Thursday, September 12, 2013

NAGU ANZISHENI UZALISHAJI SUKARI

Na John Gagarini, Bagamoyo
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji na Uwezeshaji Mary Nagu ameitaka kampuni ya Eco Energy ya wilayani Bagamoyo mkoani Pwani kuendelea na mchakato wa kufungua kiwanda cha kuzalishia sukari ili kukabiliana na upungufu wa bidhaa hiyo hapa nchini.
Aliyasema hayo juzi alipotembelea kampuni hiyo ili kuona maendeleo ya mradi wa kilimo cha miwa kwenye kijiji cha Razaba wilayani humo na kusema kuwa mara kiwanda hicho kitakapoanzishwa kitasaidia kukabiliana na upungufu huo.
Nagu alisema kuwa kiasi kikubwa cha sukari inayotumika inatoka nje ya nchi hali ambayo inayaosababisha bei ya bidhaa hiyo kuwa juu ambapo uzalishaji ungeanza ungekuwa mkombozi kwa Watanzania.
“Tunajua mnakabiliwa na changamoto nyingi lakini ni vema mkaanza kutekeleza mradi huu ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa sukari ambapo uzalishaji huo utaambatana na mazo mengine ikiwemo umeme, mafuta ya mitambo ya Ethanol na mbolea,” alisema Nagu.
Aidha alisema kuwa serikali itahakikisha inaweka mazingira mazuri kwa wawekezaji ili waweze kutekeleza miradi yao ambayo pia ina faida kubwa kwa wananchi kama ilivyo kwa mradi huo ambao utainufaisha nchi ambayo inamiliki asilimia 25 kutokana na ardhi.
“Kwa sasa kuna watu wawili wamefungua kesi kupinga wawekezaji hao kutokana na kuchukua ardhi kwa ajili ya mradi huu licha ya taratibu za malipo kufanyika hivyo isiwe sababu ya wao kuchelewa kuanza kutekeleza mradi,” aliongeza nagu.
Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa kampuni hiyo Jonathan Nkandala alisema kuwa mbali ya kuzalisha sukari tani 150,000 kwa mwaka pia mradi huo pia utazalisha megawati 25 za umeme, mafuta na mbolea ambapo eneo la mradi lina ukubwa wa hekta 22,000 huku eneo la miwa lkiwa na ukubw awa hekta 8,000.
Nkandala alisema kuwa umeme utakaozalishwa megawati 14 hadi  15 zitatumika kwenye gridi ya taifa huku nyingine zikibaki kwenye mradi huo kwa ajili ya kuendeshea mashine na mitambo mbalimbali ambapo hadi sasa umeshatumia dola milioni 50 na hadi kukamilika kwake utagharimu kiasi cha shilingi dola milioni 500 na ulianza mwaka 2007 na unatarajiwa kukamilika 2016.
Mwisho.   

No comments:

Post a Comment