Sunday, January 26, 2014

SACCOS WATAKIWA KULIPA MADENI YA MIKOPO YAO

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Kuweka na Kukopa cha KIWAO SACCOS cha wilayani Kibaha mkoani Pwani kimewapa muda wa miezi mitatu kulipa madeni ya mikopo yao baadhi ya wanachama wake wenye madeni sugu na endapo watashindwa kurejesha ndani ya muda huo watawachukulia hatua kali ikiwa ni pamoja na kuwapeleka mahakamani.
Akiongea na wanachama kwenye mkutano mkuu uliofanyika Shirika la Elimu Kibaha, mwenyekiti wa chama hicho Bi. Magdalena Kabukire alisema kuwa wanachama hao wapatao tisa wana madeni ya mikopo ya muda mrefu.
Bi. Kabukire alisema kuwa tayari wamewaandikia barua wanachama hao kuwakumbushia madeni yao ili waweze kurejesha kufanikisha wanachama wengine waweze kukopa.
“Chama chetu kinakabiliwa na changamoto hiyo ya baadhi yao kuchelewesha kurejesha mikopo hali inayosababisha wengine washindwe kukopa kutokana na fedha nyingi kuwa mikononi mwa watu,” alisema Bi Kabukire.
Naye mwenyekiti wa mtaa wa Mwanalugali kilipo chama hicho Deodatus Rwekaza alisema kuwa watashirikiana na chama hicho kuhakikisha wanarejesha mikopo hiyo.
“Wakiona wanachama hao wanashindwa kulipa kwa kipindi hicho walete majina kwenye ofisi yangu ili waangalie sheria iweze kuchukua mkoando wake, kwani mabenki na asasi za kifedha zimefanya hivyo na wadeni wamelipa,” alisema Bw Rwekaza.
Kwa upande wake ofisa ushirika wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Bw Kulwa Masambu alisema kuwa ili vyama hivyo viweze kupiga hatua lazima wanachama warejeshe mikopo kwa wakati.
Bw Masambu alisema kuwa vyama hivyo vimekuwa mkombozi kwa wananchi hususani wanawake ambao ndiyo wenye changamoto kubwa ya kuziletea maendeleo familia zao na jamii inayowazunguka.
Kwa mwaka jana chama hicho kiliweza kukopesha wanachama wake 19 kiasi cha shilingi milioni 16.4 na kupata mapato ya shilingi milioni 1.9 hisa zikiwa shilingi 638,000 akiba zikiwa ni m 4.2 na kina jumla ya wanachama 76.

Mwisho.   

No comments:

Post a Comment