Monday, January 23, 2017

BOMOA YATIKISA MAILI MOJA KIBAHA





Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la kubomoa soko la Maili Moja wilayani Kibaha pamoja na nyumba za biashara na za makazi ambavyo vilijengwa kwenye hifadhi ya barabara limefanyika na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani chini ya ulinzi mkali wa polisi.
Zoezi hilo ambalo lilianza jana majira ya asubuhi limefanyika baada ya kushindikana kufanyika kwa muda mrefu ambapo mara ya mwisho wameliki wa maeneo hayo walipewa barua na TANROADS miezi sita iliyopita.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake meneja wa wakala hao mkoa wa Pwani Injinia Yudas Msangi alisema kuwa lengo kuu la kubomoa ni kuhakikisha kuwa eneo hilo la hifadhi ya barabara inakuwa wazi.
Msangi alisema kuwa zoezi hilo limefanikiwa kutokana na kuwajulisha mapema wahusika kuwa wabomoe wenyewe kabla ya siku ya kubomoa kufanyika jana Januari 23.
“Tunashukuru kwani hakuna mtu anayelalamika kwa sababu tuliwapa taarifa mapema na wengi wametii kwa kuvunja wao wenyewe na kutoa vitu vyote vya thamani licha ya wachache ambao walishindwa kubomoa wao wenyewe,” alisema Msangi.
Alisema kuwa zoezi hilo kwa Maili Moja ndiyo limehitimisha ubomoaji kwa watu waliojenga kwenye hifadhi ya barabara katika mkoa huo ambapo mwaka jana walibomoa maeneo mengine ya wilaya zote za mkoa huo.
“Baada ya zoezi la kubomoa wananchi hawpaswi kujenga tena kwenye eneo hilo la hifadhi ya barabara ambalo lina matumizi mbalimbali kwa ajili ya magari na shughuli nyingine zinazohusu barabara,” alisema Msangi
Aidha alisema kuwa jana walivunja eneo la umbali wa mita 60 kutoka barabara kuu ya Morogoro ambazo ziko ndani ya hifadhi ya barabara ambayo ilitengwa kwa ajili ya matumizi mengine.
Naye mkaguzi wa barabara Injinia Livingstone Urio alisema kuwa zoezi hilo ni mwendelezo wa usafishaji wa maeneo ambayo ni hifadhi ya barabara ambapo pia ni usalama kwa wananchi kwani ni hatari kujenga au kufanya biashara karibu na barabara.
Urio alisema kuwa eneo hilo lilitengwa kisheria na watu hawakutakiwa kujenga makazi au vibanda vya biashara na wananchi wengi wao wanajua mmiliki wa eneo hilo.
Kwa upande wake mfanyabiashara wa soko la Maili Moja Ally Gonzi alisema kuwa wao wamepokea zoezi hilo kama lilivyo kwani tayari wlaikuwa na taarifa juu ya matumizi ya eneo hilo.
Gonzi alisema kuwa kwa kuwa wametengewa eneo la kufanyia biashara hivyo wataenda huko kwa ajili ya kuendelea na biashara zao licha ya kuwa maandalizi ya soko jipya wamechelewa.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment