Thursday, May 8, 2025

WANACHAMA WA CCM NYANG'WALE WATAKA KUHARAKISHWA UJENZI WA OFISI.

WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Nyang'hwale Mkoani Geita wametaka  ujenzi wa ofisi ya chama ufanyike kwani tayari baadhi ya wadau wamechangia fedha za ujenzi huo.

Wamesema moja ya wadau waliochangia fedha kwa ajili ya ujenzi huo ni Naibu Waziri Mkuu Dotto Biteko ambaye alichangia kiasi cha shilingi milioni 50.

Wamesema kuwa fedha hizo zilikabidhiwa kwa Mbunge wa Jimbo la Nyang'hwale Hussein Amar hivyo kutaka fedha hizo zifanye ujenzi huo ili kupata ofisi kwa kazi za chama.

"Tunataka ujenzi ufanyike kwani kama ni fedha zipo hakuna sababu ya kuchelewesha ujenzi huo wa ofisi ya chama ambapo endapo itajengwa itakuwa ya kisasa,"wamesema wanachama hao.

Waliongeza kuwa wanataka fedha hizo zijenge na kukamilisha ofisi ya chama na kwamba wao wanachotaka ni kuona CCM Wilaya ya Nyang'hwale inaendelea kama Wilaya nyingine zilivyoendelea.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Nyang'hwale Hussein Amar akizungumza kwa njia ya simu ameeleza kusitikishwa na malalamiko ya wananchama hao huku akisema jambo hilo halina usiri wowote.

Amar amesema kuwa yeye ndiye iliyemuomba  awasaidie na sio mara moja amekuwa akisaidia na bahati nzuri alipokuja yeye mwenyewe  alimkumbushia ombi hilo na akakubali kusaidia lakini hakutamka kiwango.

Aidha amesema kuwa fedha hizo zilivyoingia alimpa taarifa Mkuu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Chama, Mwenezi, kamati ya Siasa na kamati ya ujenzi na yeye ndiye aliyetafuta fundi na kuwashauri kuwa kuna fundi kwa hiyo ni vyema akatumika kwakuwa yupo vizuri.

Mbunge huyo ameongeza kuwa yeye binafsi amekuwa na mchango mkubwa sana katika ujenzi wa ofisi hiyo ya Chama maana alishawai kutoa mashine zake na magari yake (Tipa) kufanyakazi katika ujenzi huo.

"Fedha zipo mikono salama na Mei 3 niliongea na Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi kumweleza juu ya fedha kwani zinatakiwa kufanyakazi iliyokusudiwa kwa kuwa mimi sitaki kukaa nazo nipeni akaunti niwahamishie lakini alinijibu kuwa watakaa na kamati yake ya ujenzi na akasema wakati huu aendelee kukaa nazo na wakihitaji kununua vifaa watamjulisha ili atoe hizo fedha",amesema Amar.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Nyang'hwale Adam Mtore amesema kuwa kama kuna malalamiko ndani ya Chama kuuna utaratibu wake na mara nyingi huanzia ngazi ya chini ya tawi lakini kwakuwa suala hilo linagusa ngazi ya Wilaya ilitakiwa wapeleke malalamiko yao kwa Katibu wa Chama Wilaya.



Saturday, May 3, 2025

KECA YAUNGA MKONO SERIKALI UHIFADHI MAZINGIRA NA UFUGAJI NYUKI

SHIRIKA lisilo la kiserikali la Kibaha Environmental Conservation Action (KECA) limedhamiria kuunga mkono jitihada za serikali kwa uhifadhi wa mazingira na kukuza uchumi kupitia ufugaji wa nyuki.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mkurugenzi wa (KECA) ambalo linajihusisha na utoaji elimu ya ufugaji nyuki na utunzaji wa mazingira Ibrahim Mkwiru wakati wa uzinduzi wa jengo la ofisi yao.

Mkwiru alisema kuwa nia yao ni kuunga mkono juhudi za Serikali katika uhifadhi wa mazingira na kukuza uchumi wa wananchi kupitia ufugaji wa nyuki ili kuongeza kipato kwa wananchi.

"Tunaiomba Serikali kutupa kibali cha kupanda miti ya mianzi katika maeneo ya wazi karibu na chanzo cha Mto Ruvu ili kusaidia kuhifadhi mazingira na kuchochea maendeleo ya kijamii kupitia njia ya uhifadhi wa mazingira,"alisema Mkwiru.

Kwa upande wake Ofisa Tarafa ya Kibaha Catherine Njau alisema kuwa Serikali inaendelea na dhamira yake ya dhati ya kuunga mkono juhudi za wawekezaji katika sekta ya ufugaji nyuki ili kuhakikisha wafugaji wadogo waliopo vijijini wananufaika kiuchumi na kielimu. 

Njau alosema kuwa kwa muda mrefu wafugaji wa nyuki wanaoishi pembezoni mwa miji wamekuwa wakikosa elimu sahihi ya ufugaji wa kisasa na pia kukosa masoko ya uhakika kwa bidhaa zao.

Alilipongeza shirika la KECA kuwa kama daraja muhimu kwa wafugaji wa nyuki kupata elimu ya kitaalamu na fursa za kibiashara kwa wafugaji ili waweze kupata masoko makubwa.

"Nawasisitiza umuhimu wa kufanya tathmini ya kitaalamu kabla ya kupanda mianzi kwenye maeneo ya vyanzo vya maji,huku akisema baadhi ya miti ina uwezo wa kutumia maji mengi na hivyo inaweza kuhatarisha uhai wa vyanzo vya maji kama mito,"alisema Njau.

Naye Mjumbe wa Bodi ya KECA Edwin Shunda aliwahimiza wananchi na wadau wa mazingira kujitokeza kwa wingi kujifunza mbinu za ujasiriamali na ufugaji wa nyuki wa kisasa.

Thursday, May 1, 2025

MKUU WA MKOA WA PWANI ABUBAKARI KUNENGE ATOA WIKI MOJA KWA WAAJIRI WANAOKIUKA HAKI ZA WAFANYAKAZI

MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametaka utatuzi wa changamoto za wafanyakazi kufanyiwa kazi atoa wiki moja kwa taasisi zinazokiuka taratibu kufuata sheria za kazi.

Kunenge ameyasema hayo jana Mjini Kibaha wakati wa maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Duniani Mkoa wa Pwani yaliyofanyika kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha.

Amesema kuwa waajiri wanapaswa kutekeleza matakwa ya kisheria ya juu ya haki za wafanyakazi ili waweze kufanya kazi vizuri bila ya malalamiko.

"Katika risala yenu kuna baadhi ya waajiri wanakiuka taratibu ikiwa ni pamoja na kutotoa mikataba ya kazi na stahiki nyingine jambo ambalo ni kinyume cha sheria,"amesema Kunenge.

Awali mratibu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Mkoa wa Pwani Susan Shesha amesema kuwa wanaishukuru serikali kuvutia wawekezaji ambapo imewezesha vijana wengi kupata ajira.

Shesha amesema kuwa changamoto iliyopo ni baadhi ya waajiri kutotoa mikataba ya ajira, fedha za matibabu, kutothibitishwa kazini, mapunjo ya mishahara, kuzuia uwepo wa vyama vya wafanyakazi sehemu za kazi, likizo na fedha za matibabu, vitisho.

Wednesday, April 30, 2025

MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI KIBAHA MJINI YATAKIWA KUSHIRIKIANA

MASHIRIKA yasiyokuwa ya Kiserikali yanayofanya shughuli zao Halmashauri ya Mji Kibaha yamesisitizwa kufanya kazi kwa ushirikiano na kujiunga  na mitandao ya kitaifa na kimataifa.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Mtandao wa NGOs za Kibaha Mji (Kibaha Town Alliance of NGOs -KiTAN) Israel Ilunde wakati wa kikao cha wakurugenzi wa mashirika hayo na Msajili Msaidizi wa mashirika yasiyo ya kiserikali Halmashauri ya Mji Kibaha Elia Kabora.

Ilunde amesema kuwa kuna umuhimu wa mashirika hayo kufanya kazi kwa mujibu wa Sheria ikiwemo kutoa taatifa za kila robo mwaka na ripoti za mwaka bila kusahau kulipa ada ya kila mwaka.

Idara ya Maendeleo ja jamii waliwaelimisha wana AZAKI juu ya umuhimu wa malezi ya watoto ili kuwaepusha na ukatili ili waweze kutimiza ndoto zao.

Saturday, April 19, 2025

BALOZI MATINYI AAHIDI KUITANGAZA TANZANIA KIMATAIFA

BALOZI wa Tanzania nchini  Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, amesema kuwa atatumia uzoefu alioupata katika kazi yake ya  uandishi wa habari kutafuta taarifa na kung'amua mbinu za kuvutia watalii wengi kama ilivyo katika nchi hiyo ambayo inavutiwa na kutembelewa na watalii wengi.

"Nitakapofika katika nchi hizo tisa katika eneo langu la uwakilishi nitahakikisha ninatafuta na kujua ni mbinu gani wanazotumia kuvutia watalii kwani watalii wengi duniani huenda kwenye nchi hizo", alisema Mhe. Balozi Matinyi.

Alisema pia kuwa kwa kutumia uzoefu wake katika uandishi wa habari - fani ambayo hujenga tabia ya udadisi na mbinu za kutafuta taarifa za uwekezaji na pia tabia kulikamilisha jukumu la kazi baada ya kulichukua.

Balozi Matinyi alisema hayo  hivi karibuni katika mahojinao maalumu na kituo cha televisheni cha ZBC cha Zanzibar.

Alifafanua kwa kueleza kuwa diplomasia ya uchumi nchini ilianzishwa katika utawala wa awamu ya tatu ambapo ili kuujenga uchumi wetu baada ya kumaliza kuzisaidia nchi zingine za Afrika kupata uhuru.

"Hii ndiyo sababu viongozi wetu wakuu wanatusisitizia kwamba tunapokwenda nje ya nchi tukaifanyie kazi diplomasia ya uchumi," alidokeza Mhe. Balozi Matinyi.

"Nitakapofika katika nchi hizo tisa zilizoendelea kiuchumi, katika sekta ya uvuvi, kilimo katika viwanda vya mbolea na matrekta, utalii ambapo wanapokea watalii kati ya milioni 6 hadi 7 kwa mwaka wakitumia visiwa vingi na bahari kuvutia watalii, jukumu langu litakuwa kuhakikisha tunapata mbinu zao na Watanzania tunasonga mbele kiuchumi" alisema Mhe. Balozi Matinyi.

Aidha, akizungumzia namna atakakavyoiwakilisha  Zanzibar, alisema kuwa tayari ameshapata maelezo mbalimbali kutoka taasisi za uwekezaji, kama za uchumi wa buluu na utalii na hivyo kuwa katika nafasi nzuri ya kujua namna ya kuielezea Zanzibar.

"Tuna nchi tisa katika eneo ninalokwenda wenye tabia ya kutaka kufahamu vyakula vya watu wengine; hivyo, nitawaeleza kwamba Zanzibar kuna viungo vya kipekee vyenye ladha nzuri."

Mhe.  Balozi Matinyi amezitaja nchi ambazo  atakuwa mwakilishi mbali ya Sweden kuwa Denmark, Finland, Norway, Iceland, Estonia, Latvia, Lithuania na Ukrane.

Akijibu swali kuhusu mgogoro wa nchi za Ukraine na Russia, Mhe. Balozi Matinyi alisema kuwa Tanzania inasimamia amani na hivyo inataka nchi zinapokwaruzana zitafute suluhu kwa mazungumzo na si kupigana vita.


Thursday, April 17, 2025

UJENZI WA MRADI WA MAJI PANGANI KIBAHA WAANZA

 

MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) imemkabidhi mkandarasi  eneo la mradi wa maji wa Pangani Wilayani Kibaha Mkoani Pwani utakaogharimu kiasi cha shilingi bilioni 8.9.

Akizungumza na baadhi ya wananchi wa Mtaa wa Pangani Kaimu Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi Ramadhani Mtindasi alisema kuwa mradi huo ni wa miezi 12.

Mtindasi alisema kuwa Mkandarasi anayetekeleza mradi huo ni kampuni ya Shanxi Construction Engineering Corporation and Mineral Company ya China ambapo kutakuwa na hatua tatu za ujenzi wa pampu mbili, tenki la maji na usambazaji wa maji.

Alisema kuwa mradi huo utahusisha ujenzi wa matenki mawili ambapo pampu itakuwa na uwezo wa kuzalisha lita 250,000 kwa saa ambapo yatajengwa eneo la Shirika la Elimu Kibaha (KEC).

"Maji hayo yatatoka kwenye bomba kubwa la maji lililopo jirani na barabara ya Morogoro na yatapelekwa hadi Pangani kwenye tenki hilo litakalokuwa na uwezo wa ujazo wa lita milioni sita kwa mara moja,"alisema Mtindasi.

Aidha alisema kuwa ili kufanikisha ujenzi huo aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa mkandarasi anayetekeleza mradi huo ili asipate changamoto.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Shangwe Twamala alisema kuwa wanamshukuru Rais kwa kutoa fedha hizo kwa ajili ya kukabili changamoto ya maji kwenye Kata ya Pangani.

Twamala alisema kuwa ujenzi wa miundombinu ya maji itakuwa ni mkombozi kwa wananchi na kuwataka wawe walinzi wa mradi huo ambao ulipaswa kuanza tangu mwaka 2023 lakini ulichelewa.

Naye Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka alisema kuwa anaomba mkandarasi atekeleze mradi huo kwa wakati ili wananchi wapate huduma hiyo muhimu.

Koka alisema kuwa changamoto hiyo ilikuwa ni kubwa sana na wabanchi walikuwa wakilalamika sana na ni kilio kikubwa ambacho sasa kinaenda kutatuliwa ambapo wananchi zaidi ya 83,000 watanufaika na mradi huo.

Diwani wa Kata ya Pangani Agustino Mdachi alisema kuwa wananchi walikuwa wanalia sana lakini sasa wanafutwa machozi kwa mradi huo kuanza.

Mdachi alisema kuwa mradi huo utakuwa mkombozi kwani mbali ya kuhudumia Kata ya Pangani pia Kata za Maili Moja na Picha ya Ndege zitanufaika na mradi huo

Thursday, April 3, 2025

UJENZI KIWANGO CHA LAMI BARABARA YA PICHA YA NDEGE-BOKOMNEMELA UNARIDHISHA-MKIMBIZA MWENGE KITAIFA ISMAIL USSI

MWENGE wa Uhuru umeridhishwa na mradi wa ujenzi wa barabara ya Picha ya Ndege-Bomotimiza yenye urefu wa mita 550 kiwango cha lami wenye thamani ya shilingi milioni 760.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa Ismail Ussi akikagua barabara hiyo ambapo fedha hizo nikutoka serikali kuu kutokana na tozo ya mafuta amesema serikali inapenda wananchi wapate miundombinu mizuri.

Ussi amesema kuwa kutokana na mradi huo kuwa na ubora wananchi wanapaswa kuulinda na kuutunza ili ulete manufaa ya muda mrefu na kuufanyia usafi.

Amesema kuwa serikali imekuwa ikitumia gharama kubwa kutengeneza miundombinu ambapo mradi huo umejengwa kwa viwango vinavyotakiwa kutokana na usimamizi mzuri.

"Rais Dk Samia Suluhu Hassan anapenda kuona miradi kama hii inakuwa na matokeo mazuri kwani ndiyo malengo ya serikali hivyo ulindeni mradi huu ambao una gharama kubwa,"amesema Ussi.

Kwa upande wake Mhandisi Samwel Ndoveni amesema kuwa mradi huo ulianza Oktoba mwaka 2023 na ulitegemewa kukamilika Aprili 2024 lakini muda uliongezwa na kukamilika Julai 2024 kutokana na mvua za elnino.

Ndoveni amesema kuwa mradi huo kwa sasa uko katika kipindi cha matazamio hadi Julai 2025 na kukabidhiwa rasmi na kuwa kiasi kilicholipwa hadi sasa ni shilingi milioni 696.9 sawa na asilimia 91.7.

Naye Mwentekiti wa Halmashauri ambaye ni Diwani wa Kata ya Sofu Mussa Ndomba amesema kuwa baravara hiyo ambayo inaanzia barabara ya Morogoro ina urefu wa kilometa saba ni muhimu sana.

Ndomba amesema kuwa barabara hiyo inapita kwenye maeneo ya Shule, Magereza na Hospitali na inaunganisha Kata tatu za Sofu, Picha ya Ndege na Bokomnemela ambapo zamani ilikuwa ni changamoto kubwa sana kwa wananchi wa maeneo hayo.