Thursday, December 5, 2013

SITA WAFA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

WATU sita wamepoteza maisha katika matukio tofauti yaliyotokea Mkoani Pwani.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Kamishna Msiadizi Juma Yusufu Ally alithibitisha kutokea kwa matukio hayo na kueleza kuwa katika tukio la kwanza Bw Ramadhani Lubaya (35) mkulima na mkazi wa kijiji cha Kondo aliuwawa na watu wasiofahamika wakati akichunga mifugo ipatayo 90 porini ikiwa ni mchnganyiko wa ng’ombe na mbuzi mali ya Bw Malick Seif.

Tukio hilo lilitokea majira ya saa 9:00 alasiri Novemba  28 mwaka huu  katika Kijiji cha Kondo kata ya Zinga Wilaya ya Bagamoyo kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali kwenye paji la uso.

Bw Ally alisema kuwa katika tukio la pili huko kijiji cha Gwata Kata ya Mzenga Tarafa ya Mzenga Wilaya ya Kisarawe mfanya biashara Bw Peter Gumbi (28) mkazi wa Ngerengere Mkoa wa Morogoro aliuwawa kwa kupigwa risasi na watu wasiofahamika kisha kuporwa Tsh. 1,300,000/= alizokuwa nazo kwa ajili ya kwenda kununulia ng’ombe majira ya saa 8:00 mchana Novemba tarehe mwaka huu.

Alisema kuwa marehemu alikutwa na mauti wakati akitoka kijiji cha Gwata kwenda Dololo kwenye mnada akiwa amepakiwa kwenye Pikipiki. Dereva wa pikipiki hiyo anshikiliwa na Jeshi la Polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi kuhusiana na tukio hilo.

Aidha katika tukio la tatu alisema mkazi wa Kitongoji cha Madafu Kata ya Vikindu Wilaya ya Mkuranga Bw Hamadi Juma (46) fundi ujenzi aliuwawa na wananchi waliojichukulia sheria mikononi baada ya kumtuhumu kupora pikipiki ambayo mmiliki wake bado kufahamika majira ya saa 3:30 usiku Novemba 28

“Marehemu alifikwa na mauti baada ya kushambuliwa kwa mawe na vigongo sehemu mbalimbali za mwili, kutokana na tukio hilo Jeshi la Polisi linaendesha msako mkali ili kuweza kuwabaini wale waliohusika katika tukio hilo kwa kisingizio cha hasira kali,” alisema Kamanda Ally.

Alibainisha kuwa katika tukio lingine, mnamo Novemba 30 mwaka huu majira ya saa 08:30 usiku huko Kijiji cha Msata Kata ya Msata Wilaya ya Bagamoyo Bw Ally Abdallah Mlenga (56) mkulima na ambaye pia anajishughulisha na kazi za uganga wa kienyeji alivamiwa nyumbani kwake na watu nane ambao walimshambulia kwa mapanga na kumuua na kisha kumjeruhi mtoto wake aitwaye Bw Abdallah Ally (25) kwa kumkata mapanga kichwani na kifuani.

“Watu hao wanaodhaniwa kuwa ni majambazi walivamia nyumba hiyo na kuvunja mlango kwa kutumia kitu kizito na baada ya kutenda kosa hilo hawakuchukua kitu chochote,” alisema Kamanda Ally.

Aidha katika tukio linguine Bw Hassan Hamadi mkazi wa Kijiji cha Mbebetini  Kata ya Kibiti Wilaya ya Rufiji (25) aliuwawa na watu waliojichukulia sheria mkononi katika tukio lilitokea majira ya Desmba 1 mwaka huu majira ya saa 7:45 usiku baada ya kumtuhumu kuvunja duka la Bw Selapia Stephen (47).

Kamanda Ally, alithibitisha kupoteza maisha kwa Omary Milondomo (17) mkazi wa Kinguila baada ya kugongwa na gari katika barabara kuu ya Dar es Salaam – Kilwa majira ya saa 2:30 usiku wa Novemba  30 mwaka huu huko katika Kijiji cha Mbembetini Kata ya Kibiti Wilaya ya Rufiji.

Alibainisha kuwa marehemu alifikwa na mauti baada ya kugongwa na gari ambayo haikufahamika namba ambayo haikusimama baada ya kutenda kosa hilo. Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Rufiji ukisubiri kufanyiwa uchunguzi wa daktari.

Mwisho.


No comments:

Post a Comment