Monday, September 26, 2016

MAJALIWA AWASIMAMISHA MAOFISA MISITU RUFIJI

Na John Gagarini,Rufiji
WAZIRI mkuu Kassim Majaliwa amemsimamisha kazi Meneja wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Suleiman Bulenga kwa kushindwa kudhibiti na kusimamia mapato yatokanayo na shughuli za misitu hivyo kuikosesha mapato Serikali.
Mbali ya meneja huyo maafisa misitu watatu nao wamesimamishwa kutokana na kushindwa kudhibiti na kusimamia shughuli za uvunaji misitu na kusababisha wilaya kukosa mapato .
Maofisa misitu waliosimamishwa ni pamoja na Ofisa maliasili na mazingira wa wilaya Dk Paul Ligonja,Ofisa misitu Gaudence Tarimo na Jonas Nambua ambao watsimamishwa hadi hapo uchunguzi utakapokamilika.
Majaliwa alichukua hatua hiyo wilayani Rufiji wakati akizungumza na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Rufiji na wananchi wa wilaya hiyo  na kusema kuwa sekta ya misitu ni tatizo kwa kila wilaya na Rufiji ni moja ya wilaya hizo .
“Magogo yanasafirishwa bila utaratibu,na ndio wanakata miti kwenye misitu ya Utete na kupiga nyundo maeneo ya Kilwa,” alisema Majaliwa.
Alisema kuwa hakuna manufaa na TFS hivyo ameamua kusimamisha shughuli zote za uvunaji,katika wilaya hiyo na watumishi hao hadi wizara itakapotoa maelekezo mengine.
“Wilaya ya Rufiji inaongoza katika suala la utoroshaji wa misitu na kuruhusu uvunaji holela suala ambalo halikubaliki na nataka uwajibikaji na uadilifu katika maeneo ya kazi na watumishi wanapaswa wabadilike na waache kufanya kazi kwa mazoea,” alisema Majaliwa. 
Aidha Majaliwa alikemea utozwaji wa ushuru kwa watu wanaochoma mkaa unaofanywa na halmashauri ya Rufiji kwani kwa kufanya hivyo ni kuruhusu ukataji ovyo wa miti.
“Mkuu wa wilaya na mkurugenzi wa halamshauri ya Rufiji mnapaswa kusimamia mapato na matumizi ya fedha ili kuongeza mapato ya halmashauri iweze kupiga hatua ya kimaendeleo,”alisema Majaliwa.
Naye mbunge wa Rufiji,Mohammed Mchengelwa alisema kuwa nidhamu kwa watumishi inaonekana kupungua kwa baadhi ya watumishi kwenye halmashauri hiyo.

Mwisho




Friday, September 23, 2016

WAWILI WAFA AJALINI MMOJA ACHOMWA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

WATU wawili wamefariki dunia na wengine 11 kujeruhiwa mkoani Pwani kufuatia ajali iliyohusisha mabasi madogo mawili ya abiria kugongana uso kwa uso huko Kiparanganda wilayani Mkuranga.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na Kamanda wa Polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa watu hao walifariki papo hapo.

Mushongi alisema kuwa ajali hiyo ilitokea Septemba 21 mwaka huu majira ya saa 10:30 jioni T363 DCV likiendeshwa na Zidadu Mohamed (25) mkazi wa Dar es Salaam akielekea Kimazinchana liligongana na T363DHD yote aina ya Toyota Hiace likiendeshwa na Miraji Mlonga (22) akielekea Dar es Salaam.

Aliwataja waliokufa kuwa ni Zuhura Haji (21) na Neema Julius (25) wote wakazi wa Kimazinchana wilaya ya Mkuranga ambapo miili yao imehifadhiwa kwenye Hopsitali ya Wilaya ya Mkuranga kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi.

Aidha aliwataja watu waliojeruhiwa kuwa ni Majeruhi ni Mariamu Aloyce (46) wa Kimazinchana Mariamu Sultan (60) mkzai wa Chanika, Yusufu Maziku (33) mkazi wa Kimazinchana,Kulwa Abdala (30) makzi wa Mbagala,Ibrahim Hamis (3) mkazi wa Mbagala na Fatma Abdul (25) mkazi wa Chanika.

Wengine ni Salum Mohamed (54) mkazi wa Mwalusembe, Litus Mwarami (26) mkazi wa Kimazinchana Kidawa Abdala (30) mkazi wa Mbagala, Issa Hemed (2) mkazi wa Kimazinchana na Greyson Ernest (23) mkazi wa Kimazinchana.

“Tuna washikilia madereva wote waili kutokana na kusababisha ajali hiyo na watafikishwa mahakamani mara upelelezi wa kesi hiyo utakapokamilika ili kujibu tuhuma hizo zinazowakabili,” alisema Mushongi.

Kwenye tukio lingine mkazi wa Kwa Mathias Hamis Tenende (38) aliuwawa kwa kupigwa kisha kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali kwa madai ya kutaka kuiba pikipiki eneo la Umwelani.

Mwisho.
 








Monday, September 12, 2016

WAPONGEZA IDD EL HAJI KUFANYIKA KWA PAMOJA


Na John Gagarini, Kibaha

KUFUATIA sherehe ya Idd el Haji ambayo inahusisha na uchinjaji kufanyika jana ambapo waumini wa dini ya Kiislamu walisherehekea kwa pamoja tofauti na miaka mingine ambapo kila dhehebu lilikuwa likifanya siku tofauti safari hii wamefurahi kufanya kwa pamoja.

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha baadhi ya waumini wa Kiislamu wamesema kuwa utaratibu wa kusherehekea kwa pamoja ni mzuri kwani unaonyesha umoja na ni vema ukaendelea hata kwa siku zijazo.

Mrisho Halfan “Swagala”  alisema kuwa hakuna sababu wao kama waumini wa imani moja kufanya sherehe kwa wakati tofauti na kufanya kama ni imani tofauti.

“Tunaomba viongozi wa taasisi hizi za dini yetu wakae kwa pamoja na kufanya vitu kwa pamoja kwani kama mwaka huu sikukuu imependeza kwani wote tumejumuika na hali hii imeondoa tofauti na kutufanya kitu kimoja,” alisema Swagala.

Alisema kuwa kuna haja ya kuunganisha umoja wa waislamu kama hivi kwa kiufanya sherehe hiyo ambayo ni kubwa kwa Waislamu kote duniani kukumbuka yale yaliyofanywa na mtume ikiwa ni kufanya mambo yanayompendeza Mungu.

Kwa upande wake Abubakari Lipambila kutoka Masjidi Hazarajii Maili Moja Kibaha alisema kuwa sikukuu hiyo ni kwa ajili ya kurejesha furaha kwa watu wote.

Lipambila alisema kuwa waumini wa dini ya kiislamu wanapaswa kujihadhari na shetani katika kipindi hichi cha sherehe kwani naye yuko kazini kwa kuwapotosha watu ili waende kinyume na imani kwa kujiingiza kwenye vitendo viovu.

Mwisho.

Wednesday, September 7, 2016

BINTI AZAA MTOTO AMTUPA

Na John Gagarini, Kibaha

BINTI aliyetambulika kwa jina la Judith Paulo anayekadiriwa kuwa na umri katia ya miaka (18) na (22) anatuhumiwa kuzaa mtoto wa jinsia ya kike kisha kumtupa mwanae jirani na jalala.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu mwenyekiti wa Kitongoji cha Pera kata ya Pera Chalinze Mjini Hussein Mramba alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 7 majira ya saa 12 asubuhi eneo la Kwa Mwarabu.

Mramba alisema kuwa kichanga hicho chenye uzito wa kilogramu 3.2 kiliokotwa baada ya watoto waliokuwa wakiokota vitu mbalimbali jirani na jalala huku kikiwa kimewekwa kwenye mfuko wa Rambo.

“Watoto hao ndiyo waliogundua na ndipo walipotoa taarifa kwa watu wazima na kwenda kumchukua ambapo walimkuta mtoto huyo akiwa na afya njema huku akiwa hajavalishwa nguo yoyote mwilini mwake na jambo la kumshukuru Mungu kuwa mtoto huyo hakupata madhara yoyote,” alisema Mramba.

Alisema kuwa baada ya hapo ilibidi wasamaria wema wampeleke Hospitali ili kuangalia namna ya kumsaidia mtoto huyo ambaye kwa sasa yuko kwa mama mmoja ambaye amejitolea kukaa naye wakati taratibu nyingine zinafanyika ili apelekwe sehemu stahiki.

“Kwa maelezo tuliyopata baada ya kwenda Kituo cha Afya cha Chalinze ili kujua kama alijifungua hapo ilibainika kuwa binti huyo alijifungua kituoni hapo juzi majira ya saa 4 baada ya kufika hapo majira ya saa 3 usiku akiwa na uchungu wa kujifungua huku akiwa hajaongozana na mtu yoyote,” alisema Mramba.

Mramba ambaye pia ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mdogo wa Chalinze alisema kuwa baada ya kujifungua alikaa kama masaa mawili kisha kuomba kuondoka baada ya kujifungua salama na alimwomba muuguzi aondoke kwani alikuwa hajafunga mlango wa nyumba anayoishi hivyo ana hofu ya kuibiwa vitu vyake.

“Kutokana na utetezi wake huo ilibidi baadhi ya wazazi wamsaidia fedha kwa ajili ya kulipia teksi baada ya kumuonea huruma ambapo yeye alifika hapo kituoni kwa kutumia bodaboda,” alisema Mramba.

Aidha alisema kuwa binti huyo alionekana kuwa na wasiwasi alipofika kituoni hapo lakini hata hivyo baadhi ya wazazi waliokuwa hapo walijaribu kumweka sawa ili aone jambo la uzazi ni la kawaida.

Alisema kuwa taarifa hizo wamezitoa sehemu mbalimbali ikiw ani pamoja na polisi kwa ajili ya kusaidia kupatikana kwa binti huyo ambapo mita kama 100 aliposhushwa na teksi wamejaribu kuulizia lakini inavyoonekana kuwa hakuwa anakaa maeneo hayo kwani jina hilo hakuna mtu anayelifahamu.


Mwisho.