Wednesday, March 25, 2015

ABAKA WANAE KWA MIAKA MIWILI MFULULIZO

Na Mwandishi Wetu, Kibaha

MKAZI wa Miembe Saba wilayani Kibaha mkoani Pwani Said Kundum (52) anatuhumiwa kuwabaka watoto wake wawili wa kike kwa kipindi cha miaka miwili na kuwasababishia maumivu makali.

Akizungumza na waandishi wa habari mtoto mkubwa wa mtuhumiwa ambaye anasoma darasa la saba katika Shule ya Msingi ya Miembe Saba jina limehifadhiwa (15) alisema kuwa baba yake alikuwa akimbaka yeye na mdogo wake kwa nyakati tofauti.

Alisema kuwa baba yake alianza kumbaka tangu mwaka 2013 ambapo kwa kipindi chote hicho alipokuwa akiwafanyia vitendo hivyo aliwatishia kuwa atawaua endapo watasema kwa mtu yoyote.

“Baba alikuwa akitubaka kwa nyakati tofauti wakati mama akiwa anaenda sokoni Kariakoo kuuza mboga huku akituacha na baba nyumbani na kutufanyia vietendo hivyo mimi na mdogo wangu ambaye anasoma darasa la tatu shule ya Msingi Tandau akiwa na miaka (12),” alisema Mwanafunzi huyo.

Aidha alisema kuwa wakati wakifanyiwa vitendo hivyo walikuwa wakisikia maumivu makali lakini aliwaambia kuwa wajikaze kwani baadaye watazoea na hawata sikia tena maumivu.

“Tulivumilia kwa kipindi choete hicho lakini Jumamosi Machi 21 ilibidi ni mwambie mama na kusema potelea mbali liwalo na liwe kama ataniua basi lakini hatuwezi kuvumilia vitendo hivyo,” alisema mwanafunzi huyo.

Alibainisha baada ya kumwambia mama yao ilibidi atoe taarifa kwa viongozi wa serikali ya mtaa wa Miembe Saba ambao nao waliwataarifu polisi ambao walimkamata baba yake.

Naye mama mzazi wa watoto hao Rahima  Mshamu alisema kuwa yeye hakujua kinachoendelea kati ya mume wake na watoto wake kwani alikuwa akimuacha na watoto na hakutegemea kama angeweza kuwafanyia watoto wake vitendo hivyo vya ukatili.

Mshamu alisema tangu alipoona na mume wake amekuwa akifanya biashara ya kuuza mboga za majani ambazo huzikusanya nyakati za jioni hadi usiku kisha kuzipeleka sokoni Kariakoo Jijini Dar es Salaam.

“Mume wangu nilikuwa nikimuamini kama baba na sikutegemea kama angeweza kufanya hivyo na huwa nakusanya mboga kwenye maeneo mbalimbali huko mashambani majira ya saa 12 jioni baada ya hapo tunazisafirisha usiku kwenda Kariakoo ambapo kule huwa tunazifikisha usiku wa manane na ifikapo saa 11 alfajiri tunakuwa tumemaliza na tunaanza safari ya kurudi nyumbani,” alisema Mshamu.

Alisema kuwa hayo ndiyo maisha waliyokuwa wakiishi tangu walipohamia kutokea Kibamba mwaka 2012 ambapo kwa kiasi kikubwa yeye amekuwa akiiendesha familia hiyo kwani mume wake hana kazi maalumu.
“Roho inaniuma sana kwani nimekuwa nikihangaika kuhakikisha kuwa familia yangu haipati shida watoto wanakwenda shule na ana mtoto wake ambaye sijazaa naye yuko sekondari namlipia ada na michango mingine na mahitaji yote lakini mume wangu yeye haangaiki kwa chochote tukio hili limeniuma sana nashindwa hata kujizuia,” alisema huku akilia kwa uchungu.

Aidha alisema kuwa kutokana na kumpenda mume wake alimnunulia pikipiki kwa ajili ya kuongeza kipato cha familia lakini aliuza pikipiki hiyo jambo ambalo lilimfanya ashindwe kumwelewa kuwa ana tatizo gani lakini alishangazwa na afya za watoto wake kuumwa magonjwa UTI kila mara.

“Mimi na yeye hatukuwa na ugomvi wowote ambapo hivi karibuni alijaribu kuuza sehemu ya eneo letu na nilipomuuliza alikataa hadi yule mnunuzi alipokuja na kutaka kumalizia fedha zilizobaki ndipo niligundua kuwa aliuza eneo hilo kwa nguvu bila ridhaa yangu na kusema kuwa aliwabaka watoto kuwa tuna ugomvi wa eneo hilo si kweli kwani suala la eneo ni la mwezi Machi huku yeye akiwabaka watoto miaka miwili iliyopita,” alisema Mshamu.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Hamis Shomary alisema kuwa baada ya kumhoji mtuhumiwa alikiri kufanya matukio hayo na kusema kuwa aliamua kufanya hivyo kutokana na ugomvi aliokuwa nao na mke wake na kuwa alikuwa akimnyima unyumba.

Shomary alisema kuwa mtuhumiwa alifikishwa polisi kwenye kituo cha Kongowe ambako anashikiliwa kwa hatua zaidi za kisheria ikiwa ni pamoja na kusubiri kupelekwa mahakamani.

Mwalimu mkuu wa shule ya Miembe Saba anayosoma mwanafunzi huyo Rajab Chalamila alisema kuwa mwanafunzi huyo alikuwa anaonekana mnyonge na mawazo mengi.

Chalamila alisema kuwa kutokana na hali ya mwanafunzi huyo alimwita baba mzazi zaidi ya mara mbili na kumwambia kuwa ampeleke hospitali mwanae na alisema alimpeleka na kukutwa na malaria lakini hali bado ilikuwa inajirudia na kuonekana kuwa ameathirika kisaikolojia. Jeshi la polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo.  


Mwisho.

Wednesday, March 18, 2015

RIDHIWANI AENDELEA NA ZIARA JIMBONI CHALINZE

Mbunge wa Chalinze Ridhiwani Kikwete kwenye kijiji cha Mkange wakati wa ziara yake kutembelea shughuli za maendeleo, kushoto ni katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo na kulia mwenyekiti wa Kijiji hicho Said Mgaya. 

Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani akiweka udongo kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya cha Kijiji cha Mkange wakati wa ziara yake kutembelea jimbo hilo kuona shughuli za maendeleo. 

Katibu wa chama cha mapinduzi CCM wilaya ya Bagamoyo Kombo Kamote akizungumza na wajumbe wa halmashauri ya Kijiji cha Matipwili juu ya uwajibijaki kwa wananchi wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete jimboni humo. 

 Baadhi ya Wazee wa Kijiji cha Matipwili wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani alipokuwa akiwahutubia wakazi hao kwenye mkutano wa hadhara wakati wa ziara ya kutembelea shughuli za maendeleo jimboni humo.

Baadhi ya akina mama wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani  alipokuwa akiwahutubia wakazi wa Kijiji cha Matipwili wakati wa ziara yake ya kutembelea shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo.

 Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Matipwli wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alipotembelea shule hiyo wakati wa ziara yake jimbo humo kuangalia shughuli za maendeleo

Mzee Halfana Mgobanya wa kijiji cha Gongo akichota maji ya mvua kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kijiji hicho ni moja ya vijiji vya jimbo hilo vinavyokabiliwa na tatizo la uhaba wa maji.

 Baadhi ya akinamama wa kijiji cha Mkange wakiwa wanachota maji huku kukiwa na foleni kubwa ya madumu ya maji eneo hilo nalo linakabilia na tatizo la maji ambayo yamekuwa yakitoka mara chache.


 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akifyetua tofali wakati akiwa kwenye ziara ya kukagua shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo

Friday, March 6, 2015

CHAMA CHA WAIGIZAJI PWANI CHATOA MISAADA KWA WAGONJWA HOSPITALI YA TUMBI

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Waigizaji Tanzania (TFDAA) mkoa wa Pwani kimetoa misaada mbalimbali kwa wagonjwa waliolazwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo ya Tumbi iliyopo wilayani Kibaha.
Misaada hiyo kwa ajili ya wagonjwa ilitolewa na baadhi ya wasanii kwa lengo la kuwafariji ambapo baadhi hawana ndugu wa kuwafariji.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kutoa misaada hiyo katibu wa chama hicho mkoani Pwani Kadnas Nassir alisema kuwa misaada hiyo ni moja ya shughuli zinazofanywa na kundi hilo.
“Wagonjwa ni wenzetu na mtu yoyote anaweza kuumwa kwa hiyo tumeona umuhimu wa kuwasaidia misaada kama sehemu ya kuwajibika kwetu na kuwafariji ili waone kuwa kuwa jamii ya sanaa nayo iko nao katika hali walizonazo,” alisema Nassir.
Nassir alisema kuwa misaada hiyo licha ya kwamba siyo mikubwa sana lakini ni faraja kwa wagonjwa ambao waliwapatia sabuni, dawa za meno nguo za watoto pamoja na mafagio ya usafi kwa hospitali hiyo pia walifanya usafi.
“Sisi mbali ya kutoa burudani pia tunajukumu la kuisadia jamii katika masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kwenye matatizo na furaha,” alisema Nassir.
Naye moja ya wagonjwa waliopatiwa msaada huo Beatrice Shirima alisema chama hicho kimeonyesha ubinaadamu kwani baadhi ya watu wana uwezo lakini hawonyeshi kujali watu wenye matatizo.
Kwa upande wake muuguzi wa zamu wa hospitali hiyo ya Tumbi Felisia Mungulele misaada hiyo imeleta faraja kubwa kwa wagonjwa na wameona kuwa jamii inawajali na watu wengine wajitokeze kusaidia kama hivyo.

Mwisho.   

HABARI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
UKARABATI wa miundombinu ya Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (TANESCO) mkoa wa Pwani unatarajia kukamilika ifikapo Machi 20 mwaka huu na utapunguza kukatika umeme mara kwa mara.
Kazi hiyo ya ukarabati ilianza mwishoni mwa mwaka jana ulikuwa ukamilike Februari mwaka huu ulishindwa kukamilika kwa kipindi hicho kutokana na ukubwa kazi hiyo ya kubadili miundombinu ambayo imechakaa.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Meneja wa TANESCO mkoa huo Sana Idindili alisema kuwa kutokana na zoezi hilo kumesababisha baadhi ya maeneo kupata mgao wa umeme.
Idindili alisema kuwa ukarabati huo ambao uko kwenye mradi umeongeza siku kutokana na kazi hiyo kuwa na ugumu tofauti na mtazamo wa mwanzo.
“Ni kweli kumekuwa na tatizo la umeme kukatika pamoja na mgao lakini hii inatokana na ukakarabati unaoendelea lakini hadi ifikapo Machi 20 tutakuwa tumekamilisha na huduma ya umeme itaendelea kama kawaida,” alisema Idindili.
Aidha alisema kuwa siku hizo ziliongezeka kutokana na kipindi cha mwisho wa mwaka kulikuwa na sikukuu ambazo ilibidi shughuli zisifanyike ndiyo sababu ya kuongeza siku zaidi za kukamilisha zoezi hilo ambalo lilikuwa la miezi mitatu.
“Katika wiki kuna siku tatu za kukata umeme kwa ajili ya kazi lakini nawatoa hofu wananchi kuwa mara baada ya ukarabati huo watapata huduma nzuri na watafanya shughuli zao kama kawaida,” alisema Idindili.
Alibainisha kuwa katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa za ukatikaji wa umeme wamekuwa wakitoa matangazo kwa kutangaza na kwa wale wenye matumizi makubwa ya umeme wamekuwa wakiwaandikia barua juu ya hali hiyo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAKULIMA wa Matunda na Mbogamboga nchini wametakiwa kuachana na matumizi ya dawa za kuulia wadudu badala yake watumie wadudu wanaokabiliana na wadudu waharibifu ili kunusuru afya za walaji na soko la nje ya nchi.
Aidha mbinu hii ya Kibaiolojia hutumia wadudu marafiki kama vile Nyigu ambao hudhibiti inzi au wadudu waharibifu ambao hutaga mayai yao ndani ya tunda au kwenye mmea na kuharibiwa na nyigu huyo.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na ofisa Mfawidhi wa Kituo cha Taifa cha Kudhibiti Visumbufu vya Mimea na Mazao kwa Njia ya Baiolojia (NBCP), Elibariki Msami alipoongea na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.
Msami alisema kuwa njia rahisi ni kuwatumia wadudu hao ambao wameonyesha kuwadhibiti wadudu hao waharibifu kwa kiwango kikubwa hivyo kuepusha matumizi ya madawa.
“Tumekuwa tukifanya utafiti kwa muda sasa ambapo tumeweza kuwazalisha nyigu hao ili wapambane na wadudu waharibifu kwenye matunda kama vile embe, machungwa na mapera pamoja na matunda mengine,” alisema Msami.
Alisema kuwa teknolojia hiyo ya wadudu ilifanywa hasa kwenye maembe ambayo yalikuwa yakioza kutokana na inzi wa embe kuyashambulia kwa kiasi kikubwa ambapo uharibifu umefikia kati ya asilimia 50 hadi 80 ya uharibifu.
“Kuna aina mbalimbali za wadudu wanaopambana na wadudu waharibifu ambao tunawazalisha na wameonyesha uwezo mkubwa wa kukabiliana na wadudu hao waharibifu,” alisema Msami.
Alibainisha kuwa upuliziaji wa dawa husababisha athari kwa wadudu marafiki ambao hupambana na wadudu waharibifu, wakulima, mimea, wanyama na mazingira huathirika na madawa hayo.
“Kwa upande wa mbogamboga baadhi ya wakulima wamekuwa wakitumia madawa na kuwafanya wadudu hao kuwa sugu pia dawa hizo wamekuwa wakizitumia muda mfupi kabla ya kuvuna jambo ambalo si zuri kiafya,” alisema Msami.
Ofisa huyo mwandamizi wa kituo hicho alisema changamoto kubwa inayowakabili katika kuwaeneza wadudu hao ni ukosefu wa fedha unachokikabili kituo hicho na kuimba serikali kukisadia ili kiweze kuzalisha wadudu hao kwa wingi.
Alisisistiza kuwa wadudu wapya wanaoletwa toka nje ya nchi kwa njia ya mbegu zinazoingiza hapa nchini ndiyo wamekuwa changamoto kubwa na wakulima wawe na imani na teknolojia hiyo isiyo na athari zozote.
Mwisho. 
Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA bei ya Mafuta kushuka wananchi wameiomba serikali kupitia mamlaka zake kushusha bei za nauli ambazo hazijashuka licha ya hali hiyo kujitokeza.
Walibainisha kuwa kipindi cha nyuma wamiliki wa vyombo vya usafiri walikuwa wakipandisha bei mara mafuta yanapopanda bei.
Akizungumza na gazeti hili mkazi wa Maili Moja wilayani Kibaha Said Ng’ombe alisema kuwa bei ya nauli inatokana na umbali na bei ya mafuta ambayo imeshuka kwa kiasi kikubwa.
“Tunaipongeza Serikali kwa kuhakikisha bei imeshuka na kuwadhibiti wauzaji wa bidhaa hiyo kuuza kwa bei iliyopo sokoni lakini pia wangepanga bei mpya za nauli kutokana na unafuu wa mafuta ili maisha yaweze kuwa mazuri,” alisema Ng’ombe.
Ng’ombe alisema kuwa mamlaka zinazohusika zinatakiwa kuliangalia hilo kwa undani kwani nauli bado ziko palepale na hazijashuka.
“Tunaomba kuwe na uwiano kama mafuta yameshuka bei na nauli nazo zishuke kwani walikuwa wakilalamika kuwa bei ya mafuta ni kubwa ndisyo kisa cha nauli kuongezeka sasa washushe na nauli,” alisema Ng’ombe.
Kwa upande wake Kibena Mtoro alisema kuwa endapo nauli itashuka itasaidia kuwapunguzia mzigo wananchi hivyo kufanya hali ngumu ya maisha kushuka na kuwa na hali nzuri.
Mtoro alisema kuwa nauli imekuwa changamoto kubwa kwa wananchi hivyo ushukaji wa wamafuta uambatane na ushukaji wa nauli pamoja na vitu vyote vinavyotegemea mafuta.

Mwisho.

Monday, March 2, 2015

HABARI MBALIMBALI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
KAMATI za Ulinzi na Usalama mkoani Pwani zimetakiwa kujipanga vizuri ili kukabiliana na matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi na kuua askari.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo, wakati wa kuwakaribisha wakuu wa wilaya wapya walioteuliwa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete.
Ndikilo alisema kuwa kumetokea matukio mawili ya uvamizi wa vituo vya Polisi vya Kimanzichana wilayani Mkuranga na Ikwiriri wilayani Rufiji ambapo katika matukio hayo askari waliuwawa na wavamizi hao wanaosadikiwa kuwa ni majambazi.
“Wametupiga mara mbili hatutakubali kupigwa tena hivyo kamati za ulinzi na usalama kuanzia ngazi ya chini kabisa hadi ngazi ya wilaya mnapaswa kuweka mikakati ya kukabilina na uvamizi huo ambao unatishia usalama wa raia,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema msingi mkuu wa nchi yetu ni amani hivyo hatutakubali vitendo hivi viendelee tena kwenye mkoa wa Pwani na wakuu wa wilaya wanapaswa kuhakikisha amani inakuwepo na kuwadhibiti hao wanaofanya hivyo.
“Nisingependa jambo hilo lijirudie tena kwani watu wanaofanya vitendo hivyo wanavuruga amani ya nchi iliyopo na silaha wanazopora zinaweza kutumiwa kwenye uhalifu hivyo kuwanyima amani wananchi,” alisema Ndikilo.
Mkuu huyo wa mkoa wa Pwani alisema kuwa matukio ya uhalifu iwe ajenda ya kudumu kwenye vikao mbalimbali vya maendeleo ili kufanikisha kutokomeza uhalifu wa aina hiyo ambao umezidi kushika kasi kwenye nchi.
Wakuu wa wilaya waliokaribishwa na wilaya zao ni Majid Mwanga Bagamoyo, Abdala Kihato Mkuranga, Subira Mgalu Kisarawe na Dk Hassan Mohamed Mafia.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wa mkoa wa Pwani wametakiwa kubadili tabia ili kukabiliana na maambukizi mapya ya ugonjwa wa Ukimwi ambapo yako juu kwa asilimia 5.6 zaidi ya kiwango cha Taifa cha asilimia 5.2.
Akizungumza na viongozi mbalimbali wa mkoa wa Pwani mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa maambukiziu yako juu sana.
Ndikilo alisema kuwa wananchi kwa kushirikiana na wataalamu wa mkoa wanapaswa kuweka mikakati mizuri kwa pamoja kuweka kupunguza maambukizi mapya.
“Hali ni mbaya sana kwani endapo kasi hii endapo itaongezeka itasababisha madhara makubwa sana kwani nguvu kazi kubwa itapotea na familia hazitakuwa na muda wa kuzalisha na kubaki kuuguza wagonjwa hivyo kushindwa kufanya shughuli za maendeleo,” alisema Ndikilo.
Aidha alitoa mfano kwa mwezi Desemba mwaka jana watu waliopima virusi vya ugonjwa wa Ukimwi walikuwa 69,197 waliokutwa na maambukizi walikuwa watu 7,800 sawa na asilimia 7.8.
“Takwimu  hizi na wastani wa maambukizi ni mbaya kwani inaleta picha mbaya kuwa watu hawabadili mienenendo yao licha ya kupatiwa elimu mbalimbali ya kujikinga na maambukizi ya Ukimwi,” alisema Ndikililo.
Alikitaka kitengo cha mapambano dhidi ya ugonjwa huo kiendelee kutoa elimu juu ya kujikinga na ugonjwa huo ambao unaua watu wengi na watu wafuate maagizo ya wataalamu wa afya ili kujiepusha.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
WAKUU wa wilaya Mkoani Pwani wametakiwa kuachana na urasimu bali waweke mazingira mazuri kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza kwenye mkoa huo kwani kwa sasa una fursa nyingi.
Akizungumza na viongozi wa mkoa huo wakiwemo wakuu wa wilaya mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa endapo watakuwa na urasimu watawakimbiza wawekezaji.
Ndikilo alisema kuwa Pwani ina fursa nyingi za kiuewekezaji baada ya Jiji la Dr es Salaam kujaa hivyo wawekezaji kuangalia maeneo ya pembezoni mwa Jiji hilo kw alengo la kuwekeza.
“Wakuu wa wilaya lazima muweke mazingira rahisi kwa wawekezaji na siyo kuwa vikwazo kinachotakiwa ni wawekezaji hao kufuata sheria za uwekezaji zilizowekwa na nchi yetu,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa njia rahisi ni kupima maeneo hayo haraka na kuyatenga kwa ajili ya uwekezaji ili kupunguza malalamiko toka kwa wananchi kuwa maeneo yao yamechukuliwa na wawekezaji pia jengeni miundombinu ya barabara, umeme na maji kwenye maeneo hayo.
“Mkoa unapokuwa na maeneo mengi ya uwekezaji ikiwa ni pamoja na viwanda vinasaidia kuongeza ajira kukuza uchumi wa mtu mmoja, wilaya, mkoa na Taifa kwa ujumla,” alisema Ndikilo.
Alibainisha kuwa mkoa wa Pwani una fursa kubwa kutokana na kuwa na miundombinu mizuri ya usafirishaji ikiwemo kwa njia za meli, ndege, treni na barabara.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAKULIMA wa zao la Korosho mkoani Pwani wametakiwa kuacha kuuza korosho yao ikiwa shambani kwa walanguizi ili kulipandisha thamani zao hilo.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Shirikisho la vyama vya Ushirika Tanzania Jasson Kalile wakati akifungua mkutano mkuu wa Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Pwani (CORECU).
Kalile alisema kuwa wakulima wengi wa zao la korosho wamekuwa wakiuza korosho yao ikiwa shambani kwa bei ndogo hivyo kushindw akunufaika na kilimo cha zao hilo.
“Tatizo kubwa lililopo kwa wanachama wengi wa CORECU ni kuuza korosho zikiwa bado ziko shambani ambapo huuza kwa bei ndogo huku walangizi hao wakija kuuza kwa bei kubwa,” alisema Kalile.
Aidha alisema kuwa walanguzi hutumia matatizo ya wakulima hivyo kuwarubuni kwa kuwapa fedha kwa korosho zilizo shambani na zinapofikia hatua ya kuuzwa siyo mali ya mkulima.
“Inapofuikia hauta ya kuuza walanguzi hao huuza kwa bei nzuri wanayoitaka huku mkulima akibaki hana kitu na kubaki na shida zake,” alisema kalile.
Kwa upande wake Mwenyekiti aliyemaliza muda wake alisema kuwa Juma Abeid alisema kuwa kazi kubwa waliyoifanya ni kukiresjesha chama hicho kwenye hadhi yake baada ya kutokea migogoro kwa muda mrefu.
Abeid alisema kwa sasa hali ni nzuri na tayari wameweka mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuanzisha benki ya ushirika ili wakulima waweze kukopeshwa kwa riba ndogo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkuranga
KATIKA kukabiliana na changamoto kubwa ya ukosefu wa maji wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani inatarajia kukamilisha miradi mitatu mikubwa ya maji yenye thamani ya shilingi milioni 874 mwezi huu.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kikao cha baraza la Madiwani wa Halamshauri ya wilaya ya Mkuranga mhandisi wa maji wa wilaya Renard Baseli alisema miradi hiyo iko kwenye hatua za mwisho.
Baseli alisema kuwa miradi mingi inakumbwa na tatizo kubwa la ukosefu wa fedha ambazo huichelewa kufika na hazifiki kwa wakati hali inayopelekea miradi mingi kushindwa kukamilika kwa wakati.
“Miradi hii mikubwa mitatu itasaidia kwa kiais kikubwa kukabiliana na ukosefu wa maji kwa wananchi wa wilaya ya Mkuranga na kilio hicho kitapata jibu kwani miradi hiyo ni ya thamani kubwa,” alisema Baseli.
Aliitija miradi hiyo kuwa ni ule wa Mvuleni Kilimahewa Kusini wenye thamani ya shilingi milioni 545, Kilamba wenye thamani ya shilingi milioni 285 na Nyamato wenye thamani ya shilingi milioni 44.
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Lukanga Said Kubenea alisema kuwa miradi mingi ya maji imekuwa ikiahidiwa kukamilika lakini inachukua muda mrefu kukamilika huku wananchi wakiendelea kupata taabu.
Kubenea alisema kuwa ucheleweshaji wa miradi ya maji imekuwa kero kubwa kwa wananchivyo kuwataka watendaji wa idara ya maji kuhakikisha wanakamilisha miradi hiyo kwa wakati.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkuranga
WAKUU wa Idara mbalimbali wilayani Mkuranga mkoani Pwani wametakiwa kuwalipa kwa wakati watumishi wa ngazi za chini ili kuleta ufanisi wa kazi.
Hayo yalisemwa Mkuranga na Mkuu mpya wa wilaya ya Mkuranga Abdala Kihato wakati wa makabidhiano ya ofisi na aliyekuwa mkuu wa wilaya hiyo Mercy Silla na kusema kuwa hakuna kitu kinamkera kama malimbikizo kwa watumishi.
Kihato alisema kuwa kumekuwa na tabia ya baadhi ya wakuu wa idara kujilipa posho mbalimbali na kuwaacha watumishi wa ngazi za chini wakidai mishahara ya kila mwezi na kuwaambia fedha iliyoletwa haitoshi.
“Hakuna kitu nisichokipenda kama watumishi kudai kwani serikali huwa inajitahidi kuleta mishahara lakini inapokuja wakubwa wanajipendelea kwa kujilipa malipo mengine na kuwaacha watumishi wa ngazi za chini wakiwa na malalamiko,” alisema Kihato.
Aidha alisema kila mtu ana haki ya kulipwa stahiki yake bila ya kujali ngazi ya kazi kwani wote ni watumishi na hakuna sababu ya kubaguana.
“Ni vema mkagawana kilicholetwa siyo vizuri wengine wapate na wengine wakose wote wana haki sawa kulipwa kwa mujibu wa sheria na si wakubwa kujipendelea kwani kufanya hivyo ni kushusha morali ya kazi,” alisema Kihato.
Kwa upande wake Silla alisema kuwa anawashukuru watumishi wa wilaya hiyo kwa kumpa ushirikiano wa hali ya juu katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Silla alisema kuwa moja ya changamoto zilizopo kwenye wilaya hiyo ni elimu ambapo bado kiwango cha ufaulu kiko chini sana.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkuranga
BAADHI ya Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani wameitaka halmashauri hiyo kununua greda kwa ajili ya kujengea barabara ili kukabiliana na changamoto ya miundombinu hiyo kutokamilika kwa wakati.
Madiwani hao walitoa ushauri huo kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika Mkuranga na kusema kuwa upatikanaji wa greda kutasaidia kupunguza gharama za ujenzi wa barabara.
Moja ya madiwani hao Karu Kavina Diwani wa kata ya Kiparanganda alisema kuwa barabara nyingi hazikamiliki kwa muda uliopangwa kwa sababu gharama ya kukodisha greda ni kubwa.
“Halmashauri yetu ingekuwa na greda ingekuwa ni rahisi kwani gharama zingekuwa ndogo ambapo wananachi wangechangia fedha kidogo kwa kushirikiana na halmashauri yao,” alisema Kavina.
Kavina alisema kuwa karibu kila diwani ambaye ni mwakilishi wa wananchi analalamika barabara za eneo lake kutokwisha hivyo suluhisho ni kununua greda la Halmashauri.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Vianzi Hamis Kitwana alisema kuwa kumekuwa na mvutano mkubwa wa kila diwani kutaka fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hivyo njia rahisi ni kununua greda.
Kitwana alisema kuwa hata kama Halmashauri haina fedha ikope kwa ajili ya kununulia kama baadhi ya Halmashauri nyingine zinavyofanya vinginevyo hali ya barabara itakuwa ni changamoto kubwa.
Kwa upande wake mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Ana Mwakalelya alisema kuwa changamoto kubwa iliyopo ya kunua greda ni ukosefu wa fedha lakini akasema hilo ni wazo ambalo watalifanyia kazi.
Mwisho.