Friday, March 6, 2015

HABARI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
UKARABATI wa miundombinu ya Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (TANESCO) mkoa wa Pwani unatarajia kukamilika ifikapo Machi 20 mwaka huu na utapunguza kukatika umeme mara kwa mara.
Kazi hiyo ya ukarabati ilianza mwishoni mwa mwaka jana ulikuwa ukamilike Februari mwaka huu ulishindwa kukamilika kwa kipindi hicho kutokana na ukubwa kazi hiyo ya kubadili miundombinu ambayo imechakaa.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Meneja wa TANESCO mkoa huo Sana Idindili alisema kuwa kutokana na zoezi hilo kumesababisha baadhi ya maeneo kupata mgao wa umeme.
Idindili alisema kuwa ukarabati huo ambao uko kwenye mradi umeongeza siku kutokana na kazi hiyo kuwa na ugumu tofauti na mtazamo wa mwanzo.
“Ni kweli kumekuwa na tatizo la umeme kukatika pamoja na mgao lakini hii inatokana na ukakarabati unaoendelea lakini hadi ifikapo Machi 20 tutakuwa tumekamilisha na huduma ya umeme itaendelea kama kawaida,” alisema Idindili.
Aidha alisema kuwa siku hizo ziliongezeka kutokana na kipindi cha mwisho wa mwaka kulikuwa na sikukuu ambazo ilibidi shughuli zisifanyike ndiyo sababu ya kuongeza siku zaidi za kukamilisha zoezi hilo ambalo lilikuwa la miezi mitatu.
“Katika wiki kuna siku tatu za kukata umeme kwa ajili ya kazi lakini nawatoa hofu wananchi kuwa mara baada ya ukarabati huo watapata huduma nzuri na watafanya shughuli zao kama kawaida,” alisema Idindili.
Alibainisha kuwa katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa za ukatikaji wa umeme wamekuwa wakitoa matangazo kwa kutangaza na kwa wale wenye matumizi makubwa ya umeme wamekuwa wakiwaandikia barua juu ya hali hiyo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAKULIMA wa Matunda na Mbogamboga nchini wametakiwa kuachana na matumizi ya dawa za kuulia wadudu badala yake watumie wadudu wanaokabiliana na wadudu waharibifu ili kunusuru afya za walaji na soko la nje ya nchi.
Aidha mbinu hii ya Kibaiolojia hutumia wadudu marafiki kama vile Nyigu ambao hudhibiti inzi au wadudu waharibifu ambao hutaga mayai yao ndani ya tunda au kwenye mmea na kuharibiwa na nyigu huyo.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na ofisa Mfawidhi wa Kituo cha Taifa cha Kudhibiti Visumbufu vya Mimea na Mazao kwa Njia ya Baiolojia (NBCP), Elibariki Msami alipoongea na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.
Msami alisema kuwa njia rahisi ni kuwatumia wadudu hao ambao wameonyesha kuwadhibiti wadudu hao waharibifu kwa kiwango kikubwa hivyo kuepusha matumizi ya madawa.
“Tumekuwa tukifanya utafiti kwa muda sasa ambapo tumeweza kuwazalisha nyigu hao ili wapambane na wadudu waharibifu kwenye matunda kama vile embe, machungwa na mapera pamoja na matunda mengine,” alisema Msami.
Alisema kuwa teknolojia hiyo ya wadudu ilifanywa hasa kwenye maembe ambayo yalikuwa yakioza kutokana na inzi wa embe kuyashambulia kwa kiasi kikubwa ambapo uharibifu umefikia kati ya asilimia 50 hadi 80 ya uharibifu.
“Kuna aina mbalimbali za wadudu wanaopambana na wadudu waharibifu ambao tunawazalisha na wameonyesha uwezo mkubwa wa kukabiliana na wadudu hao waharibifu,” alisema Msami.
Alibainisha kuwa upuliziaji wa dawa husababisha athari kwa wadudu marafiki ambao hupambana na wadudu waharibifu, wakulima, mimea, wanyama na mazingira huathirika na madawa hayo.
“Kwa upande wa mbogamboga baadhi ya wakulima wamekuwa wakitumia madawa na kuwafanya wadudu hao kuwa sugu pia dawa hizo wamekuwa wakizitumia muda mfupi kabla ya kuvuna jambo ambalo si zuri kiafya,” alisema Msami.
Ofisa huyo mwandamizi wa kituo hicho alisema changamoto kubwa inayowakabili katika kuwaeneza wadudu hao ni ukosefu wa fedha unachokikabili kituo hicho na kuimba serikali kukisadia ili kiweze kuzalisha wadudu hao kwa wingi.
Alisisistiza kuwa wadudu wapya wanaoletwa toka nje ya nchi kwa njia ya mbegu zinazoingiza hapa nchini ndiyo wamekuwa changamoto kubwa na wakulima wawe na imani na teknolojia hiyo isiyo na athari zozote.
Mwisho. 
Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA bei ya Mafuta kushuka wananchi wameiomba serikali kupitia mamlaka zake kushusha bei za nauli ambazo hazijashuka licha ya hali hiyo kujitokeza.
Walibainisha kuwa kipindi cha nyuma wamiliki wa vyombo vya usafiri walikuwa wakipandisha bei mara mafuta yanapopanda bei.
Akizungumza na gazeti hili mkazi wa Maili Moja wilayani Kibaha Said Ng’ombe alisema kuwa bei ya nauli inatokana na umbali na bei ya mafuta ambayo imeshuka kwa kiasi kikubwa.
“Tunaipongeza Serikali kwa kuhakikisha bei imeshuka na kuwadhibiti wauzaji wa bidhaa hiyo kuuza kwa bei iliyopo sokoni lakini pia wangepanga bei mpya za nauli kutokana na unafuu wa mafuta ili maisha yaweze kuwa mazuri,” alisema Ng’ombe.
Ng’ombe alisema kuwa mamlaka zinazohusika zinatakiwa kuliangalia hilo kwa undani kwani nauli bado ziko palepale na hazijashuka.
“Tunaomba kuwe na uwiano kama mafuta yameshuka bei na nauli nazo zishuke kwani walikuwa wakilalamika kuwa bei ya mafuta ni kubwa ndisyo kisa cha nauli kuongezeka sasa washushe na nauli,” alisema Ng’ombe.
Kwa upande wake Kibena Mtoro alisema kuwa endapo nauli itashuka itasaidia kuwapunguzia mzigo wananchi hivyo kufanya hali ngumu ya maisha kushuka na kuwa na hali nzuri.
Mtoro alisema kuwa nauli imekuwa changamoto kubwa kwa wananchi hivyo ushukaji wa wamafuta uambatane na ushukaji wa nauli pamoja na vitu vyote vinavyotegemea mafuta.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment