Thursday, January 10, 2013

HABARI MOTOMOTO TOKA PWANI


Na John Gagarini, Bagamoyo
KUFUATIA wakazi wa Kijiji cha Ruvu Darajani wilayani Bagamoyo kuuondoa madarakani uongozi hatimaye tume ya watu sita imeundwa kuchunguza tuhuma zinazoukabili uongozi huo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mkuu wa wilaya hiyo Bw Ahmed Kipozi alisema tume hiyo imepewa muda wa wiki mbili ili kutoa majibu juu ya uongozi huo.
Bw Kipozi alisema kuwa tume hiyo itachunguza baadhi ya tuhuma ikiwa ni pamoja na kuuza eneo la umoja wa wauza mboga mboga wa Ruvu, kuingia mikata na wawekezaji isiyokuwa na masalahi na wananchi ikiwa ni kinyume cha taratibu, ubadhirifu wa fedha na uongozi kujihusisha na uingizwaji ngombe kinyume cha taratibu.
“Tume hii itaundwa na maofisa mbalimbali wakiwemo wale wa Taasisi ya Kuzuia na Kupamaba na Rushwa (TAKUKURU), mkagazi wa wa hesabu wa ndani, ofisa ardhi, ofisa anayehusika na Vijiji na ofisa usalama,” alisema Bw Kipozi.
Alisema kuwa tuhuma hizo endapo zitabainika viongozi hao watachukuliwa hatua za kisheria kutokana na makosa endapo yatakuwepo.
“Wananchi walikuwa na hoja za msingi kwani kwa sasa wameamka na kujua namna ya kuhoji jinsi gani rasilimali zao zinavyotumika hivyo lazima viongozi wazingatie taratibu za uongozi,” alisema Bw Kipozi.
Aidha alisema kuwa wananchi wana haki ya kuhoji pale wanapoona mali zao zinatumika vibaya na milango iko wazi kwenye ofisi yake kwa wananchi ambao wanaona kuwa kuna mambo ambayo yanakwenda kinyume.
Alisema kutokana na tatizo hilo umeteuliwa uongozi wa muda ambapo Bw Ramadhan Kondo ataongoza kama mwenyekiti na Jama Ramadhan atakuwa ofisa mtendaji wa kijiji hadi uchunguzi utakapokamilika.
Mwisho.
Na John Gagarini, Bagamoyo
WILAYA ya Bagamoyo mkoani Pwani inawafuatilia watu 11 ambao wako kwenye mtandao wa wanaowatishia watu kuwa maeneo wanayoishi ni mali yao kwenye baadhi ya Vijiji.
Mtandao huo ambao hutwaa maeneo makubwa ya Vijiji hivyo na kuyauza hali ambayo imekuwa ikileta mtafaruku kwa wakazi hao.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya hiyo Ahmed Kipozi alisema kuwa majina ya watu hao wanayo na kwa sasa wanaendelea kuwafuatilia ili kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.
“Mtandao huu ni wa watu waishio Jijini Dar es Salaam wenye asili ya Bagamoyo wamekuwa wakifanya vitendo hivyo ambavyo ni vya kitapeliwa kwa kuyachukua maeneo ya watu wakidai kuwa yaliachwa na mababu zao jambo ambalo si la kweli,” alisema Bw Kipozi.
Aidha alisema kuwa watu wanaotaka kununua maeneo au mashamba lazima wafuate taratibu za kisheria ili kukabiliana na matapeli hao ambao wanamtandao mkubwa unaowahusisha baadhi ya viongozi wa vijiji.
“Mtandao huo umekuwa ukitumia vyombo vya habari kuhalalisha utapeli wa maeneo na mashamba ya watu kwa kudai kuwa wao ni wamiliki wa maeneo husika,” alisema bw Kipozi.
Alitaja baadhi ya vijiji ambnavyo vimekumbwa na mtandao huo wa kutapeli mashamba ya watu kuwa ni pamoja na Talawanda, Masuguru na Msoga.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI wilayani Kibaha mkoa wa Pwani imetakiwa kuwadhibiti matapeli wa viwanja ambao wamekuwa wakiwaibia watu kwa kuwauzia viwanja ambavyo ni mali za watu wengine.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mchungaji kiongozi wa Kituo cha Maandiko kilichopo wilayani Kibaha Gervase Masanja alisema kuwa matapeli hao wamekuwa wakitapeli watu lakini hakuna hatua zozote zinazochukuliwa dhidi yao.
Mch Masanja alisema kuwa watu hao ambao wanajihusisha na vitendo hivyo wamekuwa wakitumia fedha kupindisha sheria pale wanapopelekwa kwenye vyombo vya sheria.
“Tunashangaa watu hawa kuendelea kutapeli watu lakini hawachukuliwi hatua zozote hata pale wanapopelekwa kwenye vyombo vya sheria tunaomba serikali iwashughulikie kwani wanafahamika,” alisema Mch Masanja.
Mch Masanja alisema kuwa hata yeye mwenyewe alitapeliwa kiasi cha shilingi milioni 2.3 kwa kuuziwa kiwanja ambacho ni mali ya mtu hata alipompeleka kwenye vyombo vya sheria malalamiko yake yaliondolewa na kupoteza fedha zake.
“Mambo kama haya ndiyo yanayoichafua serikali na kuonekana kama vile inawakumbatia watu hao ambao wamekuwa wakiwaumiza wananchi,” alisema Mch Masanja.
Aliitaka serikali kuwachukulia hatua kali baadhi ya viongozi wa vijji na mitaa kwa kushirikiana na matapeli hao katika kuwadhulumu wananchi kwani ofisi zao hutumika kufanya makubaliano ya mauzo ya maeneo.
Mwisho.          
Na Mwandishi Wetu, Kibaha

KUFUATIA aliyekuwa mgombea wa nafasi ya uenezi wilaya ya Rufiji Mkoani Pwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bw Suleiman Ndombogani kujiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema kuwa kimepata mpiganaji na si mzigo kama wanavyodai CCM.

Akizungumza na gazeti hili mjini Kibaha mwenyekiti wa Baraza la Vijana (BAVICHA) mkoa wa Pwani Bw Elison Kinyaha alisema kuwa chama hicho kimelamba dume kumpata mwanachana huyo.

Bw Kinyaha alisema kuwa Bw Ndombogani ni mtu makini na atakiletea ushindi chama hicho kwenye uchaguzi ujao na CCM wataona umuhimu wake.

“CCM wamesema kuwa huyu ni mzigo lakini kwetu ni sawa na almasi na fisi anapokosa anasema sizitaki mbichi hizi,” alisema Kinyaha.

Aidha alisema kuwa Bw Ndombogani ambaye ni mwandishi wa habari atakuwa ni mwenezi wa habari za chama hivyo watu kukijua ipasavyo.

Alisema kuwa moja ya changamoto ambayo wanataka ifanyiwe kazi ni kukuza soko la mkulima kwenye mkoa huo ambao una chanagamoto nyingi za kimaendeleo.
“Tunatarajia kuwapatia mafunzo vijana juu ya kujua haki zao za msingi ili waweze kujikwamua na changamoto mbalimbali zinazowakabili,” alisema Bw Kinyaha.

Aliwataka wanachama katika wilaya hiyo kuhakikisha kuwa wanajipanga kwenye chaguzi zijazo ili waweze kuongoza kwenye nafasi mbalimbali.

Mwisho.        




Na John Gagarini, Kibaha
BENKI ya Familia kupitia Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa imetoa kiasi cha shilingi bilioni 10 kila mkoa kwa ajili ya uanzishwaji wa benki.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha mkurugenzi wa benki hiyo Bw Dauda Salmin alisema kuwa lengo la kuanzishwa kwa benki hizo ni kuiwezesha jamii kuondokana na umaskini kwa kukopa kwa masharti nafuu.
Bw Salmin alisema kuwa uanzishwaji wa benki hizo utakuwa kwenye mpango wa operesheni jamii kukabiliana na watu wasio kuwa na ajira ili waweze kupata mikopo kwa ajili ya mitaji ya kuendeleza shughuli zao za ujasiriamali bila ya kujali itikadi ya chama cha siasa.
“Jumuiya iliamua kuanzisha benki hizo ambazo zitakuwa zikitoza riba ya asilimia 1.6 kwa kila mkopo ambapo ni ndogo ukilinganisha na taasisi nyingine za kifedha ambazo ziko kibiashara zaidi na  mbali ya kuweka riba kubwa pia zinaweka masharti magumu mfano kutoa hati ya nyumba au gari hali inayosababisha watu wengi kushindwa kukopa hasa wale wenye mitaji midogo,” alisema Bw Salmin.
Aidha alisema kuwa mikopo hiyo itatolewa kwa vikundi vya watu watano watano ambao kila mmoja atakopeshwa kiasi cha shilingi 500,00 na kila familia ambao ndiyo wakopaji lazima iwe na shughuli ambayo inaingiza kipato si chini ya shilingi 7,500 kwa siku na marejesho yatakuwa kwa kipindi cha miezi sita.
“Benki hizo ambazo zitakuwa kila kata tayari zimeshaanza kufanya kazi kwenye mkoa wa Dar es Salaam na sasa wanatarajia kuanza kutoa mikopo kwenye mkoa wa Pwani na wakopaji wataunganishwa na mifuko ya hifadhi ya jamii kwa ajili ya kukabiliana na majanga mbalimbali,” alisema Bw Salmin.
Alibainisha kuwa changamoto kubwa wanayoipata ni wakopaji wengi kuonekana kutaka kukopa kiwango kidogo cha fedha tofauti na ile iliyopangwa na watakaonufaika na mikopo hii ni wajasiraiamali wadogowadogo kama vile mama lishe, wenye magenge, waendesha bodaboda na wengineo.
Mwisho.

Wednesday, January 9, 2013

KRFA KUFANYA USAILI JANUARI 14 MWAKA HUU


Na John Gagarini
CHAMA cha soka mkoa wa Kilimanajaro (KRFA) kitafanya usaili kwa wadau walijitokeza kujaza nafasi za uongozi  Januari 14 mwaka huu.
Akizungumza kwa njia ya simu msemaji wa chama hicho Yusufu Mazimu alisema kuwa uchaguzi wa kujaza nafasi hizo uitafanyika Januari 26.
Mazimu alisema kuwa hadi sasa ni wadau sita waliojitokeza kujaza nafasi hizo ambazo zilibaki wazi kutokana na wagombea kutokuwa na sifa kwenye uchaguzi wa chama hicho uliofanyika Septemba 29 mwaka jana.
“Kwa muda uliobaki tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze ili kuwania nafasi hizo ili kukifanya chama kuwa na uongozi uliokamilika kwani kwa sasa uongozi bado haujakamilika,” alisema Mazimu.
Alizitaja nafasi hizo zilizobaki wazi kuwa ni pamoja na makamu mwenyekiti, katibu msaidizi, mjumbe kwenda TFF, mwakilishi wa soka la wanawake na wajumbe wawili wa kamati ya utendaji.
“Gharama ya fomu kwa nafasi za juu ni shilingi 100,000 huku nafasi za ujumbe zikitolewa kwa shilingi 50,000 ambapo tunawaomba wadau wajitokeze kabla ya muda wa usaili kwisha,” alisema Mazimu.
Mwisho.
Na John Gagarini
TIMU za soka za Polisi na Magadini zinatarajiwa kuchuana kwenye ligi daraja la Tatu mkoa wa Kilimanajaro Jumamosi Januari  12 mwaka huu.
Kwa Mujibu wa Msemaji wa Chama Cha soka Mkoa wa Kilimanjaro KRFA Yusufu Mazimu alisema kuwa mchezo huo utapigwa kwenye kituo cha VETA.
Mazimu alisema kuwa siku ya Jumapili Januari 13 kutakuwa na mchezo baina ya timu za Panone na Kitayosce kwenye kituo hicho.
Katika kituo cha Holili utapigwa mchezo baina ya Mwanga Asilia na Machava huku Jumapili ikiwa ni kati ya Kurugenzi na Bodaboda.
Kwenye michezo iliyopita Machava imeicharaza Bodaboda kwa magoli 2-1.
Mchezo huo ulipigwa kwenye uwanja wa Holili magoli ya washindi yalifungwa na Adam Soba dakika ya 29 na Issa Kipese dakika ya 80 na la Bodaboda lilifungwa na Paul Wliam dakika ya 17.
Kwenye kituo cha Himo Kilimanajaro iliifunga Vijana kwa magoli 2-1 wafungaji wakiwa ni Omary Juma dakika ya 24 na Ramadhan Gumbo dakika ya 36  la vijana lilifungwa na Abdala Husein dakika ya 75.
Timu ya Polisi Hai iliifunga KIA kwa mabao 4-0 mchezo uliopigwa kituo cha VETA Soweto na Forest walishindwa kutambiana baada ya kutoka suluhu ya 0-0.
Mwisho.

WANAWAKE WATAKIWA KUIMARISHA VICOBA


Na John Gagarini, Kibaha

MWENYEKITI wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) mkoa wa Pwani Bi Zainabu Vullu amewataka wanawake Mkoani humo kuimarisha vyama vyao vya kuweka na kukopa (SACCOS) ili ziweze kuwakomboa kiuchumi.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa baraza la umoja huo lililoambatana na uchaguzi viongozi wa kamati ya utekezaji ya mkoa wa Pwani.
Bi Vullu alisema kuwa wanawake kwa kiasi kikubwa ndiyo wanaoendesha familia hivyo ni vema wakaviimarisha vyama vyao vya kuweka na kukopa ili waweze kuboresha maisha yao na familia zao.
“Vyama hivi maarufu kama Vicoba vimekuwa mkombozi kwa wanawake wengi kwani zamani walikuwa na wakati mgumu kutokana na taasisi za kifedha kuwa na masharti magumu,” alisema Bi Vullu.
Bi Vullu ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu kutoka mkoani Pwani alisema kuwa Vicoba vimewasaidia wanawake na kuwafanya waweze kuwa na maisha bora na familia zao.
“Baadhi ya mafanikio waliyoyapata wanawake kupitia vyama hivi ni pamoja kujenga nyumba, kusomesha watoto, kuanzisha vitega uchumi na kuendesha familia zao,” alisema Bi Vullu.
Alizipongeza baadhi ya wilaya kwa kuweza kujiwekea akiba ambapo wilaya ya Bagamoyo imejiwekea kiasi cha shilingi milioni 11 huku wilaya ya Kisarawe wakiwa wamejiwekea kiasi cha shilingi milioni 5.
Aidha aliwataka wanawake katika mkoa huo kuanzisha miradi mbalimbali ya kimaenedeleo kwa kutumia fedha hizo za Vicoba pia wajitokeze kuwania nafasi za uongozi ndani ya chama.
Mwisho.  

Tuesday, January 1, 2013

UONGOZI WA KIJIJI WANGOLEWA



Na John Gagarini, Bagamoyo
SAKATA la viongozi wa Vijiji kuondolewa madarakani limezidi kushika kasi kwenye kata ya Vigwaza wilayani Bagamoyo ambapo juzi wananchi wa Kijiji cha Ruvu Darajani wameuondoa madarakani uongozi wa Kijiji hicho.
Vijiji vingine ambavyo uongozi wake umeondolewa na wananchi kwenye mikutano ya Kijiji ni Kitonga na Milo ambo wamewaondoa viongozi wao kutokana na tuhuma mbalimbali.
Wananchi wa Kijiji cha Ruvu Darajani waliukataa uongozi huo kwa tuhuma za kutoa eneo la soko kwa mwekezaji bila ya kupitishwa na wananchi ambao ndiyo wenye ridhaa ya kukubali maeno kupewa watu kwa ajili ya kuwekeza.
Uongozi huo chini ya Mwenyekiti Bw Kambona Athuman Kwaro na ofisa mtendaji wake Bi Mwajuma Bigo na wajumbe wa halmashauri ya Kijiji uliondolewa kwenye mkutano wa dharura  ambao uliitishwa kwa lengo la kuwapitisha wawekezaji walioomba maeneo  kwa ajili ya kuwekeza.
Mwenyekiti huyo bila ya kujua kilichokuwa kikiendelea alifungua mkutano na kusema kuwtaakuwa na ajenda mbalimbali lakini kubwa ilikuwa ni kuwapitisha wawekezaji hao ili wapatiwe hati za kumiliki maeneo hayo kwa kipindi watakachokuwa wamekubaliana.
Wananchi hao waliwapinga wawekezaji hao huku wakiwa na mabango wakiwataka viongozi wao kuachia ngazi na kusema kuwa mazingira ya kuwapitisha hayakuwahusisha wao hivyo hawako tayari kuwakubali kuwekeza kwenye kijiji hicho kwani kwa kipindi walioomba hawajaweza kutoa mchango ndani ya Kijiji.
“Mbali ya wawekezaji hawa wengine kilichotuudhi zaidi ni uongozi kumpa mwekezaji eti ajenge ofisi kwenye eneo ambalo lilipangwa kwa ajili ya soko na tayari kulishawekwa mabanda ambayo yameondolewa na kibaya hawajatushirikisha tunashangaa mtu kaanza kujenga,” alisema Bw Athuman Mnyamani.
Bw Mnyamani alisema kuwa maeneo mengi yametolewa kinyemela huku maeneo mengine wamewaongezea ukubwa tofauti na makubaliano ambapo hili eneo la soko walikubaliana ajenge lakini leo wanaitisha mkutano kutaka tumkubali au kumkataa wakati ameanza ujenzi kwa kuchimba msingi.
“Hapa hatuna hata maeneo ya wazi kwani yote yametolewa kwa wawekezaji ambao hatuoni manufaa yao kwani wanaahidi wakishapewa maeneo hayo hawatoi msaada wowote hivyo hawastahili kuwa viongozi ndiyo sababu ya sisi kuwakataa,” alisema Bw Mnyamani.
Akijibu tuhuma hizo mwenyekiti Bw Kwaro alisema kuwa ni kweli walikubalina na mwekezaji huyo kujenga ofisi kwa ajili ya mambo ya biashara lakini tulimwambia aanze ujenzi mwezi huu na si mwezi uliopita jambo ambalo alikwenda kinyume na kuanza kuchimba msingi.
“Tulikubaliana aanze ujenzi januari lakini yeye aliwahi na wakati anafanya hivyo mimi sikuwepo na tulimkubalia kwa nia njema hakukuwa na jambo lolote la kificho ambapo kama kijiji hakina uwezo wa kujenga hivyo tulikubaliana atakuwa akikilipa kijiji kiasi cha shilingi 100,000 kwa mwezi,” alisema Bw Kwaro.
Kutokana na majibu hayo watu walianza kupiga kelele za kusema kuwa hawana imani na uongozi huokila mtu aliyetakiwa kuuliza swali au akutoa mchango wake alikuwa akisema uongozi uondoke madarakani huku wananchi wengine wakizomea.
Kwa upande wake ofisa mtendaji wa kata ya Vigwaza Bw Masukuzi Masukuzi alijaribu kuwazuia wananchi hao kuacha makelelena  vurugu na kutoa hoja zao za msingi ili maamuzi yaweze kuwa sahihi.
“Kama mlivyoona wananchi wametoa kauli moja kuwa hawautaki uongozi na kikubwa ni tuhuma kuwa wametoa maeneo bila ya ridhaa yao likiwa hili la hapa ambapo ni makosa kwani wananchi ndiyo wenye maamuzi ya kumkubali au kumkataa mwekezaji,” alisema Bw Masukuzi.
Kutokana na wananchi kuukata uongozi inabidi nafasi hiyo kuongoza ichukuliwe aidha na mwalimu mkuu wa shule au ofisa ugani hadi pale halmashauri itakapotoa utaratibu mwingine namna ya kupata uongozi mwingine.
Wananchi hao kwa pamoja walimpitisha mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ruvu Darajani Bi Meri Nzowa kuongoza Kijiji hicho hadi utakapochaguliwa uongozi mwingine. Mkutano huo ulihudhuriwa na diwani wa kata hiyo Bw Mbegu Dilunga na mkuu wa kituo cha polisi Vigwaza Bw Salim Msangi
Mwisho.