Sunday, October 15, 2023

MAOFISA TEHAMA WATAKIWA KUENDANA NA TEKNOLOJIA

MAOFISA TEHAMA nchini, wameaswa kwenda na wakati ,kupenda kujifunza kulingana na teknolojia inavyobadilika ili kujiongezea uzoefu na ujuzi.

Aidha wawe wabunifu ,wajitume ili kuacha alama na tija katika kada hiyo kwenye maeneo ya kazi

Rai hiyo imetolewa na Katibu Tawala mkoa wa Pwani Rashid Mchatta, wakati alipomwakilisha Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI, kufungua kikao kazi cha mwaka 2023 ,ambacho kimefanyika Kibaha Mkoani Pwani na kukutanisha maofisa hao kutoka mikoa mbalimbali nchini ili kujadili changamoto zinazokikabili kitengo Cha TEHAMA.

 "IT ina mambo mengi sana, inabadilika kama mtu wa Tehama hufanyi updating itakupa wakati mgumu, someni masomo ya ziada kuongeza uzoefu,mkoa wa Pwani ndio mwenyeji mwaka huu tumejipanga kuhakikisha tuliyoyajadili yanafanikiwa"anasema Mchatta.

Mchatta alieleza, kada ya TEHAMA imekua kwa kasi kubwa na kupelekea kuwa mhimili mkubwa katika utendaji kazi na Serikali na Taasisi nyingine binafsi kwenye mifumo mbalimbali ikiwemo ukusanyaji mapato ya ndani ya Mamlaka za Serikali za mitaa ,mfumo wa kusimamia huduma za hospitali.

"Serikali - TAMISEMI imeipa kada hii umuhimu mkubwa kwa kuanzisha wizara rasmi inayoshughulikia TEHAMA ,hivyo tusimuangushe mh Rais"

Awali Melchiory Baltazary, Mkurugenzi Msaidizi-TEHAMA TAMISEMI alieleza kikao hicho ni kikao kazi ambacho kitafanyika siku mbili.




Mwisho

Saturday, October 14, 2023

LIONS CLUB YATOA MISAADA YA VIFAA VYA SHULE


KLABU ya Lions ya Jijini Dar es Salaam imetoa vifaa kwa Shule 15 za Msingi na Sekondari Kata ya Vigwaza Halmashauri ya Chalinze Wilayani Bagamoyo zenye thamani ya zaidi ya milioni sita ili kukabiliana na uhaba wa vifaa kwenye shule hizo.

Hayo yalisemwa kwenye  shule ya msingi Ruvu Darajani kata ya Vigwaza na Rais wa zamani wa klabu hiyo Muntazir Bharwani wakati wa kukabidhi vifaa hivyo kwa shule ambapo ziliwakilishwa na walimu wakuu wa shule hizo.

Bharwani amesema kuwa klabu yao inajihusisha na kusaidia masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kwenye sekta za elimu, afya na maji na masuala mengine ya kimaendeleo.

"Tumetoa vifaa vikiwemo vitabu vya walimu kwa ajili ya kufundishia, madaftari pamoja na mipira kwa ajili ya kuwaweka wanafunzi kwenye utimamu wa akili,"amesema Bharwani.

Akipokea misaada hiyo ofisa elimu msingi na awali wa Halmashauri ya Chalinze Miriam Kihiyo ameishukuru klabu hiyo na kuomba iendelee kusaidia kwenye sekta hiyo.

Kihiyo amesema kuwa mahitaji kwenye sekta ya elimu ni kubwa kutokana na kuwa na wanafunzi wengi na kuomba wadau wengine waendelee kujitolea misaada mbalimbali.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Vigwaza Musa Gama amesema kuwa anashukuru kwa misaada hiyo ambayo itasaidia kupunguza sehemu ya baadhi ya changamoto.

Gama amesema kuwa msaada huo ni motisha kwa walimu na wanafunzi katika kuhakikisha elimu inaboreka na kuwataka wananchi wawasimamie watoto wao ili wapate elimu ipasavyo.

WATAKA JITIHADA ZIONGEZWE WATU KUKUA KUSOMA KUHESABU NA KUANDIKA

IMEELEZWA kuwa watu wanaojua kusoma kuandika na kuhesabu nchini kwa sasa ni asilimia 77.8 ikilinganishwa na mwaka 1980 ambapo watu hao ilikuwa ni asilimia 9.6.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Profesa Michael Ng'umbi Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima Nchini wakati wa ufunguzi wa Kongamano la maadhimisho ya kitaifa ya juma la elimu ya watu wazima kitaifa.

Ng'umbi alisema kuwa mwaka 1980 Tanzania iliweza kufikia kiwango cha juu cha kufuta ujinga kwa watu wasiojua kuandika kuhesabu na kusoma na kufikia asilimia hiyo.

Akifungua mafunzo hayo kaimu mkurugenzi elimu msingi wizara ya elimu sayansi na teknolojia Josephat Luoga alisema kuwa mafunzo hayo yatawezesha kuamsha hamasa ya kutafakuri kuwa tunakwenda wapi katika utoaji elimu.

Luoga alisema kuwa mfumo wa elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi utaweza kubadilisha mtizamo juu ya uendeshaji na usimamizi na tathmini ili kuendana na dira ya maendeleo ya 2025 pamoja na mpango wa maendeleo endelevu 2030.

PROFESA MKENDA AFURAHISHWA TAASISI YA ELIMU YA WATU WAZIMA INAVYOBORESHA MFUMO HUO

WAZIRI wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema kuwa serikali itaendelea kuboresha elimu ya watu wazima nchini.

Mkenda aliyasema hayo wakati wa kufunga Kongamano la maadhimisho ya kitaifa ya juma la elimu ya watu wazima kitaifa lililofanyika Wilayani Kibaha.

Alisema kuwa serikali itaendelea kujenga uwezo na watendaji kwenye Halmashauri kwenye mikoa zitoe kipaumbele kwa program zote za elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Elimu kutoka Ofisi ya Rais Tamisemi Dk Charles Msonde alisema kuwa moja ya mkazo uliowekwa ni kuhakikisha wanafunzi wa darasa la kwanza wanajua kusoma kuandika na kuhesabu.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Profesa Caroline Nombo alisema kuwa jumla ya wanafunzi milioni 5.7 walidahiliwa kwenye elimu changamani kwenye vituo 405.

Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alisema kuwa baadhi ya changamoto katika utekelezaji wa baadhi ya program ni pamoja na walimu wa kujitolea kutokuwa na mafunzo ufinyu wa bajeti, upungufu wa vitendea kazi na kushindwa kulipa wa wezeshaji.


Mwisho.

MKUU WA MKOA WA PWANI KUNENGE ATAKA VIONGOZI WALIOHUSIKA UUZAJI VIWANJA ENEO LA MITAMBA WAKAMATWE

KUFUATIA viongozi 24 kujihisisha kuwatapeli watu na kuwauzia eneo la shamba la Mitamba mali ya Wizara ya mifugo na uvuvi Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametoa  siku 14  kukamatwa viongozi hao.

Aidha viongozi hao ni pamoja na mabalozi, wenyeviti wa mitaa, watendaji  walioshirikiana na madalali  waliohusika kuwauzia  wananchi viwanja katika eneo la shamba hilo lililopo Halmashauri ya Mji Kibaha.

Kunenge alitoa maagizo hayo wakati wa mkutano wa hadhara na wananchi wa Kata ya Pangani uliowahusisha watalaam kutoka Halmashauri ya Mji Kibaha na mkoa kwa ajili ya kutoa msimamo wa serikali kuhusu maamuzi ya eneo hilo ambalo limevamiwa na wananchi kwa ajili ya makazi.

Alisema orodha na majina ya viongozi hao na madalali  waliohusika kuwauzia kinyemela wananchi viwanja katika eneo hilo ambalo linamilikiwa na serikali na kwamba anayakabidhi kwa Taasisi ya  Kuzuia na Kupambana na Rushwa Takukuru pamoja na Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria.

Naye Mpimaji Ardhi Halmashauri ya Mji Kibaha Aron Shushu alisema kuwa kiwanja hicho kilipimwa upya kwa kuzingatia sheria namba 8 ya mipango miji na kwamba  mwaka 2021 kilifanyika kikao na wananchi hao kwa ajili ya kutoa katazo la kutovamia shamba hilo.

Shushu alisema kuwa jitihada za kuwakataza wazanchi hao ziliendelea huku baadhi wakionekana kuendelea na shughuli za ujenzi   na kukaidi na walipokea mapendekezo kutoa Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Alisema kuwa kuhusu upimaji wa eneo hilo hekta 150 zilitolewa kwa ajili ya Matumizi ya Wakala wa Maabara ya Vetenari Tanzania (TVLA) hekta 188 kwa ajili ya matumizi ya Taasisi za  Umma, 486  uwekezaji wa viwanda na 200  makazi.


Tuesday, October 10, 2023

DC OKASHI ATAKA WAHUJUMU WAFICHULIWE MIRADI YA MAJI RUWASA BAGAMOYO

MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo Halima Okashi amewataka wananchi kuwafichua watu wanaohujumu miradi ya maji ambayo serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 1.9 kwa ajili ya uboreshaji wa  huduma ya upatikanaji maji kupitia Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA).

Ameyasema hayo Wilayani Bagamoyo wakati alipokuwa akifungua mkutano na wadau wa maji kwenye wilaya hiyo ambayo inaundwa na Halmashauri mbili za Bagamoyo na Chalinze. 

Okashi amesema kuwa serikali imetoa fedha hizo kwa lengo la kuhakikisha miradi inatekelezwa ili huduma ya maji safi na salama inapatikana kwa wananchi vijijini kwa umbali usiozidi mita 400.

Kwa upande wake Meneja wa RUWASA Wilaya ya Bagamoyo James Kionaumela amesema kuwa Wilaya ina vyanzo vikuu viwili vya maji ambavyo ni chini ya ardhi kupitia visima vya kuchimba virefu na vifupi kukiwa na visima 215.

Kionaumela amesema kuwa chanzo cha pili ni maji ya juu inayojumuisha maji ya mito, mabwawa na chemichemi na wilaya hiyo ina vyombo vya watoa huduma 17 ambapo imevipunguza na kufikia vyombo vitano.

Naye mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Bagamoyo Abdul Sharifu amesema kuwa wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya uboreshaji upatikanaji huduma ya maji.

Diwani wa Kata ya Kibindu na makam mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze Ramadhan Mkufya amesema kuwa Vijiji viwili vya Kwa Msanja na Kwa Konje ndiko kuna changamoto ya maji.

Mwentekiti wa vyombo vya watumiaji maji Wilaya ya Bagamoyo Jitihada Mwinyimkuu ameiomba serikali kuvihudumia vyombo hivyo kwani vingine vinashindwa kufanya kazi kutokana na vifaa kufa na kushindwa kuvikarabati.


Mwisho.

Sunday, October 8, 2023

WAFANYABIASHARA WAZITAKA MAMLAKA KUBORESHA MIUNDOMBINU

WAFANYABIASHARA wa Tengeru Mkoani Arusha wamewataka baadhi ya viongozi wa mamlaka mbalimbali za Serikali Wilayani humo kuboresha miundombinu ili kutekeleza maagizo ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan yenye dhamira njema kwa wafanyabiashara.

Hayo yamesemwa leo na wafanyabiashara wa Tengeru wakati wa Mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) na wafanyabiashara wa eneo hilo uliofanyika kwa lengo ikiwa ni kupokea, kuchakata na kutolea ufafanuzi wa kero, changamoto na maoni ya wafanyabiashara.

Mmoja wa wafanyabiashara hao Aloyce Mallya amebainisha ukosefu wa soko katika eneo hilo na hata eneo ambalo linatumika kama soko lina miundombinu mibovu ikiwemo huduma za vyoo pamoja na barabara hali inayohatarisha afya za wafanyabiashara na watumiaji wengine wa eneo hilo.

Wamesema kuwa hata hivyo eneo wanalofanyia biashara ni finyu kwa biashara siku za minada hivyo wanaiomba serikali kuwapa eneo ambalo litatumika kufanyia biashara zao.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania Hamis Livembe amesema kuwa  nia ya Serikali ya awamu ya sita ni kutatua kero zote za wafanyabiashara nchini hivyo kero hizo zote wanazifikisha sehemu husika kwa ajili ya kuzipatia ufumbuzi.

Awali  Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania Abdalla Salim amewataka wafanyabiashara wawe wazi kusema kero zao ili kupata ufafanuzi na ufumbuzi wa kero zao na kuwahimiza kujaza fomu ili wasajiliwe na kupata vitambulisho kwani kila Sekta duniani ina utambulisho wake. 

Pia kupitia vitambulisho  hivyo vitawasaidia kutatuliwa changamoto zao na viongozi wa Jumuiya kwa kushirikiana na Mamlaka husika kutatua changamoto hizo.

Naye  Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Mkoa wa Tanga Ismail Masoud amesema kuwa Rais Samia anawapenda wafanyabiashara ndiyo maana ametoa fursa ya kufanya mikutano nchi nzima ili wafanyabiashara waweze kuwasilisha changamoto na kero zao na amewasisitiza wafanyabiashara kutumia Jumuiya kama chombo cha utatuzi wa kero zao.