Thursday, March 5, 2026

MAOFISA USAFIRISHAJI WATAKIWA KUUNDA VIKUNDI WAKOPE HALMASHAURI





MAOFISA Usafirishaji maarufu kama Bodaboda kwenye Mtaa wa Mwendapole B wametakiwa kuunda vikundi ili waweze kukopa vyombo vya usafiri vinavyotolewa na Halmashauri kuachana na mikopo ya taasisi za watu binafsi ambazo zina gharama kubwa.

Aidha alisema kuwa gharama za mikopo ya Halmashauri ni ndogo na marejesho yake ni madogo tofauti na mikopo ya vyombo hivyo kwenye taasisi au watu binafsi.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Mtaa huo Abubakar Matumla wakati wa kikao na waendesha pikipiki wa Mtaa huo na kuwa wanashindwa kufanikiwa kwa kukopa pikipiki kwa riba kubwa.

Matumla alisema kuwa gharama za kukopa pikipiki kwa watu binafsi imekuwa ikiwafanya wasifanikiwe kutokana na gharama kuwa kubwa za mikopo hiyo hivyo hujikuta wanashindwa kujiongezea kipato.

"Serikali imewawekea mazingira mazuri ya mikopo yake kwani mnauwezo wa kukopa pikipiki, bajaji na Toyo kwa gharama nafuu na unarejesha kiasi kilekile ulichokopa na hakuna riba ya mkopo unaokopa hivyo ni wakati wenu wa kujiunga na kuwa na vikundi na mtumie fursa ya mikopo pale Halmashauri fedha zipo za kutosha na vyombo vya moto vipo,"alisema Matumla.

Alisema kuwa yuko tayari kuwasimamia kuhakikisha wanapata mikopo hiyo kwani hapendi kuona waendesha pikipiki wakitaabika ili hali kuna sehemu wanaweza kukopa bila ya kuwa na marejesho makubwa pia aliwataka kutoa taarifa kwa wale wanaojihusisha na vitendo vya kiuhalifu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa waendesha pikipiki hao Abdulatif Mbonganga alisema kuwa tayari wameshaanzisha kikundi kimoja na tayari kimeshasajiliwa kikiwa kinasubiri wakati ukifika waende kukopa.

Mboganga alisema kuwa changamoto kubwa kwao ni kukosa vyombo vya usafiri hali inayowabidi kukopa vyombo hivyo kwenye taasisi za watu binafsi ambazo zinagharama kubwa na kujikuta wakitumia nguvu kubwa kwenye marejesho.

Moja ya maofisa usafirishaji Salum Msaku alisema kuwa changamoto ya uhalifu inatokana na baadhi yao kuwapa ma "day worker" hasa nyakati za usiku ambapo wanawaletea sifa mbaya.

Msaku alisema kuwa ili kudhibiti hali hiyo kila mwendesha pikpiki aendeshe pikipiki yake na siyo kumpa mtu mwingine pia wahakikishe wanavaa riflector ambazo zitawatambua kwa namba zinazoandikwa mgongoni inakuwa rahisi katika ufuatiliaji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtaa wa Miembe Saba B Nuru Awadh alisema kuwa wanapaswa kuwa na ushirikiano na kuunda vikundi vya bodaboda ili wapate mikopo nafauu.

Awadh aliwataka wajiheshimu na wasijiunge na makundi mabaya kwani Rais amewapa kipaumbele vijana katika uongozi na sehemu mbalimbali ili wawe vinara kwa utendaji kazi.

Tuesday, March 3, 2026

KAMBI SAMIA ARDHI KLINIKI YAANZA PWANI

HALMASHAURI ya Manispaa Kibaha kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeweka kambi ya Samia Ardhi Kliniki ikiwa ni maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani.

Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa katika kambi hiyo ya siku sita, Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Pwani Rugambwa Banyika alisema kuwa kliniki hiyo inalenga kutoa ushauri wa kisheria kuhusu masuala ya ardhi.

Banyika alisema kuwa shughuli nyingine zitakuwa ni kufanya makadirio ya pango la ardhi, kuandaa nyaraka za umiliki, kujibu changamoto za upimaji, urasimishaji, upangaji miji na michoro pamoja na kutoa hati za umiliki.

"Wananchi wote wanakaribishwa ili kupata huduma zote zihusiananazo na masuala ya ardhi ambapo huduma zimesogezwa ili kila mwananchi apate fursa katika kipindi hichi kuanzia Machi 2 hadi 7 kuelekea kilele cha siku ya Wanawake Duniani Machi 8,"alisema Banyika. 

Alisema kuwa kambi hiyo maalum ina lengo la kushughulikia changamoto mbalimbali za ardhi kwa wananchi hususan wanawake na wasichana katika masuala yanayohusiana na ardhi.

Baadhi ya wananchi Mariam Juma na Ahmed Abdala wameishukuru Serikali kwa kusogeza huduma hizo karibu yao na kueleza kuridhishwa na namna wanavyohudumiwa na wataalamu wa ardhi kwani wanatoa elimu ya kujitosheleza.

Kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kimkoa kinatarajiwa kufanyika Machi 8 2026 katika Uwanja wa Ujamaa Kata ya Umwe Tarafa ya Ikwiriri Halmashauri ya Mji wa Rufiji ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge.

Sunday, March 1, 2026

PWANI YAANZA MAANDALIZI MAADHIMISHO SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

MKOA wa Pwani umeanza maandalizi ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo kilele cha maadhimisho kimkoa yatafanyika Machi 8, 2026 katika Uwanja wa Ujamaa, Kata ya Umwe, Tarafa ya Ikwiriri, Halmashauri ya Mji Rufiji. 

Mratibu wa maadhimisho hayo, Roseline Kimaro, amesema mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge.

Akizungumza kuhusu maandalizi, Kimaro amesema maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Haki kwa Wanawake na Wasichana: Msingi wa Maendeleo Jumuishi Dira 2050,” ikisisitiza umuhimu wa usawa wa kijinsia na haki kama nguzo ya maendeleo endelevu. 

Amesema lengo ni kutambua na kuenzi mchango wa wanawake katika nyanja za kijamii, kisiasa na kiuchumi, sambamba na kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia.

Amebainisha kuwa kuanzia Machi 1 hadi 7 kutafanyika shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo utoaji wa elimu kwa umma na kampeni za uhamasishaji kuhusu usawa wa kijinsia,  kilele cha maadhimisho Machi 8. 

Ameongeza kuwa maandalizi yanaendelea vizuri na kutoa wito kwa wananchi na wadau wa maendeleo kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuunga mkono jitihada za kulinda na kuimarisha haki za wanawake na wasichana.