Tuesday, October 31, 2023

TAKUKURU PWANI YAFANIKISHA MTENDAJI KUREJESHA MILIONI 4 ZA KIJIJI ALIZOZICHUKUA ZA MAUZO YA ARDHI

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kurejesha kiasi cha shilingi milioni nne za Kijiji cha Kanga zilifanyiwa ubadhirifu na kaimu mtendaji wa Kata ya Kanga wilayani Mafia.

Aidha fedha hizo ambazo ni asilimia tano ni tozo ya mauzo ya kiwanja cha Kijiji hicho ambacho kiko ufukweni mwa Bahari ya Hindi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Pwani Sadiki Alli akitoa taarifa ya miezi mitatu ya utendaji kazi kuanzia Julai hadi Septemba mwaka huu. 

Alli amsema kuwa mtuhumiwa huyo jina linahifadhiwa fedha hizo hakuziwasilisha ofisini wala kuzipeleka benki kwenye akaunti ya kijiji.

Amesema mtuhumiwa huyo ambaye pia ni ofisa mazingira wa kata alibainika kwenye mkutano wa Takukuru Rafiki ambapo wananchi waliibua kero hiyo na ndipo walipofanya uchunguzi juu ya tukio hilo na kufanya ufuatiliaji.

"Baada ya uchunguzi tulibaini kuwa tukio hilo ni la kweli na alirejesha fedha hizo na tumemwandikia mwajiri wake ili achukuliwe hatua zaidi za kisheria kuhusu tukio hilo,"amesema Alli.

Amesema kuwa mafanikio hayo yanatokana na mkutano wa Takukuru Rafiki na kuwataka wananchi watumie mikutano hiyo ili kutoa kero zao juu ya vitendo vya rushwa.

"Wananchi watoe kero zao za rushwa kupitia mikutano tunayoiandaa kupitia Takukuru Rafiki kwani hapo ni moja ya sehemu wanazoweza kutoa taarifa kama watashindwa kutuletea taarifa ofisini,"amesema Alli.

Katika hatua nyingine amesema kuwa jumla ya matukio 126 ambapo 92 yalihusu masuala ya rushwa huku 34 hayakuhusu rushwa na 27 wahusika walipewa ushauri manne yalifungwa na matatu yalihamishiwa idara nyingine.

Ameanisha idara ambazo zinaongoza kwa malalamiko kuwa ni Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) yenye malalamiko 44, na elimu 17, ardhi 15, ushirika sita, binafsi tano na polisi nne.

Ameongeza kuwa idara nyingine ni afya na kilimo tatu, bandari, fedha, madini, maji, misitu na utawala malalamiko mawili kila moja, idara ya biashara, ofisi ya mkuu wa wilaya, mifugo, maendeleo ya jamii, Mamlaka ya Mapato TRA, uchukuzi, ujenzi, Tanesco, utalii na viwanda lalamiko moja moja kila idara.

Wednesday, October 25, 2023

RC KUNENGE ATAKA UJENZI WA MALL YA HALMASHAURI YA MJI UKAMILIKE NDANI YA SIKU 14


MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametoa siku 14 kwa Mkandarasi anayejenga Maduka Makubwa (Mall) inayomilikiwa na Halmashauri ya Mji Kibaha kukamilisha ujenzi wa mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni nane.

Ameyasema hayo wakati wa ziara yake kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye Halmashauri hiyo ambapo mradi huo uko kwenye kitovu cha mji karibu na stendi mpya ya Maili Moja Kibaha.

Kunenge amesema kuwa mradi huo ni mkubwa ambao utakapokamilika utagharimu kiasi cha shilingi bilioni nane hivyo lazima ukamilike ndani ya muda huo ambapo matarajio ni kuingiza kiasi cha shilingi milioni 450 kwa mwaka.

"Nataka mkandarasi Elray asizidishe zaidi ya wiki mbili ahakikishe anakamilisha ndani ya muda huo tunachotaka akamilishe mradi huu ili biashara zianze kufanyika na Halmashauri ianze kupata mapato,"amesema Kunenge.

Kwa upande wake Mhandisi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Brighton Kisheo amesema kuwa Halmashauri hiyo ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni nane mwaka 2018-2019 kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo ambapo wafanyabiashara 253 watapata fursa za biashara na litahudumia watu zaidi 2,000 na unatarajiwa kukamilika Novemba mwaka huu.

Naye mwenyekiti wa Wamachinga Mkoa wa Pwani Filemon Maliga amesema kuwa wanaishukuru serikali kwa kuwapatia eneo jirani na Mall hiyo ili wafanye biashara zao na wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kulirasimisha kundi lao ambapo sasa wanatambulika na wanapata fursa mbalimbali zikiwemo za mikopo.

Miradi mingine aliyoitembelea mkuu huyo wa mkoa ni barabara, ujenzi wa madarasa ya sekondari kata ya Mkuza na maandalizi ya ujenzi wa kiwanda cha utengenezaji wa mitungi ya gesi ya kampuni ya Taifa Gas.


Mwisho.

Wednesday, October 18, 2023

SOKO LA KISASA KUJENGWA MLANDIZI BILIONI 7 KUTUMIKA

KATIKA kuhakikisha Mji wa Mlandizi unavutia Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha inatarajia kujenga soko kubwa na la kisasa kwa ajili ya wakazi wa mji wa Mlandizi ambalo litagharimu kiasi cha shilingi bilioni saba.

Hayo yamesemwa Mlandizi na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Michael Mwakamo wakati wa kuhitimisha kampeni ya Simika Bendera kwenye Jimbo hilo.

Mwakamo alisema kuwa eneo maarufu kama kwa Mama Salmini tayari limeshapatikana baada ya kununuliwa na mkandarasi wa ujenzi amepatikana na utaratibu unaanza kwa ajili ya ujenzi.

"Soko la sasa ni dogo lakini eneo tulilopata ni kubwa na litachukua wafanyabiashara wengi na litakuwa na huduma nyingi tofauti na la sasa ambalo hata sehemu ya magari kupaki hakuna,"amesema Mwakamo.

Amesema fedha hizo zimetengwa kwenye baheti ya mwaka wa fedha 2023/2024 na tayari bilioni mbili zimetolewa kwa ajili ya kuanza kazi na litaubadilisha Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlandizi.

Naye Mwenyekiti wa CCM Kibaha Vijijini Mkali Kanusu alisema kuwa chama kinataka viongozi waliopo kwenye madarakani wawe na mahusiano mazuri na wananchi.

Kwa upande wake katibu wa CCM Kibaha Vijijini Zainabu Mketo amesema kuwa hamasa ya Simika Bendera imeleta mafanikio kwani wamevuna wanachama wapya 3,500 na kupitia mabalozi wote lengo likiwa ni kuimarisha chama ndani ya chama.


Mwisho.

Sunday, October 15, 2023

MAOFISA TEHAMA WATAKIWA KUENDANA NA TEKNOLOJIA

MAOFISA TEHAMA nchini, wameaswa kwenda na wakati ,kupenda kujifunza kulingana na teknolojia inavyobadilika ili kujiongezea uzoefu na ujuzi.

Aidha wawe wabunifu ,wajitume ili kuacha alama na tija katika kada hiyo kwenye maeneo ya kazi

Rai hiyo imetolewa na Katibu Tawala mkoa wa Pwani Rashid Mchatta, wakati alipomwakilisha Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI, kufungua kikao kazi cha mwaka 2023 ,ambacho kimefanyika Kibaha Mkoani Pwani na kukutanisha maofisa hao kutoka mikoa mbalimbali nchini ili kujadili changamoto zinazokikabili kitengo Cha TEHAMA.

 "IT ina mambo mengi sana, inabadilika kama mtu wa Tehama hufanyi updating itakupa wakati mgumu, someni masomo ya ziada kuongeza uzoefu,mkoa wa Pwani ndio mwenyeji mwaka huu tumejipanga kuhakikisha tuliyoyajadili yanafanikiwa"anasema Mchatta.

Mchatta alieleza, kada ya TEHAMA imekua kwa kasi kubwa na kupelekea kuwa mhimili mkubwa katika utendaji kazi na Serikali na Taasisi nyingine binafsi kwenye mifumo mbalimbali ikiwemo ukusanyaji mapato ya ndani ya Mamlaka za Serikali za mitaa ,mfumo wa kusimamia huduma za hospitali.

"Serikali - TAMISEMI imeipa kada hii umuhimu mkubwa kwa kuanzisha wizara rasmi inayoshughulikia TEHAMA ,hivyo tusimuangushe mh Rais"

Awali Melchiory Baltazary, Mkurugenzi Msaidizi-TEHAMA TAMISEMI alieleza kikao hicho ni kikao kazi ambacho kitafanyika siku mbili.




Mwisho

Saturday, October 14, 2023

LIONS CLUB YATOA MISAADA YA VIFAA VYA SHULE


KLABU ya Lions ya Jijini Dar es Salaam imetoa vifaa kwa Shule 15 za Msingi na Sekondari Kata ya Vigwaza Halmashauri ya Chalinze Wilayani Bagamoyo zenye thamani ya zaidi ya milioni sita ili kukabiliana na uhaba wa vifaa kwenye shule hizo.

Hayo yalisemwa kwenye  shule ya msingi Ruvu Darajani kata ya Vigwaza na Rais wa zamani wa klabu hiyo Muntazir Bharwani wakati wa kukabidhi vifaa hivyo kwa shule ambapo ziliwakilishwa na walimu wakuu wa shule hizo.

Bharwani amesema kuwa klabu yao inajihusisha na kusaidia masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kwenye sekta za elimu, afya na maji na masuala mengine ya kimaendeleo.

"Tumetoa vifaa vikiwemo vitabu vya walimu kwa ajili ya kufundishia, madaftari pamoja na mipira kwa ajili ya kuwaweka wanafunzi kwenye utimamu wa akili,"amesema Bharwani.

Akipokea misaada hiyo ofisa elimu msingi na awali wa Halmashauri ya Chalinze Miriam Kihiyo ameishukuru klabu hiyo na kuomba iendelee kusaidia kwenye sekta hiyo.

Kihiyo amesema kuwa mahitaji kwenye sekta ya elimu ni kubwa kutokana na kuwa na wanafunzi wengi na kuomba wadau wengine waendelee kujitolea misaada mbalimbali.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Vigwaza Musa Gama amesema kuwa anashukuru kwa misaada hiyo ambayo itasaidia kupunguza sehemu ya baadhi ya changamoto.

Gama amesema kuwa msaada huo ni motisha kwa walimu na wanafunzi katika kuhakikisha elimu inaboreka na kuwataka wananchi wawasimamie watoto wao ili wapate elimu ipasavyo.

WATAKA JITIHADA ZIONGEZWE WATU KUKUA KUSOMA KUHESABU NA KUANDIKA

IMEELEZWA kuwa watu wanaojua kusoma kuandika na kuhesabu nchini kwa sasa ni asilimia 77.8 ikilinganishwa na mwaka 1980 ambapo watu hao ilikuwa ni asilimia 9.6.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Profesa Michael Ng'umbi Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima Nchini wakati wa ufunguzi wa Kongamano la maadhimisho ya kitaifa ya juma la elimu ya watu wazima kitaifa.

Ng'umbi alisema kuwa mwaka 1980 Tanzania iliweza kufikia kiwango cha juu cha kufuta ujinga kwa watu wasiojua kuandika kuhesabu na kusoma na kufikia asilimia hiyo.

Akifungua mafunzo hayo kaimu mkurugenzi elimu msingi wizara ya elimu sayansi na teknolojia Josephat Luoga alisema kuwa mafunzo hayo yatawezesha kuamsha hamasa ya kutafakuri kuwa tunakwenda wapi katika utoaji elimu.

Luoga alisema kuwa mfumo wa elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi utaweza kubadilisha mtizamo juu ya uendeshaji na usimamizi na tathmini ili kuendana na dira ya maendeleo ya 2025 pamoja na mpango wa maendeleo endelevu 2030.

PROFESA MKENDA AFURAHISHWA TAASISI YA ELIMU YA WATU WAZIMA INAVYOBORESHA MFUMO HUO

WAZIRI wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema kuwa serikali itaendelea kuboresha elimu ya watu wazima nchini.

Mkenda aliyasema hayo wakati wa kufunga Kongamano la maadhimisho ya kitaifa ya juma la elimu ya watu wazima kitaifa lililofanyika Wilayani Kibaha.

Alisema kuwa serikali itaendelea kujenga uwezo na watendaji kwenye Halmashauri kwenye mikoa zitoe kipaumbele kwa program zote za elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Elimu kutoka Ofisi ya Rais Tamisemi Dk Charles Msonde alisema kuwa moja ya mkazo uliowekwa ni kuhakikisha wanafunzi wa darasa la kwanza wanajua kusoma kuandika na kuhesabu.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Profesa Caroline Nombo alisema kuwa jumla ya wanafunzi milioni 5.7 walidahiliwa kwenye elimu changamani kwenye vituo 405.

Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alisema kuwa baadhi ya changamoto katika utekelezaji wa baadhi ya program ni pamoja na walimu wa kujitolea kutokuwa na mafunzo ufinyu wa bajeti, upungufu wa vitendea kazi na kushindwa kulipa wa wezeshaji.


Mwisho.