Monday, October 6, 2014
Thursday, October 2, 2014
WANAFUNZI WAASWA KUHUSU TEKNOLOJIA
Na John Gagarini, Kibaha
WAZAZI wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kuwalinda
watoto wao waepukane na matumizi mabaya ya Teknolojia ya mawasiliano ili
wasifuate tamaduni mbaya za nchi za Magharibi ambazo zimewaharibu vijana
Tanzania.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mkurugenzi wa Halmashauri ya
Mji wa Kibaha, Jenifa Omollo wakati wa
mahafali ya tisa ya darasa la saba ya shule ya awali na Msingi ya Kibaha
Independent (KIPS).
Omollo alisema kuwa teknolojia ya mawasiliano ni nzuri endapo
inatumiwa vizuri lakini ina athari endapo itatumiwa vibaya hasa kwa vijana
kuiga tamaduni za nje zinazohamasisha vitendo viovu.
“Tuko kwenye utandawazi ambao unatumia teknolojia ya
mawasiliano na kuifanya dunia kuwa Kijiji na kumekuwa na muingiliano mkubwa wa
tamaduni ambazo nyingine ni mbaya zinazokinzana na maadili ya kitanzania ikiwa
ni pamoja na mavazi, ngono, matumizi ya dawa za kulevya na matumizi mabaya ya
mitandao ya kuangalia picha za ngono,” alisema Omollo.
Alisema kuwa kundi la vijana limeathiriwa kwa kiasi kikubwa
na tamaduni hizo mbaya ambapo vijana hao wanafikiri ndiyo kwenda na wakati
kumbe wanajiharibia maisha yao ya baadaye.
“Kwa sasa kuna matumizi mabaya ya teknolojia kupitia njia za
simu, kompyuta na televisheni hivyo lazima wazazi wawaelekeze matumizi sahihi
ya vifaa hivyo ambavyo endapo vitatumiwa vizuri vinaweza kuwa na manufaa mazuri
kwa watumiaji,” alisema Omollo.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mkurugenzi wa shule hiyo Said
Mfinanga alisema kuwa shule yao moja ya vitu inavyozingatia ni maadili mazuri
ya Kitanzania ili wanafunzi wanapotoka hapo wawe na tabia njema.
Mfinanga alisema kuwa licha ya shule kufundisha masomo ya
mawasiliano ya Kompyuta lakini wanazingatia maadili ili kuepuka na matumizi
mabaya ya Teknolojia na kuzingatia kutoa elimu bora.
Shule hiyo ni ya kutwa na bweni ilianzishwa mwaka 2002 na ina
jumla ya wanafunzi 480 na ni miongoni mwa shule zinazofanya vizuri kwenye
wilaya hiyo pamoja na mkoa ambapo mwaka huu jumla ya wahitimu 39 walipewa vyeti
vya kuhitimu darasa la saba.
Mwisho.
KIBAKA AUWAWA KWA KUCHOMWA MOTO KWA WIZI WA PIKPIKI
Na John Gagarini,
Kibaha
KIJANA mwenye umri
kati ya miaka (25) na (30) anayedahaniwa kuwa ni kibaka ambaye jina lake
halikuweza kufahamika ameuwawa kwa kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kwa
tuhuma za kuiba pikipiki.
Wananchi hao walifikia
hatua hiyo baada ya kubaini kuwa mtuhumiwa huyo akiwa na mwenzake waliiba
pikipiki hiyo huko Gairo mkoani Morogoro na kutaka kuiuza Chalinze wilayani
Bagamoyo mkoani Pwani.
Akithibitisha kutokea
kwa tukio hilo kaimu kamanda wa Polisi mkoani humo Athuman Mwambalaswa alisema
kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 25 mwaka huu majira ya saa 1 asubuhi eneo la
Pera Chalinze wilaya ya Bagamoyo.
Kamanda Mwambalaswa
alisema kuwa watuhumiwa hao wawili walikuwa na pikipiki ainaya ya Toyo yenye
namba za usajili T 336 BZC ambayo inadhaniwa kuwa waliiba huko Gairo na
walifika Chalinze kwa lengo la kutaka kuiuza.
“Vijana hao ambao ni
wa kabila la Kimasai walifika hapo huku wakitafuta wateja wa pikipiki hiyo na
wananchi hao walipowauliza uthibitisho wa pikipiki hiyo yaani kadi walishindwa
kuonyesha na ndipo walipoanza kuwapiga na mmoja alifanikiwa kukimbia huku
mwingine akipigwa kisha kuchomwa moto,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Alisema kuwa mwili wa
marehemu ulikutwa mashambani ukiwa umechomwa moto na kuharibika vibaya sehemu
mbalimbali za mwili.
Aidha aliwataka
wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani ni kinyume cha sheria na
kuwataka kuwapeleka kwenye vyombo vya sheria ikiwa ni pamoja na polisi ili
hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.
Mwisho.
SHERIA ZA USHIRIKA ZIMEPITWA NA WAKATI, UMRI WA URAIS UPUNGUZWE
Na John Gagarini, Mkuranga
MKUU wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza amesema kuwa sheria za
Ushirika zimepitwa na wakati hali ambayo
inasababisha baadhi ya watu kutumia mwanya kuwadhulumu wakulima wa zao hilo
hapa nchini.
Kutokana na fedha nyingi kutumiwa kwa matumizi binafsi na
baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika kumesababisha chama kikuu cha ushirika
cha mkoa CORECU kuwa na madeni makubwa ambapo mabenki yamekataa kukikopesha
fedha kwa ajili ya ununuzi wa zao la korosho.
Aliyasema hayo wilayani Mkuranga wakati wa mkutano wa mfuko
wa wakfu wa kuendeleza zao la korosho (CIDTF) kwa wakulima na wataalamu wa mkoa wa Pwani na bodi ya zao
la korosho nchini juu ya msimu mpya wa uuuzaji na ununuzi wa zao hilo.
Mahiza alisema kuwa baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika
vya zao la korosho mkoani humo wamewadhulumu wakulima malipo ya korosho walizo
wauzia wanunuzi hali iliyosababisha hasara kubwa kwa mkoa.
“Mfano mkoa wa Pwani ulikidhamini chama kikukuu cha ushirika
cha mkoa (CORECU) kupata mikopo toka kwenye mabenki ambapo CRDB ilitoa bilioni
6 na NMB ilitoa biloni 3 lakini fedha hizo zimeshindwa kurejeshwa hali
ilioyosababisha chama hicho kishindwe kukopeshwa tena,” alisema Mahiza.
Alisema kuwa kila wanapojaribu kuwachukulia hatua viongozi
hao inashindikana kutokana na sheria zilizopo za ushirika ambazo zinaonekana
zinawalinda viongozi hao hivyo kushindwa kuadhibiwa huku wakulima wakiendelea
kudai fedha zao.
“Ukiwashitaki kwa makosa ya jinai ushirika unasema huwezi
kuwashitaki kwa kosa la jinai lakini baada ya kufuata taratibu za kisheria
tayari tunaweza kuchukua hatua ambazo ni stahiki kwa viongozi hao ambao baadhi
yao wamezitumia fedha hizo kwa manufaa binafsi,” alisema Mahiza.
Aidha alisema kuwa sheria hizo si nzuri kwani zinawaumiza
wakulima lakini kwa sasa mkoa umefikia hatua nzuri za kuweza kuwashtaki
waliohusika na kula fedha za wakulima kwani ushirika sio kudhulumu watu bali ni
kuboresha maslahi ya wakulima.
Kwa upande wake mwenyekiti wa mfuko wa kuendeleza zao la
korosho Athuman Nkinde alisema kuwa maandalizi ya msimu wa kilimo kwa zao hilo
tayari zimeanza na mkoa wa Pwani utapatiwa pembejeo za dawa za kupulizia pamoja
na miche bora ya zao hilo ipatayo 70,000.
Nkinde alisema kuwa matarajio ni mkoa huo kuzalisha zao hilo
kwa wingi ili kuboresha kipato cha wakulima kwani zao hilo ni utajiri endapo
wakulima na wataalamu watawaelekeza kilimo bora cha zao hilo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MWENYEKITI wa Umoja wa Vijana (UVCCM) Taifa Sadifa Juma
ameomba suala la umri wa kugombea Uspika na Urais liangaliwe ili kuwapa nafasi
vijana kuweza kugombea nafasi hizo kwa kupunguza umri wa sasa wa miaka 40 na
kuwa 30.
Aliyasema hayo wakati wa akiwahutubia vijana wa umoja huo
kutoka Jimbo la Kibaha Mjini, alipokuwa akifunga kambi ya mafunzo ya vijana ya
siku 10 ambayo yalifunguliwa na katibu mkuu wa Abdulrahman Kinana Septemba 19.
Sadifa alisema kuwa kwenye Ubunge unaruhusu umri wa kuanzia
miaka 21 lakini kwenye nafasi hizo umri ni kuanzia miaka 40 jambo ambalo ameona
kuwa vijana hawatendewi haki.
“Kama ubunge ni miaka 21 na Uspika pamoja na Urais angalau
iwe kuanzia miaka 30 na kuendelea kwani kwa umri huo bado kijana ana nguvu na
anaweza kutekeleza vema majukumu yake tofuati na kumchagua Rais mwenye umri
mkubwa,” alisema Sadifa.
Alisema kuwa mambo yanabadilika ifike wakati sasa vijana nao
wapate nafasi kutokana na uwezo wake kwani vijana ndiyo wenye nguvu na
wanauwezo mkubwa wa kutekeleza majuku yao ikiwa ni pamoja na kuongoza.
“Nchi kama Kongo na Korea Marais wao ni vijana lakini
wanaongoza vizuri hivyo hakuna sababu ya kuwawekea mazingira magumu ya kugombea
nafasi hizo za juu wapewe nafasi kama watafanikiwa kuchaguliwa basi wachaguliwe
kwani kiongozi siyo umri bali ni uwezo wa kuongoza,” alisema Sadifa.
Kw upande wake kamanda wa Vijana wa Kibaha Mjini Silvestry
Koka alitoa sare 50 kwa makamanda wa umoja huo Green (Guard) zenye thamani ya
shilingi milioni 2.5 na kuwataka vijana hao kuyatumia mafunzo hayo kukiimarisha
chama.
Awali akisoma risala
ya kambi hiyo ya vijana katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM Kibaha Mjini Khalid King
alisema kuwa kambi hiyo iliwafundisha vijana 101 juu ya masuala mbalimbali
yakiwemo ya itikadi za chama, ujasiriamali, uongozi na masuala mbalimbali ya
kisiasa.
Mwisho.
WATOTO WANUNUA SIMU KUWASILIANA NA WAPENZI WAO
Na John Gagarini, Kibaha
IMEBAINIKA kuwa baadhi ya watoto wanaojishughulisha na
biashara ndogondogo wilayani Kibaha mkoani Pwani wamejiingiza kwenye mahusiano
ya kimapenzi ambapo fedha wanazopata wananunulia simu za mkononi ili
kuwasiliana na wapenzi wao.
Watoto hao licha ya kuwa na umri mdogo lakini tayari wanajiingiza
kwenye masuala ya mapenzi jambo ambalo ni hatari na linalosababisha kuingia
kwenye ngono wakiwa na umri mdogo hivyo kuongeza vitendo vya ubakajiani ndani
ya jamii.
Akizungumza mjini Kibaha wakati wa mafunzo ya kupinga vitendo
vya ukatili kwa watoto kwa timu za kuzuia vitendo hivyo ndani ya jamii kwenye
kata ya Kibaha wilayani humo mwenyekiti wa mafunzo hayo Alkhas Katopola alisema
kuwa baadhi ya watoto wanamiliki simu ambazo wanazitumia kwa ajili ya
mawasiliano na wapenzi.
“Inashangaza sana kuona watoto wadogo wanamiliki simu za
mkononi na kikubwa wanachokifanya na hizo simu ni masuala ya mapenzi hivyo
kutokana na umri wao kuwa mdogo ni kama vile wanabakwa kwa sasabu wengi wana
mahusiano ya kimapenzi na watu wazima,” alisema Katopolo.
Katopola alisema kuwa wengi wa watoto hao ni wale ambao
hawakupata nafasi ya kwenda au kuacha shule kutokana na sababu mbalimbali za
kimaisha au wenyewe kukataa kuendelea na masomo.
“Pia baadhi ya watoto hawa wanategemewa na familia zao kwa
ajili ya mahitaji ya nyumbani hivyo wazazi au walezi wanashindwa kuwadhibiti
mara wafanyapo vitendo visivyofaa ikiwa ni pamoja na kujihusisha kwenye masuala
ya mahusiano ya kimapenzi,” alisema Katopola.
Kwa upande wake mratibu wa shirika lisilo la kiserikali la
(KICODET) la Kibaha lililoandaa mafunzo hayo Dk Rose Mkonyi alisema kuwa lengo
la mafunzo hayo ni kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa watoto kwenye
Halmashauri ya Mji wa Kibaha.
“Vitendo vya ukatili kwa watoto ni vingi na ndiyo sababu ya
kuandaa mafunzo hayo ili jamii iweze kujua namna ya kutoa taarifa kwenye vyombo
vya sheria na si kuvifumbia macho kama baadhi ya familia zinavyofanya kwani
baadhi ya wanaofanya vitendo vya ukatili ni ndugu hivyo kuhofia mahusiano
kuvunjika,” alisema Dk Mkonyi.
Dk Mkonyi alisema kuwa mafunzo hayo ambayo yatatumika kuunda
timu za ufuatiliaji wa matukio mbalimbali ya ukatili kwa watoto yamewajengea
uwezo wa kuweza kuwa na mtandao baina yao na vyombo vya sheria kama vile
viongozi wa mitaa, waalimu, jeshi la polisi, mahakimu na wadau wengine
wanaohusika kukabiliana na vitendo hivyo.
Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo Faustina Kayombo
ambaye ni ofisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha alisema kuwa
tatizo kubwa ni usiri unaofanywa na umaskini imekuwa ni vyanzo chanzo vikuu vya
kuendela kwa vitendo hivyo.
Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo mafunzo hayo
yamefadhiliwa na Plan International, UNICEF, Save the Children na Jumuiya ya
Ulaya na serikali kwa kushirikiana na shirika hilo la KICODET.
Mwisho.
MABANDA UMIZA YAONGEZA VITENDO VYA UBAKAJI
Na John Gagarini, Kibaha
BAADHI ya wadau wa watoto wilayani Kibaha mkoani Pwani
wameiomba serikali kuyafutia usajili mabanda ya video ambayo yamekuwa chanzo kikuu
cha watoto wadogo kufanyiwa vitendo vya ubakaji.
Mabanda hayo yamekuwa yakitumiwa na baadhi ya watu wazima
ambao wanawafanyia watoto hao vitendo hivyo baada ya kuwarubuni kuwaingiza
kwenye mabanda hayo kisha kuwapakata na kuwaingilia watoto hao ikiwa ni pamoja
na kinyume cha maumbile.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mratibu wa shirika lisilo la
kiserikali la (KICODET) Dk Rose Mkonyi wakati wa mafunzo ya kupinga vitendo vya
ukatili kwa watoto kwa wadau mbalimbali kwenye kata ya Kibaha wilayani
humo alisema moja ya vyanzo vya ongezeko
la vitendo vya ubakaji watoto ni mabanda hayo.
“Vitendo vya ubakaji watoto ambapo ni moja ya ukatili vimekithiri
na kuongezeka wilayani Kibaha na moja ya sababu ni mabanda hayo ambayo
yanaonyesha video chafu za ngono bila ya kujali umri,” alisema Dk Mkonyi.
Dk Mkonyi alisema kuwa mabanda hayo yamejaa kwenye mitaa na
vijiji hayajali umri licha ya sheria kutaka watoto wenye umri chini ya miaka 18
kutoingia lakini wamiliki wamekuwa wakiwaruhusu watoto hao ambao ni wanafunzi kuingia
pia kufunguliwa muda wa kazi ambapo wanafunzi hao wamekuwa wakiishia humo na
kuacha kwenda shule.
Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo Faustina Kayombo ambaye
ni ofisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha alisema kuwa tatizo
kubwa ni usiri unaofanywa na umaskini imekuwa ni chanzo kikuu cha kuendela kwa
vitendo hivyo.
Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni mwenyekiti
wa mafunzo hayo Alkhas Katopola alisema kuwa mafunzo hayo yamtawafanya waweze
kujua namna ya kukabilina na vitendo hivyo ndani ya jamii ikiwa ni pamoja na
kutoa taarifa kwenye vyombo vya sheria.
Katopolo alisema kuwa baadhi ya matukio hayo yamekuwa
yakiendelea kutokana na wanafamilia kuficha kuogopa mahusiano mabaya au
kurubunia kwa kupewa fedha ili wasitoe taarifa za vitendo hivyo.
Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo mafunzo hayo
yamefadhiliwa na Plan International, UNICEF, Save the Children na Jumuiya ya
Ulaya na serikali kwa kushirikiana na shirika hilo la KICODET.
Mwisho.
WANAFUNZI KIDATO CHA SITA WAZAWADIWA FEDHA
Na John Gagarini, Kibaha
SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Piniel Medical Mission la
Jijini Dar es Salaam limewapa fedha wanafunzi wanne wa shule ya sekondari
Kilangalanga ambao wamefaulu daraja la kwanza kwenye mtihani wa Taifa wa kidato
cha sita.
Waliozawadiwa fedha hizo ni pamoja na Peter Didas, Ally
Makutubu, Obote Juma na Venance Peter ambao kila mmoja alikabidhiwa kiasi cha shilingi
100,000 kila mmoja.
Akiwakabidhi fedha hizo mgeni rasmi kwenye makabidhiano hayo
ambayo yalifanyika shuleni hapo Mlandizi Kibaha mwakilishi wa ofisa elimu
wilaya ya Kibaha Blandina Mwenura aliwapongeza wanafunzi hao na kuwataka wanafunzi
watakaofanya mitihani hiyo kutoogopa masomo ya sayansi.
Mwenura alisema kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakifanya
vibaya kutokana na kuyaogopa masomo hayo ambayo ndiyo masomo muhimu katika
kupata wataalamu mbalimbali.
“Nalipongeza shirika hili kwa kujitolea kuhamasisha masomo
haya ambayo wanafunzi wamekuwa wakiyakimbia na kukimbilia masomo ya Sanaa
wakidhani kuwa ndiyo rahisi,” alisema Mwenura.
Aidha aliwataka wadau wengine kujitokeza zaidi kuwatia moyo
wanafunzi wanaosoma masomo hayo ili kujenga nchi yenye wataalamu wenye uwezo
mzuri kwani watafanya kazi kwa mapenzi kwa kile walichokisomea.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa shirika hilo Jaqline
Ngoma alisema kuwa walitoa ahadi kwa wanafunzi wa shule hiyo kuwa endapo
mwanafunzi wa kidato cha sita atapata daraja la kwanza watampatia kiasi hicho
cha fedha na huo ndiyo utekelezaji wa ahadi hiyo.
“Lengo letu ni kuwatia moyo wanafunzi wanaosoma masomo ya
sayansi wawe na ujasiri na kuondoa woga kwani wataalamu kwa sasa wanapungua
mfano wataalamu wa afya hivyo lazima tutumie njia ya kuwahamasisha ili wengi
wajiunge na masomo hayo,” alisema Ngoma.
Shule hiyo ya serikali ni ya kutwa ni ya wavulana na
wasichana na bweni kwa wanafunzi wa kidato cha tano na sita wavulana wanaochukua
masomo ya mchepuo wa Sayansi.
Mwisho.
Subscribe to:
Posts (Atom)