Thursday, December 5, 2013

WAOMBA KUCHOTA MAJI KWENYE MSITU

Na John Gagarini, Kibaha

WANANCHI WA Kitongoji cha Mpiji wilayani Kibaha mkoani Pwani wameuomba uongozi wa Wakala wa Misitu (TFS) Kanda ya Mashariki kuwaruhusu kupita kwenye eneo la msituo huo ili waweze kupata huduma ya maji ya kisima.

Akizungumza kwenye mkutano ulioandaliwa na Mradi wa Mama Misitu moja ya wananchi wa Kitongoji hicho Bw Shaban Nyoka alisema kuwa wamekuwa wakichapwa bakora na walinzi wa msitu huo mara wanedapo kuchota maji.

Bw Nyoka alisema kuwa kutokana na ukosefu wa maji kwenye Kitongoji hicho huwapasa kwenda kuchota maji kwenye visima vilivyopo kwenye hifadhi ya msitu huo.

“Tumekuwa tukichapwa bakora mara tunapokwenda kuchota maji kwenye visima hivyo vya maji lakini cha kushangaza mifugo ya moja ya wawekezaji kijijini hapo imekuwa haichukuliwi hatua yoyote, tunaomba waturuhusu tuwe tunachota maji huko,” alisema Bw Nyoka.
Alisema kuwa watu wamekuwa wakienda kuchota maji huko lakini wanapokutwa huko na walinzi wa msitu wamekuwa wakiadhibiwa kama vile wahalifu jambo limekuwa likiwafadhaisha.
“Sisi tunaomba hifadhi ituruhusu tuchote maji kwani hatufanyi uharibifu wowote kwani lengo letu ni kwa ajili ya kupata maji tu na si kingine hivyo ni vema wanegeturuhusu tupite huko kwa ajili ya kupata maji tu na si vingenevyo,” alisema Bw Nyoka.
Kwa upande wake mratibu wa mradi huo Bw Yahaya Mtonda alisema kuwa tatizo kubwa linatokana na uharibifu ambao umekuwa ukifanywa ndani ya msitu ambapo sheria hairuhusu kufanyika kwa shghuli yoyote.
Bw Mtonda alisema kuwa mipaka iliyowekwa imevikuta visima hivyo vikiwa ndani ya hifadhi hiyo hivyo kama wanataka kutumia visima hivyo ni vema wakaandika barua kwa meneja ili waweze kuruhusiwa kuchota maji kwenye msitu huo.
“Kama mnataka kufanya hivyo ni vema mkaandika barua rasmi kwenye wakala wa misitu wao ndiyo wenye uwezo wa kuruhusu nyie kupata huduma hiyo ya maji lakini lengo si kuwasumbua wananchi,” alisema Bw Mtonda.
Aliwataka wananchi kutumi kamati za misitu kudhibiti waharibifu wa misitu kwani uharibifu umekuwa mkubwa hali ambayo ina hatarisha misitu hiyo ya hifadhi ambayo ni chanzo kikuu cha utunzaji wa mazingira.

Mwisho.     

No comments:

Post a Comment