Friday, June 7, 2013

WANAFUNZI WATAKIWA KULALA ILI WASISIKILIZE WENZAO WAKIFUNDIHSWA

Na John Gagarini, Bagamoyo
SHULE ya Msingi Ludiga wilayani Bagamoyo mkoani Pwani inakabiliwa na uhaba wa madarasa hali ambayo inasababisha baadhi ya wanafunzi wa madarasa mawili kusoma chumba kimoja cha darasa huku wengine wakitakiwa kulala ili wasisikilize wanachofundishwa wenzao.
Akizungumza mbele ya mbunge wa Jimbo la Chalinze Said Bwanamdogo alipotembelea Kijiji cha Talawanda kata ya Talawanda, mwalimu mkuu  msaidizi wa shule hiyo Selestin Casian alisema kuwa shule hiyo ina madarasa matatu tu.
Casian alisema kuwa mbali ya wanafunzi wa madarasa mawili kusomea chumba kimoja pia wanafunzi wengine husomea nje kwenye miti kutokana na upungufu huo wa vyumba vya madarasa.
“Inabidi tuwaambie wanafunzi wa darasa moja walale ili wasisikilize kinachofundishwa na mwalimu ambaye yuko darasani hasa pale mwalimu mwingine anapokuwa bado hajaingia,” alisema Casian.
Aidha alisema kuwa licha ya shule hiyo kuwa na mwaka wa 10 sasa tangu kuanzishwa kwake shule hiyo ina walimu watano ambapo ina jumla ya wanafunzi 320.
“Kwa kweli tunachangamoto kubwa ya madarasa hali ambayo inasababisha wanafunzi kutopatiwa elimu ipasavyo hivyo tunaiomba halmashauri kutusaidia ili tuweze kuepukana na adha hii kwani wanafunzi wanashindwa kusoma vema,” alisema Casian.
Kwa upande wake mbunge wa Bwanamdogo alisema kuwa atapeleka suala hilo halmashauri ili iweze kutatua changamoto hiyo ambayo inakabili baadhi ya shule za Jimbo hilo.
“Changamoto ya madarasa na walimu ni kubwa katika Jimbo la Bagamoyo, lakini kama mnavyojua tatizo kubwa ni fedha kwani halmashauri yetu haina fedha za kutosha hata hivyo tutaendelea kuhimiza ujenzi kwa kushirikiana na wananchi,” alisema Bwanamdogo.
Aliitaka jamii kujitolea kwenye ujenzi wa madarasa na si kuisubiri serikali kwani nayo inakabiliwa na mambo mengi ya kimaendeleo hivyo wahimizane kuchangania kujenga madarasa.
Mwisho.

    

No comments:

Post a Comment