Friday, April 3, 2015

HABARI MPYA ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo amewataka wadau wa mchezo wa bao kuwafundisha vijana ili kuendeleza mchezo huo ambao ulipendwa na wapigania uhuru wa nchi akiwemo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
Alitoa rai hiyo mjini Kibaha alipokuwa akizungumza na viongozi wa Jumuiya ya Wazazi ya Kibaha Mjini wakati wa juma la jumuiya hiyo lililoadhimishwa kwa shughuli mbalimbali ikiwemo mchezo wa bao uliodhaminiwa na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ili kumuenzi Baba wa Taifa aliyekuwa akiupenda mchezo huo.
Ndikilo alisema kuwa kwa sasa mchezo huo unachezwa zaidi na wazee kuliko vijana hivyo kuna umuhimu wa kuwafundisha vijana ili waupende mchezo huo na kuuendeleza.
“Tunampongeza mbunge kudhamini mashindano ya bao ambayo yalishirikisha timu kutoka mitaa yote ya kata 11 za Kibaha Mjini na kuwashirikisha wazee huku vijana wakiwa ni wachache,”alisema Ndikilo.
Alisema kuwa ili kumujenzi Baba wa Taifa wadau mbalimbali wa mchezo huo wanapaswa kuwaweke mazingira mazuri ya kushiriki mchezo huo ambao ni maarufu kwa wakazi wa mikoa ya Pwani.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kudhamini mashindano ni kuuhamasisha mchezo huo ili usipotee na kuwafanya wazee nao wapate kushiriki michezo.
Koka alisema kuwa ataendelea kuhamasisha mchezo huo hasa kwa vijana ili uweze kupendwa na kuwavutia wengi kuliko kungangania baadhi ya michezo kwani hata huo una nafasi yake.
Katika mashindano hayo timu ya Kata ya maili Moja ilifanikiwa kuwa bingwa na kujinyakulia kiasi cha shilingi 300,000 huku kata ya Kibaha wakijinyakulia 200,000 na kata za Mkuza, Mbwawa, Misugusugu, Tumbi, Visiga, Pangani, Kongowe na Picha ya Ndege zilijinyakulia 100,000 kila moja kwa ushiriki wao.
Aidha mashindano ya kukuna nazi wanawake Zuhura Rashid alijinyakulia 70,000, akifuatiwa na Sara Alfred aliyejipatia 50,000 huku Zuhura Ally akipata 30,000 huku washiriki wengine wakijinyakulia 20,000 kila mmoja kwa ushiriki wao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani amemwomba mkuu wa mkoa wa Pwani kuzihimiza Halmashauri kuwawezesha wajasiriamali wanawake na vijana kupata asilimia 10 ya mikopo kwa ajili yao.
Aliyasema hayo mjini Kibaha mbele ya mkuu wa mkoa huo Evarist Ndikilo alipokuwa akiongea na viongozi wa Jumuiya ya Wazazi ya Mji wa Kibaha wakati wa maadhimisho ya juma la Wazazi.
Koka alisema kuwa upatikanaji wa fedha hizo toka halmashauri ni changamoto kwa makundi hayo hali inayowafanya walalamike kutopatiwa fedha hizo ambazo zimetengwa kwa ajili ya vikundi vya ujasiriamali.
“Mkuu wa mkoa naomba usaidie uwaandikie barua wakurugenzi wa Halmashauri za wilaya za mkoa huu kuhakikisha zinawapatia fedha hizo makundi ya akinamama na vijana ili waweze kujikwamua kiuchumi kwa kuendeleza shughuli zao za ujasirimali,” alisema Koka.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Kibaha Mjini Dk Athuman Mokiwa alisema kuwa moja ya changamoto ianyowakabili ni ukosefu wa fedha kwa ajili ya kupima kiwanja chao kilichopo Simbani.
Dk Mokiwa alisema wanaomba Halmashauri iwapimie kiwanja chao ili waweze kuwa hati ya umiliki na kuweza kuweka wawekezaji ili Jumuiya iweze kujiongezea kipato.
Naye mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo alisema kuwa maombi yote yaliyotolewa na Jumuiya ya Wazazi yapelekwe kwa maandishi ofisini kwake ili aweze kuwafikishia ujumbe wahusika.
Ndikilo aliipongeza Jumuiya hiyo na kusema ndiyo Jumuiya kiongozi kwani imeyabeba makundi yote ya chama wakiwemo vijana, akinamama na wazee hivyo lazima iwe mfano wa kuwa muhimili wa chama.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kisarawe
IMEELEZWA kuwa uanzishwaji wa Masjala za Ardhi kutasaidia kukabiliana na migogoro na kupandisha thamani ya ardhi kwa ajili ya uwekezaji kwenye vijiji mkoani Pwani.
Akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Chakenge wilayani Kisarawe wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo alipotembelea Masjala ya Kijiji hicho, kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo Cheyo Nkelege alisema kuwa uanzishwaji wa Masjala hizo huwafanya wanakijiji kuwa na hati za umiliki za kimila.
Nkelege alisema kuwa Masjala hizo zina faida kubwa hususani kwa wananchi wa vijijini kwani wanaweza kuwa na hati miliki za mashamba yao ambazo zinaweza kuwasaidia katika mambo mbalimbali ikiwemo dhamana na rehani.
“Faida za kuanzishwa Masjala hizi kwanza inasaidia kupata hati za umiliki za kimila, kurasimisha ardhi kwa wawekezaji, kuongeza thamani ya ardhi, kuhifadhi nyaraka za ardhi na kupunguza migogoro ya mipaka ambayo imesababisha hadi vifo,” alisema Nkelege.
Alisema kuwa faida nyingine ni kuwa na mipaka inayoeleweka na kupunguza migogoro ya ardhi ambayo imekithiri baina ya wananchi na Vijiji kwa Vijiji hivyo ni mpango mzuri unaopaswa kuigwa sehemu mbalimbali nchini.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa Ndikilo alisema kuwa Masjala hiyo ni kichocheo cha maendeleo kwani itatunza kumbukumbu mbalimbali za ardhi na itawaondolea umaskini.
Ndikilo alisema kuwa jambo jema kwani hati miliki hizo zitatambulika kisheria na zitaweza kutumika kwa ajili ya mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuweka dhamana kwa ajili ya kukopa fedha kwa ajili ya shughuli za maendeleo.
Akisoma risala juu ya ujenzi huo Belina Denisa alisema kuwa ujenzi huo umekamilika ambao umegharimu kiasi cha shilingi milioni 40 bila ya samani za ndani ambayo ni fidia iliyotolewa na kampuni ya Sun Bio Fuel kwa kijiji hicho baada ya kuchukua shamba kijijini hapo. Kutokana na ubora wa Masjala hiyo mkuu wa mkoa huyo aliahidi kuwapatia 500,000 na 500,000 zitatolewa na mbunge wa Jimbo la Kisarawe Hussein Jaffo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ametumia kiasi cha zaidi ya milioni 400 kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali waliojiunga kwenye vikundi 150.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa kongamano la wajasiriamali wa Jimbo hilo na kusema kuwa lengo ni kuwafikia wajasiriamali woete kwenye mitaa na kata hasa wale waliojiunga kwenye vikundi.
Koka alisema kuwa vikundi hivyo vinajishughulisha na shughuli mbalimbali za ujasairiamali ikiwemo biashara pamoja na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali ambazo huziuza kwenye masoko mkoani humo na nje ya mkoa.
“Tumedhamiria kuwawawezesha wajasiriamali kiuchumi kwa kuwapatia fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli zao za kiuchumi za kuweza kujiongezea kipato na kuinua uchumi wa familia,” alisema Koka.
Alisema kuwa wajasiriamali wana uwezo wa kuinua kipato cha jamii kwani ndiyo shughuli za kiuchumi zinazoweza kuwawezesha kumudu maisha kuliko ajira za kuajiriwa ambazo ni chache.
“Kama mnavyojua ujasiriamali umechukua nafasi kubwa ya kiuchumi na umewasaidia watu wengi kujiajiri hususani vijana na akinamama hivyo kuacha kuwa tegemezi,” alisema Koka.
Kwa upande wa mke wa Mbunge huyo Selina Koka ambaye ni mlezi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) CCM Kibaha Mjini amekuwa akiwapatia mafunzo ya ujasiriamali alisema kuwa kwa sasa wanawake wengi wameamka na kuendesha familia kupitia shughuli hizo.
Selina alisema kuwa wajasirimali wanachotakiwa ni kuhakikisha wanajiunga kwenye vikundi ili waweze kupata misaada ya fedha kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kisarawe           
HOSPITALI ya Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani imekamilisha ujenzi wa chumba kipya cha kuhifadhia maiti kwenye hospitali ya wilaya hiyo ambayo ilikuwa inakabiliwa na changamoto ya kuwa na chumba kidogo hali iliyokuwa ikiwafanya kupeleka kuhifadhi maiti hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Akisoma risala mbele ya mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo aliyetembelea hospitali hiyo ya wilaya, mganga mkuu wa wilaya Dk Happiness Ndosi alisema kuwa hali hiyo ilikuwa changamoto kubwa.
Dk Ndosi alisema kuwa ndugu wa marehemu walikuwa wakipata taabu kuhifadhi maiti na kuzipeleka Jijini Dar es Salaam hivyo kutumia gharama kubwa hadi wakati wa mazishi.
“Chumba cha maiti cha zamani kilikuwa na uwezo wa kuhifadhi maiti wawili tu na kilijengwa miaka ya 1950 hivyo kushindwa kukidhi mahitaji ya kuhifadhi miili ya marehemu ambapo huwabidi kuipeleka Muhimbili,” alisema Dk Ndosi.
Alisema kuwa chumba hicho cha sasa hivi kitakuwa na uwezo wa kuhifadhi miili 36 kwa wakati mmoja endapo itatumika vizuri hivyo kuondoa changamoto hiyo.
“Mradi huu umegharimu kiasi cha shilingi milioni 102 ambazo zimetoka serikali kuu ikiwa ni maombi maalumu ambapo umekamilika kwa asilimia 99 na kwa sasa imebaki kuingiza umeme pekee na utaingia muda wowote kuanzia sasa na mafundi wanaendelea na kazi,” alisema Dk Ndosi.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kisarawe Subira Mgalu alisema wanaishukuru serikali kwa kutoa fedha za ujenzi wa chumba hicho kwani imewaondolea mzigo wa kuhifadhi maiti.
“Ilikuwa ni shida mtu akifa apelekwe Muhimbili halafua arudishwe gharama zilikuwa ni kubwa sana hivyo imesaidia kupunguza usumbufu hivyo watu wataweza kujipanga kuandaa shughuli za mazishi kwa nafasi,” alisema Mgalu.
Mgalu alisema kuwa kukamilika kwa mradi huo ambao umefanywa na serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu na kwa gharama nafuu kwani sasa hawatapata usumbufu tena wa kuhifadhi maiti.
Naye mkuu wa mkoa Ndikilo alisema kuwa utu wa binadamu utalindwa kwani kipindi cha nyuma mwili ulikuwa unazikwa harakahara kwani ukikaa muda hata siku mbili una haribika hivyo kutoitendea haki maiti na utawapunguzia gharama.
Ndikilo alisema watapata muda mzuri wa kuweza kuandaa mipango ya mazishi kwa ajili ya kuwahifadhi wapendwa wao ambapo nyuma walikuwa wakikosa muda wa kuweka mipango mizuri.
Mwisho.
 

         

Wednesday, April 1, 2015

HABARI LEO

Na John Gagarini, Kibaha
KITUO cha Afya cha Mkoani wilayani Kibaha mkoani Pwani kinakabiliwa changamoto ukosefu wa vitanda  40 kwenye wodi ya wajawazito hali inayosababisha kitanda kimoja kulaliwa na akinamama wanne.
Hayo yalibainika wakati wa ziara ya Jumuiya ya Wazazi ya Kibaha Mjini na kwenye kituo hicho kilichopo mjini Kibaha kwenye maadhimisho ya wiki ya Jumuiya hiyo.
Ziara hiyo ya kutembelea kituo hicho iliongozwa na mlezi wa Jumuiya ya Wazazi Selina Koka ikiwa ni sehemu ya maadhimisho hayo ambayo huambatana na shughuli mbalimbali za Kijamaii.
Ofisa Muuguzi wa Kituo hicho Prisca Nyambo alisema kuwa changamoto hiyo ni kubwa sana kwani vitanda vilivyopo ni nane.
“Kama mnavyoona vitanda viko nane tu kwa ajili ya mama wajawazito lakini idadi ya wajawazito wanaokuja kwa mwezi ni 250 hadi 300 ambapo idadi hiyo ni kubwa sana kwa kituo chetu,” alisema Nyambo.
Nyambo alisema kuwa idadi ya wajawazito waliojifungua mwezi Januari walikuwa 342 na Februari walikuwa 344 ambapo hadi Machi 31 mama wajawazito 300 walikuwa tayari wameshajifungua.
“Idadi ya mama wajawazito wanaohudumiwa hapa ni wengi sana na tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kuchangia vitanda na magodoro yake ili tukabiliane na changamoto hii,” alisema Nyambo.
Aidha alisema kuwa vifo vya watoto kwa mwezi Januari ilikuwa ni tisa na mwezi Februari vilikuwa vifo saba ambavyo vinatokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na akinamama hao kwenda wakiwa katika hatua za mwisho kabisa pamoja na matumizi ya dawa za kienyeji za kuongeza uchungu.
Kwa upande wake mlezi huyo wa Jumuiya ya Wazazi Selina Koka alisema kuwa anaguswa na hali hiyo ambapo alitoa vitu mbalimbali vikiwemo vifaa vya kujifungulia zikiwemo dawa, pamba na vifaa vy kukatia vitovu.
Selina alisema kuwa changamoto zingine atazifanyia kazi kwa kushirikiana na mbunge wa Jimbo hilo Silvestry Koka ili kuwaondoa adha wanayoipata akianamama wajawazito wanaokwenda kujifungua kituoni hapo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MTOTO Joel Roman (3) wa mtaa wa Ungindoni wilayani Kibaha mkoani Pwani amefariki dunia baada ya kutumbukia kwenye kisima cha maji alipokuwa akicheza.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Geofrid Nombo alisema kuwa mtoto huyo aliondoka nyumbani na kuelekea kisimani akiwa peke yake.
Nombo alisema kuw atukio hilo lilitokea Machi 30 mwaka huu majira ya saa 4 asubuhi baada ya mtoto huyo kuondoka bila ya mama yake Marry Ngowi kujua.
“Alipoondoka mama yake alimtafuta bila ya mafanikio ndipo alipowaambia majirani wenzake kisha kuanza kumtafuta na ndipo walipokuta ndala zake zikiwa nje ya kisima huku yeye akiwa amedumbukia kwenye kisiama hicho,” alisema Nombo.
Aidha alisema kuwa mtoto huyo alikuwa akienda na mama yake kisimani hapo hivyo akawa amekariri eneo hilo ambalo si mbali na nyumba waliyokuwa wakiishi.
“Kisima hicho cha maji ni kirefu unaokaribia kufika futi tano na hutumiwa na watu wa eneo hilo kwa ajili ya matumizi ya kufulia na kuogea wakati wa kiangazi lakini kwa bahati mbaya kilikuwa wazi na hakikuzibwa juu,” alisema Nombo.
Aliongeza kuwa kutokana na tukio hilo alimwamuru mmiliki wa kisima hicho ambaye alimtaja kwa jina moja la Frank akifunike au akifukie ili kuepusha matukio kama hayo yasiweze kutokea. Jeshi la polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo. 
Mwisho.
Na John Gagarini, Chalinze
KIJIJI cha Wafugaji cha Mindutulieni kata ya Lugoba wilayani Bagamoyo kinapoteza ngombe zaidi ya 600 wanaokufa kutokana na ugonjwa wa Ndigana unaosababisha hasara ya shilingi milioni 200 kila mwaka.
Akisoma risala ya wanakijiji hao ofisa mtendaji Meisi Sokoroti kwa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete wakati wa ziara yake alisema kuwa ugonjwa huo umekuwa unawatia hasara kubwa.
Sokoroti alisema kuwa vifo vingi vinatokana na baadhi ya magonjwa ukiwemo huo ambao unawaletea ngombe homa kali na kusababisha vifo .
“Hata hivyo baadhi ya dawa zimekuwa na gharama kubwa ambapo dawa kama Butalex inauzwa kwa bei ya shilingi 50,000 hali ambayo inawasababisha baadhi ya wafugaji kushindwa kumudu gharama hiyo,” alisema Sokoroti.
Alisema kuwa tatizo hilo la ngombe kufa kwa wingi lmedumu kwa kipindi cha miaka minne sasa ambapo dawa mbalimbali za mifugo zimekuwa zikiuzwa kwa gharama kubwa sana.
“Ili kukabiliana na changamoto hii tunaomba serikali ituletee dawa za mifugo zenye ruzuku ya serikali ili kupunguza hasara hiyo,” alisema Sokoroti.
Aidha alisema kuwa ni vyema serikali ikavitumia vyama vya wafugaji katika kuwapatia ruzuku ya dawa kwani kwa sasa wauzaji wa dawa hizo wanawauzia kwa gharama kubwa mno.
Kwa upande wake alisema kuwa kutokuwa na madawa ya ruzuku kumetokana na ufinyu wa bajeti toka halmashauri lakini mara bajeti itakapokuwa nzuri wataweka ruzuku kwenye dawa hizo.
Ridhiwani alisema kuwa changamoto kubwa ni ukosefu wa fedha ndiyo unachangia changamoto hiyo na kuwa serikali inafanyia kazi suala hilo.
Mwisho.  

 Na John Gagarini, Kibaha
IMEELEZWA kuwa mabaraza ya wafanyakazi katika sehemu za kazi ni vyombo muhimu katika kuongeza ufanisi wa kazi ikiwa ni pamoja kufanya maamuzi mbalimbali yanayohusu maslahi ya wafanyakazi taasisi na Taifa kwa ujumla.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki mjini Kibaha na mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo wakati akifungua mkutano wa Baraza la Wafanyakzi wa Ofisi ya Rais Tume ya Mipango.
Ndikilo alisema kuwa wajibu wa mabaraza haya kama vyombo vya ushauri na usimamizi ni kuhakikisha kuwa waajiri na watumishi wanatambua wajibu wao na haki zao na wanazingatia maadili ya utumishi wao ili kuleta matokeo makubwa ya utendaji kazi wenye tija, staha na upendo.
“Hata kama kutakuwa na sera, sheria na kanuni nzuri za kazi kama hakuna malenbgo ya pamoja na ushirikiano baina ya mwajiri na mwajiriwa ni vigumu taasisi hiyo kuwa na tija hivyo mabaraza yana wajibu wa kumshauri mwajiri ili kuleta tija na mashikamano wa pamoja,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa si vizuri kwa watumishi kutumia muda mwingi katika kudai maslahi mazuri zaidi kuliko kupima kiwango cha utekelezaji wa wajibu wao wa kazi hivyo viongozi  wa mabaraza wana wajibu wa kuwahimiza wafanyakazi kutimiza wajibu wao ili kufikia malengo.
“Nyie mmepewa majukumu makubwa kitaifa kama vile kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Taifa  na kufanya mapitio ya utekelezaji wa mpango wa maendeleo wa miaka mitano kuandaa mwongozo wa usimamizi wa utekelezaji wa umma na kukamilisha tafiti mbalimbali zinazoharakisha maendeleo ya uchumi wan chi yetu na mahitaji ya kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya maendeleo mwaka 2015,” alisema Ndikilo.
Kw upande wake mwenyekiti wa baraza hilo Florence Mwanri alisema kuwa tume imeendelea kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa fedha katika kutekeleza majukumu yake pamoja na kupata wataalamu wenye weledi.
Mwanri ambaye pia ni Naibu Katibu Mtendaji anayesimamia klasta ya huduma za jamii na idadi ya watu alisema kuwa katika kuhakikisha watumishi wanafanya kazi iapasavyo wamekuwa wakiwajengea uwezo kupitia mafunzo ya muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi ili kuwaongezea ufanisi katika utendaji kazi wao.
Mwisho.     

Na John Gagarini, Kibaha
MKE wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Selina Koka anatarajia kuanzisha mfuko wa kutoa mikopo isiyokuwa na riba kwa wajasiriamali wa jimbo hilo utakaojulikana kama Chap Chap wa kuwasaidia waweze kuinua uchumi wao.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa mkutano na wajasiriamali wanawake ambao wamewezeshwa mafunzo ya utengenezaji wa bidhaa mbalimbali.
Selina alisema kuwa ameamua kufanya hivyo kwa lengo la kuwapunguzia mzigo wajasiriamali kwani taasisinyingi za kifedha zinaweka riba kubwa kwenye mikopo.
“Wajasiriamali wengi wanashindwa kuendeleza shughuli zao kutokana na riba kubwa wanazotozwa ambazo haziwezi kuwakomboa kiuchumi lakini mfuko huu utakuwa hauwatozi riba yoyote,” alisema Selina.
Alisema kuwa mkopo huo utaanzia kiasi cha shilingi 50 hadi 200,000 lakini lengo ni kwa wale wenye biashara ndogo kabisa.
“Tunatarajia kuwakopesha watu mmoja mmoja na vikundi kwa kupitia kwa mabalozi, wenyeviti wa mitaa na madiwani kwenye kata zote 11 za Kibaha Mjini bila ya kujali itikadi ya chama lengo ni kuwainua wajasiriamali,” alisema Selina.
Aidha alisema hadi sasa tayari hadi sasa wamevifikia vikundi 150 na kutumia gharama ya kiasi cha shilingi milioni 150.
Alibainisha kuwa mfuko huo unatrajia kuanza kukopesha kabla ya mwishoni mwa mwaka huu na kusema kwa sasa wako kwenye taratibu za kuandaa namna ya kutoa mikopo hiyo kisheria na kuwataka wale watakaokopeshwa wawe waaminifu katika kurejesha.
Kwa upande wake Mbunge huyo alisema kuwa anampongeza mkewe kwa kuweza kumsaidiaa katika kuwawezesha wajasiriamali hususani wanawake.
Koka alisema kuwa yeye kwa kushirikiana na mke wake watahakikisha malengo ya kuanzishwa mfuko huo yanafikiwa ili kuwakwamua wanakibaha.
Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha
VIONGOZI wa dini wametakiwa kuacha kujiingiza kwenye siasa badala yake wawahudumie waumini wao katika masuala ya kiroho.
Hayo yalisemwa na Mwangalizi mkuu wa Kituo cha Maandiko cha (PMC) kilichopo Kibaha mkoani Pwani, Mchungaji Gervase Masanja alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Mch Masanja alisema kuwa viongozi wa dini kazi yao kubwa ni kuwaelekeza mambo muhimu ya kumjua Mungu pamoja na kuishi kwa amani baina ya mtu na mtu na taifa kwa taifa.
“Viongozi wa dini tuna kazi kubwa kwani waumini wanahitaji huduma kubwa za kiroho hivyo haipendezi kujiingiza kwenye siasa na tudumishe amani iliyopo hapa nchini,” alisema Mch Masanja.
Alisema kuwa kazi ya siasa ni vema ikaendeshwa na wanasiasa wenyewe huku viongozi wa dini wakiwa ni wapatanishi na walinda amani ya nchi.
“Pia tusisahau kushiriki kwenye masuala makubwa yaliyopo mbele yetu yakiwemo kujiandikisha kwenye Daftari la wapiga kura, kura za maoni ya katiba inayopendekezwa na kushiriki kwenye uchaguzi mkuu mwezi Oktoba,” alisema Mch Masanja.
Aidha alisema anawaomba wakristo na wananchi kujitokeza kwa wingi katika upigaji wa kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na si kususia.
“Kuipigia kura katiba inayopendekezwa ni haki yako ya msingi hivyo mwananchi hupaswi kuisusia na kura utakayopiga ni siri yako lakini si vema kutopiga kura hiyo kwa mustakbali wan chi yetu,” alisema Mch Masanja.
Mwisho.
    














Wednesday, March 25, 2015

ABAKA WANAE KWA MIAKA MIWILI MFULULIZO

Na Mwandishi Wetu, Kibaha

MKAZI wa Miembe Saba wilayani Kibaha mkoani Pwani Said Kundum (52) anatuhumiwa kuwabaka watoto wake wawili wa kike kwa kipindi cha miaka miwili na kuwasababishia maumivu makali.

Akizungumza na waandishi wa habari mtoto mkubwa wa mtuhumiwa ambaye anasoma darasa la saba katika Shule ya Msingi ya Miembe Saba jina limehifadhiwa (15) alisema kuwa baba yake alikuwa akimbaka yeye na mdogo wake kwa nyakati tofauti.

Alisema kuwa baba yake alianza kumbaka tangu mwaka 2013 ambapo kwa kipindi chote hicho alipokuwa akiwafanyia vitendo hivyo aliwatishia kuwa atawaua endapo watasema kwa mtu yoyote.

“Baba alikuwa akitubaka kwa nyakati tofauti wakati mama akiwa anaenda sokoni Kariakoo kuuza mboga huku akituacha na baba nyumbani na kutufanyia vietendo hivyo mimi na mdogo wangu ambaye anasoma darasa la tatu shule ya Msingi Tandau akiwa na miaka (12),” alisema Mwanafunzi huyo.

Aidha alisema kuwa wakati wakifanyiwa vitendo hivyo walikuwa wakisikia maumivu makali lakini aliwaambia kuwa wajikaze kwani baadaye watazoea na hawata sikia tena maumivu.

“Tulivumilia kwa kipindi choete hicho lakini Jumamosi Machi 21 ilibidi ni mwambie mama na kusema potelea mbali liwalo na liwe kama ataniua basi lakini hatuwezi kuvumilia vitendo hivyo,” alisema mwanafunzi huyo.

Alibainisha baada ya kumwambia mama yao ilibidi atoe taarifa kwa viongozi wa serikali ya mtaa wa Miembe Saba ambao nao waliwataarifu polisi ambao walimkamata baba yake.

Naye mama mzazi wa watoto hao Rahima  Mshamu alisema kuwa yeye hakujua kinachoendelea kati ya mume wake na watoto wake kwani alikuwa akimuacha na watoto na hakutegemea kama angeweza kuwafanyia watoto wake vitendo hivyo vya ukatili.

Mshamu alisema tangu alipoona na mume wake amekuwa akifanya biashara ya kuuza mboga za majani ambazo huzikusanya nyakati za jioni hadi usiku kisha kuzipeleka sokoni Kariakoo Jijini Dar es Salaam.

“Mume wangu nilikuwa nikimuamini kama baba na sikutegemea kama angeweza kufanya hivyo na huwa nakusanya mboga kwenye maeneo mbalimbali huko mashambani majira ya saa 12 jioni baada ya hapo tunazisafirisha usiku kwenda Kariakoo ambapo kule huwa tunazifikisha usiku wa manane na ifikapo saa 11 alfajiri tunakuwa tumemaliza na tunaanza safari ya kurudi nyumbani,” alisema Mshamu.

Alisema kuwa hayo ndiyo maisha waliyokuwa wakiishi tangu walipohamia kutokea Kibamba mwaka 2012 ambapo kwa kiasi kikubwa yeye amekuwa akiiendesha familia hiyo kwani mume wake hana kazi maalumu.
“Roho inaniuma sana kwani nimekuwa nikihangaika kuhakikisha kuwa familia yangu haipati shida watoto wanakwenda shule na ana mtoto wake ambaye sijazaa naye yuko sekondari namlipia ada na michango mingine na mahitaji yote lakini mume wangu yeye haangaiki kwa chochote tukio hili limeniuma sana nashindwa hata kujizuia,” alisema huku akilia kwa uchungu.

Aidha alisema kuwa kutokana na kumpenda mume wake alimnunulia pikipiki kwa ajili ya kuongeza kipato cha familia lakini aliuza pikipiki hiyo jambo ambalo lilimfanya ashindwe kumwelewa kuwa ana tatizo gani lakini alishangazwa na afya za watoto wake kuumwa magonjwa UTI kila mara.

“Mimi na yeye hatukuwa na ugomvi wowote ambapo hivi karibuni alijaribu kuuza sehemu ya eneo letu na nilipomuuliza alikataa hadi yule mnunuzi alipokuja na kutaka kumalizia fedha zilizobaki ndipo niligundua kuwa aliuza eneo hilo kwa nguvu bila ridhaa yangu na kusema kuwa aliwabaka watoto kuwa tuna ugomvi wa eneo hilo si kweli kwani suala la eneo ni la mwezi Machi huku yeye akiwabaka watoto miaka miwili iliyopita,” alisema Mshamu.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Hamis Shomary alisema kuwa baada ya kumhoji mtuhumiwa alikiri kufanya matukio hayo na kusema kuwa aliamua kufanya hivyo kutokana na ugomvi aliokuwa nao na mke wake na kuwa alikuwa akimnyima unyumba.

Shomary alisema kuwa mtuhumiwa alifikishwa polisi kwenye kituo cha Kongowe ambako anashikiliwa kwa hatua zaidi za kisheria ikiwa ni pamoja na kusubiri kupelekwa mahakamani.

Mwalimu mkuu wa shule ya Miembe Saba anayosoma mwanafunzi huyo Rajab Chalamila alisema kuwa mwanafunzi huyo alikuwa anaonekana mnyonge na mawazo mengi.

Chalamila alisema kuwa kutokana na hali ya mwanafunzi huyo alimwita baba mzazi zaidi ya mara mbili na kumwambia kuwa ampeleke hospitali mwanae na alisema alimpeleka na kukutwa na malaria lakini hali bado ilikuwa inajirudia na kuonekana kuwa ameathirika kisaikolojia. Jeshi la polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo.  


Mwisho.

Wednesday, March 18, 2015

RIDHIWANI AENDELEA NA ZIARA JIMBONI CHALINZE

Mbunge wa Chalinze Ridhiwani Kikwete kwenye kijiji cha Mkange wakati wa ziara yake kutembelea shughuli za maendeleo, kushoto ni katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo na kulia mwenyekiti wa Kijiji hicho Said Mgaya. 

Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani akiweka udongo kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya cha Kijiji cha Mkange wakati wa ziara yake kutembelea jimbo hilo kuona shughuli za maendeleo. 

Katibu wa chama cha mapinduzi CCM wilaya ya Bagamoyo Kombo Kamote akizungumza na wajumbe wa halmashauri ya Kijiji cha Matipwili juu ya uwajibijaki kwa wananchi wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete jimboni humo. 

 Baadhi ya Wazee wa Kijiji cha Matipwili wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani alipokuwa akiwahutubia wakazi hao kwenye mkutano wa hadhara wakati wa ziara ya kutembelea shughuli za maendeleo jimboni humo.

Baadhi ya akina mama wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani  alipokuwa akiwahutubia wakazi wa Kijiji cha Matipwili wakati wa ziara yake ya kutembelea shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo.

 Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Matipwli wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alipotembelea shule hiyo wakati wa ziara yake jimbo humo kuangalia shughuli za maendeleo

Mzee Halfana Mgobanya wa kijiji cha Gongo akichota maji ya mvua kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kijiji hicho ni moja ya vijiji vya jimbo hilo vinavyokabiliwa na tatizo la uhaba wa maji.

 Baadhi ya akinamama wa kijiji cha Mkange wakiwa wanachota maji huku kukiwa na foleni kubwa ya madumu ya maji eneo hilo nalo linakabilia na tatizo la maji ambayo yamekuwa yakitoka mara chache.


 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akifyetua tofali wakati akiwa kwenye ziara ya kukagua shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo

Friday, March 6, 2015

CHAMA CHA WAIGIZAJI PWANI CHATOA MISAADA KWA WAGONJWA HOSPITALI YA TUMBI

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Waigizaji Tanzania (TFDAA) mkoa wa Pwani kimetoa misaada mbalimbali kwa wagonjwa waliolazwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo ya Tumbi iliyopo wilayani Kibaha.
Misaada hiyo kwa ajili ya wagonjwa ilitolewa na baadhi ya wasanii kwa lengo la kuwafariji ambapo baadhi hawana ndugu wa kuwafariji.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kutoa misaada hiyo katibu wa chama hicho mkoani Pwani Kadnas Nassir alisema kuwa misaada hiyo ni moja ya shughuli zinazofanywa na kundi hilo.
“Wagonjwa ni wenzetu na mtu yoyote anaweza kuumwa kwa hiyo tumeona umuhimu wa kuwasaidia misaada kama sehemu ya kuwajibika kwetu na kuwafariji ili waone kuwa kuwa jamii ya sanaa nayo iko nao katika hali walizonazo,” alisema Nassir.
Nassir alisema kuwa misaada hiyo licha ya kwamba siyo mikubwa sana lakini ni faraja kwa wagonjwa ambao waliwapatia sabuni, dawa za meno nguo za watoto pamoja na mafagio ya usafi kwa hospitali hiyo pia walifanya usafi.
“Sisi mbali ya kutoa burudani pia tunajukumu la kuisadia jamii katika masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kwenye matatizo na furaha,” alisema Nassir.
Naye moja ya wagonjwa waliopatiwa msaada huo Beatrice Shirima alisema chama hicho kimeonyesha ubinaadamu kwani baadhi ya watu wana uwezo lakini hawonyeshi kujali watu wenye matatizo.
Kwa upande wake muuguzi wa zamu wa hospitali hiyo ya Tumbi Felisia Mungulele misaada hiyo imeleta faraja kubwa kwa wagonjwa na wameona kuwa jamii inawajali na watu wengine wajitokeze kusaidia kama hivyo.

Mwisho.   

HABARI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
UKARABATI wa miundombinu ya Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (TANESCO) mkoa wa Pwani unatarajia kukamilika ifikapo Machi 20 mwaka huu na utapunguza kukatika umeme mara kwa mara.
Kazi hiyo ya ukarabati ilianza mwishoni mwa mwaka jana ulikuwa ukamilike Februari mwaka huu ulishindwa kukamilika kwa kipindi hicho kutokana na ukubwa kazi hiyo ya kubadili miundombinu ambayo imechakaa.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Meneja wa TANESCO mkoa huo Sana Idindili alisema kuwa kutokana na zoezi hilo kumesababisha baadhi ya maeneo kupata mgao wa umeme.
Idindili alisema kuwa ukarabati huo ambao uko kwenye mradi umeongeza siku kutokana na kazi hiyo kuwa na ugumu tofauti na mtazamo wa mwanzo.
“Ni kweli kumekuwa na tatizo la umeme kukatika pamoja na mgao lakini hii inatokana na ukakarabati unaoendelea lakini hadi ifikapo Machi 20 tutakuwa tumekamilisha na huduma ya umeme itaendelea kama kawaida,” alisema Idindili.
Aidha alisema kuwa siku hizo ziliongezeka kutokana na kipindi cha mwisho wa mwaka kulikuwa na sikukuu ambazo ilibidi shughuli zisifanyike ndiyo sababu ya kuongeza siku zaidi za kukamilisha zoezi hilo ambalo lilikuwa la miezi mitatu.
“Katika wiki kuna siku tatu za kukata umeme kwa ajili ya kazi lakini nawatoa hofu wananchi kuwa mara baada ya ukarabati huo watapata huduma nzuri na watafanya shughuli zao kama kawaida,” alisema Idindili.
Alibainisha kuwa katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa za ukatikaji wa umeme wamekuwa wakitoa matangazo kwa kutangaza na kwa wale wenye matumizi makubwa ya umeme wamekuwa wakiwaandikia barua juu ya hali hiyo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAKULIMA wa Matunda na Mbogamboga nchini wametakiwa kuachana na matumizi ya dawa za kuulia wadudu badala yake watumie wadudu wanaokabiliana na wadudu waharibifu ili kunusuru afya za walaji na soko la nje ya nchi.
Aidha mbinu hii ya Kibaiolojia hutumia wadudu marafiki kama vile Nyigu ambao hudhibiti inzi au wadudu waharibifu ambao hutaga mayai yao ndani ya tunda au kwenye mmea na kuharibiwa na nyigu huyo.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na ofisa Mfawidhi wa Kituo cha Taifa cha Kudhibiti Visumbufu vya Mimea na Mazao kwa Njia ya Baiolojia (NBCP), Elibariki Msami alipoongea na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.
Msami alisema kuwa njia rahisi ni kuwatumia wadudu hao ambao wameonyesha kuwadhibiti wadudu hao waharibifu kwa kiwango kikubwa hivyo kuepusha matumizi ya madawa.
“Tumekuwa tukifanya utafiti kwa muda sasa ambapo tumeweza kuwazalisha nyigu hao ili wapambane na wadudu waharibifu kwenye matunda kama vile embe, machungwa na mapera pamoja na matunda mengine,” alisema Msami.
Alisema kuwa teknolojia hiyo ya wadudu ilifanywa hasa kwenye maembe ambayo yalikuwa yakioza kutokana na inzi wa embe kuyashambulia kwa kiasi kikubwa ambapo uharibifu umefikia kati ya asilimia 50 hadi 80 ya uharibifu.
“Kuna aina mbalimbali za wadudu wanaopambana na wadudu waharibifu ambao tunawazalisha na wameonyesha uwezo mkubwa wa kukabiliana na wadudu hao waharibifu,” alisema Msami.
Alibainisha kuwa upuliziaji wa dawa husababisha athari kwa wadudu marafiki ambao hupambana na wadudu waharibifu, wakulima, mimea, wanyama na mazingira huathirika na madawa hayo.
“Kwa upande wa mbogamboga baadhi ya wakulima wamekuwa wakitumia madawa na kuwafanya wadudu hao kuwa sugu pia dawa hizo wamekuwa wakizitumia muda mfupi kabla ya kuvuna jambo ambalo si zuri kiafya,” alisema Msami.
Ofisa huyo mwandamizi wa kituo hicho alisema changamoto kubwa inayowakabili katika kuwaeneza wadudu hao ni ukosefu wa fedha unachokikabili kituo hicho na kuimba serikali kukisadia ili kiweze kuzalisha wadudu hao kwa wingi.
Alisisistiza kuwa wadudu wapya wanaoletwa toka nje ya nchi kwa njia ya mbegu zinazoingiza hapa nchini ndiyo wamekuwa changamoto kubwa na wakulima wawe na imani na teknolojia hiyo isiyo na athari zozote.
Mwisho. 
Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA bei ya Mafuta kushuka wananchi wameiomba serikali kupitia mamlaka zake kushusha bei za nauli ambazo hazijashuka licha ya hali hiyo kujitokeza.
Walibainisha kuwa kipindi cha nyuma wamiliki wa vyombo vya usafiri walikuwa wakipandisha bei mara mafuta yanapopanda bei.
Akizungumza na gazeti hili mkazi wa Maili Moja wilayani Kibaha Said Ng’ombe alisema kuwa bei ya nauli inatokana na umbali na bei ya mafuta ambayo imeshuka kwa kiasi kikubwa.
“Tunaipongeza Serikali kwa kuhakikisha bei imeshuka na kuwadhibiti wauzaji wa bidhaa hiyo kuuza kwa bei iliyopo sokoni lakini pia wangepanga bei mpya za nauli kutokana na unafuu wa mafuta ili maisha yaweze kuwa mazuri,” alisema Ng’ombe.
Ng’ombe alisema kuwa mamlaka zinazohusika zinatakiwa kuliangalia hilo kwa undani kwani nauli bado ziko palepale na hazijashuka.
“Tunaomba kuwe na uwiano kama mafuta yameshuka bei na nauli nazo zishuke kwani walikuwa wakilalamika kuwa bei ya mafuta ni kubwa ndisyo kisa cha nauli kuongezeka sasa washushe na nauli,” alisema Ng’ombe.
Kwa upande wake Kibena Mtoro alisema kuwa endapo nauli itashuka itasaidia kuwapunguzia mzigo wananchi hivyo kufanya hali ngumu ya maisha kushuka na kuwa na hali nzuri.
Mtoro alisema kuwa nauli imekuwa changamoto kubwa kwa wananchi hivyo ushukaji wa wamafuta uambatane na ushukaji wa nauli pamoja na vitu vyote vinavyotegemea mafuta.

Mwisho.

Monday, March 2, 2015

HABARI MBALIMBALI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
KAMATI za Ulinzi na Usalama mkoani Pwani zimetakiwa kujipanga vizuri ili kukabiliana na matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi na kuua askari.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo, wakati wa kuwakaribisha wakuu wa wilaya wapya walioteuliwa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete.
Ndikilo alisema kuwa kumetokea matukio mawili ya uvamizi wa vituo vya Polisi vya Kimanzichana wilayani Mkuranga na Ikwiriri wilayani Rufiji ambapo katika matukio hayo askari waliuwawa na wavamizi hao wanaosadikiwa kuwa ni majambazi.
“Wametupiga mara mbili hatutakubali kupigwa tena hivyo kamati za ulinzi na usalama kuanzia ngazi ya chini kabisa hadi ngazi ya wilaya mnapaswa kuweka mikakati ya kukabilina na uvamizi huo ambao unatishia usalama wa raia,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema msingi mkuu wa nchi yetu ni amani hivyo hatutakubali vitendo hivi viendelee tena kwenye mkoa wa Pwani na wakuu wa wilaya wanapaswa kuhakikisha amani inakuwepo na kuwadhibiti hao wanaofanya hivyo.
“Nisingependa jambo hilo lijirudie tena kwani watu wanaofanya vitendo hivyo wanavuruga amani ya nchi iliyopo na silaha wanazopora zinaweza kutumiwa kwenye uhalifu hivyo kuwanyima amani wananchi,” alisema Ndikilo.
Mkuu huyo wa mkoa wa Pwani alisema kuwa matukio ya uhalifu iwe ajenda ya kudumu kwenye vikao mbalimbali vya maendeleo ili kufanikisha kutokomeza uhalifu wa aina hiyo ambao umezidi kushika kasi kwenye nchi.
Wakuu wa wilaya waliokaribishwa na wilaya zao ni Majid Mwanga Bagamoyo, Abdala Kihato Mkuranga, Subira Mgalu Kisarawe na Dk Hassan Mohamed Mafia.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wa mkoa wa Pwani wametakiwa kubadili tabia ili kukabiliana na maambukizi mapya ya ugonjwa wa Ukimwi ambapo yako juu kwa asilimia 5.6 zaidi ya kiwango cha Taifa cha asilimia 5.2.
Akizungumza na viongozi mbalimbali wa mkoa wa Pwani mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa maambukiziu yako juu sana.
Ndikilo alisema kuwa wananchi kwa kushirikiana na wataalamu wa mkoa wanapaswa kuweka mikakati mizuri kwa pamoja kuweka kupunguza maambukizi mapya.
“Hali ni mbaya sana kwani endapo kasi hii endapo itaongezeka itasababisha madhara makubwa sana kwani nguvu kazi kubwa itapotea na familia hazitakuwa na muda wa kuzalisha na kubaki kuuguza wagonjwa hivyo kushindwa kufanya shughuli za maendeleo,” alisema Ndikilo.
Aidha alitoa mfano kwa mwezi Desemba mwaka jana watu waliopima virusi vya ugonjwa wa Ukimwi walikuwa 69,197 waliokutwa na maambukizi walikuwa watu 7,800 sawa na asilimia 7.8.
“Takwimu  hizi na wastani wa maambukizi ni mbaya kwani inaleta picha mbaya kuwa watu hawabadili mienenendo yao licha ya kupatiwa elimu mbalimbali ya kujikinga na maambukizi ya Ukimwi,” alisema Ndikililo.
Alikitaka kitengo cha mapambano dhidi ya ugonjwa huo kiendelee kutoa elimu juu ya kujikinga na ugonjwa huo ambao unaua watu wengi na watu wafuate maagizo ya wataalamu wa afya ili kujiepusha.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
WAKUU wa wilaya Mkoani Pwani wametakiwa kuachana na urasimu bali waweke mazingira mazuri kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza kwenye mkoa huo kwani kwa sasa una fursa nyingi.
Akizungumza na viongozi wa mkoa huo wakiwemo wakuu wa wilaya mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa endapo watakuwa na urasimu watawakimbiza wawekezaji.
Ndikilo alisema kuwa Pwani ina fursa nyingi za kiuewekezaji baada ya Jiji la Dr es Salaam kujaa hivyo wawekezaji kuangalia maeneo ya pembezoni mwa Jiji hilo kw alengo la kuwekeza.
“Wakuu wa wilaya lazima muweke mazingira rahisi kwa wawekezaji na siyo kuwa vikwazo kinachotakiwa ni wawekezaji hao kufuata sheria za uwekezaji zilizowekwa na nchi yetu,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa njia rahisi ni kupima maeneo hayo haraka na kuyatenga kwa ajili ya uwekezaji ili kupunguza malalamiko toka kwa wananchi kuwa maeneo yao yamechukuliwa na wawekezaji pia jengeni miundombinu ya barabara, umeme na maji kwenye maeneo hayo.
“Mkoa unapokuwa na maeneo mengi ya uwekezaji ikiwa ni pamoja na viwanda vinasaidia kuongeza ajira kukuza uchumi wa mtu mmoja, wilaya, mkoa na Taifa kwa ujumla,” alisema Ndikilo.
Alibainisha kuwa mkoa wa Pwani una fursa kubwa kutokana na kuwa na miundombinu mizuri ya usafirishaji ikiwemo kwa njia za meli, ndege, treni na barabara.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAKULIMA wa zao la Korosho mkoani Pwani wametakiwa kuacha kuuza korosho yao ikiwa shambani kwa walanguizi ili kulipandisha thamani zao hilo.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Shirikisho la vyama vya Ushirika Tanzania Jasson Kalile wakati akifungua mkutano mkuu wa Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Pwani (CORECU).
Kalile alisema kuwa wakulima wengi wa zao la korosho wamekuwa wakiuza korosho yao ikiwa shambani kwa bei ndogo hivyo kushindw akunufaika na kilimo cha zao hilo.
“Tatizo kubwa lililopo kwa wanachama wengi wa CORECU ni kuuza korosho zikiwa bado ziko shambani ambapo huuza kwa bei ndogo huku walangizi hao wakija kuuza kwa bei kubwa,” alisema Kalile.
Aidha alisema kuwa walanguzi hutumia matatizo ya wakulima hivyo kuwarubuni kwa kuwapa fedha kwa korosho zilizo shambani na zinapofikia hatua ya kuuzwa siyo mali ya mkulima.
“Inapofuikia hauta ya kuuza walanguzi hao huuza kwa bei nzuri wanayoitaka huku mkulima akibaki hana kitu na kubaki na shida zake,” alisema kalile.
Kwa upande wake Mwenyekiti aliyemaliza muda wake alisema kuwa Juma Abeid alisema kuwa kazi kubwa waliyoifanya ni kukiresjesha chama hicho kwenye hadhi yake baada ya kutokea migogoro kwa muda mrefu.
Abeid alisema kwa sasa hali ni nzuri na tayari wameweka mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuanzisha benki ya ushirika ili wakulima waweze kukopeshwa kwa riba ndogo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkuranga
KATIKA kukabiliana na changamoto kubwa ya ukosefu wa maji wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani inatarajia kukamilisha miradi mitatu mikubwa ya maji yenye thamani ya shilingi milioni 874 mwezi huu.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kikao cha baraza la Madiwani wa Halamshauri ya wilaya ya Mkuranga mhandisi wa maji wa wilaya Renard Baseli alisema miradi hiyo iko kwenye hatua za mwisho.
Baseli alisema kuwa miradi mingi inakumbwa na tatizo kubwa la ukosefu wa fedha ambazo huichelewa kufika na hazifiki kwa wakati hali inayopelekea miradi mingi kushindwa kukamilika kwa wakati.
“Miradi hii mikubwa mitatu itasaidia kwa kiais kikubwa kukabiliana na ukosefu wa maji kwa wananchi wa wilaya ya Mkuranga na kilio hicho kitapata jibu kwani miradi hiyo ni ya thamani kubwa,” alisema Baseli.
Aliitija miradi hiyo kuwa ni ule wa Mvuleni Kilimahewa Kusini wenye thamani ya shilingi milioni 545, Kilamba wenye thamani ya shilingi milioni 285 na Nyamato wenye thamani ya shilingi milioni 44.
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Lukanga Said Kubenea alisema kuwa miradi mingi ya maji imekuwa ikiahidiwa kukamilika lakini inachukua muda mrefu kukamilika huku wananchi wakiendelea kupata taabu.
Kubenea alisema kuwa ucheleweshaji wa miradi ya maji imekuwa kero kubwa kwa wananchivyo kuwataka watendaji wa idara ya maji kuhakikisha wanakamilisha miradi hiyo kwa wakati.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkuranga
WAKUU wa Idara mbalimbali wilayani Mkuranga mkoani Pwani wametakiwa kuwalipa kwa wakati watumishi wa ngazi za chini ili kuleta ufanisi wa kazi.
Hayo yalisemwa Mkuranga na Mkuu mpya wa wilaya ya Mkuranga Abdala Kihato wakati wa makabidhiano ya ofisi na aliyekuwa mkuu wa wilaya hiyo Mercy Silla na kusema kuwa hakuna kitu kinamkera kama malimbikizo kwa watumishi.
Kihato alisema kuwa kumekuwa na tabia ya baadhi ya wakuu wa idara kujilipa posho mbalimbali na kuwaacha watumishi wa ngazi za chini wakidai mishahara ya kila mwezi na kuwaambia fedha iliyoletwa haitoshi.
“Hakuna kitu nisichokipenda kama watumishi kudai kwani serikali huwa inajitahidi kuleta mishahara lakini inapokuja wakubwa wanajipendelea kwa kujilipa malipo mengine na kuwaacha watumishi wa ngazi za chini wakiwa na malalamiko,” alisema Kihato.
Aidha alisema kila mtu ana haki ya kulipwa stahiki yake bila ya kujali ngazi ya kazi kwani wote ni watumishi na hakuna sababu ya kubaguana.
“Ni vema mkagawana kilicholetwa siyo vizuri wengine wapate na wengine wakose wote wana haki sawa kulipwa kwa mujibu wa sheria na si wakubwa kujipendelea kwani kufanya hivyo ni kushusha morali ya kazi,” alisema Kihato.
Kwa upande wake Silla alisema kuwa anawashukuru watumishi wa wilaya hiyo kwa kumpa ushirikiano wa hali ya juu katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Silla alisema kuwa moja ya changamoto zilizopo kwenye wilaya hiyo ni elimu ambapo bado kiwango cha ufaulu kiko chini sana.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkuranga
BAADHI ya Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani wameitaka halmashauri hiyo kununua greda kwa ajili ya kujengea barabara ili kukabiliana na changamoto ya miundombinu hiyo kutokamilika kwa wakati.
Madiwani hao walitoa ushauri huo kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika Mkuranga na kusema kuwa upatikanaji wa greda kutasaidia kupunguza gharama za ujenzi wa barabara.
Moja ya madiwani hao Karu Kavina Diwani wa kata ya Kiparanganda alisema kuwa barabara nyingi hazikamiliki kwa muda uliopangwa kwa sababu gharama ya kukodisha greda ni kubwa.
“Halmashauri yetu ingekuwa na greda ingekuwa ni rahisi kwani gharama zingekuwa ndogo ambapo wananachi wangechangia fedha kidogo kwa kushirikiana na halmashauri yao,” alisema Kavina.
Kavina alisema kuwa karibu kila diwani ambaye ni mwakilishi wa wananchi analalamika barabara za eneo lake kutokwisha hivyo suluhisho ni kununua greda la Halmashauri.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Vianzi Hamis Kitwana alisema kuwa kumekuwa na mvutano mkubwa wa kila diwani kutaka fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hivyo njia rahisi ni kununua greda.
Kitwana alisema kuwa hata kama Halmashauri haina fedha ikope kwa ajili ya kununulia kama baadhi ya Halmashauri nyingine zinavyofanya vinginevyo hali ya barabara itakuwa ni changamoto kubwa.
Kwa upande wake mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Ana Mwakalelya alisema kuwa changamoto kubwa iliyopo ya kunua greda ni ukosefu wa fedha lakini akasema hilo ni wazo ambalo watalifanyia kazi.
Mwisho.