Thursday, August 20, 2015

WATUMISHI WA DINI WAASWA KUELEKEA UCHAGUZI

Na John Gagarini, Morogoro
WATUMISHI wa Dini nchini wametakiwa kumtanguliza Mungu katika utumishi wao ili kuendelea kudumisha amani ya nchi iliyopo hasa katika kipindi hichi cha kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Ushauri huo umetolewa huko Lugoba wilayani Bagamoyo mkoani Pwani na Mtawa Sista Perpetua Mlamwaza (72) wakati wa maandalizi ya Jubilei ya miaka 50 ya Utawa kwenye kanisa la Katoliki na kusem akuwa siri kubwa ya mafanikio yake ya utendaji yanatokana na kumtanguliza mbele Mungu.
Mlamwaza alisema kuwa watumishi wa Mungu wana nafasi kubwa ya kuifanya nchi iendelee kudumu ni kwa wao kumtanguliza Mungu na kuliombea Taifa letu ili liwe amani ambayo imedumu tangu nchi kupata Uhuru.
“Kipindi hichi tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu hivyo lazima tupige magoti kumwomba Mungu azidi kutudumishia amani yetu iliyopo kwani yeye ndiye mwenye uwezo wa kutunusuru na hali yoyote ambayo inaashiria uvunjifu wa amani,” alisema Mlamwaza.
Mlamwaza ambaye aliwalea kiroho hadi kufanikiwa kupata upadri Mhashamu Askofu Antony Banzi wa Jimbo la Tanga na padri Peter Kunambi alisema kuwa watumishi ni kiungo muhimu kati ya wanadamu na Mungu.
“Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuweza kumtumikia Mungu kwa kipindi chote cha miaka 50 ya utumishi wangu lakini amani hii iliyopo inapaswa kulindwa na kuendelezwa ili tuendelee kupata mafanikio ya kimaendeleo,” alisema Mlamwaza.
Aidha alisema kuwa Watanzania wote wanapaswa kufanya maombi ya kila wakati ikiwa ni pamoja kufunga ili kumwomba Mungu aendelee kutudumishia amani iliyopo hasa ikizingatiwa Tanzania ni Kisiwa cha amani.
Aliwataka wazazi kuhakikisha wanawapeleka shule watoto wao hususani wale wa kike ili waweze kuwarithisha elimu ambayo itakuwa ni mkombozi katika maisha yao na si mali kama baadhi ya watu wanavyofikiri.
Mwisho.
  

   

MAILI MOJA WAENDELEA NA UJENZI WA SHULE ILIYOBOMOKA

> Na John Gagarini, Kibaha
UJENZI wa madarasa manne kwenye shule ya msingi Maili Moja umeanza ambapo kwa sasa wanafunzi 200 wanasoma kwenye darasa moja kutokana na baadhi ya madarasa kushindwa kutumika kutokana na kuwa mabovu hivyo kuhatarisha usalama wa wanafunzi.
Shule hiyo ambayo ndiyo shule ya kwanza kujengwa kwenye mji wa Kibaha kwenye miaka ya 70 madarasa yake yamebomoka na baadhi yameanguka kutokana na kutumika kwa muda mrefu sasa kwani yamefikisha umri wa miaka 40 sasa.
Akizungumza na waandishi wa habari shuleni hapo mwalimu mkuu wa shule hiyo Reginald Fanuel alisema kuwa ujenzi huo ambao ambao utaanza na madarasa mawili tayari ujenzi umefikia hatua ya msingi na unatarajiwa kukamilika baada ya miezi mitatu kuanzia sasa.
Fanuel alisema kuwa fedha zilizotumika kujenga msingi huo wa madarasa manne ni michango ya wazazi na wadau mbalimbali huku wakisubiria kutoa fedha ambazo ziko benki kiasi cha shilingi milioni 36 zilizotolewa na Halmashauri ya Mji wa Kibaha ambazo ndiyo zitakamilisha ujenzi wa madarasa hayo mawili
“Kwa kweli hali ni mbaya kwa sasa kwani darasa moja linachukua wanafunzi 200 tofauti na wastani wa wanafunzi 45 kwa darasa moja lakini kutokana na ubovu madarasa imebidi mengine yasitumike kutokana na kubomoka na yanaweza kuanguka hivyo usalama wa wanafunzi na walimu kuwa mdogo,” alisema Fanuel.
Alisema kuwa shule hiyo ina jumla ya madarasa 14 lakini mazima ni manne tu ndiyo yenye unafuu kidogo licha ya kuwa si mazima huku mawili ndiyo mazima na yako imara na yanafaa kwa matumizi ya kufundishia.
“Ujenzi ulisimama kidogo kutokana na kukosekana vitabu vya hundi kutoka benki hivyo kushindwa kuwalipa wazabuni na wakandarasi na tulitumia muda mrefu zaidi ya mwezi mmoja kupata vitabu hivyo kwani akaunti ya shule ilikufa hivyo tukaanza kuifufua upya hali iliyotumia muda mrefu kufunguliwa lakini kwa sasa zoezi hilo limekamilika na wataanza kulipwa ili ujenzi uendelee,” alisema Fanuel.
Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Lusanda Wiliam alisema kuwa michango iliyochangwa ni mizuri kwani walitoa mifuko 250 ya saruji ambayo iilifyatuliwa tofali zaidi ya 585 na mifuko 50 ilitumika kwa ajili ya msingi uliojengwa.
Wiliam alisema kuwa wazazi ambao watoto wao wanasoma shuleni hapo walitakiwa kulipia shilingi 5,000 kila mmoja kwa ajili ya ujenzi huo na walifanikiwa kupata kiasi cha shilingi 500,000 na kuwaomba wadau wengine wajitokeze kuchangia ujenzi huo.

Mwisho.

WAWEZESHAJI KAYA MASKINI KIBAHA WAASWA

Na John Gagarini, Kibaha
WAWEZESHAJI wa mradi wa kutoa ajira za muda kwa kaya maskini kwenye Halmashauri ya wilaya ya Kibaha mkoani Pwani kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Nchini (TASAF) wametakiwa kutowapangia miradi kwa utashi wao bali wao wabaki kama washauri tu.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha Tatu Suleiman wakati akifungua mafunzo kwa wawezeshaji wa mradi huo awamu ya tatu na kusema kuwa wananchi ndiyo wenye kufahamu wanahitaji mradi gani.
Seleman alisema kuwa waratibu hao kazi yao ni kutoa ushauri kwa wananchi wanapobainisha mradi wanaoutaka kwani wanaopata changamoto ni wao na si kuelekezwa na wawezeshaji hao ila wao wanatakiwa kushauri namna ya kutekeleza miradi hiyo.
“Nyie ni wataalamu mnapaswa kuwapa ushauri wananchi ili wafanikishe miradi hiyo lakini siyo kuwapangia kuwa wafanye mradi gani kwani wao ndiyo wanaojua mahitaji yao lengo likiwa ni wao kutatua changamoto zinazowakabili,” alisema Suleiman.
Alisema kuwa utekelezaji wa miradi ya kunusuru kaya maskini umefikia hatua nzuri ambapo kaya maskini za vijijini zimeweza kuongeza kipato na kuzifanya zisiwe kwenye hali ngumu wakati wa kaipindi cha Hari ambacho kinakuwa baada ya muda wa mavuno kupita.
“Tumeona akaya nyingi sasa zimeweza kupita mwaka mzima zikiwa bado na hali nzuri ya chakula kwani kwa kipindi cha nyuma zilikuwa zinaishiwa chakula kutokana na kuuza chakula ili kupata kipato cha kujikimu,” alisema Suleiman.
Awali mwakilishi wa mkurugenzi mkuu wa TASAF Mercy Mandawa alisema kuwa mradi huo wa awamu ya tatu emelenga kaya maskini zenye hali duni kwa lengo la kuongeza kipato kwenye mamlaka za serikali 161 nchini.
Mandawa ambaye ni Mtaalamu wa Mafunzo na Ushirikishaji wa Jamii TASAF makao makuu alisema kuwa hadi sasa miradi hiyo imeweza kuzifikia kaya milioni moja kote nchini tangu kuanzishwa mpango wa kuzisaidia kaya maskini mwaka 2012 ambayo ilizinduliwa na Rais Dk Jakaya Kikwete.
“Lengo la mradi huu ni kuhakikisha kaya maskini zinakuwa na kipato cha kuweza kujikimu kwa kuwapa ajira za muda ambapo mafanikio yameonekana kwani zimeweza kuwa na kipato na kuondokana na umaskini,” alisema Mandawa.
Aidha alisema kuwa Halmashauri zinatakiwa kuhakikisha zinapeleka fedha kwa wakati ili kuondoa malalamiko kwa walengwa ambapo kulikuwa na tatizo la ucheleweshaji wa utoaji wa fedha za ruzuku kwa kaya maskini.
Mradi huo kwa wilaya ya Kibaha utazifikia kaya 5,690 kwenye miradi ya kuhifadhi maji ya mvua, hifadhi ya misitu, miradi midogo midogo ya umwagiliaji, kilimo misitu cha kuchanganya mazao na miti, usafi wa mazingira maeneo ya mjini  (uzoaji wa taka ngumu), mafunzo hayo yamewahusisha wawezeshaji 24.

Mwisho.

HABARI MBALIMBALI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
UMOJA wa Wafanyakazi wa Viwanda na Biashara Tanzania (TUICO) kimewataka wanachama wake kukitumia chama chao ili kujileta maendeleo.
Hayo yalisemwa hivi karibuni mjini Kibaha na mwenyekiti wa chama hicho Betty Msimbe mara baada ya uchaguzi wa chama hicho ambapo alifanikiwa kuwa mwenyekiti wa chama hicho
Msimbe alisema kuwa baada ya kupata nafasi hiyo ya kukiongoza chama hicho atahakikisha kuwa wanachama wanapata maendeleo kwa kutumia chama chao ambacho kina lengo la kuwaletea umoja na kutetea haki zao.
“Malengo yangu ni kuongeza wingi wa wanachama, kutetea haki za wafanyakazi kuhakikisha mkoa unavuka malengo yake ya kazi, haki na maslahi ya wafanyakazi sehemu za kazi,” alisema Msimbe.
Alisema kuwa atafanya mafunzo maeneo ya kazi ili wafanyakazi wapate elimu juu ya haki zao na elimu kwa viongozi wa matawi kuhusu kutetea maslahi ya wafanyakazi ili waweze kuboresha utendaji kazi wao.
“Kikubwa ninachokiomba toka kwa wanachama na viongozi wenzangu ni ushirikiano ambao utasaidia kukipeleka mbele chama na kufikia malengo ya kuhakikisha haki za wafanyakazi zinapatikana,” alisema Msimbe.
Naye Naibu Katibu Mkuu Msaidizi sekta ya biashara TUICO Taifa Peles Jonathan alisema kuwa atahakikisha anasimamia haki na maslahi ya wafanyakazi kwa nchi nzima na kufanya umoja huo kuwa na demokrasia ya uwakilishi wa kulinda na kutetea haki za wanachama.
Jonatahan alitoa wito  kwa sekretarieti kufanya kazi kwa pamoja ili chama kiweze kufikia malengo waliyojiwekea ili kuwaunganisha kwa pmoja wafanyakazi ili waweze kuwajibika vizuri.
Katika uchaguzi huo ambao ulisimamiwa na katibu wa chama hicho Kassim Matewele ambaye alimtangaza Msimbe kuwa mshindi kwa kura (41) ambaye alimshinda Abimelick Magoma aliyepata kura (18).
Kwenye nafasi ya wajumbe wa kamati ya utendaji mkoa nafasi mbili nafasi ya  Viwanda ni Hasan Kindagule aliyepata kura (35) na Msaidizi wake Athuman Makonga kura (22), upande wa Biashara Shukuru Goso aliyepata kura (32) na msaidizi wake Joyce Kalumuna kura (29).
Kwa upande wa Fedha Furaha Mbwambo  alishinda kwa kupata kura (45) na msaidizi wake ni Zaituni Mtoro aliyepata kura (41), Huduma na ushauri mshindi alikuwa ni Tumaini Kivuyo na msaidizi wake Kandrid Ngowi ambaye alipata kura (35).
Waliochaguliwa Mkutano Mkuu Kanda, Viwanda ni Masiku Serungwi aliyepata kura (35), biashara ni Kamatanda Kamatanda aliyepata kura (57), Fedha Furaha Mbwambo aliyepata kura (60), kwa upande wa huduma na ushauri mshindi alikuwa ni Kandrid Ngowi aliyepata kura (40).
Wajumbe wa mkutano mkuu Taifa upande wa Viwanda  mshindi ni Athuman Makonga kura (59), Biashara ni Shukuru Ngoso kura (58), Fedha Zaituni Mtoro kura (57) na huduma na Ushauri Margareth Chaleo kura ( 45).
Mwisho.

Na John Gagarini, Mkuranga

KIJIJI cha Mwanambaya Kata Mipeko wilaya ya Mkuranga kimewaomba wadau mbalimbali wa maendeleo kuwasaidia kupata kiasi cha  milioni 150 kwa ajili ya mradi wa kuvuta maji kutoka kijiji jirani cha Kisemvule.

Akizungumza na waandishi wa habari msemaji wa kijiji hicho Abubakar Sisaga alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto kubwa ya maji hivyo wameanza mchakato wa kuvuta maji kutoka kijiji cha Kisemvule.

Sisaga alisema kuwa awali walikuwana wazo la kuchimba visima lakini kutokana na uwezo kutokana na gharama za uchimbaji kisima kuwa ni kubwa.

“Tunawaomba wadau mbalimbali wa maendeleo wajitokeze kutusaidia tufanikishe zoezi hilo la uvutaji maji ili kukabiliana na changamoto hiyo ya ukosefu wa maji kwani kwa sasa wanatumia maji ya visima vifupi ambavyo kipindi cha kiangazi hukauka,” alisema Sisaga.

Alisema kuwa endapo watafanikiwa kupata maji yatawasaidia kuweza kutumia muda wao kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo tofauti na sasa wanatumia muda mwingi kuhangaika na maji jambo ambalo ni changamoto kubwa.

“Mbali ya changamoto ya maji kijiji kinakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo ni za kawaida lakini wanakijiji wanajitahidi kuzitatua kadiri ya uwezo wao hivyo tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutuunga mkono kwenye jitihada zetu za kuleta maendeleo,” alisema Sisaga.

Aidha alisema kuwa wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kwa pamoja waweze kufanikiwa na kujikwamua na hali duni na kujiletea maendeleo.

Naye Mwenyekiti wa kijiji hicho Leyla Chabruma alisema kuwa wana ushirikiano mkubwa na wadau wa maendeleo ambao wanashirikiana na wananchi kwa ujumla hali inayoleta maendeleo ndani ya kijiji hicho ambacho kinategemea mapato yake kwa mauzo ya bidhaa mbalimbali ikiwemo mashamba, viwanja na vitu mbalimbali.

MWISHO.

Na John Gagarini, Kibaha

BAADHI ya wafanyabiashara na wasafiri wanaotumia kituo cha mabasi cha Maili Moja wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani kuhakikisha wanatatua tatizo la taa kutowaka kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa na kuwasababishia usumbufu mkubwa wataumiaji wa stendi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari moja ya wafanyabiashara wanaofanya biashara kwenye stendi hiyo nyakati za usiku Said Pengo alisema kuwa wamekuwa wakifanya biashara kwenye mazingira magumu kwenye eneo hilo.

Pengo alisema kuwa ukosefu wa taa hapo stendi ni changamoto kubwa sana inayowafanya kushindwa kufanya biashara kwa vizuri kutokana na kuzingirwa na giza.

“Tunaiomba Halmashauri yetu itusaidie tuweze kupatiwa huduma ya taa kwani taizo la ukosefu wa taa linatusababishia usumbufu mkubwa na tunashindwa kufanya biashara zetu kwa uhuru kutokana na giza linalokuwa linatanda,” alisema Pengo.

Alisema kuwa ni hatari kwa hali ya usalama wao pamoja na wateja wanaotumia eneo hili la stendi ya Maili Moja ambayo inatumiwa na watu wengi.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa wa Maili Moja Chichi Mkongota alikiri juu ya ukosefu wa umeme kwa kipindi hicho na kusema tayari alishatoa taarifa kwa mamlaka husika juu ya tatizo hilo.

Mkongota alisema kuwa alipotoa taarifa Halmashauri aliambiwa kuwa wanafanya utaratibu wa kutatua tatizo hilo ikiwa ni pamoja na kuangalia namna ya kupata taa za muda ili kukabiliana na tatizo hilo.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Jenifa Omolo alisema kuwa tatizo lililopo ni kubwa kidogo kwani taa zilizowekwa zimeharibika na wanafanya mchakato wa kupata nyingine.

Omolo alisema taa zote 16 zilizopo hapo stendi zimeharibika ambapo gharama zake pamoja na kufungwa ni kiasi cha shilingi milioni 18 ambazo wanazitafuta kwa ajili ya kuzifunga.

“Tunafikiria kwa sasa tufunge taa za kawaida kwani hizo zilizopo ziliharibika na si mara ya kwanza kuzifunga kwani kila wakati zimekuwa zikiharibika,” alisema Omolo.

Aidha alisema kuwa wanahangaika kutafuta fedha hizo ili kuondoa changamoto hiyo ambayo imekuwa kero hata kwa wakala wanaokusanya ushuru wa stendi kutokana na usalama kuwa mdogo.

Mwisho.







Monday, August 10, 2015

CCM WATAKIWA KUACHA MAKUNDI

 Na John Gagarini, Kibaha
WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kibaha Mjini wametakiwa kuacha tabia ya kukumbatia makundi mara baada ya uchaguzi wa ndani kumalizika kwani yanasababisha chama kushinda kwa tochi.
Hayo yalisemwa juzi na mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Maulid Bundala wakati akiwanadi watia nia waliojitokeza kuwania kuchaguliwa na chama hicho kupeperusha bendera kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
Bundala alisema kuwa makundi hayo yanachangia kwa kiasi kikubwa chama kushindwa kutokana na mshikamano na ushirikiano kutokuwepo kwenye chaguzi mbalimbali ambazo zinahusisha vyama vingi vya siasa.
“Kipindi hichi ni kigumu sana kuwa na kundi siyo tatizo lakini mara atakapopatikana mgombea mmoja wa ubunge makundi yanatakiwa kwisha na kubakia kundi moja tu la CCM ambalo linatakiwa lipambane na wapinzani,” alisema Bundala.
Alisema kuwa kwanini chama kishindwe kwa mbinde kwa ushindi wa tochi wakati kina wanachama wengi ukilinganisha na vyama vya upinzani lakini inaonekana kushindwa kunatokana na kukumbatiwa kwa makundi hayo.
“Makundi yanatakiwa yaishe mara uteuzi wa mwanachama mmoja ambaye atawakilisha chama kwenye uchaguzi tatizo linguine ni wanachama kumpenda mtu badala ya kukipenda chama na kuachana na tabia ya kuwasema vibaya wagombea kwani wote ni Wanaccm,” alisema Bundala.
Aliwataka wanaccm ambao wanasifa ya kupiga kura za maoni za kuchagua mbunge kwenye kura za maoni wanapaswa kuwa hai kwa kulipia kadi za chama, wawe wameorodheshwa kwenye daftari la tawi na wawe na kadi ya kupigia kura.

Mwisho.   

HABARI ZA PWANI


Na John Gagarini, Bagamoyo
KATIKA kukabiliana na changamoto ya huduma ya afya kwa wananchi wa kijiji cha Kidomole Kata ya Fukayosi, wilaya ya Bagamoyo, mkoa wa Pwani, wamejenga zahanati kwa thamani ya 58.7
Akizungumzia kuhusu ujenzi huo ofisa mtendaji wa Kijiji hicho Sef Mayala alisema kuwa ujenzi wa zahanati hiyo unaondoa adha ya kufuata huduma ya afya nje ya kijiji hicho.
Mayala alisema kuwa katika kufanikisha ujenzi huo kila mwananchi wa Kijiji hicho alitoa kiasi cha shilingi 5,000 kabla ya kuungwa mkono na wadau wengine na kufanikiwa kukamilisha ujenzi huo.
“Mradi huu wa ujenzi wa zahanati uliibuliwa na wananchi kupitia mkutano ulioitishwa na uongozi wa serikali ya kijiji ambao ulianza mwaka 2009 na kukamilika mwaka huu 2015,” alisema Mayala.
Alisema kuwa kuwa katika kuhakikisha ujenzi wa zahanati hiyo unakamilika kwa wakati Halmashauri kupitia ruzuku ya maendeleo ya serikali ilichangia pia kwenye ujenzi huo.
“Ujenzi wa zahanati hii umetokana na utekelezaji wa sera ya afya ya kijiji kuwa na zahanati na pia kuwepo kwa ongezeko la watu katika kijiji cha Kidomole na uhitaji mkubwa wa huduma za afya,,” alisema Mayala.
Aidha alisema kwenye ujenzi huo nguvu za wananchi wamechangia kiasi cha shilingi milioni 45.9, wadau mbalimbali shilingi. milioni 2.8, ruzuku ya serikali shilingi milioni 10 huku Mbunge jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akichangia bati 129.
Diwani wa kata ya Fukayosi Ally Issa aliwashukuiru wananchi wa kijiji hicho na Kata kwa ujumla kwa kuwa na mwamko wa kimaendeleo kwa kuchangia ujenzi wa zahanati hiyo hadi kukamilika.
Issa alisema kuwa anawashukuru wananchi kwa kujitolea pia kwani niaba ya viongozi ngazi mbalimbali anawashukuru kwa michango yao ya hali na mali kwa kujitolea kwa ajili ya shughuli za maendeleo kwenye Kijiji na kata kwani zahanati hiyo ni faida kwa wanancho wote.
Mwisho 
Na John Gagarini, Kibaha
WAUMINI wa Kanisa la Angikana na Watanzania kwa ujumla wametakiwa kutunza vitambulisho vyao vya kupigia kura ili waweze kushiriki kikamilifu zoezi la upigaji kura kwa ajili ya kuwapata viongozi mbalimbali akiwemo Rais atakayeongoza Taifa letu kwa amani na utulivu.
Aidha kanisa linaamini kuwa kutokana na baadhi ya watu kufunga kwa ajili ya kuombea uchaguzi huo kuwa wa amani ni dhahiri Watanzania wasiwe na wasiwasi wakati wa uchaguzi kikubwa ni kuepukana na watu wanaohamasisha uvunjifu wa amani.
 Hayo yalisemwa na Mchungaji wa Kanisa la  Anglikana Tumbi wilayani Kibaha Mkoani Pwani Methew Mwela kwenye baraza  la Halmashauri  kuu ya kanisa hilo lililoketi kwaajili ya kujadili maswala ya maendeleo ya Kanisa hilo na waumini  wake ambapo alisema kuwa kinachotakiwa kufanywa na waumini hao ni kutunza  vitambulisho vyao vya mpiga kura na kushiriki zoezi hilo kikamilifu siku itakapofika.
"Nawakumbusheni waumini na Watanzania kwamba dhambi ya manung'uniko ni mbaya sana na hata kwenye vitabu vitakatifu imeandikwa kuwa iliwatafuna wana wa Israel hivyo kama mtakaa bila kwenda kupiga kura kisha akachaguliwa kiongozi  ambaye hamkupenda achaguliwe na mkaanza kunung'unika mtakuwa mnajitafutia dhambi,"alisema Mch Mwela.
Mch Mwela alisema kuwa wanachopaswa kufanya hivi sasa waumini hao ni kutunza vitambulisho vyao vya mpiga kura na siku ikifika wafike mapema kwaajili ya kupiga kura na kwamba ili kuwawezesha waumini wake kushiriki kikamilifu ibada ya siku hiyo itaanza mapema na kuisha mapema .
"Ili kuhakikisha wote mnapata haki yenu ya msingi  ya kupiga kura ibada ya tarehe hiyo ya siku ya uchaguzi itaanza mapema hapa kanisani kwetu ili waumini wangu wote wenye kadi ya mpiga kura aende akapige kura ili kuchagua viongozi anaowapenda kadri Mungu atakavyomuonyesha,”alisema Mch Mwela.

Aliwashauri waleambao kwa bahati mbaya ama kwa sababu mbalimbali walishindwa kufanikiwa kupata kadi za mpiga kura kuwa watulivu na wanayopaswa kufanya ni kumuomba Mungu ili viongozi watakaochaguliwa waiongoze nchi kwa haki na kweli pasipo na upendeleo wa aina yoyote ili taifa liendelee kuwa na amani.

“Nawaomba Watanzania kuondoa hofu na mashaka juu ya kuwepo na uwezekano wa kuzuka vurugu kabla na baada ya uchaguzi huo mkuu nchini kwani wanachopaswa kutambua ni kuwa mungu amesha mchagua Rais atakayewaongoza watu wake,” alisema Mch Mwela.

MWISHO

Na John Gagarini, Kibaha

ABIRIA wanaosafiri kutumia vyombo mbalimbali vya vya moto mkoani Pwani wametakiwa kuacha tabia kuwashabikia madereva wanaoendesha mwendo wa kasi wakati wakisafiri kwani ni hatari kwa maisha ya wasafiri.

Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na mgeni rasmi kwenye kilele cha wiki nenda kwa usalama barabarani kimkoaFlorence Mwenda iliyofanyika mjini Kibaha na kusema kuwa kuwa pamoja na juhudi zinazofanywa na Jeshi hilo kuhakikisha ajali za barabarani zinapungua bado kuna changamoto mbalimbali hususa kwa  upande wa abiria ikiwemo kuhamasisha madereva kwenda na mwendo kasi wakiwa safarini.
Mwenda ambaye ni ofisa wa jeshi la polisi alisema kuwa kikosi cha usalama barabarani kimeendelea kutoa elimu kwa watumiaji wa barabara juu ya matumizi sahihi ya barabara lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na baadhi ya abiria kushangilia mwendo wa kasi.

“Vitendo kama hivi na vingine havipaswi kufumbiwa macho kwani vinahatarisha usalama wa abiria pamoja na uharibifu wa mali lakini endapo madereva watazingatia matumizi sahihi ya barabara itasaidia kupunguza ajali ambazo zimekuwa ni moja ya vyanzo vikuu vya vifo pamoja na ulemavu,” alisema Mwenda.

Aidha alisema kuwa kikosi cha usalama barabarani kimetoa  elimu ya matumizi sahihi ya   barabara  kwa wanafunzi  wa shule za msingi na sekondari  mkoani humo wapatao 1,568 lengo likiwa ni kuielimisha jamii na makundi mbalimbali   juu ya matumizi salama ya barabara ili kupunguza ajali zisizokuwa za lazima.

“Makundi mbalimbali yamepatiwa elimu hiyo ikiwa ni pamoja na madereva wa magari wapatao 905,waendesha pikipiki1,220 na abiria 16,802 wa magari  ya aina mbalimbali ambapo zoezi hilo litakuwa endelevu  hali itakayosaidia  kupunguza ajali ambazo zimekuwa zikigharimu maisha na mali,” alisema Mwenda.

Alibainisha kuwa kamati ya usalama barabarani  ya Mkoa huo pia ilifanya mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na huduma ya  upimaji wa macho bure kwa wananchi wa kawaida na madereva wa vyombo vya moto.

MWISHO