaaminika hakufa maji.

“Chanzo cha mtumbwi huo kuzama bado kinachunguzwa na miili ya marehemu imefanyiwa uchunguzi na kukabidhiwa ndugu zao kwa ajili ya mazishi,” alisema Shana.

Aliwataka wamiliki wa vyombo hivyo kuhakikisha vinakuwa kwenye hali nzuri ili kuepukana na ajali kama hizo ambazo zinapoteza uhai wa watu kutokana na ubovu.

Mwisho.