Monday, August 26, 2013

MWANALUGALI WATWAA UBINGWA



Na John Gagarini, Kibaha
TIMU ya soka ya Mwanalugali imenyakua ubingwa wa Micho Cup baada ya kuifunga timu ya Bamba zote za wilayani Kibaha mkoani Pwani kwa magoli 2-1.
Mchezo huo ilipigwa kwenye uwanja wa Kwa Mbonde wilayani Kibaha ulikuwa mkali na wa kusisimua muda wote na kuwafanya mashabiki waliojazana uwanjani hapo kushindwa kukaa kwenye viti vyao.
Washindi walianza kupata bao la kuongoza dakika ya nane ya mchezo kupitia kwa Makida Makida baada ya gonga za hapa na pale na kuwainua mashabiki wake.
Huku Bamba wakiwa hawajajiweka sawa walishtukia wakipachikwa bao la pili kupitia kwa Laurence Mugia dakika ya 13, hata hivyo Bamba walifanikiwa kupata bao la kufuta machozi dakika ya 44 ya mchezo.
Naye wandaaji wa mashindano hayo Athuman Shija alisema kuwa jumla ya timu 14 zilishiriki mashindano hayo ambayo yalikuwa na lengo la kuhamasisha michezo kwenye wilaya hiyo.
Kwa upande wake meneja wa kampuni ya 3 J’s ambao ndiyo wadhamini wa mashindano hayo Samwel Mwegoha alisema kuwa wataendelea kudhamini michezo ili vijana waweze kupata ajira kupitia michezo.   
Kufuatia ushindi huo wa Mwanalugali washindi walipata zawadi za jezi seti mbili, mipira miwili na mipira miwili, Bamba walipata mipira miwili  na fedha taslimu kiasi cha shilingi 150,000.
Mwisho.

Tuesday, August 20, 2013

MAJAMBAZI YAVAMIA KWA DAVIS MOSHA YAPORA




Na John Gagarini, Kibaha

WATU 10 wanaozaniwa kuwa ni majambazi wakiwa na silaha za jadi kama marungu na mapanga wamevamia kituo cha mafuta cha Delina mali ya Davis Mosha na kufanikiwa kupora vitu  mbalimbali ambavyo thamani yake bado haijaweza kufahamika mara moja.

Akithibitisha kutokea tukio hilo kamanda wa Polisi mkoa Pwani  Ulrich Matei alisema tukio hilo lilitokea usiku saa saba Agosti 19 eneo la Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani humo.

Matei alisema kuwa watu hao walifika kituoni hapo wakiwa na gari mbili moja  aina ya Prado na nyingine aina ya Saloon rangi nyeupe walizoegesha karibu na pampu za kuwekea mafuta.

“Baada ya hapo walimkamata mfanyakazi wa zamu  aitwaye Samsoni Rufunga na mlinzi wa kituo hicho Mohamed Shaban na kuwafunga  kamba  za miguu na mikono na kuwafungia ndani ya chumba kimoja kilichopo katika kituo hicho na kupora fedha hizo ambazo bado hazijafahamika,” alisema Matei.

Aidha alisema kuwa majambazi hao yalimkamata Frank Nyamahaga ambaye ni dereva mkazi wa Tabata nakumpora laki moja ,simu mbili za laki mbili na funguo za gari lake aina ya scania lililokuwa limeegeshwa kituoni hapo.

“Watu hao walimkamata Isack Silinu  ambaye alikuwa utingo wa scania hiyo ambaye naye aliporwa simu aina ya Itel yeny thamani ya sh.38,000, wakati Shabani Ramadhani aliporwa simu aina ya nokia yenye thamani ya sh. 45,000, Issa Mohamed aliyeporwa
simu aina ya nokia yenye thamani ya sh.75,000 na pesa taslimu sh.68,000  na wote walikuwa  wakisafiri katika lori aina ya scania
likitokea Iringa kuelekea Dar,” alisema Matei.

Aliongeza kuwa kama haitoshi watu hao walimpora Juma Seleman wa Mwanalugali, pikipiki aina ya Sanlg na fedha kiasi cha shilingi 46,000 alipokwenda kituoni hapo kwa ajili ya kununua mafuta.

Alibainisha kuwa katika tukio hilo hakuna mtu aliyejeruhiwa katika tukio hilo na jeshi hilo linaendelea na jitihada za kuwasaka majambazi hao ili waweze kutiwa nguvuni.
Mwisho.

Thursday, August 15, 2013

KIFAA KIPYA KUDHIBITI MADEREVA WAENDAO MWENDO KASI CHAINGIA NCHINI

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la polisi nchini limeanza mradi wa majaribio wa matumizi ya kifaa cha kisasa cha kuangalia mwenendo wa magari yanayokwenda mwendo kasi ili kupunguza ajali.

Akizungumza na waandishi wa habari jana wakati wakifanya majaribio ya vifaa hivyo kwenye barabara ya morogoro, kamanda wa kikosi cha usalama barabarani mkoani Pwani Nasoro Sisiwaya   alisema kuwa vifaa hivyo vimeanza kufanya majario mkoani humo kwa majaribio.

Sisiwaya alisema kuwa vifaa hivyo ni vya kisasa kwani vitafungwa sehemu ya juu na kuyaona magari tofauti na vile vya awali ambavyo hushikwa mkononi na vilikuwa havina taarifa za kutosha hasa wakati wa kuthibitisha kosa .

“Kifaa hichi kina uwezo wa kutoa taarifa za gari ambalo limeonekana kwenda kwa mwendo kasi  kwani kinauwezo wa kuonyesha kasi ya gari, muda na namba za gari husika, tofauti na kile cha zamani ambacho kinaonyesha mwendo kasi pekee ambapo dereva ana uwezo wa kukana kwani hakuna ushahidi wa kutosha,” alisema Sisiwaya.   

Naye mwakilishi wa kikosi cha usalama barabarani nchini Notker Kilewa, alisema kuwa kifaa hichi cha kisasa na kinauwezo wa kufungwa sehemu ambayo kitaona magari na mienendo yao na kulitambua gari lenye mwendo kasi kinyume cha sheria.

Kwa upande wake mwakilishi wa kampuni ya TMT ya Afrika Kusini, hapa nchini Twaha Ngambi ambayo inasambaza vifaa hivyo alisema kuwa kifaa hicho kitasaidia kukabiliana na madereva wanaokwenda mwendo wa kasi pamoja na makosa mengine ya barabarani.

Ngambi alisema kuwa kifaa hicho kitakuwa na uwezo wa kuona umbali wa mita 200 toka kilipofungwa hivyo itaondoa usumbufu wa kulisimamisha ghafla gari ambalo linabainika kuwa kwenye mwendo wa kasi.

Mwisho.



 Moja ya wataalamu toka Afrika Kusini kupitia kampuni ya TMT akiunganisha mitambo wakati wa wakifanya majaribio ya namna ya kutumia kifaa hicho ambacho kitakuwa na uwezo wa kuona magari ambayo yanakwenda kwa mwendo kasi kinyume na sheria za usalama barabarani, huko Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani.
 

YATIMA WTENGEWE ENEO

Na John Gagarini, Bagamoyo

KATA ya Miono wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani imetakiwa kutenga eneo kwa ajili ya kufanya shughuli za watoto yatima na wale waishio kwenye mazingira magumu.

Akizungumza jana kwenye kata hiyo wakati wa kuzindua mfuko wa kusaidia watoto yatima na wale wanaoishi kwenye mazingira magumu Meya wa mji mdogo wa Bagamoyo Abdul Sharifu alisema lazima viongozi wa vijiji wanapaswa kutenga maeneo kwa ajili ya kundi hilo.

Sharifu alisema kuwa kundi hilo limekuwa halitendewi haki hasa zinapotokea fursa mbalimbali kutokana na baadhi ya viongozi kutoona umuhimu wa watoto hao na kuwaona kama hawastahili kwenye jamii.

“Watoto yatima na wale waishio kwenye mazingira magumu ni sawa na watoto wengine na wanastahili kuwekewa mazingira mazuri ili waweze kuishi na kupata huduma muhimu za kijami hivyo ni vema mkawatengea eneo lao kwa ajili ya kufanyia shughuli zao,” alisema Sharifu.

Alisema kuwa katika eneo hilo watakuwa wakilitumia kwa ajili ya mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kusoma, michezo, kujifunza ufundi na masuala mengine kwa ajili ya watoto.

“Mimi mwenyewe nilikuwa yatima baada ya kufiwa na wazazi wangu ndiyo sababu nimeguswa na jambo hili la kuanzisha mfuko kwa ajili ya kuwasaidia kwani najua taabu wanazozipata na sisi ndiyo wa kuwasemea na kuwasaidia,” alisema Sharifu.

Kwa upande wake moja ya watoto yatima Yusuph Ally alisema kuwa jambo alilolifanya meya ni la kuigwa na viongozi wengine pamoja na jamii inayowazunguka.

Katika uzinduzi huo Meya huyo alichangia kiasi cha shilingi 500,000 kwa ajili ya mfuko huo na kuahidi kutoa shilingi milioni 2 mara ufunguaji wa akaunti utakapokamilika, jumla ya watoto zaidi 200 walihudhuria.    

Mwisho.

 
Meya wa mji wa Bagamoyo mkoani Pwani Abdul Sharifu katikati akiangalia watoto walipokuwa wakicheza wakati wa uzinduzi wa mfuko wa watoto yatima kata ya Miono wilayani humo.

WAKURUGENZI WA HALMASHAURI WASHUKIWA

Na John Gagarini, Bagamoyo

WAKURUGENZI wa Halmashauri za wilaya na Miji mkoani Pwani wametakiwa kuwashirikisha maofisa tarafa kwenye vikao mbalimbali vya maendeleo kwani wao ni wasimamizi wa mambo yote kwenye tarafa zao.

Hayo yalisemwa mjini Bagamoyo na katibu tawala wa mkoa wa Pwani Beatha Swai, wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo maofisa tarafa wa mkoa huo.

Swai alisema kuwa anawashangaa wakurugenzi wa halmashauri kutowatenga maofisa hao ambao ni kiungo muhimu baina ya serikali na wananchi lakini wamekuwa wakiwekwa pembeni na kuonekana kama hawastahili kushiriki kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo.

“Inashangaza hata kwenye vikao vya uongozi juu ya maendeleo hawashirikishwi kama ilivyo kwa wataalamu wengine kwenye halmashauri hawa nao wanapaswa kupewa kipaumbele katika michakato mbalimbali ya maendeleo,” alisema Swai.

Alisema kuwa tayari serikali ilishawapa waraka wakurugenzi hao kuwashirikisha kwenye masuala yote yanayohusu utendaji kazi ili wafanye kazi kwa pamoja lakini bado wanakaidi maagizo hayo.

“Tumeona kuwa kwenye vikao vya uongozi juu ya maendeleo hawashirikishwi jambo ambalo ni kinyume cha taratibu hivyo tutawachukulia hatua kali za kisheria wakurugenzi wote ambao wanakiuka taratibu za kazi,” alisema Swai.

Aidha alisema kuwa wakurugenzi hao wamekuwa na dhana kuwa maofisa tarafa hao wanakwenda kwa ajili ya kupata posho jambo ambalo halina ukweli kwani kushiriki kwenye vikao kama hivyo ni haki yao.
Awali akifungua mafunzo hayo mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza alisema kuwa baadhi ya maofisa tarafa wengine hawajui wajibu wao.

Mahiza alisema kuwa maofisa tarafa hao wanapaswa kujua wajibu wao kwa kutimiza malengo ambayo yanawekwa na halmashauri na wanapaswa kuwa na taarifa zote za shughuli za maendeleo na changamoto ndani ya tarafa zao.

Mwisho.

 
mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza akizungumza na maofisa tarafa wa mkoa huo alipokuwa akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo kwenye ukumbi wa chuo cha uongozi cha ADEM Bgamaoyo mkoani Pwani

baadhi ya maofisa tarafa wa mkoa wa Pwani wakimsikiliza mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza hayupo pichani wakati akifungua mafunzo kwa maofisa hao kwenye ukumbi wa chuo cha uongozi cha ADEM Bagamoyo mkoani Pwani.

Sunday, August 4, 2013

HABARI ZA MKOA WA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

HALMASHAURI ya Mji Kibaha mkoani Pwani imesema kuwa haijarudisha hazina fedha za ujenzi wa barabara kiasi cha shilingi milioni 700 bali fedha hizo zilichelewa kutumika kutokana na makandarasi kukiuka taratibu za ujenzi.

Hayo yalisemwa jana na mwenyekiti wa halmashauri ya mji huo Adhudadi Mkomambo, kwenye kikao cha madiwani kilichofanyika mjini Kibaha.

Mkomambo alisema kuwa kwenye kikao cha bunge kilichopita waziri wa ujenzi John Magufuli alisema kuwa mji huo umeshindwa kutumia fedha hizo kwanini waombe fedha nyingine.

“Licha ya Halmashauri kupata mafanikio makubwa kwa mwaka uliopita ikiwa ni pamoja na kuweza kukusanya fedha kiasi cha zaidi ya bilioni moja changamoto kubwa ni ya makandarasi wa barabara kushindwa kazi hivyo kushindwa kulipwa kwa wakati,” alisema Mkomambo.

Alisema kuwa matatizo mengi ya kihandisi kwani baadhi yao walioomba kazi hawajasajiliwa na wengine wametumia hati feki kupata kazi hizo licha ya kwamba mchakato wa kuwapata ulizingatia taratibu za kihandisi.

“Fedha hizi tunatarajia ifikapo Septemba 30 tutakuwa tumezifanyia kazi fedha hizo ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa ya kuboresha barabara za mji wetu ambao kwa sasa ndiyo unajengeka,” alisema Mkomambo.

Aidha alisema kuwa fedha hizo zipo na hazijarudishwa hazina tutahakikisha kuwa halmashauri inafanya tathmini ya hali ya juu kuwapata makandarasi bora ili kuachana na wakandarasi feki.

Aliwataka watendaji wa halmashauri hiyo kufanya kazi kwa kuzingatia maslahi ya wananchi ili waweze kuwaletea maendeleo kwani bila ya wao kuwa na uchungu hawataweza kuwafikisha kwenye maisha bora.

Mwisho.

Na John Gagarini, Bagamoyo

MEYA wa Mji wa Bagamoyo mkoani Pwani Abdul Sharifu amewataka waumini wa dini za Kikristo na Kiislamu mkoani Pwani waungane katika kipindi hichi cha mfungo kuiombea nchi ili isiingie kwenye mgawanyiko wa kiimani.

Aliyasema hayo wakati alipokuwa akitoa chakula cha futari kwenye shule za sekondari za Kimange, Changarikwa, Lugoba, Wazee wa CCM wa kata ya Lugoba na kata ya Miono wilayani humo.

Sharifu alisema kuwa viongozi na waumini wa dini wana nafasi kubwa ya kuweza kuhakikisha kuwa nchi ina amani kwa kufanya maombi ikiwa ni pamoja na kufunga.

“Nawaombeni waumini na viongozi wa dini zote kuliombea Taifa ili lisiingie kwenye machafuko ambayo yatasabisha amani kutoweka hivyo watu na nchi kushindwa kufanya shughuli za maendeleo,” alisema Sharifu.

Meya huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo alisema kuwa mbali ya viongozi wa dini na waumini kufanya maombi maalumu pia viongozi na wafuasi wa vyama vya siasa nao wanapaswa kutochochea uvunjifu wa amani.

“Endapo nchi itaingia kwenye machafuko hakuna kitakachoweza kufanyika kwani watu hawataweza kusali hata hao wanasiasa hawataweza kufanya siasa hivyo ni vema wanasiasa nao wakafanya siasa ambazo hazitaleta chuki na kuwagawa watu kutokana na itikadi za dini na siasa,” alisema Sharifu.

Aidha alisema kuwa watu wanapaswa kuheshimu mamlaka zilizopo na kushangazwa na baadhi ya wanasiasa kuchochea vurugu hali ambayo si nzuri kwani vita ikitokea athari hazitaangalia chama, dini wala rangi.

Aliwataka Watanzania kutokubali kugawanywa kwani endapo watakubali hali hiyo kuingia nchini itasababisha watu waishi kwenye hali ngumu na kushindwa kuwa na amani ambayo iko kwa sasa.
Mwisho.

Na John Gagarini, Kisarawe

BAADHI ya wakazi kutoka mikoa mbalimbali wamevamia msitu wa hifadhi wa Ruvu Kusini na kufanya uharibifu mkubwa kwa kukata miti kwa ajili ya kuchoma mkaa na mbao kwenye maeneo mbalimbali ya vijiji kikiwemo Kijiji cha Mtamba wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye kijiji hicho wakati wa operesheni ya kuwaondoa wavamizi hao, ofisa wa kampeni ya (Mama Misitu) kupitia shirika lisilo la Kiserikali la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), kwenye hifadhi ya Ruvu Kusini Yahaya Mtonda amesema kuwa licha ya watu hao kufukuzwa lakini bado wanaenbdelea na uharibifu.

Mtonda amesema kuwa Mama Misitu ni kampeni yenye lengo la kuzuia na kupunguza uvunaji haramu wa mazao ya misitu na kuboresha utawala bora kwenye sekta ya misitu ili jamii ipate manufaa na misitu hiyo.

Amesema kuwa kweli hali ilikuwa mbaya kabla ya mradi huo wa miaka mitano kuanza kwani watu hao wamekuwa wakiwaondoa lakini bado wanarudi ambapo wamnevamia msitu huu na kukaa kwenye vijiji vilivyo jirani na hifadhi na kufanya uharibifu mkubwa licha ya kuwachukulia hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutaifisha vyombo vyao vya usafiri kama vile magari, pikipiki na baiskeli na kuwapiga faini au vipiga mnada lakini bado wanendelea.

Amesema kuwa watu hao wamevamia kijiji hicho kwenye eneo linaloitwa kwa Bibi Hindu na kujifanya wanaishi hapo ambapo ni jirani kabisa na hifadhi hiyo ambapo wakishafanya shughuli za kuharibu misitu hurudi kijijini ili kuficha kile wanachokifanya.

Aidha amesema kampeni ya Mama Misitu imefanikiwa kwa kiasi kikubwa licha ya changamoto hizo za wavamizi kurejea mara kwa mara, lakini wameweza kuwawezesha wanajamii kuanzisha kamati za uhifadhi misitu ambapo endapo watakamata mali za wahalifu hao asilimia 20 ya vifaa vinavyokamatwa mara baada ya kuuzwa kwa nji ya mnada hubaki kijijini.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji hicho Nasoro Mzeru amesema kuwa watu hao walipewa notisi ya kuondoka miezi mili iliyopita lakini wanaonekana kukaidi agizo hilo la serikali.

Mzeru amesema kuwa eneo hilo lilitengwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu lakini watu hawea walivamia na kufanya makazi huku wakijihusisha na uharibifu wa msitu huo wa Ruvu Kusini na kila wakati wanaondolewa lakini wanarudi.

Mwenyekiti huyo amesema mbali ya kuharibu misitu pia wamekuwa wakijihusisha na vitendo viovu vikiwemo vya ubakaji, uvutaji bangi, uuzaji wa pombe haramu na wanawake kufanyabiashara za ngono jambo ambalo ni hatari na eneo hili ni hatarishi kwani watu hao licha ya kuitwa waishi kijijini wamekataa na kukaa kwenye eneo hilo la kwa Bibi Hindu,” alisema Mzeru.

Aidha amesema kuwa makazi ya yalichomwa moto hivi karibuni kwa lengo la kuwaondoa na kutakiwa kuondoka ambapo baadhi yao waliondoka lakini wengine walirudi na kuendelea na uharibifu wa msitu.

Mradi huo wa Mama Misitu kwenye hifadhi ya Msitu wa Ruvu Kusini una ukubwa wa Hekta 35,000 unaofadhiliwa na nchi za Finland na Norway, ulipewa jina hilo kwa lengo la kumuenzi mwanamke kwani endapo misitu itaharibiwa mwathirika mkuu ni mwanamke, na unatekelezwa kwenye vijiji 16 kwenye wilaya za Kibaha na Kisarawe ambapo hadi mwaka 2010 zaidi ya 40 za msitu huo ziliharibiwa na endapo udhibiti hautakuwepo msitu huo utatoweka ifikapo 2025

Mwisho.  

Na John Gagarini, Kibaha

WAZIRI wa Viwanda na Biashara Dkt Abdala Kigoda amesema kuwa uchumi wa Tanzania hauwezi kutegemea kilimo pekee bali viwanda ndivyo vinaweza kuinua uchumi na kuifanya nchi kuwa ya viwanda ifikapo mwaka 2025.

Ameyasema hayo kwenye Mtaa wa Zegereni wilayani Kibaha mkoani Pwani, wakati akizindua kiwanda cha kutengenezea Jipsamu cha kampuni kutoka China ijulukanayo kama Sun Shine Gypsum Limited  Group na kusema kuwa viwanda ndiyo moja ya vyanzo vya nchi kupata fedha nyingi.

Dkt Kigoda amesema kuwa hata nchi zilizoendela zilianza na viwanda vidogo na viwanda vya kati hadi vikafikia kuwa na utajiri mkubwa walionao sasa ambapo China ni moja wapo ya nchi zilizoanza kwa utaratibu huo lakini kwa sasa iko mbali kiuchumi.

Waziri amesema kuwa Viwanda vinachangia asilimia 30 ya pato la Taifa huku asilimia 40 ya wananchi wakiwa wameajiriwa kwenye sekta ya viwanda hapa nchini na kufanya uchumi kutegemewa kwa kiasi kikubwa kupitia sekta hiyo ambayo kwa sasa inaendelea kukua licha ya baadhi ya watu wakidai kuwa eti Tanzania haina viwanda vingi jambo ambalo si kweli.

Aidha amesema kuwa hata wajasiriamali wa tanzania wanaweza kuungana kujenga viwanda kama hivi ambavyo ni vya daraja la kati hasa ikizingatiwa malighafi za kutengenezea bidhaa hiyo zote zinapatikana hapa hapa nchini.

Ameongeza kuwa wamiliki hao wanapaswa kutoa kipaumbele cha ajira kwa wakazi wa Kibaha ili nao wafaidi matunda ya uwepo wa kiwanda hicho na wasaidie huduma za kijamii na kujenga mahusiano mazuri pia wazingatie viwango ili bidhaa hizo ziweze kuwa na soko ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ameipongeza kampuni hiyo na kusema kuwa dhana ya kurudisha uchumi kwa wananchi sasa imeanza kuonekana kwani baadhi ya wakazi wa hapa wamepata ujuzi na ajira.

Koka amesema kuwa kampuni hiyo imezingatia suala la ajira kwani hadi sasa watu 60 wamepata ajira huku baadhi yao wakipewa kazi za umeneja na si kuwa zile za ufagizi tu kwani hayo ndiyo yanayopaswa kufanywa na viwanda vingine ili kuweka usawa wa utendaji kazi 

Amebainisha kuwa Mji uliamua eneo hilo la Kata ya Visiga kuwa eneo la viwanda hivyo wajasiriamali na watu mbalimbali wana nafasi kubwa ya kuweka viwanda vyao hapo na si kung'ang'ania kujenga Dar es Salaam pekee ambapo hadi sasa eneo hilo tayari kuna viwanda vinne vingine vikiwa ni cha kusafishia mafuta, madini na nondo,  vimeshajengwa.

Kiwanda hicho kilianzishwa mwaka jana na kina thamani ya dola za Kimarekani milioni tatu na kimeajiri watu 60 na tayari kimeanza uzalishaji ambapo bidhaa zake zinauzwa ndani na nje ya nchi.

mwisho.