Thursday, July 27, 2017

MBUNGE ATOA MAGARI MAWILI YA KUBEBA WAGONJWA

Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa kulia akimkabidhi kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha Beda Mmbaga funguo za magari mawili ya kubebea wagonjwa na moja liliotolewa na Rais Dk John Magufuli kwa vituo vya afya vya Halmashauri hiyokulia ni mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mansour Kisebengo.
 
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiwasha gari lililotolewa na Rais Dk John Magufuli kwa ajili ya kituo cha Afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani wanaoshuhudia ni Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha na mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya Mansour Kisebengo.
Vitanda vitatu vya kuzalishia wanawake wajawazito vilivyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa kwa ajili ya vituo vya afya vya Jimbo hilo. 

POLISI PWANI WAKAMATA VIFAA VYA UVUVI HARAMU




                          Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia Makamba Sixbert (32) na Doto Mwinyi (45) wakazi wa Mlingotini wilayani Bagamoyo kwa tuhuma za kukutwa na vifaa vya uvuvi haramu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana alisema kuwa watu hao walikamatwa kwenye msako.

Shana alisema kuwa mtuhumiwa Sixbert  na Mwinyi walikamatwa Julai 25 majira ya saa 8 usiku maeneo ya Mlingotini kata ya Zinga baada ya msako maalumu wa makosa mbalimbali ukihusisha askari wa Jeshi la polisi wilaya ya Bagamoyo, Polisi Makao makuu, Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na maofisa uvuvi na mifugo wa wilaya hiyo.

“Mtuhumiwa huyo wa kwanza alikutwa na Scoopy Net moja, vioo vya kuogelea vitatu, mitarimbo mitatu, bunduki moja ya kuulia samaki, mikuki ya kuulia samaki mitatu na viatu vya kuogelea (Slipers) pea tatu huku mtuhumiwa wa pili akishikwa na Cylinder Gas walivyokuwa wakivitumia kwenye uvuvi haramu,” alisema Shana.

Kwenye tukio lingine madereva wawili wa pikpiki Juma Ally (37) na Mduga Agustino (25) kwa tuhuma za kupatikana na mitambo mitano ya kutengenezea pombe ya Moshi maarufu kama Gongo.

Kamanda Shana alisema kuwa tukio hilo limetokea Julai 25  majira ya saa tano asubuhi maeneo ya Lugoba kata ya Lugoba wilaya ya Kipolisi Chalinze wilayani Bagamoyo.

“Madereva hao wa pikipiki pia walikutwa na pombe ya Moshi lita 40 na lita 60 za Molasesi wakiwa wamezipakiza kwenye pikipiki yenye namba za usajili T 399 BHS aina ya Sanlg,” alisema Shana.

Aidha walifanikiwa kuwakamata Ahmada Hassan (45) mkazi wa Gogoni na wenzake watano kwa tuhuma za wizi wakiwa na Sabufa aina ya Kodec inayodhaniwa kuwa ni ya wizi.

Shana alisema watu hao walikamatwa maeneo ya Dunda kata ya Dunda Tarafa ya Mwambao wakituhumiwa kujihusisha na matukio ya uhalifu ikiwa ni pamoja na uporaji nyakati za usiku kwenye maeneo mbalimbali wilayani

“Misako wanayoifanya ni endelevu na askari shupavu wametawanywa kila kona kuhakikisha hali ya amani inakuwepo kwenye makazi ya wananchi na sehemu za biashara,” alisema Shana.

Aliwataka watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu kuacha mara moja kwa kutafuta shughuli nyingine za kufanya za kuwaingizia kipato halali kwani hawatasita kuwachukulia hatua kali za kisheria.

Mwisho 


WAZIRI WA AFYA ARIDHIA MLANDIZI HOSPITALI WILAYA





                                       Na John Gagarini, Kibaha

WAZIRI wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amekubali maombi ya Kituo cha Afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani kuwa Hospitali ya wilaya.

Alitoa tamko hilo kwenye uwanja wa Mtongani Mlandizi wilayani Kibahya wakati akipokea Magari mawili ya kubeba wagonjwa na vitanda vitatu vya kuzalishia mama wajawazito kutoka kwa Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa na gari moja kutoka kwa Rais Dk John Magufuli.

Alisema kuwa ombi lililotolewa na Mbunge huyo kwa viongozi wa ngazi za juu na kwake amelikubali hivyo mganga mkuu wa wilaya anapaswa kuandika barua na kuzipeleka sehemu husika kisha zifikishwe wizarani kwa ajili ya utekelezaji.

“Mbunge wenu amekuwa akipigania kituo hichi kwa muda mrefu kama alivyosema hivyo naona hakuna kipingamizi ili mradi tu taratibu zifuatwe ili kufikia hatua hiyo lengo kubwa ni kuboresha huduma kwa wananchi,” alisema Mwalimu.

Awali mbunge wa Jimbo hilo Hamoud Jumaa lisema kuwa maombi hayo alishayatoa kwa viongozi mbalimbali ikiwemo kwa Rais wa Awamu ya nne Dk Jakaya Kikwete na Rais Dk John Magufuli.
Jumaa alisema kuwa kituo hicho kwa sasa kinahudumia watu wengi tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo kwa sasa wanakaribia watu 100,000 hivyo kuna haja kabisa ya kuwa hospitali ya wilaya.

“Tuliambiwa tufanye maboresho mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujenga jengo la upasuaji, chumba cha kuhifadhia maiti pamoja na kuweka uzio vitu vyote hivyo tayari tumevifanya hivyo ombi letu hilo tunaomba ulifanyie kazi kwani tunaamini huduma zitaboreka,” alisema Ummy.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Kibaha Beda Mmbaga alisema kuwa watahakikisha wanaboresha mahitaji yote yanayotakiwa ili kutoa huduma za ubora kwa wananchi wanaokwenda kuhudumiwa hapo.


Mwisho.   

Wednesday, June 28, 2017

WAWILI WAUWAWA KWA RISASI KIBITI

Na John Gagarini, Pwani

WATU wasiofahamika wameendelea kufanya mauaji wilayani Kibiti ambapo wamewaua viongozi wawili wa Kijiji cha Mangwi kata ya Mchukwi kwa kuwapiga.

Viongozi waliouwawa ni pamoja na Michael Nicholaus Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mangwi na mtendaji wa Kijiji hicho Shamte Makawa.

Taarifa kutoka eneo la tukio zinasema kuwa tukio hilo lilitokea Juni 27 majira ya usiku kwenye Kijiji hicho na watu hao baada ya kufanya tukio hilo walichoma nyumba moto kisha kutoweka.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Pwani Onesmo Lyanga alipoulizwa juu ya tukio hilo alikiri kutokea na kusema kuwa bado wanaendelea kufuatilia ili kuwabaini wahusika wa matukio hayo.    

Mwisho.
      

Tuesday, June 20, 2017

DK MAGUFULI AWATAKA VIONGOZI WASIOWAJIBIKA WAJIONDOE



Na John Gagarini, Kibaha

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John Magufuli amewataka viongozi mbalimbali ambao wanashindwa kwenda na kasi ya awamu ya tano wajitathmini kwa kujiondoa wenyewe endapo watashindwa kuwajibika.

Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati akihutubia wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Bwawani wilayani Kibaha mkoani Pwani.

Dk Magufuli alisema kuwa kiongozi ambaye ndani ya miezi kadhaa hadi mwaka hajui alichokifanya ni vema akajiondoa mwenyewe na asisubiri kuondolewa.

“Serikali ya awamu huu ni ya uwajibikaji na si kutaka kufaidi ukubwa kufanya kazi lengo kubwa likiwa ni kuwatumikia wananchi hasa wale wanyonge ambao wanahitaji huduma zetu kwa kuwatumikia,” alisema Dk Magufuli.

Alisema kuwa kwa sasa tumeweka utaratibu wa kupeleka fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo na si matumboni bali ziguse maslahi ya wananchi wengi.

“Fedha hizo si matumboni, semina wala posho au safari za nje ambapo nimepata mialiko zaidi ya 50 ya nje ya nchi lakini nimekataa kwenda nataka kwanza tunyooshane wenyewe kwanza maana nikitoka watajisahau,” alisema Dk Magufuli.

Aidha alisema kuwa baadhi ya viongozi waliotumia vibaya rasilimali atapambana nao kwani Tanzania haiwezi kuwa nchi maskini kwani ni nchi ya pili duniani baada ya Barazili kwa nchi zenye rasilimali nyingi duniani.

“Tunakila aina ya madini, wanyama, maji, maziwa na mlima mrefu Afrika haiwezekani kuwa wasindikizaji wa matarajiri na sisi ni matajiri haiwezekani watu wale mlo mmoja, wanakosa dawa na huduma nyingine hii haiwezekani tutahakikisha wananchi wanaishi maisha yanayoendana na hali halisi ya mali zetu naombeni mniombee,” alisema Dk Magufuli.

Alisema ataendelea kutumbua ambapo kwa sasa wachache wanalalamika na kulia ni wale  waliokuwa wakijinufaisha huku wengi wakiumia huku wengine wakijinufaisha.


Alisema kuwa baadhi ya viongozi walishiriki kuhujumu nchi kwa kuingia mikataba mibovu hasa kwenye upande wa umeme ambapo baadhi ya walidiriki kusaini mikataba mibovu.

“Kwa sasa tuna mipango ya umeme wa uhakika ambapo nilipokwenda Ethiopia nilikutana na waziri mkuu nilimuuliza anafanyaje kupata umeme wa uhakika na kuuza nje tuliongea mengi na sasa wataalamu wake watakaja kwa ajili ya kuweka mazingira ya upatikanaji wa umeme wa uhakika,” alisema Dk Magufuli.

Akizungumzia kuhusiana na mauaji yanayoendelea wilaya za Kibiti na Rufiji alisema kuwa serikali ya awamu hii si ya kuchezea kwani wanaohusika wataona moto kwani watashughulikiwa kikamilifu.

“Tutawanyoosha na tayari tumeanza kuwanyoosha wanafikiri watapita hawatapita kikubwa kinachotakiwa ni wananchi kutoa ushirikiano kwa kuwafichua watu hao kwani baadhi ni ndugu jamaa na marafiki na kuendelea kuwaficha ni kujicheleweshea maendeleo ambapo kwa sasa wilaya hizo hazina viwanda kutokana na mauaji hayo,” alaisema Dk Magufuli.

Alibainisha kuwa mafanikio yaliyopatikana kwenye uongozi wake ni pamoja na makusanyo kuongezeka kutoka bilioni 880 na kufikia kiasi cha shilingi trilioni 1.3 kwa mwezi ambapo fedha hizo zimeweza kulipa elimu bure, pensheni ambazo hazikulipwa tangu mwaka 2010.
“Tumeweza kulipa madeni ambayo yalifikia kiasi cha shilingi trilioni 1.3 sasa yaliyobaki ni bilioni mbili ambapo tutaendelea kulipa madeni hayo kwa watu mbalimbali wanaodai halali na siyo madeni hewa,” alisema Dk Magufuli.

Alibainisha kuwa kutokana na makusanyo hayo serikali imeweza kufuta ada kwenye shule za msingi na sekondari ambapo kwa sasa zinatolewa kiasi cha shilingi bilioni 81.7 kwa ajili ya uendeshaji wa shule.

“Kutokana na elimu bure idadi ya wanafunzi wa darsa la kwanza wanaoandikishwa kwenye shule ya msingi wamefikia milioni mbili toka milioni moja na wanaojiunga na shule za sekondari wamefikia asilimia 27 huku mikopo ya elimu ya juu ikiongezeka toka watu 95,000 hadi 125,000 na bajeti kwa sasa ni bilioni 483,” alisema Dk Magufuli.

Aliupongeza mkoa wa Pwani kuwa na viwanda vingi ambapo na kuwa moja ya mikoa ambayo imetekeleza agizo la kuwa na viwanda ili kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na kuvutia uwekezaji.

Awali akimkaribisha Rais Dk Magufuli mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kwa sasa mkoa una viwanda 371 huku zaidi ya 80 vikiwa ni vikubwa na vya kati na vidogo 260.

Ndikilo alisema hata hivyo pamoja na mafanikio hayo changamoto kubwa ni upungufu wa umeme ambapo mahitaji ni megawati 60 lakini zinazopatikana ni 40, maji yasiyo na uhakika, baadhi ya maeneo kutokuwa na nishati ya gesi na baadhi ya barabara kutokuwa na lami.

Mwisho.











Monday, April 3, 2017

WATUHUMIWA UHALIFU WALIOVALIA HIJABU WAUWAWA NA POLISI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU watatu waliokuwa wamepakizana kwenye pikipiki moja wanaodhaniwa kuwa ni wahalifu wakiwa wamevalia hijabu wameuwawa kwa kupigwa risasi na polisi baada ya kukaidi amri ya kutakiwa kusimama.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Onesmo Lyanga alisema kuwa pikipiki nyingine mbili zilifanikiwa kukimbia.
Lyanga akielezea juu ya tukio hilo alisema kuwa lilitokea Aprili 2 mwaka huu majira ya saa 12:00 mchana eneo la kizuizi cha Mwembe Muhoro wilaya ya Rufiji mkoani Pwani barabara kuu ya Dar es Salaam Lindi.
“Siku ya tukio askari walipata taarifa kuwa kulikuwa na pikipiki tatu zikitokea Kibiti kwenda mikoa ya Kusini zikiwa zimebeba watu watatu kila moja huku miongoni mwa pikipiki hizo kati yake mbili wamebebwa watu waliovaa hijabu,” alisema Lyanga.
Alisema kuwa askari wa barabarani walipewa taarifa katika kizuizi cha Mparange na kuwasimamisha ili wawahoji lakini walikataa na kupita ambapo waliwajulisha wenzao kwenye kizuizi cha Ikwiriri lakini walikaidi kusimama.
“Baada ya hapo walifika kizuizi cha Ikwiriri lakini bado walikaidi kusimama na kuendelea kukimbia ndipo walipofika kituo cha Muhoro hata hivyo hawakusimama na askari waliokuwa doria wakiwa kwenye gari waliwafuatilia wakijaribu kuwafuatilia na wakavuka daraja la Mkapa na waliwapa onyo kwa kupiga risasi hewani,” alisema Lyanga.
Aidha alisema kuwa baada ya hapo watu hao waliruka kwenye pikipiki na kuanza kukimbilia msituni na ndipo askari walipowapiga risasi za miguu na kiunoni na kufanikiwa kuwakamata.
“Majeruhi hao walijulikana ni wanaume hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika na walikuwa kwenye pikipiki yenye namba za usajili MC 272 BLW aina ya Boxer yenye rangi nyeusi ambapo watu hao wanaodhaniwa kuwa ni wahalifu kwa mwonekano wao walijaribu kuwawahisha Hospitali ya Misheni ya Mchukwi,” alisema Lyanga.
Lyanga alisema kuwa walipofikishwa hospitali daktari alithibitisha kuwa watu hao wamefariki dunia ambapo hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika huku pikipiki nyingine mbili zilitoroka na kuelekea mkoa wa Lindi na taarifa zimetolewa polisi ili wawakamate.
Aliwataka wananchi kuwa watulivu pale wanaposimamishwa na askari polisi badala ya kujaribu kutoroka na kwa sasa jeshi hilo limeimarisha doria katika kukabiliana na uhalifu.
Mwisho.

Tuesday, March 28, 2017

MBUNGE AZINDUA UJENZI WA UZIO WA KITUO CHA AFYA



 Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa akionyesha shehena na saruji mifuko 500 kwa ajili ya uzio wa Kituo cha Afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani

 Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa akiwa amebeba saruji ambayo itatumika kwenye ujenzi wa uzio wa kituo cha afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani 







 Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa akizindua ujenzi wa uzio wa Kituo cha afya cha Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani


Na John Gagarini, Kibaha

KITUO cha Afya cha Mlandizi kimeanza mchakato wa kuelekea kuwa Hospitali ya wilaya kwa kuanza ujenzi wa uzio ambapo Mbunge wa Jimbo la Kibaha 
Vijijini wilayani Kibaha mkoani Pwani Hamoud Jumaa amewataka wafadhili mbalimbali kujitokeza kusaidia ujenzi wa uzio huo ambao utagharimu kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 200.

Akizungumza na waandishi wa habari Mlandizi wakati akizindua ujenzi huo mbunge huyo alisema kuwa wameanza kuboresha huduma zinazotolewa kituoni hapo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa uzio huo ikiwa ni moja ya vigezo vinavyotakiwa kufikia hadhi hiyo.

Jumaa alisema kuwa Kituo hicho cha afya ni tegemeo kubwa kwa wakazi wa Jimbo hilo ambalo kwa sasa lina wakazi 70,000 na wilaya jirani za Bagamoyo na miji ya Chalinze na Kibaha wanapata huduma hapo.

“Mpango huu nimeuanzisha kwa jitihada zangu binafsi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ambapo hadi sasa nimepata mifuko 500 ya saruji, kokoto lori saba mchanga, mchanga na tani moja ya nondo ambavyo vitasaidia katika ujenzi wa uzio huu tunaomba wadau wengine waendelee kutusaidia,” alisema Jumaa.

Alisema kuwa kutokana na kituo hicho cha afya kuwa tegemeo kubwa kwa wameona kuna haja ya kuwa Hospitali ya Wilaya ili waweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi watakaokuwa wanapata huduma hapo.

“Tumekubaliana vitongoji 26 na madiwani sita watoe 240,000 huku mfuko wa jimbo ukitoa kiasi cha shilingi milioni 4 kwa ajili ya tofali za uzio ambao utasaidia kuondoa uingiaji holela wa watu bila ya sababu za msingi ndani ya eneo la Kituo cha afya,” alisema Jumaa.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Mlandizi Eufrasia Kadala alisema kuwa wataungana na Mbunge huyo kuhakikisha wanafanikisha ujenzi huo ili kuboresha kituo hicho cha afya.

Kadala alisema kuwa kutokana na kutokuwa na uzio kumekuwa na mwingiliano wa watu kuingia kiholela hasa kutokana na kituo hicho kuwa jirani na makazi ya watu. 

Naye mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mdogo wa Mlandizi Tatu Jalala alisema kuwa waliupokea mkono mpango huo na kuupeleka kwa jamii kwa lengo la kumuunga mkono mbunge wao.

Jalala alisema kuwa wanaendelea kuihamasisha jamii ili iweze kuchangia ujenzi huo wa uzio ukamilike kwa wakati lengo likiwa ni kufanikisha harakati za kuwa Hosptali ya wilaya.

Mwisho.