Monday, January 27, 2014

WAANDISHI WAPIGWA MSASA JUU YA PETS



Na John Gagarini, Kibaha
IMEELEZWA kuwa ili nchi iweze kuendelea watendaji na mamalaka zikiwemo halmashauri hapa nchini zimetakiwa kuwa na uwazi na uwajibikaji ili kuwaletea wananchi maendeleo.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na mkuu wa shule kuu ya uandishi wa habari ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam, Dkt Herbert Makoye  wakati akifungua mafunzo ya ufuatiliaji wa rasilimali za Umma (PETS) kwa waandishi wa habari kutoka vyombo vya habari vya Business Times na Mlimani.
Dkt Makoye alisema kuwa kumekuwa na malalamiko mengi toka kwa wananchi juu ya matumizi mabaya ya fedha za Umma zinazotolewa na serikali hivyo kusababisha huduma muhimu za kijamii.
“Tumeona tufanya mafunzo haya kwa lengo la kuwajengea uwezo waandishi wa habari juu ya kuweza kuandika taarifa juu ya matumizi ya fedha hizo ambazo madhumuni yake ni kuwapunguzia kero wananchi hivyo watapata taarisa sahihi,” alisema Dkt Makoye.
Alisema bila ya uwazi kutakuwa hakuna uwajibikaji hali ambayo itasababisha kutokuwa na maendeleo ya haraka ya mwananchi kujikwamu na hali ngumu ya kimaisha.
“Kupitia mafunzo haya waandishi wanapaswa kuyatumia kwa lengo la kuwapatia wananchi taarifa sahihi juu ya michakato mbalimbali ya matumizi ya fedha hizo na zitasaidia watendaji kuwajibika kwani watakuwa na hofu ya kufuja fedha kwani kuna vyombo vinavyowafuatilia,” alisema Dkt Makoye.
Kwa upande wake Mhariri Mtendaji wa gazeti la Majira Bw Imma Mbuguni alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwa waandishi katika ufuatiliaji wa rasilimali za umma zikiwemo fedha zinazotolewa na serikali kwa maendeleo ya wananchi.
Bw Mbuguni alisema pia mafunzo hayo yatasaidia kuibua mijadala mbalimbali juu ya matumizi sahihi ya fedha za Umma ambapo baadhi ya watendaji wanaonekana kutozitumia kwa malengo yaliyowekwa au mahitaji ya wananchi.
Mafunzo hayo yameandaliwa kwa pamoja na Shule Kuu ya Uandishi wa Habari ya Chuo kikuu cha Dar es Salaam kwa kushirikiana na kampuni ya Business Times kutokana na ufadhili wa Mfuko wa Ufadhili wa Vyombo vya Habari (TMF).
Mwisho.

Sunday, January 26, 2014

SACCOS WATAKIWA KULIPA MADENI YA MIKOPO YAO

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Kuweka na Kukopa cha KIWAO SACCOS cha wilayani Kibaha mkoani Pwani kimewapa muda wa miezi mitatu kulipa madeni ya mikopo yao baadhi ya wanachama wake wenye madeni sugu na endapo watashindwa kurejesha ndani ya muda huo watawachukulia hatua kali ikiwa ni pamoja na kuwapeleka mahakamani.
Akiongea na wanachama kwenye mkutano mkuu uliofanyika Shirika la Elimu Kibaha, mwenyekiti wa chama hicho Bi. Magdalena Kabukire alisema kuwa wanachama hao wapatao tisa wana madeni ya mikopo ya muda mrefu.
Bi. Kabukire alisema kuwa tayari wamewaandikia barua wanachama hao kuwakumbushia madeni yao ili waweze kurejesha kufanikisha wanachama wengine waweze kukopa.
“Chama chetu kinakabiliwa na changamoto hiyo ya baadhi yao kuchelewesha kurejesha mikopo hali inayosababisha wengine washindwe kukopa kutokana na fedha nyingi kuwa mikononi mwa watu,” alisema Bi Kabukire.
Naye mwenyekiti wa mtaa wa Mwanalugali kilipo chama hicho Deodatus Rwekaza alisema kuwa watashirikiana na chama hicho kuhakikisha wanarejesha mikopo hiyo.
“Wakiona wanachama hao wanashindwa kulipa kwa kipindi hicho walete majina kwenye ofisi yangu ili waangalie sheria iweze kuchukua mkoando wake, kwani mabenki na asasi za kifedha zimefanya hivyo na wadeni wamelipa,” alisema Bw Rwekaza.
Kwa upande wake ofisa ushirika wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Bw Kulwa Masambu alisema kuwa ili vyama hivyo viweze kupiga hatua lazima wanachama warejeshe mikopo kwa wakati.
Bw Masambu alisema kuwa vyama hivyo vimekuwa mkombozi kwa wananchi hususani wanawake ambao ndiyo wenye changamoto kubwa ya kuziletea maendeleo familia zao na jamii inayowazunguka.
Kwa mwaka jana chama hicho kiliweza kukopesha wanachama wake 19 kiasi cha shilingi milioni 16.4 na kupata mapato ya shilingi milioni 1.9 hisa zikiwa shilingi 638,000 akiba zikiwa ni m 4.2 na kina jumla ya wanachama 76.

Mwisho.   

Thursday, January 23, 2014

MWINJILISTI AU AJINYONGA

Na John Gagarini, Kibaha
MWINJILISTI wa Kanisa Anglikana Eliakia Daniel (35) amekufa kwa kujinyonga baada ya kumuua mkewe Bi Mboni Patrick (28) kutokana na wivu wa kimapenzi.
Kwa mujibu wa kamanda wa Polisi mkoani Pwani kamishna Msaidizi Mwandamizi Ulrich Matei alisema kuwa marehemu walikuwa ni wakulima wa Kijiji cha Gama - Makaani wilayani Bagamoyo.
Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea Januari 20 mwaka huu majira ya saa 10 jioni kijijini hapo ambako walikuwa wakifanya shughuli ya kuchoma mkaa.
“Mwinjilisti huyo alimwua mkewe baada ya kutokea wivu wa kimapenzi ndipo alipochukua panga na kumkata kichwani upande wa kulia na kumsababishia majeraha makubwa yaliyosababisha kifo chake,” alisema Kamanda Matei.
Alisema baada ya kumwua mkewe alimfunika kwa magogo sehemu waliyokuwa wakifanyia shughuli zao hizo za kuchoma mkaa kwa ajili ya biashara.
“Baada ya kumwua mkewe alijinyonga umbali wa mita 300 kutoka eneo la tukio,” alisema Kamanda Matei.
Alibainisha kuwa chanzo cha mauaji hayo ni kutokana na wivu wa kimapenzi na kupelekea tukio hilo kutokea ambalo limewasikitisha wananchi wa kijiji hicho.
Mwisho.

MBUNGE KUZIKWA MIONO

Na John Gagarini, Pwani
MBUNGE wa Jimbo la Chalinze Wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Bw Said Bwanamdogo ambaye alifariki dunia asubuhi Januari 22 mwaka huu katika hospitali ya Muhimbili Jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu ya tatizo la ugonjwa wa tumbo kwa miaka mitatu anatarjiwa kuzikwa Januari 24 Kijijini kwao Miono wilayani humo.
Akitoa tarifa juu ya msiba huo huko Makondeko msemaji wa familia ambaye ni baba mdogo wa marehemu Bw Omary Nguya alisema kuwa msiba huo utahudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Jakaya Kikwete ambaye yuko ziarani nchini Uholanzi.
Bw Nguya alisema mazishi hayo yalikuwa yafanyike Januari 23 lakini yalisogezwa mbele ili kumsubiri Rais ambaye baada ya kupata taarifa aliomba mazishi yahairishwe hadi siku ya Ijumaa ambapo mwili wa marehemu utasafirishwa Ijumaa asubuhi kwenda Kijijini kwake Miono.
 “Marehemu alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa tumbo kwa muda mrefu hali iliyosababisha kuanzishiwa matibabu nchini India ambapo mbali ya jitihada zilizofanywa na madaktari hazikuweza kufanikiwa ambapo marehemu alfariki dunia asubuhi Januari 22 akiwa hospitali ya Muhimbili kwa matibabu na marehemu ameacha watoto sita,” alisema Bw Nguya.
Kwa upande wake Katibu wa CCM Mkoani Pwani Bi Sauda Mpambalioto alisema wamepokea msiba huo kwa mshtuko mkubwa na kukiri kubadilishwa kwa siku ya mazishi.
“Mbali ya msiba huo pia jana Januari 21 tumemzika mjumbe wa halmashauri kuu CCM Taifa (MNEC) kupitia wilaya ya Mkuranga Bi Rukia Msumi ambaye alipata ajali ya pikipiki ambayo ilisababisha kifo chake,” alisema Mpambalioto.
Naye mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Bw Silvestry Koka alisema msiba huo ni pigo kwake kwani walikuwa karibu na marehemu kwa kushirikiana kikazi na kupeana mawazo ya kiutendaji.
Alisema Bwanamdogo alikuwa ni mtu mcheshi ,msikivu ,asiye na majivuno ,alipenda kuzungumza na kila rika pasipo kuwa na majivuno hali inayomfanya awe na kitu cha kuiga kwake.
Kwa upande wake mbunge wa zamani wa Jimbo la Kibaha ambaye kwasasa ni katibu mwenezi mkoani Pwani Dkt Zainab Gama alisema sifa za mbunge wa Chalinze ni nyingi, lakini cha kujivunia kwake ni uadilifu na ucheshi aliokuwa nao.
Dkt Gama alisema enzi za uhai wake atakumbukwa kwa utendaji kazi na kutokuwa mbaguzi kwa wengine.
Mwisho
 

MAENEO YANAUZWA



Maeneo yanauzwa hekari  2,000 liko Mikese kilomita 2 barabara kuu lina hati linauzwa m 400, hekari 1,000 liko Chalinze, liko barabarani  lina hati bei m 500, hekari 900 liko Soga Kibaha lina hati b 3.15, hekari 200 zinauzwa ziko Zogowale km 8 toka barabara kuu ya Moro halina hati linauzwa m 60, hekari 11 na hosteli liko Miembe Saba umbali wa km 1 kutoka barabara kuu ya Moro lina hati m 400, hekari 4 na nyumba zinauzwa liko Kibamba barabarani hati zipo m 400, hekari 100 liko Kwala km 25 kutoka barabara kuu halina hati m 40, hekari 100 liko Mbwawa km 10 toka barabara kuu,  hekari 38 liko Mpiji  lina hati m 133, hekari tano liko Misugusugu barabarani lina hati m 600, hekari 30 liko Misugusugu km 8 toka barabara kuu lina hati m 375, hekari 6 liko Miembe Saba km 2.5 toka barabara kuu halina hati m 100, hekari 6 liko Miembe Saba liko barabarani lina hati m 400, hekari 40 liko Mlandizi km 8 toka barabara kuu lina hati m 400, hekari 9 liko Chalinze liko barabarani lina hati m 400, hekari 11 liko Miembe Saba  km 4 toka barabara kuu lina hati m 35, hekari 20 liko Viziwaziwa/ Kibaha Kwa Mfipa halina hati m 40, hekari 30 liko Kumba Kwa Mfipa km 7 toka barabara kuu halina hati lianuzwa m 60. Kwa mawasiliano piga simu namba 0783 989168, 0754 393118 au 0656 046424.