Thursday, May 5, 2016

UGAWAJI VIWANJA WAINGIA MTAFARUKU MADIWANI WATAKA KUJUA UNDANI WA ZOEZI HILO

Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la ugawaji wa viwanja kwenye eneo la Mitamba limeingia dosari baada ya Madiwani wa Halamshauri ya Mji Kibaha kutaka ufafanuzi juu ya utaratibu wa kugawa viwanja vilivyopo kwenye eneo hilo kabla ya kuvigawa kwa wananchi ambao walilivamia.
Madiwani hao walitaka ufafanuzi wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika Mjini Kibaha na kusema kuwa kabla ya zoezi hilo wataalamu wanapaswa kuwajulisha utaratibu wa jinsi watakavyovigawa viwanja hivyo.
Eneo hilo lilikuwa chini ya Wizara ya Mifugo Kilimo na Umwagiliaji lakini lilivamiwa na wananchi hali ambayo ilibidi Halmashauri igawane na wananchi nusu kwa nusu ambapo kuna jumla ya viwanja 6,500 kwenye hekari 747.
Diwani wa kata ya Sofu Yusufu Mbonde alisema kuwa mradi huo ambao una thamani ya shilingi bilioni 2.7 ulitakiwa uanze kutekelezwa mwezi huu hauko wazi hasa katika suala zima la jinsi fedha zitakavyotumika katika kuutekeleza kwake.
Mbonde alisema kuwa kwa kuwa serikali imeamua kulipima eneo hilo na kugawana na wavamizi hao wapatao 350 ni vema kukawa na uwazi kwa lengo la kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa.
“Tunachokitaka ni kupewa ufahamu juu ya zoezi hili kabla halijaanza kutekelezwa ili tuweze kujua kitakachofanyika pale kwani mradi huo ni mkubwa na utakuwa na faida kubwa kwa wananchi pamoja na Halmashauri hivyo ni vema kukawa na uwazi,” alisema Mbonde.
Kwa upande wake diwani wa Viti Maalumu Tuaje Ponza alisema kuwa moja ya vitu ambavyo vinashangaza ni kukodisha greda kwa ajili ya kazi hiyo huku Halmashauri nayo ikiwa na greda lake kwanini lisitumike hilo.
“Katika kupunguza gharama ni vema tukatumia greda letu kwani hatuwezi kukodisha wakati tuna la kwetu tulinunua kwa ajili ya kufanyia kazi zetu hivyo ni vema tukatumia la kwetu,” alisema Ponza.
Akijibu hoja mbalimbali mkuu wa Idara ya Mipangomiji Lucy Kimoi alisema kuwa viwanja hivyo vitatolewa kwa vipindi vinne tofauti ambapo awamu ya kwanza itakuwa viwanja 500 awamu ya pili viwanja 1,500 ya tatu 2,000 na ya tatu viwanja 2,500.
Kimoi alisema kuwa kutokana na ukosefu wa fedha zoezi hilo la ugawaji wa viwanja hivyo utafanywa na Halmashauri pamoja na wazabuni ambapo vitapimwa kwa shilingi 334,500 huku wazabuni wakivipima kwa shilingi 150,000 kwa kiwanja kimoja.
“Ni kweli tuna greda letu lakini kutoakana na zoezi hilo kuwa la muda mrefu ndiyo sababu tunahitaji mawili kwa ajili ya kufanikisha ugawaji huo kwani moja itabidi lisitoke eneo la kazi huku lingine likifanya kazi za nje kwani kazi zitakuwa ni nyingi sana ikiwa ni pamoja na sehemu ya huduma za jamii, makazi na huduma nyingine muhimu,” alisema Kimoi.

Naye kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Leah Lwanji alisema kuwa ombi la madiwani kuwapa uelewa juu ya mradi huo limekubaliwa na watakaa nao kabla ya kuanza ugawaji huo.
Mwisho.

MADIWANI WATAKA UDHIBITI WA MAPATO UPOTEVU BILIONI 1.1 KWA MWAKA

Na John Gagarini, Kibaha
MADIWANI wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wameitaka Halmashauri kudhibiti upotevu wa fedha kiasi cha bilioni 1.1 kwa mwaka kutokana makusanyo kuwa chini hivyo kushindwa kufikia malengo.
Wakizungumza kwenye baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo baadhi ya madiwani walisema kuwa kuna upotevu wa fedha nyingi ambapo endapo mianya hiyo ya kupotea fedha itazibwa itasaidia kudhibiti hali hiyo.
Akizungumzia namna fedha hizo zinavyopotea Diwani wa Kata ya Tumbi Hemed Chanyika alisema kuwa wao kama madiwani walifanya utafiti kwenye vyanzo vya mapato na kugundua mapungufu makubwa katika ukusanyaji.
Chanyika alisema mfano ni mapato ya ushuru wa mchanga ambako waligundua kuwa magari yanayoingia kuchukua machanga kwa siku ni magari 103 ambapo gari moja linalipia kiasi cha shilingi 3,000 kwa mwaka mapato ni bilioni 1.1 lakini makiso yaliyowekwa ni milioni 264.6 kwa mwaka tofauti ya milioni 900.
Alisema kwa upande wa stendi  ya Maili Moja makisio yalikuwa ni shilingi milioni 320 kwa mwaka ambapo magari yanayopita ni zaidi ya magari 500 kwa siku ni milioni 503 hadi 564 kwa mwezi ambapo upotevu ni kiasi cha shilingi milioni 183.6 huku Machinjio yakikadiriwa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 25 na kufanya upotevu kuwa milioni 56 ambapo kwa siku wanachinjwa ngombe 45 ushuru ukiwa ni shilingi 5,000 kwa mwaka 25.
“Upotevu huu wa fedha ni mkubwa sana hivyo kuna haja ya Halmashauri kujipanga ili kudhibiti hali hii kwnai endapo hali itaendelea hivi hatutaweza kufikia malengo ambayo tumejiwekea kwa mwaka,” alisema Chanyika.
Kwa upande wake Addhu Mkomambo alisema kuwa kwa sasa makusanyo yamefikia asilimia 54 ambapo ilipaswa kuwa yamefikia asilimia 75 kwa kipindi hichi cha robo mwaka wa bajeti.
Mkomambo alisema kuwa kwa miaka mitatu mfululizo Halmashauri ilikuwa ikifikia malengo lakini kwa mwaka huu ni tofauti ambapo ili kuziba pengo hilo inapaswa kufanyike operesheni maalumu kukusanya mapato ili kufikia lengo.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Leonard Mlowe Halmashauri alisema kuwa katika kuhakikisha makusanyo hayo yanafikia asilimia 100 atakuwa akikutana na watendaji wa serikeli za mitaa na kata kujadili namna ya kukusanya mapato hayo.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Leah Lwanji alisema kuwa suala hilo watalifanyia kazi kwa kulirudisha kamati ya fedha kwa ajili ya namna ya kudhibiti upotevu wa fedha hizo ili kuweza kufikia malengo yaliyowekwa.
Mwisho.   

MRADI WATAFUNA BILIONI 2 HAUJAKAMILIKA KWA MIAKA 10 SASA

Na John Gagarini, Msoga
MKOA wa Pwani umeunda tume kufuatilia maradi wa Skimu ya Umwagiliaji wa Bwawa hilo lililopo Kijiji cha Msoga kata ya Msoga wilaya ya Bagamoyo ambalo ujenzi wake umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 2 kwa kipindi cha zaidi ya miaka 10 bila ya kukamilika.
Akizungumza jana baada ya kufanya ziara kwenye mradi huo wa umwagiliaji mkuu wa Mkoa wa Pwani, Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa fedha zilizotumika ni nyingi lakini hakuna kinachoendelea na bado zinahitajika fedha nyingine ili kuukamilisha mradi huo.
Mradi huo ambao unasimamiwa na Halmashauri na Wizara ya Maji na Umwagiliaji Tume ya Umwagiliaji Kanda ya Mashariki ambayo makao yake makuu mkoani Morogoro umeshindwa kukamilika katika kipindi hicho huku kiwango kikubwa cha fedha kikiwa kimetumika.
Ndikilo alisema kuwa thamani ya fedha na mradi haviendani hivyo kuna haja ya kuufuatilia kwa kina mradi huo ambao ni mali ya wananchi wa kijiji hicho ambao ulilenga kuendesha kilimo cha umwagiliaji, maji kwa ajili ya kunywa kunyweshea mifugo, ufugaji wa samaki na kilimo cha mbogamboga.
Akielezea kuhusu mradi huo mhandisi mkazi wa kanda wa ofisi ya umwagiliaji Idd Said alisema kuwa mradi huo ulianza mwaka 2009 kwa uchimbaji wa Bwawa ambalo lilikamilika mwaka 2010 kwa gharama ya shilingi bilioni 1,697,444,266 kwa ajili ya tuta kubwa la bwawa, sehemu ya utoro, bomba kuu pamoja na chemba zake na birika la kunyweshea mifugo.
Said alisema kuwa mkataba wa pili ulisainiwa mwaka 2011 hadi mwaka 2012 na ulikuwa na thamani ya shilingi milioni 350,000,000 kwa ajili ya miundombinu ya umwagiliaji ambapo mkataba huu ulivunjwa kwa makosa ya mkandarasi kabla ya kazi kukamilika ambapo Halmashauri iliingia mkataba na mkandarasi mwingine ambaye hata hivyo naye alishindwa kukamilisha kazi hiyo.
“Kutokana na ujazo wa bwawa kuwa mdogo halmashauri iliomba kupata fedha nyingine tena kiasi cha shilingi milioni 300,000,000 kwa ajili ya kuchimba visima virefu ili kupata maji zaidi ya umwagiliaji kwa njia ya matone hata hivyo maji hayakupatikana katika visima vitatu vilivyochimbwa kwa urefu wa hadi mita 180,” alisema Said.
Alisema kuwa Halmashauri iliomba kubadilishiwa matumizi ya fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya mikataba hiyo ya awali na kuhamishiwa katika kazi ya sasa ya ujenzi wa kuongeza ukubwa wa bwawa kutoka mita za ujazo 427,600 hadi mita za ujazo 970,480 kwa ajili ya matumizi ya hekari 125.
“Baada ya changamoto hizo mkandarasi wa sasa ambaye ni wa tatu anaendelea na kazi aliingia mkataba wa shilingi milioni 915, 648 494 ambapo fedha aliyolipwa hadi sasa ni shilingi milioni 135,340,444 na mkataba huu ulisaini mwaka 2015  na alitakiwa kumaliza Machi 2016 lakini hadi sasa hajamaliza kazi na kuomba kuongezewa muda hadi Aprili 30 lakini hakukamilisha kazi,” alisema Said.
Alisema kuwa changamoto kubwa ya kazi hiyo ni kutokana na udongo unaotumika kuwa wa mfanyinzi ambao ukipata mvua kidogo unanata na kuwa vigumu kuchimba na kuubeba udongo huo.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Bagamoyo Marry Kisimbo alisema kuwa mradi huo umekumbwa na changamoto ya awakandarasi kushindwa kukamilisha kazi kwa madai ya udongo kuwa mbaya pale inaponyesha mvua.
Naye ofisa kilimo wa wa Halmashauri hiyo dionis mahilane alikiri kuwepo na tatizo katika utekelezaji wa mradai huo na kusema kuwa kwa upande wa malipo wakandarasi walilipwa kutokana na kazi waliyoifanya.
Kutoakana na maelezo hayo mkuu wa mkoa alisema kuwa haridhiki na maelezo hayo kwani haiwezekani kama bwawa lilishakamilika kwanini hawakuanza kutumia maji yaliyopo lakini wao wakataka kuongeza chanzo kingine cha maji.
Ndikilo alisema kuwa mradi huo unaonekana kuna dalili za matumizi mabaya ya fedha kwani haiwezekani mradi huo ushindwe kukamilika kwa kipindi cha miaka 10 wakati serikali na wadau wa maendeleo walikuwa wakitoa fedha kwa ajili ya mradi huo.
“Wote waliohusika na mradi huu hata kama wamehamishwa au wako masomoni wanapaswa kuja kutoa maelezo juu ya fedha hizi zilizotumika hapa hata wale wa halmashauri ambao wlaikuwa wakiwalipa wakandarasi ambao wamekuwa hawamalizi kazi na kuondoka baada ya kulipwa kwa watakaobainika kuwa walihujumu mradi huu sheria kali zitachukuliwa dhidi yao baada ya tume itakayoanza kazi kuanzia sasa na baada ya wiki watanipa majibu baada ya uchunguzi kuangalia kama kuna ubadhirifu,” alisema Ndikilo.
Mwisho.

ACHINJA MKE NA MTOTO WAKE KISA WIVU WA MAPENZI

John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani linamshikilia Frowin Peter Mbwale (26) mkazi wa Kawe Jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za kuwa ua kwa kuwachinja mkewe Oliver Erasto (23) na mtoto wake Emanuel Frowin (3) kutokana na wivu wa mapenzi.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa kwa waandishi wa habari Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 10:30 usiku eneo la Zinga kata ya Dunda Tarafa ya Mwambao wilayani Bagamoyo.
Mushongi alisema kuwa katika hali isiyo kuwa ya kawaida juzi siku ya tukio mtuhumiwa akiwa na mwenzake alijulikana kwa jina la Rajabu Juma (20) Mkazi wa Makongo Jijini Dar es Salaam waliwaua watu hao kwenye vichaka vilivyopo kwenye eneo hilo la Kaole.
“Muda huo mtuhumiwa akiwa na mwenzake alimhadaa mke wake kuwa waende kwenye nyumba yao ambayo inaendelea kujengwa kwa lengo la kuitazama ambapo mke wake alikubali na kumbeba na mtoto wao na kwenda huko ambako aliwachinja shingoni,” alisema Kamanda Mushongi.
Alisema kuwa mtuhumiwa kumbe lengo lake halikuwa kuangalia ujenzi wa nyumba yao huko Kaole kumbe alikuwa na lengo lingine la kufanya unyama huo ambao aliutekeleza akiwa na rafiki yake huyo ambaye walishirikiana kumchinja mke na mtoto wake.
“Chanzo cha mauaji hayo ni mtuhumiwa huyo alikuwa akimtuhumu mume wake kuwa ana uhusiano na mwanaume mwingine aitwaye Hamza mkazi wa Kawe Jijini Dar es Salaam na kusababisha mauaji hayo ya kusikitisha ambayo yamewaumiza watu wengi,” alisema Mushongi.
Alibainisha kuwa miili ya marehemu hao ilikutwa ikiwa imechinjwa na watu hao umbali wa mita 100 kutoka barabara ya magari itokayo Kaole kwenda eneo la Mbegani.
Aidha alisema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa majira ya saa 3:30 usiku baada ya wananchi Zinga kuwatilia mashaka walipokuwa wakijaribu kutaka kutoroka na wanatarajiwa kufikishwa mahakamani mara upelelezi utakapokamilika, miili ya marehemu imehifadhiw akwenye Hospitali ya wilaya ya Bagamoyo kusubiri ndugu kwa ajaili ya mazishi.
Mwisho.
  



Monday, May 2, 2016

MADIWANI WATAKA BODI YA TENDA KUVUNJWA

Na John Gagarini, Kibaha
MADIWANI wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wameridhia kuvunjwa kwa Bodi ya Tenda kwa kushindwa kutekeleza vizuri majukumu yake hivyo kusababisha miradi mingi kukwama.
Wakizungumza kwenye kikao cha Madiwani kilichofanyika mjini Kibaha madiwani hao walisema kuwa kutokana na bodi hiyo kutokuwa makini imesababisha wakandarasi wengi kuidai Halmashauri huku miradi mingi ikiwa imejengwa chini ya kiwango.
Akizungumza kwenye kikao hicho Diwani wa Kata ya Tumbi Hemed Chanyika alisema kuwa wazabuni wengi wameingia kwenye mgogoro na Halmashauri kwani wengi wameshindwa kufikia vigezo vya kazi wanazopewa huku mawakala wakishindwa kupeleka fedha za makusanyo kwa wakati.
Chanyika alisema kuwa bodi hiyo imeshindwa kuchagua wazabuni ambao wana uwezo wa kufanya kazi na inafanya kazi kwa mazoea pia ni ya muda mrefu hivyo inapaswa kubadilishwa ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi kwa wazabuni kwa lengo la kuleta maendeleo.
“Baadhi ya miradi mingi imekwama kwani wazabuni wengine wameshindwa kukamilisha kazi zao wengine wamekuwa wakiachia kazi bila ya kukamilika na kuondoka matokeo yake ni kuitia hasara Halmashauri na kudumaza maendeleo ya Mji wetu,” alisema Chanyika.
Kwa upande wake Kambi Legeza alisema kuwa miradi mingi iko chini ya kiwango kutokana na kutokuwa na wakandarasi wasiokuwa na uwezo pia mapato ya Halmashauri yameshuka hivyo kuna haja ya kuibadili ili kupata bodi nyingine itakayokuja na mawazo mapya.
Legeza alisema kuwa bodi hiyo ya tenda ndiyo yenye uwezo wa kuwapitisha wazabuni mbalimbali ambao wanapaswa kuwa na uwezo lengo likiwa ni kuleta maendeleo kwa halmashauri ambayo yanaleta manufaa kwa wananchi ambao ndiyo wanaolengwa.
Akijibu hoja hizo kaimu mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Leah Lwanji alisema kuwa ofisi yake imelipokea suala hilo na italifanyia kazi kama mapendekezo ya madiwani yalivyotolewa.
Lwanji alisema kuwa kuna taratibu za kisheria za kuvunja bodi hivyo lazima zifuatwe na endapo itabidi kufanya hivyo itafanyika ili kuhakikisha taratibu zinafuatwa kwa lengo la kuboresha.
Mwisho.

RC AWAPA SIKU TATU WAKURUGENZI KUWALIPA WAFANYAKAZI BORA

Na John Gagarini, Mkuranga
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo ametoa muda wa siku tatu hadi Mei 3 kwa wakurugenzi wa Halmashauri tatu za mkoa huo kuwapa zawadi za fedha watumishi  bora kwa mwaka huu baada ya Halmashauri hizo kutoa zawadi hewa kwenye Sherehe za siku kuu ya wafanyakazi May Mosi .
Sambamba na wakurugenzi hao wa Halmashauri pia ofisi ya Katibu Tawala mkoa (RAS) pamoja na mkurugenzi wa Shirika la Elimu nao wametakiwa kuwalipa wafanyakazi ambao walifanya vizuri kwenye vitengo vyao ambapo walipewa vyeti tu bila ya fedha kama taratibu zinavyokuwa za kuwapa fedha taslimu au hundi.
Ndikilo alitoa agizo hilo wilayani Mkuranga kwenye sherehe hizo ambazo kimkoa zilifanyika wilayani humo na kusema kuwa hayo ni masihara na yeye hayuko tayari kufanyiwa mzaha katika suala ambalo liliandaliwa kwa muda mrefu na kuwakopa zawadi hizo za fedha kwani nyingine toka mwaka jana hazijalipwa .
“Katika risala ya Shirikisho la Vyama Huru Vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) mkoa wa Pwani walilalamika kuwa kumekuwa na tabia ya baadhi ya waajiri kuwakopa zawadi za fedha watumishi wanaofanya vizuri  kama motisha lakini kwa hali hili siwezi kukubaliana nalo  nawapa siku tatu muwe mmewalipa watumishi hao vinginevyo atakayeshindwa aje ofisini kwangu akutane na adhabu niliyoiandaa,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa hawezi kuvumilia watu wazembe wanaofanya dharau kwenye mambo mazito na kwamba atachukua hatua kali kwa Halmashauri ambazo zitashindwa kutoa zawadi hizo kwani zingene zimetoa kwanini wengine washindwe.
“Mimi siyo mtani wenu wala si saizi yenu haiwezekani mniite nije kutoa zawadi hewa ndo maana hatoa zikichukuliwa za kinidhamu mnasema mnaonewa ikifika Jumatano muwe mmeshawapa zawadi zao wahusika huu ni mzaha umepitiliza kiwango anayedhani tunatania aendelee aone,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa ameshangazwa na kitendo hicho cha wao kumfanya atoe zawadi hewa kwani hiyo ni dharau Ras Pwani, Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Halmashauri ya Mji Kibaha, Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji na Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha.
“Hatutaniani hapa huu ni mzaha uliopitiliza kiwango ujumbe umefika namna hii mnakatisha tamaa watumishi kwa kudai kuwa mchakato bado ni jambo ambalo halijanifurahisha na nisingependa hali hii isijitokeze tena,” alisema Ndikilo.
Awali akisoma risala ya TUCTA Amini Msambwa alisema kuwa wafanyakazi wana haki ya kutimiziwa haki zao za msingi na siyo lazima zipatikane kwa shinikizo la maandamano, migomo na hata kufungia nje waajiri.
Msambwa alisema kuwa moja ya changamoto ni baadhi ya wawekezaji wa nje na wandani kuwanyima fursa wafanyakazi kujiunga na vyama vyao sehemu za kazi ambayo ni haki yao ya kisheria na kwa kuzingatia kauli mbiu ya mwaka huu ya Dhana ya Mabadiliko ilenge kuinua hali za wafanyakazi.
Aidha wameomba Halmashauri kuruhusu kuwa na mabaraza ya wafanyakazi na ambako yako yakutane kwenye vikao vyao vya kisheria lakini yanafanyika kwa ajili ya kupitisha bajeti za halmashauri.
Mwisho.

TCCIA PWANI WACHAGUANA ADAMJEE MWENYEKITI

Na John Gagarini, Kibaha
CHEMBA ya Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) mkoa wa Pwani imemchagua Zainuddin Adamjee kuwa mwenyekiti wake ambaye ataongoza kwa kipindi cha miaka mitatu.
Uchaguzi huo ulifanyika Mjini Kibaha mwishoni mwa wiki ambapo Adamjee ambaye aliwahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Kawe alichaguliwa bila ya kupingwa kutokana na kutokuwa na mpinzani ambapo uchaguzi huo uliitishwa baada ya uongozi uliopita kumaliza muda wake.
Viongozi wengine waliochaguliwa ni Ana Maridadi ambaye ni makamu mwenyekiti biashara, Karim Mtambo makamu mwenyekiti Kilimo na Mohamed Kiaratu mwakilishi wa mkutano mkuu Taifa.
Wengine waliochaguliwa ni Frank Mzoo mweka Hazina na Attiki Mohamed ambaye ni mjumbe wa kamati ambapo wagombea hao wote hawakuwa na wapinzani.
Akizungumza na wanachama na viongozi waliochaguliwa Rais wa TCCIA Taifa Injinia Peter Kisawilo alisema kuwa viongozi waliochaguliwa wanapaswa kuhakikisha wanawawekea mazingira mazuri wanachama ili waweze kuingia kwenye soko la ushindani la kimataifa.
Kisawilo alisema kuwa nchi ya Tanzania imeingia kwenye mikataba ya masoko makubwa yakiwemo yale ya Comesa, Sadc na la Afrika Mashariki ambapo wafanyabiashara wanapaswa kutengeneza bidhaa zitakazoingia kwenye ushindani na si kuwa watazamaji.
Kwa upande wake Adamjee alisema kuwa lengo lake ni kuhakikisha mkoa wa Pwani unakuwa moja ya mikoa ambayo inainua uchumi wake kutekeleza agizo la Rais Dk John Magufuli la kuwa na viwanda ili nchi iwe na uchumi wa kati.
Adamjee alisema kuwa kwa kuwa mkoa huo una uzalishaji mkubwa wa bidhaa mbalimbali za kilimo, ufugaji viwandani na rasilimali za uvuvi hivyo una nafasi kubwa ya kuinua kipato cha wananchi wa mkoa.
Awali mwakilishi wa mgeni rasmi Anatoly Mhango ambaye alimwakilisha mkuu wa wilaya ya Kibaha alisema kuwa chemba hiyo ina nafasi kubwa ya kuwainua wanachama wake kupitia masoko ya ndani na nje.
Mhango alisema kuwa njia mojawapo wanayopaswa kuitumia ni kujitangaza ili watu waweze kujua fursa zinazopatikana kupitia chemba hiyo pia kupitia Chama Cha Kuweka na Kukopa SACCOS kilichopo ndani yake wanachama wanapaswa kurejesha mikopo kwa wakati ili watu wengi waweze kukopa.
Mwisho.